Wednesday, May 13, 2020

MHE.PROF. PALAMAGAMBA KABUDI AWASILISHA BUNGENI MAKADIRIO YA MAPATO NA MATUMIZI YA WIZARA KWA MWAKA WA FEDHA 2020/2021

  
 Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Prof. Palamagamba John Kabudi awasilisha Bungeni Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara kwa mwaka wa Fedha 2020/2021. 

Wizara imeliomba Bunge liiidhinishie jumla ya Shilingi bilioni mia moja tisini na tisa, milioni mia saba hamsini, laki sita themanini na nne elfu (199,750,684,000) zikiwa ni fedha kwa ajili ya Matumizi ya Kawaida na  bajeti ya miradi ya maendeleo.
 

Akiwasilisha makadirio hayo, Mhe. Prof. Kabudi ameelezea mafaniko ambayo Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki imeyapata katika kipindi hiki cha kwanza cha Serikali ya Awamu ya Tano 2015-2020.
            Mafanikio hayo ni: 
 * Ufunguzi wa Balozi mpya nane katika nchi za Qatar; Uturuki; Sudan; Cuba; Israel; Algeria; Jamhuri ya Korea; na Namibia;  
* Kuifanya lugha ya Kiswahili kutumika katika Jumuiya ya Kimataifa na nchi mbalimbali;
* Kufanikisha kufanyika kwa viwango vya juu Mkutano wa 39 wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) uliofanyika Dar es Salaam mwezi Agosti 2019;
*Kuhamasisha watalii kuja nchini kutembelea vivutio mbalimbali vya utalii;
*Kufanikisha uenyekiti wa Tanzania katika Jumuiya ya Afrika Mashariki ambapo mwezi Machi 2016 nchi yetu iliteuliwa kwa mara ya pili mfululizo kuwa Mwenyekiti wa Jumuiya hiyo;
*Kuratibu Mkutano wa 18 wa Mawaziri wa Mambo ya Nje wa Afrika na Nordic (Africa - Nordic Foreign Ministers’ Meeting) uliofanyika kwa mafanikio makubwa mwezi Novemba 2019 jijini Dar es Salaam;
*Kufanikisha ujumuishwaji wa miradi ya Tanzania katika miradi ya kipaumbele ya miundombinu iliyoidhinishwa na Wakuu wa Nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki;
*Kutekeleza Itifaki ya Umoja wa Forodha na Itifaki ya Soko la Pamoja za Jumuiya ya Afrika Mashariki;
Mafanikio mengine ni pamoja na;
*Kuratibu upatikanaji wa mkopo wa masharti nafuu kutoka Benki ya Maendeleo Afrika (AfDB) wenye thamani ya Dola za Marekani Milioni 200 kwa ajili ya ujenzi wa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa Msalato jijini Dodoma na upatikanaji wa mkopo wenye masharti nafuu wenye thamani ya Dola za Marekani Milioni 180 kutoka Benki hiyo kwa ajili ya ujenzi wa barabara ya pete katika jiji la Dodoma na
* Kushawishi nchi marafiki kutufutia madeni, kuyapunguza au kuweka masharti nafuu ya kuyalipa.

   
  

HOTUBA YA BAJETI 2020/202

Saturday, May 9, 2020

SERIKALI: DAWA YA COVID 19 KUTOKA MADAGASCAR NI KWA AJILI YA UTAFITI KWANZA


Serikali kupitia Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, imesema kuwa dawa ambayo nchi ya Madagascar imeitoa kama msaada kwa Serikali ya Tanzania ni kwa ajili ya utafiti kwanza.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamagamba John Kabudi (Mb) amewaambia waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam kuwa dawa hiyo inayojulikana kaitaalamu kama "COVIDORGANICS" ni kwa ajili ya utafiti na siyo kwa ajili ya matumizi ya binadamu.

