Wednesday, December 7, 2016

Waziri Mahiga akutana na Waziri wa Mambo ya Nje wa Korea


TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Waziri Mahiga akutana na Waziri wa Mambo ya Nje wa Korea jijini Addis Ababa.

Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamhuri ya Korea, Mhe. Yun Byung-se ametangaza kuwa Tanzania itapokea msaada mkubwa zaidi wa maendeleo kuliko nchi yeyote barani Afrika inayotolewa na Serikali ya Korea kwa ajili ya bara hilo.
Hayo aliyabainisha leo alipofanya mazungumzo na Waziri wa Mambo ya  Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dkt. Augustine Mahiga kando ya Mkutano wa Ushirikiano kati ya nchi za Afrika na Korea ulioanza jana  jijini Addis Ababa, Ethiopia.

Katika mazungumzo hayo, Dkt. Mahiga aliipongeza Korea kwa hatua ya maendeleo iliyofikia ambapo katika kipindi kifupi imeweza kuendelea kiviwanda na teknolojia ili hali wakati nchi za Afrika zinapata uhuru katika miaka ya 60 Korea ilikuwa ni moja ya nchi masikini duniani.

Waziri Mahiga aliishukuru Jamhuri ya Korea kwa misaada inayoipatia Tanzania. Alisema misaada hiyo ni kwa ajili ya watu masikini kwa kuwa inaelekezwa maeneo yanayogusa watu wa chini kama vile afya, maji, elimu na miundombinu ya mawasiliano.

Waziri Mahiga aliweka wazi kuwa Tanzania itaendelea kufanya kazi kwa karibu na Korea kwa dhamira ya kujifunza namna nchi hiyo ilivyopiga hatua ya maendeleo ya viwanda na teknolojia ili nayo iweze kufikia azma ya Serikali ya awamu ya tano ya kuifanya Tanzania kuwa nchi ya viwanda.

"Tunahitaji kushirikiana na Korea katika maeneo ya viwanda, nishati jadilifu, miundombinu, madini, tehama na gesi na mafuta.  Kutokana na  hatua ya maendeleo iliyofikiwa na Korea,  Tanzania ina matumaini makubwa kuwa nchi hiyo itatoa msukumo mkubwa katika kuendeleza maeneo hayo".

Aliongeza kuwa Tanzania inahitaji sio ilimradi viwanda bali viwanda vitakavyotumia malighafi za kilimo na madini ambavyo licha ya kutoa soko kwa wakulima bali pia vitaongeza ajira kwa wananchi.

Aidha, Dkt. Mahiga aliishauri Korea kuangalia namna itakavyoshirikiana na bara zima la Afrika, hususan kusaidia miradi ambayo itakuwa alama ya kudumu ya  ushirikiano kati ya nchi hiyo na bara la Afrika. Alitolea mfano wa mradi wenye sifa hiyo ni Korea kufadhili ujenzi wa jengo la Makao Makuu ya Mahakama ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu yenye makao yake jijini Arusha, Tanzania. Mahakama hiyo ni muhimu katika uimarishaji wa utawala wa sheria na demokrasia barani Afrika.

Halikadhalika, Waziri Mahiga alipendekeza Chuo cha Diplomasia cha Tanzania na kile cha Korea vianzishe ushirikiano wa kindugu ili vibadilishane uzoefu na kutatua changamoto zinazovikabili vyuo hivyo kwa pamoja.

Vile vile. Mhe. Waziri alimfahamisha Waziri mwenzake kuwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli alishateua Balozi kwa ajili ya kuiwakilisha Tanzania nchini Korea kwenye Ofisi ya Ubalozi itakayofunguliwa hapo baadaye katika mwaka wa fedha 2016/2017.

Kwa upande wake, Mhe. Yun alieleza kuwa Tanzania ni mshirika mkubwa wa Korea na kusisitiza umuhimu wa Serikali kuboresha zaidi mazingira ya uwekezaji ili makampuni ya Korea yaje kwa wingi kuwekeza Tanzania. Alisisitiza umuhimu wa kukamilisha Mkataba wa Kulinda Vitega Uchumi na ule wa Kuepuka Tozo ya Kodi mara mbili kama moja ya njia ya kuvutia wawekezaji kutoka Korea.

Aidha, alikumbusha kuwa  mahusiano ya kidiplomasia kati ya Tanzania na Korea yanatimiza miaka 25 mwaka 2017 tokea yalipoanzishwa mwaka 1992, hivyo alihimiza umuhimu wa nchi hizi mbili kuangalia namna zitakavyoadhimisha miaka 25 ya ushirikiano huo.



Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
06 Desemba, 2016.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Augustine Mahiga (kulia) akiwa katika mazungumzo na Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamhuri ya Korea, Mhe. Yun Byung-se.  Mazungumzo hayo yalifanyika jijini Addis Ababa kando ya Mkutano wa Ushirikiano wa nchi za Afrika na Korea
 
Bw. Benedict Msuya na Bi. Berther Makilagi ambao ni maafisa kutoka Wizara ya Mambo ya Nje wakinukuu masuala muhimu ya mazungumzo ya Waheshimiwa Mawaziri wa Korea na Tanzania.
Maafisa walioambatana na Waziri wa Mambo ya Nje wa Korea nao wakinukuu taarifa za mazungumzo.

Mhe. Mahiga na Mhe. Yun wakishikana mikono ya kuombeana kheri baada ya kukamilisha mazungumzo yao.

Tuesday, December 6, 2016

Afrika na Korea zajadili maendeleo jijini Addis Ababa

Balozi wa Tanzania nchini Ethiopia na katika Umoja wa Afrika, Mhe. Naimi Aziz akipitia makabrasha ya Mkutano wa nne wa Ushirikiano kati ya nchi za Afrika na Jamhuri ya Korea unaofanyika kwenye makao makuu ya Umoja wa Afrika jijini Addis Ababa, Ethiopia. Nyuma ya Mhe. Balozi ni Afisa wa Ubalozi wa Tanzania nchini Ethiopia, Bi. Suma Mwakyusa.


JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
WIZARA YA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI 


TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Afrika na Korea zajadili maendeleo jijini Addis Ababa

Mkutano wa nne wa siku mbili wa Ushirikiano kati ya nchi za Afrika na Jamhuri ya Korea kwa ngazi ya Mawaziri ambao kwa mara ya kwanza unafanyika barani Afrika umeanza leo jijini Addis Ababa, Ethiopia kwa kikao cha Maafisa Waandamizi. Katika kikao hicho ambapo Tanzania inawakilishwa na Balozi wake nchini Ethiopia, Mhe. Naimi Aziz ni kwa ajili ya kuandaa mkutano wa Mawaziri utakaofanyika kesho tarehe 07 Desemba 2016, ambapo Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dkt. Augustine Mahiga tayari alishawasili Ethiopia kuiwakilisha Tanzania.

Maafisa Waandamizi pamoja na mambo mengine, walipata fursa ya kupokea taarifa mbalimbali ikiwemo kupitia Azimio la Addis Ababa litakaloidhinishwa na Mkutano wa Mawaziri pamoja na utekelezaji wa mpango kazi (Kati Ya mwaka 2013-2015) katika maeneo yaliyoafikiwa katika Mkutano wa tatu wa Korea-Afrika uliofanyika mwaka 2012, Seoul, Jamhuri ya Korea. Mkutano wa kwanza na wa pili ilifanyika mwaka 2006 Na 2009, Seoul, Korea.

Maeneo ambayo Nchi za Afrika zilikubaliana kushirikiana na Korea ni pamoja na maendeleo endelevu, elimu, afya, kilimo, mabadiliko ya tabianchi, biashara, uwekezaji na uchumi, amanina usalama na masuala ya mtambuka kama vile masuala ya jinsia, wanawake na watoto, masuala Ya TEHAMA n.k.

Wajumbe walielezwa kuwa katika maeneo yote hayo Korea ilitekeleza wajibu wake ipasavyo kwa kuongeza fedha takriban katika kila eneo kuanzia mwaka 2012 hadi 2015.

Kwa upande wa kilimo Korea imekuwa ikishirikiana na nchi za Afrika kwenye ujenzi wa miundombinu ya kilimo cha umwagiliaji na masuala mengine ya kiufundi ambapo kiasi cha msaada katika eneo hilo kimeongezeka kutoka Dola za Marekani bilioni 16 mwaka 2012 na kufikia Dola bilioni 40 mwaka 2015. Kwa upande wa Tanzania; Zanzibar imefaidika na fedha hizo ambapo imepokea Dola milioni 50 kwa ajili ya uendelezaji wa kilimo cha mwani.

Eneo lingine ambalo Korea iliwekeza fedha za kutosha ni lile la afya ambapo kiasi kilichotolewa kimefikia Dola milioni 27 mwaka 2015 ukilinganisha na kiasi cha Dola milioni 16 kilichotolewa mwaka 2012. Jiji la Dar es Salaam limefaidika na fedha hizo kwa kujengewa hospitali ya uchunguzi ya afya ya mama kwenye eneo la Chanika wilayani Ilala ambayo inatarajiwa kukamilika mwaka 2017.

