Monday, March 25, 2019

Nafasi za ajira katika Jumuiya ya Ukanda wa Maziwa Makuu


TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

NAFASI ZA AJIRA KATIKA JUMUIYA YA NCHI ZA UKANDA WA MAZIWA MAKUU (ICGLR)

Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki inawahimiza Watanzania wenye sifa kuomba nafasi za ajira katika Sekretarieti ya Jumuiya ya Ukanda wa Maziwa Makuu (ICGLR) yenye makao makuu Bujumbura, Burundi; Kituo cha Kikanda cha Kupambana na Ukatili na Unyanyasaji wa Kijinsia (Regional Training Facility on SGBV) kilichopo Kampala, Uganda na Kituo cha Demokrasia na Utawala Bora cha Levy Mwanawasa (Levy Mwanawsa Regional Centre for Democracy and Good Governance) kilichopo Lusaka, Zambia. Ajira hizo ni kama ifuatavyo:-

SEKRETARIETI YA MAZIWA MAKUU

  1. Mkurugenzi wa Utawala na Fedha (Director, Administration and Finance);
  2. Mkurugenzi wa Nyaraka na Mikutano (Director, Documentation and Conferences);
  3. Mkurugenzi wa Mawasiliano (Director, Communications);
  4. Mshauri wa Masuala ya Sheria (Legal Adviser).

KITUO CHA DEMOKRASIA NA UTAWALA BORA CHA LEVY MWANAWASA

  1. Mkurugenzi wa Kanda (Regional Director);
  2. Mkuu wa Utafiti (Head, Research);
  3. Mkuu wa Jukwaa na Uchunguzi (Head, Fora and Observatories).

KITUO CHA KIKANDA CHA KUPAMBANA NA UKATILI NA UNYANYASAJI WA KIJINSIA
  1. Mratibu wa Mafunzo (Training Coordinator) na
  2. Mratibu wa masuala ya TEHAMA, Utafiti na Elimu (IT, Research and Knowledge Coordinator).
Waombaji wa nafasi hizo wanapaswa kuwasilisha barua za maombi katika Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kabla ya tarehe 4 Aprili 2019 ili yaweze kuwasilishwa kwenye Sekretarieti ya ICGLR kwa wakati.


Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,
Dodoma
25 Machi 2019


Sunday, March 24, 2019

Prof. Kabudi afungua Mkutano wa Baraza la Wafanyakazi wa Wizara ya Mambo ya Nje

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Profesa Palamagamba John Kabudi amelitaka Baraza la Wafanyakazi la Wizara hiyo kubuni mikakati na mbinu mpya za utekelezaji na namna ya kukabiliana na changamoto zitakazojitokeza na kuhimiza Wafanyakazi kujituma na kuondokana na uzembe katika utumishi wa Umma.

Profesa Palamagamba John Kabudi ameyasema hayo Dodoma wakati akizungumza na wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa mara ya kwanza tangu ateuliwe na Rais Dkt John Pombe Magufuli kuiongoza Wizara hiyo na kuongeza kuwa, ni wajibu wa Baraza hilo kubuni mbinu na mikakati mipya ya kukabiliana na changamoto mbalimbali zinazojitokeza  pamoja na kuhimiza ushirikishwaji wa watumishi badala ya kusubiri mtu mwingine kuzitatua changamoto hizo.

“Sote tunatambua kuwa ushirikishwaji wa watumishi kwenye mipango ya Taasisi na Wizara ni jukumu la kisheria na kwa miaka yote Serikali imekuwa ikisisitiza taasisi kujenga na kutekeleza utaratibu wa kuwashirikisha watumishi kwa kuwa kunaongeza umiliki wa mipango iliyowekwa” 

Aidha, Waziri Profesa Palamagamba John Kabudi amelisisitiza Baraza hilo kupitia upya vipaumbele vilivyowekwa na jinsi gani ya kuvitekeleza, akitolea mfano namna ya kutekeleza kipaumbele cha diplomasia ya uchumi kwa kuvutia wawekezaji na wafanyabiashara kutoka nje, watalii na kutafuta fursa mbalimbali ikiwemo masoko ya bidhaa za kilimo kutoka Tanzania.