"Huu mzigo (dawa) ni kwaajili ya kufanyiwa utafiti…….na kazi kubwa tunayoianza leo ni na wataalamu wetu wa afya ni kufanya utafiti," Amesema Prof. Kabudi

Prof. Kabudi ameongeza kuwa dawa hiyo siyo kwa ajili ya kugawa kwa wananchi, bali ni kwa ajili ya utafiti na mara baada ya utafiti kukamilika wataalamu wa afya watatoa maelekezo ya jinsi ya utumiaji wa dawa hiyo.

Aidha, dawa hiyo imegawanyika katika makundi mawili ambapo kundi la kwanza la dawa ni kwa ajili ya kujikinga na maambukizi ya COVID 19 kwa wale ambao hawajaambukizwa ugonjwa wa Corona. Kundi la pili ni kwa ajili ya matibabu kwa wananchi ambao tayari wameathirika na COVID 19.

"Dawa hii tuliyokuja nayo jana kutoka Madagascar mara baada ya utafiti kukamilika na kupata ushauri wa kitaalamu kutoka kwa wataalamu wetu wa afya itatumika kukinga wananchi ambao hawajaathirika na kutibu wale walioathirika," Prof. Kabudi

Kwa upande wake Mganga Mkuu wa serikali Prof. Abel Makubi amesema kuwa mara baada ya kupokea dawa hiyo kazi ya kwanza ya ni kuanza utafiti ambao utaonesha kama dawa hiyo ni salama na haina madara kwa wananchi na pili utafiti wa kuangalia ubora wa kutibu au kupunguza makali ya COVID 19.

"Mara baada ya utafiti wa dawa hii kukamilika itatumika katika makundi matatu ambayo kundi la kwanza ni wagonjwa kutumia dawa ya kawaida, kundi la pili watapata dawa ya kawaida na hii iliyotoka Madagascar na kundi la tatu wagonjwa watatumia dawa ya kawaida na ile inayozalishwa na Taasisi ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu (Nimr)," Amesema Prof. Makubi

Prof. Makubi pamoja na mambo mengine, ametoa wito kwa watanzania kuchukua tahadhari katika kujikinga na ugonjwa wa COVID 19 na wasibweteke na lolote.
Nae Mkurugenzi wa Taasisi ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu (Nimr) Prof. Yunus Mgaya amesema kuwa Nimr imejipanga kushirikiana na taasisi nyingine za Serikali hasa Ofisi ya Mkemia Mkuu wa Serikali katika kuhakikisha inafanya utafiti wa kina juu ya matumizi ya dawa hiyo. 

"Nimr inafanya tafiti mbalimbali za kupambana na ugonjwa huu wa COVID 19 na itaendelea kufanya tafiti hizo ili kuwasaidia watanzania," amesema Prof. Mgaya

Kwa upande wake Mkemia Mkuu wa Serikali, Dkt. Fidelice Mafumiko amesema kuwa Ofisi ya Mkemia Mkuu inalo jukumu lakuchunguza dawa au sumu zozote kwenye sampuli, kukadiria kwa usahihi kiasi cha dawa, umetaboli au sumu.

Drkt. Mafumiko ameongeza kuwa, kupitia utafiti wa dawa hiyo, ofissi yake kwa kushirikiana na wataalamu wa afya watatafsiri matokeo ya uchunguzi katika dawa hiyo kutoa maelekezo sahihi juu ya matumizi yake kwa mwananchi.

Mkutano huu ulihudhuriwa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamagamba John Kabudi (Mb), Mganga Mkuu wa serikali Prof. Abel Makubi, Mkurugenzi wa Taasisi ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu (Nimr) Prof. Yunus Mgaya, Mkemia Mkuu wa Serikali, Dkt. Fidelice Mafumiko pamoja na Mkuu wa Kitengo cha Tiba za Asili Dkt. Paul Mkama.   


