Friday, October 26, 2018

Dkt. Ndumbaro awa Mgeni Rasmi maadhimisho ya Siku ya Mfalme wa Ubelgiji

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Dkt. Ndumbaro awa Mgeni Rasmi maadhimisho ya Siku ya Mfalme wa Ubelgiji

 Kampuni 32 kutoka Ubelgiji zilizowekeza Tanzania ni chache ukilinganisha na uwingi wa fursa za uwekezaji zilizopo nchini ambazo kwa kiasi kikubwa bado hazijatumika kikamilifu.
Kauli hiyo ilitolewa na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Damas Ndumbaro (Mb) katika hafla ya kuadhimisha Siku ya Mfalme wa Ubelgiji iliyofanyika kwenye makazi ya Balozi jijini Dar Es Salaam tarehe 26 Oktoba 2018.

“Tanzania ina fursa nyingi za uwekezaji katika sekta mbalimbali kama vile; kilimo, ujenzi wa miundombinu, nishati, madini, teknolojia ya habari na mawasiliano, afya, viwanda vya uzalishaji, mafuta na gesi ambazo hazijatumika ipasavyo. Hivyo, Ubelgiji na Tanzania zikijizatiti zinaweza zikafanya biashara na kufanya uwekezaji mkubwa na wenye manufaa kwa pande zote mbili), Dkt. Ndumbaro alisema.

Alielezea matumaini yake kuwa ujio wa Makampuni makubwa ya Ubelgiji zaidi ya 40 ambayo yamekuwa na mazungumzo yenye tija na Makampuni ya Tanzania na sekta nyingine zinazohusika na uwekezaji kwa siku tatu zilizopita, utaleta ongezeko la uwekezaji na kuimarika kwa kiwango cha biashara kati ya Ubelgiji na Tanzania.

Kwa upande wa biashara kati ya Tanzania na Ubelgiji, Mhe. Naibu Waziri ameridhishwa na urari wa biashara uliopo, ingawa alisisitiza umuhimu wa kuimarisha zaidi. Kwa mujibu wa takwimu za mwaka 2016, biashara kati ya Ubelgiji na Tanzania imefikia kiwango cha Dola milioni 332 huku Tanzania ikiuza bidhaa zenye thamani ya Dola milioni 208 nchini Ubelgiji.

Dkt. Ndumbaro alihitimisha hotuba yake kwa kuishukuru Ubelgiji kwa kuendelea kuwa mshirika mkubwa wa jitihada za Serikali ya awamu ya tano chini ya Mhe. Dkt. John Pombe Joseph Magufuli ya kuwaletea Watanzania maendeleo. Alitoa mfano wa programu mbalimbali za maendeleo nchini zinazogharamiwa na Serikali ya Ubelgiji kwa kiasi cha Euro milioni 20.

Programu hizo zinajumuisha upatikanaji wa maji safi vijijini na uendelezaji endelevu wa sekta ya kilimo katika mkoa wa Kigoma. Utekelezaji wa miradi hiyo imesaidia kuboresha usimamizi mzuri wa vyanzo vya maji, usimamizi wa rasilimali na mnyoro wa thamani katika kilimo, hususan kwa wakulima wadogo.

Kwa upande wake, Balozi wa Ubelgiji nchini Tanzania Mhe. Peter van Acker alisema kuwa Ubelgiji itaendelea kuunga mkono jitihada za Serikali ya awamu ya tano za kubadalisha maisha ya watu masiikini. Alisema jitihada hizo pamoja na mambo mengine, zitaeendelea kuunga mkono juhudi za Tanzania za kuleta utulivu wa kisiasa katika eneo la maziwa makuu ikiwemo usuluhishi wa mgogoro wa Burundi.

Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,
Dar Es Salaam, Tanzania
27 Oktoba 2018

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Dkt. Damasi Ndumbaro (Mb.) akihutubia kwenye hafla ya maadhimisho ya siku ya Mfalme wa Ubelgiji yaliyofanyika katika makazi ya Balozi wa Ubelgiji jijini Dar Es Salaam jana. Maadhimisho hayo yamehudhuriwa pia na Naibu Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Mhe. Mhandisi Stella Manyanya.  
Balozi wa Ubelgiji nchini Tanzania, Mhe. Peter van Acker akihutubia kwenye maadhimisho ya siku ya Mfalme wa Ubelgiji yaliyofanyika katika makazi yake jana.  
Wageni waalikwa wakisikiliza kwa makini hotuba zilizokuwa zikitolewa  
Dkt. Ndumbaro akiendelea kuhutubia. 
Dkt. Ndumbaro akigonganisha glasi na Balozi Peter van Acker kwa kuwatakia afya njema Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Joseph Magufuli na Mfalme Philippe Leopold Louis Marie wa Ubelgiji.  
Naibu Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji Mhe. Mhandisi Stella Manyanya (Mb.) wa kwanza kulia akizungumza na Meneja wa mauzo wa Kimataifa wa kampuni ya Cardolite kutoka Ubelgiji Bw. Hans Carleer pamoja na Afisa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Bw. Mohamed Kamal (wa kwanza kushoto).

Balozi Dkt. Slaa awasilisha Hati zake za Utambulisho kwa Rais wa Finland

Balozi wa Tanzania kwenye Nchi za Nordic, na Baltic Mhe. Wilbrod Slaa awasilisha Hati zake za Utambulisho kwa Rais wa Finland, Mheshimiwa Sauli Niinistö  jijini Helsinki
Balozi Dkt. Slaa akiwa katika picha ya pamoja na Mhe. Sauli Niinistö.


Thursday, October 25, 2018

Ubelgiji yaambiwa iongoze uwekezaji nchini, Mhandisi Manyanya


TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Ubelgiji yaambiwa iongeze uwekezaji nchini, Mhandisi Manyanya

Ubelgiji imetakiwa kuongeza kiwango cha uwekezaji nchini ili kuchochea zaidi kasi ya azma ya Serikali ya awamu ya tano ya kuifanya Tanzania kuwa nchi ya viwanda na uchumi wa kati ifikapo mwaka 2025.

Kauli hiyo ilitolewa leo na Naibu Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Mhe. Mhandisi Stella Manyanya (Mb) alipokuwa anatoa hotuba ya ufunguzi wa Kongamano la Wafanyabiashara wa Ubelgiji na Tanzania linalofanyika katika Hoteli ya Serena jijini Dar Es Salaam.

“Kuna miradi 32 yenye thamanai ya Euro milioni 902 ambayo imeajiri wafanyakazi 1814 inayomilikiwa na wawekezaji kutoka Ubelgiji nchini Tanzania. Hivyo, kuna umuhimu wa kuongeza uwekezaji huo kwa kuwa mazingira ya uwekezaji nchini ni mazuri na yanavutia”, Mhandisi Manyanya alisema.

Mhe. Naibu Waziri aliwahamiza wawekezaji hao ambao ni wafanyabiashara wakubwa nchini Ubelgiji kuwekeza katika sekta za kilimo, hususan kwenye maeneo ya viwanda vya nguo, sukari, mafuta ya kupikia, maziwa, ngozi, nyama, mbegu, matunda na maua,

Sekta nyingine aliyoitaja ni ya nishati hasa katika miundombinu ya kuzalisha na kusambaza gesi asilia na nishati jadilifu.
Maeneo mengine yaliyosisitizwa na Mhe. Naibu Waziri ni pamoja na sekta ya utalii, madini, uvuvi katika bahari kuu, miundombinu, maeneo maalum ya viwanda (industrial parks) na ujenzi wa majengo hususan katika mji mkuu wa Dodoma ambapo mahitaji ni makubwa.

 Uzalishaji wa dawa za binadamu na wanyama, vifaa tiba na uzalishaji wa samani za kisasa ni maeneo ambayo Mhe. Naibu Waziri aliwasihi wawekezaji hao kuyapa jicho la pekee.