Pia kwa mwaka huu wa 2019 amelitaka Baraza hilo la Wafanyakazi wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kujiandaa mapema na kuwashirikisha wote wanaohusika katika na mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Jumuiya ya Maendeleo kusini mwa Afrika  (SADC) kwa kuwa mwezi Agosti  2019 Tanzania itachukua nafasi ya uenyekiti wa Jumuiya hiyo.

“ Hili ni tukio kubwa ambalo ni lazima tujipange vizuri, mara baada ya kazi ya kuandaa bajeti ya wizara ya 2019/2020 lazima tuanze kazi ya kujiandaa kwa mkutano wa SADC mara moja”

Profesa Palamagamba John Kabudi amelitaka pia Baraza la wafanyakazi la wizara hiyo kutathmini kwa kina shughuli zitakazotekelezwa katika kipindi hiki cha mwaka wa fedha na kuyapitia kwa umakini maeneo yote yaliyopewa kipaumbele na serikali na kubaini mipango na mikakati mizuri katika kutekeleza vipaumbele hivyo.

Imetolewa na: 
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,
Dodoma, Tarehe 24 Machi 2019

=======================================================================

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamagamba John Kabudi akizungumza na Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi wa  Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki (hawapo pichani) wakati wa ufunguzi rasmi wa  Mkutano wa Baraza hilo uliofanyika jijini Dodoma, tarehe 24 Machi 2019. Prof. Kabudi aliwataka wajumbe wa Baraza hilo ambao ni wawakilishi wa watumishi wote wa Wizara kuhakikisha wanatekeleza majukumu kwa kuzingatia vipaumbele vya Wizara ikiwemo Diplomasia ya Uchumi ili kukuza uwekezaji na biashara pamoja na kuvutia utalii  kwa maslahi mapana ya Taifa
Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki wakimsikiliza Mhe. Prof. Kabudi (hayupo pichani)


Sehemu nyingine ya wajumbe wa Baraza wakati wa mkutano wao wa mwaka

Wafanyakazi wa Wizara ya Mambo ya Nje ambao ni wajumbe wa Baraza la wafanyakazi wakifuatilia mkutano

Mkutano wa Baraza la Wafanyakazi ukiendelea na wajumbe wakifuatilia


Wajumbe wa Baraza
Mhe. Prof. Kabudi akiwa katika picha ya pamoja  na wajumbe wa meza kuu mara baada ya kufungua Mkutano wa Baraza la Wafanyakazi wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki. Kulia kwake ni Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki na Mwenyekiti wa Baraza, Balozi Ramadhan Muombwa Mwinyi, kushoto kwake ni Katibu wa  Baraza, Bw. Magabilo Murobi. Kushoto ni Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Utawala na Usimamizi wa Rasilimali Watu, Bibi Savera Kazaura na kushoto ni Mwenyekiti wa TUGHE Tawi la Wizara , Bw. Hassan Mnondwa

Mhe. Prof. Kabudi akiwa katika picha ya pamoja na Wajumbe wa TUGHE wa Wizara

Picha ya pamoja na Wajumbe wa Baraza

Rais Nyusi aishukuru Tanzania kwa misaada ya dawa na chakula



TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI


Rais wa Msumbiji, Mhe. Filipe Nyusi na Wananchi wake  wamemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Joseph Magufuli na Wananchi wa Tanzania kwa kuwa miongoni mwa nchi za mwanzo kabisa kutoa misaada ya Madawa, Magodoro na vyakula kwa watu wa Msumbiji walioathirika na kimbunga.

Kimbunga kilichopita katikati ya Jamhuri ya Msumbiji  kilicho anza tarehe 14 Machi 2019,  kimesababisha madhara makubwa katika mji wa Beira ambao ni wa tatu kwa ukubwa na wa pili kibiashara baada ya Maputo.

Upepo uliambatana na mvua uling'oa miti, mapaa ya nyumba za mabati na vigae na kuvunja madirisha ya vioo bila huruma katika mji huo.

Kufuatia janga hilo ambalo limezikumba pia nchi za Malawi na Zimbabwe, Rais Magufuli alitangaza kutoa msaada wa haraka ambapo ndege kubwa za JWTZ zilipeleka misaada hiyo kama inavyoonekana katika picha. 

Mjini wa Beira na wilaya  za jirani ziko kwenye uwanda wa tambarale. Mji huo pia una mito miwili mikubwa inayoingia katika bahari ya Hindi na hiyo ndiyo sababu ya mara kwa mara unakabiliwa na mafuriko.