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamagamba John Kabudi (Mb) akiwaonesha waandishi wa habari (hawapo pichani) dawa ambayo imetolewa na Madagascar leo Jijini Dae es Salaam



Mganga Mkuu wa serikali Prof. Abel Makubi akiongea na waandishi wa habari (hawapo pichani) wakati wa mkutano uliofanyika leo Jijini Dae es Salaam



Mkurugenzi wa Taasisi ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu (NIMR) Prof. Yunus Mgaya akiongea na waandishi wa habari (hawapo pichani) wakati wa mkutano uliofanyika leo Jijini Dae es Salaam



Mkemia Mkuu wa Serikali, Dkt. Fidelice Mafumiko akiongea na waandishi wa habari (hawapo pichani) wakati wa mkutano  



Mkuu wa Kitengo cha Tiba za Asili Dkt. Paul Mkama akiongea na waandishi wa habari (hawapo pichani) wakati mkutano ukiendelea 




Wednesday, May 6, 2020

SERIKALI YAENDELEA KUSHUGHULIKIA CHANGAMOTO ZINAZOJITOKEZA MIPAKANI


 Serikali ya Tanzania kupitia Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki imesema changamoto zinazojitokeza katika mipaka mbalimbali ya Tanzania wakati wa usafirishaji wa bidhaa hususan katika kipindi hiki cha janga la COVID-19 zinaendelea kutatuliwa kwa majadiliano.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Kanali Wilbert Ibuge ameyasema hayo alipokutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa Tanzania Nchini Zambia Mhe. Benson Keith Chali ili kuangalia namna ya kutatua changamoto mbalimbali za usafirishaji wa bidhaa hususani zile zinazotoka katika bandari ya Dar es Salaam kuelekea katika nchi za Ukanda wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika SADC.

Ameongeza kuwa katika kipindi hiki cha janga la COVID – 19 unaosababishwa na virusi vya Corona changamoto mbalimbali zimejitokeza katika utoaji wa huduma za usafirishaji wa huduma na bidhaa mbalimbali na hivyo serikali inafanya jitihada za majadiliano na baadhi ya nchi katika mipaka ili kutatua changamoto zinazojitkeza na kuwezesha huduma ya usafirishaji kuendelea bila ya vikwazo.

Nae Balozi wa Zambia nchini Tanzania, Mhe. Chali amemuahidi Balozi Kanali Ibuge kuwa Serikali ya Zambia imeshaanza kuzifanyia kazi changamoto zinazojitokeza. "Suala hili limeshaanza kufanyiwa kazi na kila kitu kitakuwa sawa hivi karibuni," amesema Balozi, Chali.  

Katika tukio jingine Balozi Kanali Wilbert Ibuge amekutana na kufanya mazungumzo na Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) Bi. Christine Musisi ambapo katika mazungumzo hayo wameongelea zaidi namna ya kushirikiana na kuwezesha kujenga uwezo wa kuzalisha bidhaa mbalimbali kwa wawekezaji wadogo na wakati wa Tanzania na kuwa na ubia na wawekezaji wakubwa hususani katika kipindi hiki cha COVID – 19 na baada ya COVID – 19 ili kuunusuru uchumi wa Taifa kuanguka.

"Tumekubaliana kuongea ushirikiano katika sekta za afya, maji, maendeleo na uwekezaji …….kwa hili tunawashukuru sana UNDP kwa kazi wanayoifanya lakini pia hata katika ushirikiano wa kisera tumekuwa tukishirikiana nao jambo ambalo linazidi kuimarisha uhusiano wetu hasa katika wakati huu wa COVID - 19 kwani jambo hili linasaidia kunusuru uchumi wa taifa kuanguka," amesema Balozi, Kanali Ibuge. 

Katika hatua nyingine, Balozi Ibuge amekutana na kufanya mazungumzo kwa nyakati tofauti na Balozi wa Uingereza nchini Bi. Sarah Cooke pamoja na Mratibu Mkazi wa Shughuli za Umoja wa Mataifa (UN) nchini Tanzania Bw. Zlatan MiliÅ¡ić ambapo wamezungumzia masuala mbalimbali ya ushirikiano hususani katika kipindi hiki cha janga la COVID – 19.