Aidha, kwa kutambua umuhimu wa amani na usalama katika maendeleo ya Bara la Afrika, Korea imekuwa ikifadhili programu mbalimbali ndani ya Umoja wa Afrika zinazolenga kutatua migogoro na kuleta amani ya kudumu barani humo. 

Katika kikao hicho wajumbe walisisitiza umuhimu wa kufikia malengo yaliyowekwa na ushirikiano huo kwa kutekeleza kikamilifu miradi ya maendeleo iliyoainishwa na Umoja wa Afrika ili kuweza kupiga hatua za kiuchumi kwa faida ya Afrika kwa ujumla.

Mkutano huo unatarajiwa kukamilika kwa kutolewa Tamko ambalo pamoja na mambo mengine litainisha maeneo mapya ya ushirikiano kati ya Korea na nchi za Afrika kwa kipindi cha miaka mitano ijayo 2017 - 2021.

Imetolewa na: KITENGO CHA MAWASILIANO YA SERIKALI, WIZARA YA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI.

06 DESEMBA, 2016

Friday, December 2, 2016

Waziri Mahiga ashiriki maadhimisho ya siku ya Kitaifa ya Umoja wa Falme za Kiarabu

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Dkt. Augustine Mahiga akisalimiana na Balozi wa Umoja wa Falme za Kiarabu nchini Mhe.Abdulla Ibrahim Ghanim Alsuwaidi alipowasili katika ofisi za ubalozi huo kushiriki sherehe ya madhimisho ya miaka 45 ya muungano.Tanzania na UAE zimepiga hatua kubwa za ushirikiano hususan ya kiuchumi ambapo kwa takwimu za Kituo cha Uwekezaji nchini (TIC) hadi Juni, 2015 makampuni 67 ya uwekezaji kutoka UAE yamewekeza hapa nchini katika sekta mbalimbali wenye thamani ya USD 497.12 Millioni na kuajiri Watanzania 9,044. Taifa la Umoja wa Falme za Kiarabu unaundwa na falme saba ambazo ni Abu Dhabi, Dubai, Sharjah, Ras Al Khaimah, Fujairah, Ajman na Umm al-Quwain
                                           
Rais Mstaafu wa Serikali ya Awamu ya nne ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete akiwa katika picha ya pamoja na Balozi wa Taifa la Umoja wa Falme za Kiarabu Mhe.Abdulla Ibrahim Ghanim Alsuwaidi wakati wa sherehe ya maadhimisho ya miaka 45 ya muungano wa falme hizo

Mhe.Waziri Balozi Dkt.Mahiga akivalishwa skafu maalum

Mhe.Waziri Balozi Dkt. Mahiga akiwa katika picha ya pamoja na Balozi Mhe.Abdulla Ibrahim Ghanim Alsuwaidi


Wageni waalikwa wakifuatilia jambo

Balozi wa Taifa la Umoja wa Falme za Kiarabu Mhe.Abdulla Ibrahim Ghanim Alsuwaidi akizungumza wakati wa maadhimisho 

Mhe. Waziri Balozi Dkt. Mahiga akitoa hutuba fupi wakati wa maadhimisho ya sherehe hizo


Mkurugenzi wa Idara ya Mashariki ya Kati Balozi Abdalla Kilima akisalimiana na Mhe. Balozi wakati wa sherehe za maadhimisho
         ------------------------------------------------------------------------------------------------------                                                                  

Tanzania na Umoja wa Nchi za Kiarabu (UAE) zimepiga hatua kubwa za ushirikiano hususan wa kiuchumi ambapo kwa takwimu za Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) hadi Juni, 2015 Makampuni 67 kutoka UAE yamewekeza hapa nchini katika sekta mbalimbali kwa mtaji wa thamani ya Dola za Marekani  milioni  497.12  na kuajiri Watanzania zaidi ya 9,044. 
 
Hayo yalibainishwa jana katika sherehe za kuadhimisha Siku ya Kitaifa ya UAE zilizofanyika jijini Dar Es Salaam ambapo Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Augustine Mahiga alikuwa Mgeni Rasmi. 

Tanzania na UAE  zinatarajiwa kufanya Mkutano wa Kwanza wa Tume ya Pamoja ya Kudumu ya Ushirikiano (JPC) ambao utakuwa chachu ya kuimarisha mahusiano baina ya nchi hizi mbili hususan ya kiuchumi. 