Mhe Manyanya alisema wawekezaji watakaoamua kuwekeza nchini hawatajutia uamuzi wao kwa kuwa Tanzania kuna mazingira mazuri. Mazingira hayo ni pamoja na amani na usalama, rasilimali za kutosha na uhakika wa soko kwa kuwa Tanzania ni mwanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki na Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika na hatua zinakamilishwa kuwa na eneo huru la biashara barani Afrika.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Kukuza Uwekezaji kutoka Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC), Bw. John Mathew Mnali aliwahakikishia wawekezaji hao kuwa TIC itatoa msaada unaohitajika kupitia kituo chake cha kutoa huduma kwa pamoja (One Stop Centre) kwa mfanyabiashara yeyote mwenye dhamira ya kuwekeza nchini. Alitaja msaada wanaotoa kupitia kituo hicho ni pamoja na msaada wa kupata vibali vya kazi na makazi, kupata ardhi ya kuwekeza, miongozo ya kodi ikiwemo kupata Namba ya Utambulisho ya Mlipa Kodi (TIN), kuthibitisha bidhaa kutoka Shirika la Viwango Tanzania, Mamlaka ya Chakula na Dawa na masuala ya kupata vibali vya mazingira (environment clearance).

Bw. Mnali alibainisha kuwa kuna bandari kubwa tatu nchini zinaunganisha nchi jirani ambazo hazina bandari. Aidha, Tanzania inaongoza kikanda kupokea miradi ya moja kwa moja ya uwekezaji kutoka nje (FDI) na pia ni miogoni mwa nchi ambazo uchumi wake unakua kwa kasi duniani. Alisema sababu hizo ni vigezo tosha vya kuichagua Tanzania kuwa kimbilio la uwekezaji.

Mkurugenzi Mtendaji wa Kundi la Wafanyabiashara la Umoja wa Ulaya nchini, Bi. Marie Strain alisema kuwa nchi za umoja huo zinashika nafasi ya pili kwa kufanya biashara na Tanzania. Hivyo kundi hilo linatoa huduma mbalimbali kwa Wafanyabiashara zikiwemo za ushauri, taarifa za masoko na maeneo ya uwekezaji pamoja na kufanya majadiliano na Serikali namna ya kuboresha zaidi mazingira ya uwekezaji.

Katika mahojiano na waandishi wa habari, Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Ulaya na Amerika kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bw. Jestas Nyamanga alisema kuwa ujio wa wawekezaji hao unatokana na juhudi za Ubalozi wa Tanzania nchini Ubelgiji za kuvutia wawekezaji. Alisema Ubalozi umefanya hivyo, huku ukitambua kuwa takwimu zinaonesha kuwa Ubelgiji ni moja ya nchi kumi duniani zinazoongoza kwa kufanya uwekezaji nje ya nchi.

Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,
Dar Es Salaam, Tanzania
25 Oktoba 2018

Naibu Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Mhe. Mhandisi Stella Manyanya akitoa hotuba ya ufunguzi kwenye kongamano la biashara kati ya Tanzania na Ubelgiji. kongamano hilo lilifanyika katika Hoteli ya Serena jini Dar Es Salaam.
Mkurugenzi wa Kukuza Uwekezaji kutoka Kituo cha Uwekezaji Tanzania, Bw. John Mathew Mnali akiongea katika kongamano hilo.
Wafanyabiashara kutoka Ubelgiji na Tanzania na wageni waalikwa wakimsikiliza Naibu Waziri wakati akitoa hotuba ya ufunguzi wa kongamano la biashara katika Hoteli ya Serena

Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Ulaya na Amerika kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bw. Jestas Nyamanga (kulia) pamoja na wafanyabiashara kutoka Ubelgiji wakimsikiliza Mhe. Naibu Waziri Manyanya
Wafanyabiashara katika kongamno
Wafanyabiashara na wajumbe wengine wakiendelea kumsikiliza Naibu Waziri.
Wafanyabiashara wa Tanzania na Ubelgiji wakiwa katika majadiliano ya ana kwa ana.