Tarehe 6 Aprili, 2020 ulifanyika Mkutano wa Dharura wa Baraza la Mawaziri wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) ambapo pamoja na mambo mengine, mkutano huo ulijadili janga la COVID-19 unaosababishwa na virusi vya Corona. Mkutano huo ulihusisha Mawaziri wenye dhamana ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Fedha,Viwanda,Biashara, Utalii, Mambo ya Ndani na Uchukuzi, kutoka nchi 16 wanachama wa SADC.  

Katika mkutano huo, Baraza la Mawaziri lilitoa mwongozo kuhusu Usafirishaji wa Bidhaa Muhimu na Huduma katika Nchi za SADC katika kipindi hiki cha janga la Virusi vya Corona. Mwongozo huu unatumika katika kipindi hiki unalenga kupunguza safari zisizo za lazima na kuwezesa usafirishaji wa bidhaa muhimu wakati huu wa janga la COVID - 19.



  Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na UShirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Kanali Wilbert Ibuge akimueleza jambo Balozi wa Uingereza nchini Mhe. Sarah Cooke wakati walipokutana kwa mazungumzo leo jijini Dar es Salaam

Balozi wa Uingereza nchini Mhe. Sarah Cooke akiongea na Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na UShirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Kanali Wilbert Ibuge wakati walipokutana kwa mazungumzo leo jijini Dar es Salaam



Balozi wa Zambia nchini Mhe. Benson Keith Chali akiongea na Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na UShirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Kanali Wilbert Ibuge wakati walipokutana kwa mazungumzo leo jijini Dar es Salaam



Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na UShirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Kanali Wilbert Ibuge akiongea na Balozi wa Zambia nchini Mhe. Benson Keith Chali leo jijini Dar es Salaam



Mratibu Mkazi wa Shughuli za Umoja wa Mataifa (UN), Bw. Zlatan Milišić akimuelezea jambo Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na UShirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Kanali Wilbert Ibuge wakati walipokutana kwa mazungumzo leo jijini Dar es Salaam



Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na UShirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Kanali Wilbert Ibuge akiongea na Mratibu Mkazi wa Shughuli za Umoja wa Mataifa (UN), Bw. Zlatan Milišić wakati walipokutana kwa mazungumzo leo jijini Dar es Salaam



Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP), Bi. Christine Musisi akimuelezea jambo Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na UShirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Kanali Wilbert Ibuge wakati walipokutana kwa mazungumzo leo jijini Dar es Salaam




Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na UShirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Kanali Wilbert Ibuge akimfafanulia jambo Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP), Bi. Christine Musisi






Tuesday, April 28, 2020

TANZANIA NA KUWAIT ZAAHIDI KUIMARISHA USHIRIKIANO

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Damas Ndumbaro (Mb) akizungumza na Balozi wa Kuwait nchini, Mhe. Mubarak Mohammed Faleh Alsehaijan alipomtembelea katika ofisi za wizara Jijini Dodoma tarehe 28 Aprili 2020.

Mazungumzo yao yalijikita katika kujadili namna bora ya kuuenzi na kuimarisha ushirikiano wa kidiplomasia iliopo baina ya mataifa yao ili uweze kuleta tija na kuongeza maeneo mapya ya ushirikiano kwa manufaa ya wananchi wa Tanzania na Kuwait.

Vilevile wawili hao walipata fursa ya kujadili masuala mbalimbali ya utekelezezaji katika sekta ya afya, na utawala ambapo kwa pamoja wamekubaliana kufanya ufuatiliaji wa karibu ili kuhakikisha mambo yaliyokubaliwa kwa nyakati tofauti katika sekta hizo yanakamilika kwa wakati.

Tanzania na Kuwait zimekuwa na ushirikiano wa muda mrefu katika sekta ya kilimo, afya, biashara, maji, pamoja na ujenzi wa miundombinu wezeshe katika sekta hizo kwa lengo la kuhakikisha utekelezaji wa diplomasia ya uchumi unafikiwa kwa wakati. 

Balozi wa Kuwait nchini, Mhe. Mubarak Mohammed Faleh Alsehaijan akifafanua jambo kwa Naibu Waziri, Mhe. Dkt. Ndumbaro ambapo pamoja na mambo mengine walipata nafasi ya kushirikishana hatua mbalimbali zinazochukuliwa na mataifa yao katika kukabiliana na janga la ugonjwa wa Corona unaoikabili dunia kwa sasa.