Akiongea katika hafla hiyo, Mhe. Waziri alilipongeza taifa hilo kwa kuadhimisha siku yake ya Kitaifa ikiwa imepiga hatua kubwa ya kimaendeleo ya kichumi, kijamii na kisiasa. Mhe.  Waziri alisema kuwa siku hiyo ni inatoa fursa pia ya kutathmini mahusiano mazuri yaliyopo baina ya Tanzania na UAE.

Kwa upande wake, Balozi wa UAE hapa nchini, Mhe. Abdulla Ibrahim Ghanim Alsuwaidi aliishukuru Serikali ya Tanzania kwa ushirikiano mkubwa inayotoa kwa Ubalozi huo ambao unamwezesha kutekeleza majukumu yake kwa wepesi ikiwa ni pamoja na kuimarisha mahusiano ya nchi hizi mbili. Mhe. Balozi aliahidi kuendeleza ushirikiano huo hususan katika kutimiza azma ya Serikali ya Awamu ya Tano ya Kuifanya Tanzania kuwa nchi ya Viwanda. 

Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) unajumusha falme saba ambazo ni Abu Dhabi, Dubai, Sharjah, Ras Al Khaimah, Fujairah, Ajman na Umm al-Quwain huadhimisha siku yake ya Kitaifa tarehe 02 Disemba ya kila mwaka tokea mwaka 1971.






Thursday, December 1, 2016

Mkutano wa ushirikiano kati ya Afrika na Jamhuri ya Korea kufanyika Addis Ababa

Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali na Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bi. Mindi Kasiga akizungumza kwenye mkutano na Waandishi wa Habari. Katika mkutano huo Bi. Kasiga aliwaeleza Waandishi wa Habari kuhusu Mkutano wa Nne wa Mawaziri wa nchi za Afrika na Korea utakaofanyika Mjini Addis Ababa, Ethiopia tarehe 06 na 07 Desemba, 2016. Mkutano huo utajadili masuala mbalimbali ya ushirikiano baina ya Afrika na Korea pamoja na maeneo mapya ya mashirikiano.
Afisa Mambo ya Nje, Bi. Bertha Makilagi akifuatilia mkutano kati ya Bi. Kasiga na Waandishi wa Habari. Wengine ni Waandishi wa Habari waliohudhuria mkutano huo.
Sehemu ya Waandishi wa Habari wakisikiliza na kunukuu kwa makini mkutano uliokua ukiendelea
Mkutano ukiendelea



TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Mkutano wa Nne wa Mawaziri wa Mambo ya Nje wa nchi za Afrika na Korea ujulikanao kama Korea-Africa Ministerial Forum unaotarajiwa kufanyika kwa mara ya kwanza Barani Afrika, Addis Ababa, Ethiopia tarehe 06 na 07 Desemba, 2016. Mikutano mitatu ya kwanza ilifanyika Seoul, Korea mwaka 2006, 2009 na 2012.

Mkutano huu ambao umeandaliwa na Serikali ya Korea kwa kushirikiana na Umoja wa Afrika una lenga kukuza ushirikiano pamoja na kuandaa maeneo mapya ya ushirikiano baina ya Korea na mataifa ya Afrika katika miaka mitatu ijayo.

Tanzania ni moja ya nchi nne (4) za Afrika ambazo Korea imezichagua kuanzisha mahusiano ya kimkakati “strategic partnership” yatakayozifanya nchi hizo kupewa kipaumbele katika kupokea misaada na mikopo nafuu kutoka Korea katika kipindi cha miaka mitano ijayo kati ya 2016 hadi 2020.
Katika kipindi hicho, Tanzania itapokea kiasi cha Dola za Kimarekani milioni 300 ikiwa ni asilimia 17.1 ya msaada utakaotolewa Barani Afrika, hivyo kuifanya Tanzania kuwa nchi inayoongoza Barani Afrika kupokea misaada kutoka Jamhuri ya Korea. Nchi nyingine ni Msumbji, Ethiopia na Angola.
Msaada huo unategemea kufadhili miradi katika sekta za umeme, viwanda na TEHAMA. 