Majadiliano ya ana kwa ana kati ya wafanyabiashara wa Tanzania na Ubelgiji

Majadiliano yanayoonesha dalili ya kuzaa matunda ya ushirikiano kati ya Wafanyabiashara wa Tanzania na Ubelgiji

Majadiliano yanaendelea

Tunataka tushirikiane ili tuweze kuwekeza nchini Tanzania

mjadiliano ya ana kwa ana

Njoo uwekeze Tanzania mazingira ni mazuri.




Balozi wa Palestina amekutana na Dkt. Ndumbaro

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Dkt. Damas Ndumbaro (Mb.), amekutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa Palestina nchini Mhe. Hamdi Abduli, katika mazungumzo yao yaliyojikita kwenye kukuza zao na soko la Korosho nchini Tanzania, ambapo Palestina wanauhitaji wa bidhaa ya korosho. 

Pia Mhe. Hamdi Abduli amemshukuru Dkt. Ndumbaro kuwa ushirikiano anaoupata kupitia Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki  wakati wa utekelezaji wa majukumu yake hapa nchini
Watumishi wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki wakifuatilia kwa makini mazungumzo hayo, wa kwanza kushoto ni Katibu wa Naibu Waziri Bw. Charles Faini na Bi. Happy Godfrey. 
Dkt. Ndumbaro akiwa katika picha ya pamoja na Balozi Abduli mara baada ya kumalizika kwa mazungumzo yao.
Balozi wa Abduli pamoja na Dkt. Ndumbaro wakiwa katika picha ya pamoja na Maafisa Mambo ya Nje.



Dkt. Ndumbaro amekutana kwa mazungumzo na Balozi wa China

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Dkt. Damas Ndumbaro (Mb.), amekutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa Jamhuri ya watu wa China Mhe. Wang Ke, katika mazungumzo hayo yaliyojikita katika kuimarisha mahusiano kwenye sekta mbalimbali zikiwemo Elimu, biashara, kilimo na teknolojia. Pamoja na mambo mengine Dkt. Ndumbaro amemshukuru Mhe. Wang Ke, kwa kuendelea kuliwakilisha Taifa lake vyema hapa nchini. Mazungumzo hayo yamefanyika katika Ofisi ndogo ya Wizara ya Mambo ya Nje jijini Dar es Salaam Tarehe 25 Octoba, 2018
Maafisa Mambo ya Nje wakifuatilia kwa makini mazungumzo kati ya Dkt. Ndumbaro na Mhe. Wang Ke
Sehemu ya maafisa wa Ubalozi wa China wakifuatilia kwa makini mazungumzo kati ya Dkt. Ndumbaro na Mhe. Wang Ke.
Balozi Wang Ke akimwelezea Dkt. Ndumbaro zawadi ya sahani yenye mchoro wa maua
Dkt. Ndumbaro akiwa katika picha ya pamoja na Mhe. Wang Ke (wa tatu kutoka kushoto), kulia ni maafisa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki na kushoto ni Maafisa Ubalozi wa China.




Wednesday, October 24, 2018

Dkt. Ndumbaro aanza na Makampuni 41

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Dkt. Damas Ndumbaro (Mb.), akizungumza na waandishi wa Habari juu ya ujio wa Ujumbe mkubwa wa wawekezaji kutoka Ubelgiji, katika mkutano huo na waandishi wa habari Dkt. Ndumbaro aliwaeleza waandishi kuwa "Ushirikiano wetu na Ubelgiji umekuwa mkubwa sasa na kupitia Ubalozi wetu nchini humo umewezesha ujio huu ambapo leo mchana tunawapokea rasmi wangeni hao na tuna imani utafungua ajira mbalimbali zikiwemo za moja kwa moja". hivyo watanzania wachangamkie fursa zitakazoletwa na wawekezaji hao.