Kutoka kushoto ni Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Mashariki ya Kati katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bw. Ayoub Mndeme na Msaidizi wa Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bw. Charles Faini wakifatilia mazungumzo.

Mazungumzo yakiendelea.


Thursday, April 23, 2020

MUONGOZO WA USAFIRISHAJI BIDHAA KATIKA NCHI ZA SADC

 MWONGOZO WA USAFIRISHAJI WA BIDHAA MUHIMU NA HUDUMA KATIKA NCHI ZA SADC KWA KIPINDI HIKI CHA JANGA LA VIRUSI  VYA CORONA (COVID – 19)

23 APRILI, 2020, DODOMA

Tarehe 6 Aprili, 2020 ulifanyika Mkutano wa Dharura wa Baraza la Mawaziri wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC). Mkutano huo ulijadili janga la mlipuko wa ugonjwa wa homa kali ya mapafu (COVID-19) unaosababishwa na virusi vya Corona. Mkutano huo ulihusisha Mawaziri wenye dhamana ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Fedha,Viwanda,Biashara, Utalii, Mambo ya Ndani na Uchukuzi, kutoka nchi 16 wanachama wa SADC ambazo ni Angola, Botswana, Malawi, Mauritius, Msumbiji, Namibia, Jamhuri ya Visiwa vya Ushelisheli, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo na Zambia.

Katika mkutano huo, Baraza la Mawaziri lilitoa mwongozo kuhusu Usafirishaji wa Bidhaa Muhimu na Huduma Katika Nchi za SADC katika kipindi hiki cha janga la Virusi vya Corona. Mwongozo huu utatumika katika kipindi hiki unalenga kupunguza safari zisizo za lazima na usafirishaji wa bidhaa ambazo ni za muhimu tu na unazitaka Nchi Wanachama kuzingatia na kutekeleza sera na miongozo mbalimbali iliyotolewa na inayoendelea kutolewa na Shirika la Afya Duniani (WHO), Shirika la Forodha Duniani (WCO), Shirika la Usafiri wa Anga Duniani (ICAO) na Shirika la Usafiri wa Maji Duniani (IMO).

Kwa mujibu wa Muongozo huo Malori na magari yatakayoruhusiwa kusafirisha mizigo ni yale yatakayobeba bidhaa za Vyakula; Vifaa tiba na Dawa, vifaa binafsi vya kujikinga; Mafuta na makaa ya mawe; Pembejeo za kilimo; vifungashio, vipuri vya magari na mashine. 

Raia wanaorejea katika nchi zao wanatakiwa kuzingatia sheria za nchi zilizowekwa za kupimwa na ikiwa atagundulika mgonjwa mwenye Virusi vya Corona, atatakiwa kutengwa kwa kuwekwa kizuizini kwa muda uliowekwa; Kupunguza idadi ya wasafiri katika mabasi na vyombo vingine vya usafiri; Kutumia miongozo ya WHO ya usafi katika vyombo vya usafiri, vituo vya mabasi na maeneo mengine ambayo mabasi yatasimama; Madereva/waendeshaji kutoa taarifa mbalimbali kuhusu njia za kupambana na COVID-19 kwa wasafiri katika lugha za wasafiri na; Kujaza fomu zinazohoji maeneo waliopita wasafiri na kuhakikisha fomu hizo zinawasilishwa kwa kituo cha maafisa afya.