Sanjari na Mkutano huo, ujumbe wa Tanzania utafanya mkutano wa pande mbili na ujumbe wa Serikali ya Korea kuzungumzia masuala ya ushirikiano baina ya nchi zetu mbili. Tanzania itatumia fursa hiyo kuiomba Korea kuongeza kasi ya utekelezaji wa miradi mipya ikiwemo mradi wa Daraja la Selander ambao unatarajiwa kuanza mwaka 2017 na kukamilika 2020.
Aidha, ushiriki wa Tanzania kwenye mkutano wa Afrika na Korea ni fursa muhimu ya kukuza mahusiano baina ya nchi zetu mbili hususan katika Nyanja ya uchumi. Serikali ya Korea ilitoa ahadi ya kuongeza uwekezaji Barani Afrika hususan katika sekta za nishati, miundombinu na viwanda. 

 Miradi ambayo Tanzania imefaidika tokea kuanzishwa mikutano hii mwaka 2006 ni pamoja na mradi wa kuendeleza kilimo cha Mwani Zanzibar wenye thamani ya Dola za Kimarekani milioni 3.6 na Awamu ya Pili ya Mradi wa Huduma ya Uchunguzi wa Afya ya Uzazi Jijini Dar es Salaam wenye thamani ya Dola za Kimarekani milioni nne (4).

Miradi mingine ambayo Jamhuri ya Korea imeshirikiana na inaazimia kushirikiana na Tanzania ni:-
·        Ujenzi wa Mradi wa Daraja la Kikwete kwenye Mto Malagarasi Mkoani Kigoma ambao umekamilika; Ujenzi wa Hospitali ya Kimataifa iliyopo eneo la Mloganzila; Dar es Salaam   na Hospitali ya Mama na Mtoto iliyopo Chanika, Dar es Salaam.

·        Kadhalika, hivi karibuniTanzania imesaini
o   Makubaliano ya kupanua miundombinu ya Majitaka jijini Dar es Salaam; na
o   Makubaliano ya kutekeleza miradi utakaofadhiliwa kwa pamoja na benki ya Maendeleo ya Afrika na Serikali ya Jamhuri ya Korea.

Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
Dar es Salaam, 01 Desemba, 2016.





Katibu Mkuu wa Mambo ya Nje afungua mkutano wa JPC kati ya Tanzania na Kenya

Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dkt. Aziz Mlima akizungumza wakati wa ufunguzi wa mkutano wa Tume ya Pamoja ya Kudumu ya Ushirikiano (JPC) kati ya Tanzania na Kenya uliofanyika kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Julius Nyerere Jijini Dar es Salaam. Mkutano huo pamoja na mambo mengine utajadili maeneo mbalimbali ya ushirikiano ikiwemo sekta ya Elimu, Afya na Kilimo.
Balozi wa Kenya hapa nchini, Mhe. Chirau Ali Mwakwere akifuatilia ufunguzi wa Mkutano wa Tume ya Pamoja ya Kudumu ya Ushirikiano kati ya Tanzania na Kenya
Kaimu Balozi wa Tanzania nchini Kenya, Bi. Talha Mohammed (kulia) naye akifuatilia ufunguzi wa Mkutano wa JPC.
Balozi Ben Ogutu, Kiongozi wa Ujumbe wa Kenya akizungumza wakati wa ufunguzi wa mkutano wa JPC kati ya Tanzania na Kenya
Mkurugenzi wa Idara ya Afrika katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Samwel Shelukindo akizungumza wakati wa Mkutano wa JPC kati ya Tanzania na Kenya
Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki ambaye pia alikuwa mshereheshaji akizungumza, Bi. Mindi Kasiga
Sehemu ya wajumbe kutoka Kenya wakifuatilia ufunguzi wa Mkutano wa JPC
Sehemu nyingine ya wajumbe kutoka Tanzania wakifuatilia mkutano

Waziri Mahiga asaini kitabu cha maombolezo ya Rais Mstaafu wa Cuba Fidel Castro

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Dkt. Augustine Mahiga akisalimiana na Balozi wa Cuba nchini Mhe. Jorge Luis Lopez Tormo alipowasili nyumbani kwa Balozi huyo mapema leo kusaini kitabu cha maombolezo kufuatia kifo cha Rais Msataafu wa Cuba Fidel Castrol, Jijini Dar es Salaam 

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Dkt. Augustine Mahiga akimfariji Balozi wa Cuba nchini Mhe. Jorge Luis Lopez nyumbani kwake Jijini Dar es Salaam kabla ya kusaini kitabu cha maombolezo

Mhe. Waziri Balozi Dkt. Augustine Mahiga akitoa heshima mbele ya picha ya  Rais wa zamani wa Cuba hayati Fidel Castro alipoenda kusaini kitabu cha maombolezo

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Dkt. Augustine Mahiga akisaini kitabu cha maombolezo