Tanzania inaomba Mungu mvua zipungue kwa majirani hao ili waweze kuidhibiti hali hii ya mafuriko inayoendelea sasa baada ya Kimbunga kupita.

Mji wa Beira umeharibika vibaya ambapo asilimia 97 ya majengo, miundombinu, na mali za wananchi zimeathiriwa na kimbunga hicho.

Balozi wa Tanzania nchini Msumbiji, Mhe. Rajab Luhwavi ambaye alipokea shukrani hizo kwa niaba ya Serikali ameihakikishia Msumbiji kuwa, Tanzania itaendelea kushirikiana na nchi hiyo  kwa hali na mali. 

Aidha, Mhe. Balozi ametoa pongezi kwa Mhe. Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Prof. Palamagamba John Kabudi, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki na wadau wengine kwa kufanikisha msaada huo.

Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali, 
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, 

Dodoma, Tarehe 24 Machi 2019

==============================================================================

....Picha zinazoonesha madhara yaliyotokana na Kimbunga...









Saturday, March 23, 2019

Waziri wa Mambo ya Nje azungumza na Watumishi wa Wizara

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Prof. Palamagamba John Kabudi akipokelewa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mahsariki, Dkt. Faraji Kasidi Mnyepe mara baada ya kuwasili kwenye eneo la Ukumbi wa Mikutano la Informatics lililopo Chuo Kikuu cha Dodoma kwa ajili ya kukutana kwa mara ya kwanza na Watumishi wa Wizara tarehe 23 Machi 2019
Mhe. Prof. Kabudi akizungumza na Watumishi wa Wizara (hawapo pichani) alipokutana nao kwa mara ya kwanza  baada ya kuteuliwa na Mhe. Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwenye nafasi hiyo tarehe 3 Machi 2019. Pamoja na mambo mengine, Mhe. Prof. Kabudi aliwataka Watumishi wa Wizara kubadilika na kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia sheria, kanuni, taratibu miongozo na maelekezo mbalimbali pamoja na kuwa wazalendo na kufanya kazi zao kwa kushirikiana na  kwa weledi ili kufikia malengo yaliyokusudiwa.


Sehemu ya Watumishi wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki wakimsikiliza Mhe. Prof. Kabudi ambaye haonekani pichani alipozungumza nao


Sehemu nyingine ya Watumishi wakifurahia jambo wakati wakimsikiliza Mhe. Prof. Kabudi (hayupo pichani)


Watumishi wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki wakiwa kwenye mkutano wao na Mhe. Waziri


Mkutano ukiendelea huku Watumishi wa Wizara wakifuatilia

Sehemu nyingine ya Watumishi


Mhe. Prof. Kabudi alitumia fursa ya mkutano wake na Watumishi wa Wizara kugawa Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2015 kwa Wakuu wa Idara na Vitengo wa Wizara na kuwaagiza kuitekeleza kwani ni miongoni mwa miongozo muhimu katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku. Pichani Mhe. Waziri akimkabidhi Mkurugenzi wa Ofisi ya Mambo ya Nje Zanzibar, Balozi Mohammed Hamza Ilani hiyo
Mhe. Waziri akimkabidhi Mkurugenzi wa Idara ya Siasa, Ulinzi na Usalama Ilani ya Chama cha Mapinduzi
Mhe. Prof. Kabudi akimkabidhi Ilani ya Chama cha Mapinduzi Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Sera na Mipango, Bw. Joachim Otaru
Mhe. Prof. Kabudi akimkabidhi Ilani ya Chama cha Mapinduzi, Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Afrika, Bw. Wilbroad Kayombo
Mkurugenzi wa Idara ya Siasa, Ulinzi na Usalama akitoa neno la shukrani kwa niaba ya Watumishi na kuahidi kutekeleza maelekezo yote yaliyotolewa na Mhe. Waziri
Mhe. Waziri (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na wajumbe wa meza kuu. Kulia kwake ni Katibu Mkuu, Dkt. Mnyepe na kushoto kwake ni Naibu Katibu Mkuu, Balozi Ramadhan Muombwa Mwinyi. Kushoto ni Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Utawala na Usimamizzi wa Rasilimali Watu, Bibi Savera Kazaura na kulia ni Bw. Hassan Mnondwa, Mwenyekiti wa TUGHE Wizarani .