Vyama vya wasafirishaji vinatakiwa Kushirikiana na maafisa afya kuandaa na kutekeleza programu ya uhamasishaji kwa wasafirishaji magari na waajiri wake;Kuwaelekeza madereva wa malori kujaza fomu maalum zinazoonyesha maeneo ambayo watapita, maeneo watakayosimama wakati wa safari na kituo cha mwisho cha safari ambazo zitawekwa katika ofisi za maafisa afya zilizopo mipakani ili kuweza kuwasiliana na kufuatilia madereva kwa uchunguzi;

Wasafirishaji magari wanatakiwa kushirikiana na Serikali kuangalia jinsi taarifa za gari zinavyoweza kutumika wakati wa kuifuatilia; Kuhakikisha madereva wanaovuka mipaka wanabeba sabuni na maji ya kunawa; Kuwaelekeza madereva kutobeba watu wasiohusika katika magari yao; Kuelekeza madereva wa malori kuzingatia umbali wa mita moja kati yao wakati wa safari; na; Kugawa vifaa maalum kwa wafanyakazi na waajiriwa ambao wapo katika mazingira hatarishi ya kupata maambukizi. 

Madereva wa malori watalazimika kuweka bayana kituo cha mwisho cha safari yao na wanaaswa kusimama katika vituo maalum vilivyopangwa na endapo dereva au wahudumu wa chombo husika wataonesha dalili za kuugua COVID-19 lori hilo litalazimika kupitia hatua za usafishaji kabla ya kuruhusiwa kuendelea na safari, watoa huduma wa chombo hicho watengwa katika eneo maalum (Quarantine) au kupelekwa kituo cha matibabu kwa gharama zao; Mmiliki wa lori atalazimika kuandaa dereva na watoa huduma wengine ili kuwezesha bidhaa kufika mahali zilipokusudiwa.

Dereva na wasaidizi wake wakishusha mzigo watapaswa kukaa watengwa katika eneo maalum ( Quarantine) kwa siku 14 na kutofanya safari nyingine ya nje katika kipindi hicho na wataalamu wa afya waliopo mpakani mwa nchi husika watalazimika kuwasiliana kwa kina na wataalamu wa afya wa nchi mwenyeji wa lori husika ili kupata taarifa zitakazo saidia kuchukua hatua ya kuwatenga katika eneo maalum dereva na wasaidizi wake wakati wa kushusha au kupakia mzigo.

Vyombo vya usafiri wa majini kutoka nchi ambazo zipo hatarini zaidi katika maambukizi au zenye wasaidizi au abiria waliopo kwenye hali hatarishi zaidi ya maambukizi watalazimika kutengwa katika eneo maalum kwa siku 14 kwa gharama zao kabla ya kuruhusiwa kutoka eneo ambalo chombo hicho kilitia nanga na chombo kilichobeba abiria na wasaidizi walioathirika na COVID-19 hakitaruhusiwa kutia nanga. 

Ndege zinazofanya safari katika maeneo mbalimbali zitalazimika kufuata hatua zote za usafishaji kwa kupuliziwa dawa na hatua zingine za kujikinga ambazo kila ndege iliyobeba abiria walioathirika au washukiwa wa COVID 19 inapaswa kuzipitia.

SADC ilikubaliana kuwa hakutakuwa na zuio dhidi ya wasafirishaji wa nje waliosajiliwa la kuingia nchi mwanachama endapo wanaendesha shughuli zao kwa kuzingatia taratibu, kanuni na sera za usalama za nchi husika. 


Imetolewa na:

 Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali 
WIZARA YA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI 


Wednesday, April 8, 2020

TAARIFA KWA UMMA



SADC YAAZIMIA USAFIRISHAJI WA BIDHAA MUHIMU KUDHIBITI COVID - 19


Mwenyekiti wa Baraza la Mawaziri wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini Mwa Afrika (SADC), ambaye pia  ni Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki wa Tanzania, Prof. Palamagamba John Kabudi Akizungumza katika Mkutano na waandishi wa habari (hawako pichani) kuhusu maazimio ya Mkutano wa dharura wa Jumuiya hiyo kuhusu Covid-19 kwa Nchi za SADC uliofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa Julius Nyerere Jijini Dar es Salaam, Tanzania
Mwenyekiti wa Mkutano wa Maafisa Waandamizi wa  Jumuiya ya Nchi za Kusini  Mwa Afrika(SADC)  ambaye pia  ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki wa Tanzania, Balozi Kanali.Wilbert Ibuge.