Aidha ujumbe huo wa wawekezaji utakuwepo nchini kuanzia Tarehe 24 mpaka 28 Octoba 2018, ambapo wawekezaji hao wanataraijiwa kufanya Kongamano kubwa la biashara hapo kesho katika Hoteli ya Serena iliyopo jijini Dar es Salaam   
Balozi wa Ubelgiji nchini Mhe. Peter VanAcker naye akizungumza kwenye mkutano huo na waandishi wa Habari (hawapo pichani).
Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Amerika na Ulaya Bw. Jestas Nyamanga akifafanua jambo wakati wa mazungumzo hayo.
Sehemu ya waandishi wa Habari na wageni waalika wakifuatilia mkutano uliokuwa ukiendelea.
Mkutano ukiendelea.




Dkt. Ndumbaro atembelea Ubalozi wa Jamhuri ya Sudani nchini.

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Dkt. Damasi Ndumbaro akiweka saini kwenye kitabu cha maombolezo ya aliyekuwa Rais wa zamani wa Jamhuri ya Sudani Mhe. Field Marshall Abdelrahman SwaralDahab ambaye alifariki dunia tarehe 18 Octoba, 2018, tukio hilo limefanyika kwenye ubalozi wa Jamhuri ya Sudani jijini Dar es Salaam Tarehe 24 Octoba, 2018.
Dkt. Ndumbaro akimsikiliza Balozi wa Jamhuri ya Sudani nchini Mhe. Mahgoub A. Sharfi, mara baada ya kumaliza kuweka saini kwenye kitabu cha maombolezo. 
Dkt. Ndumbaro akiagana na Balozi Sharfi.




Umoja wa Mataifa wadhimisha miaka 73 tangu kuanzishwa.

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Majaliwa Kassim akihutubia katika maadhimisho ya miaka 73 tangu kuanzishwa kwa Umoja wa Mataifa, katika hotuba yake Mhe. Majaliwa amesema kwamba nchini Tanzania hakuna ubanaji wa uhuru wa vyombo vya habari wala taasisi zisizo za kiserikali.
Aidha, amesema jambo hilo linadhihirishwa na uwepo wa jumla ya vituo vya redio 152, ambavyo kati yake ni vituo vitatu tu ndivyo vinavyomilikiwa na Serikali. Maadhimisho hayo yamefanyika kwenye Viwanja vya Karimjee jijini Dar es Salaam 24 Octoba 2018 
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Dkt. Damasi Ndumbaro naye akihutubia kwnye maadhimisho hayo kabla ya kumkaribisha Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa
Juu na Chini ni sehemu ya wageni waalikwa waliohudhuria maadhimisho hayo wakifuatilia kwa makini hotuba zilizokuwa zikitolewa na Mhe. Kassim Majaliwa (hayupo pichani).


Waziri Mkuu akiwa kwenye Jukwaa maalumu la kupokea heshima wakati wa maadhimisho hayo
Viongozi kwenye jukwaa kuu nao wakiwa wamesimama wakati wimbo ya Taifa ikipigwa

Sehemu ya Mabalozi wanaoziwakilisha nchi zao hapa nao wakiwa wamesimama wakati wimbo ya Taifa ikipigwa, wa kwanza kulia ni Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Ushirikiano wa Kimataifa wa Wizara ya Mambo ya Nje Bw.  Deusdedit Kaganda
Mhe. Kassim Majaliwa kaiwa katika picha ya pamoja na Naibu Waziri wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Dkt. Ndumbaro, Mratibu wa Mkazi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Mwakilishi wa Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) Bw. Alvaro Rodrigues pamoja na mabalozi mbalimbali wanaoziwakilisha nchi zao nchini.

Mhe. Kassim Majaliwa akiagana na Dkt. Ndumbaro mara baada ya kumalizika kwa maadhimisho hayo.
Mratibu wa Mkazi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Mwakilishi wa Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) Bw. Alvaro Rodrigues naye akiagana kwa furaha na Mhe. Kassim Majaliwa