Mhe. Prof. Kabudi akiwa katika picha ya pamoja na Wakuu wa Idara na Vitengo


Friday, March 22, 2019

Prof. Kabudi awasilisha taarifa ya utekelezaji wa bajeti ya Wizara kwa Kamati ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Prof. Palamagamba John Kabudi (Mb.) akiwasilisha Taarifa ya utekelezaji wa bajeti ya Wizara kwa mwaka wa fedha 2018/2019 na Taarifa kuhusu makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara kwa mwaka wa fedha 2019/2020 mbele ya Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama (NUU) (hawapo pichani) wakati wa kikao kati ya Kamati hiyo na Wizara kilichofanyika kwenye Ofisi za Bunge, Dodoma tarehe 22 Machi, 2019. Kulia ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dkt. Faraji Kasidi Mnyepe na kushoto ni Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki  Balozi Ramadhan M. Mwinyi.
Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama (NUU), Mhe. Mussa Azan Zungu akimsikiliza Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Prof. Palamagamba John Kabudi (Mb.) (hayupo pichani), wakati akiwasilisha taarifa kuhusu bajeti ya Wizara yake wakati wa kikao kati ya Kamati hiyo na Wizara kilichofanyika Ofisi za Bunge, Dodoma tarehe 22 Machi, 2019. Wakati wa kikao hicho, Mhe. Zungu alitumia fursa hiyo kwa niaba ya Kamati, kumpongeza Mhe. Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa hatua ya kupeleka haraka misaada ya chakula na dawa kwa nchi za Malawi, Msumbiji na Zimbabwe baada ya kupatwa na maafa  yaliyosababishwa na kimbunga kikali kilichozikumba nchi hizo.
Kikao kati ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama na Wizara ya mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kikiendelea
Sehemu ya Wabunge ambao ni Wajumbe wa Kamati hiyo wakifuatilia kikao
Sehemu ya Wakurugenzi kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki wakiwa kwenye kikao na Kamati ya Bunge ya NUU
Wajumbe wa Kamati wakimsikiliza Mhe. Waziri (hayupo pichani)
Wakuu wa Idara na Vitengo kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki wakifuatilia kikao
Mjumbe wa Kamati akichangia hoja wakati wa kikao hicho
Sehemu nyingine ya Wakuu wa Idara na Vitengo wa Wizara wakiwa kwenye kikao na Kamati ya Bunge ya NUU
Mjumbe wa Kamati akichangia jambo wakati wa kikao na Wizara
Mjumbe mwingine wa Kamati ya Bunge ya NUU akichangia hoja wakati wa kikao kati ya Kamati hiyo na Wizara
Mhe. Mbunge akichangia hoja 

Wakuu wa Vyombo vya usalama wajadili usalama wa bomba la mafuta

Juu na chini ni Mkutano wa Pamoja wa Uganda na Tanzania wa Wakuu wa vyombo vya Ulinzi na Usalama (wawakilishi wao) walipokutana hivi karibuni kuzungumzia mambo muhimu ya usalama wa Bomba la Mafuta kati ya Tanzania na Uganda.

Kamati Maalum wakiwa katika picha ya Pamoja. Ujumbe wa Tanzania uliongozwa na Mnadhimu Mkuu wa JWTZ, Luteni Jenerali Yacoub Mohamed na Ujumbe wa Uganda uliongozwa na Mnadhimu Mkuu wa UPDF Luteni Jenerali Joseph Musanyufu.


Thursday, March 21, 2019

Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Mambo ya Nje wa Qatar aitembelea Tanzania




Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Mambo ya Nje wa Qatar, Mhe. Mohammed Bin Abdulrahman Al-Thani, amewasili  nchini na kupokelewa na Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dkt. Faraji Kasidi Mnyepe, jana tarehe 20 Machi, 2019. Mhe. Al-Thani atakuwa nchini kwa siku moja ambapo atakutana na kufanya mazungumzo na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli, kabla ya kuondoka kuelekea Rwanda.


Sehemu ya ugeni huo ukiwasili.
Wajumbe wa msafara huo wakisalimiana na viongozi wa serikali waliofika katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere, kuwapokea akiwemo Balozi wa Tanzania nchini Qatar  Mhe. Fatma Mohammed Rajab na Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Mashariki ya Kati wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Ayoub Mndeme.

Mmoja kati ya maafisa wa msafara huo akisalimiana na afisa wa Ubalozi wa Qatar nchini.