MAAZIMIO YA MKUTANO WA DHARURA KUHUSU COVID - 19 WA BARAZA LA MAWAZIRI WA JUMUIYA YA MAENDELEO KUSINI MWA AFRIKA (SADC)

Baraza la Mawaziri la Jumuiya ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC), limeridhia usafirishaji wa bidhaa muhimu katika ukanda  huo wakati wa janga la homa ya mapafu (Covid-19) ili kuzuia maambukizi ya ugonjwa huo kwa nchi wanachama.


Akizungumza katika Mkutano wa dharura wa SADC, kuhusu Covid-19,  uliofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa Julius Nyerere (JNICC), Mwenyekiti wa Baraza la Mawaziri wa SADC na Waziri wa Mambo ya Nje wa Tanzania, Prof.Palamagamba John  kabudi amesema Baraza limepitisha mapendekezo ya Mkutano wa Dharura wa Mawaziri wa Afya uliofanyika Machi 9, 2020, Dar es Salaam, Tanzania.

“Mkutano wa Dharura wa Mawaziri wa Afya wa tarehe 9, Machi 2020, ulitoa mapendekezo ambayo yamefanyiwa kazi na Mkutano wa Baraza la Mawaziri yakiwa ni   ufuatiliaji na utekelezaji masuala ya afya kuhusu mlipuko wa Covid-19, kujadili namna ya kujiandaa na kukabiliana na virusi vya Covid -19,kubaini wagonjwa na kufuatilia waliokutana nao na huduma za tiba katika ukanda wetu” Alisema Prof. Kabudi.

Ameongeza kuwa masuala mengine ni uchunguzi na upimaji wa kimaabara, uzuiaji na udhibiti wa maambukizi, uelimishaji wa madhara na ushirikishwaji wa jamii, uratibu wa kikanda wa kukabiliana na Covid-19, uwezeshaji na usafirishaji wa bidhaa muhimu katika ukanda huo wa SADC wakati huu wa Covid-19.

Mengine yaliyopitishwa ni Covid-19 na uwezeshaji wa biashara, Covid-19 na masuala ya udhibiti biashara na usimamizi wa majanga hatarishi katika ukanda huo wa Nchi za Kusini mwa Afrika, mapendekezo hayo yanatokana na ukweli kwamba  Covid-19 imeendelea kusambaa  duniani kwa hiyo Jumuiya imeona iweke mikakati madhubuti kukabiliana na ugonjwa huo.

“Mkutano huu wa Baraza la Mawaziri SADC uliitishwa kutokana na kuongezeka kwa kasi kwa maambukizi na vifo katika baadhi ya nchi Duniani, kwa mujibu wa taarifa namba 76 ya Shirika la Afya Duniani(WHO), ya April 5, 2020 inaeleza kuwa takribani watu 1,133,759 wameambukizwa ugonjwa huo na kati ya hao matukio mapya ni 82,061 na vifo 62,784 huku Afrika kwa nchi 51 kuna wagonjwa 9,198 na vifo viko chini ya watu 500, lakini kwa ukanda wetu wa SADC kuna matukio 2,127 katika nchi 14 huku vifo vikiwa 38” Alisema Prof.Kabudi.

Aidha, Prof. Kabudi ameeleza kuwa Mkutano wa Dharura wa Baraza la Mawaziri uliofanyika sambamba na Mkutano wa Maafisa Waandamizi wa SADC ulilenga katika kupokea taarifa ya wataalamu pamoja na muongozo wa urazinishaji (harmonization) na uwezeshaji usafirishaji wa bidhaa muhimu na huduma katika nchi za SADC wakati huu wa mlipuko wa Covid-19.

Bidhaa zilizopitishwa kwenye muongozo ni pamoja na usafirishaji wa vyakula, vifaa tiba, Dawa na vifaa vya kujinga na Corona, mafuta na mkaa wa mawe, pembejeo za kilimo na madawa, vifungashio, bidhaa zote zinazotumika katika utengenezaji, uchakataji na uhifadhi wa vyakula na vifaa ambavyo vinahusu usalama na dharura kwenye majanga mbalimbali.

Prof. Kabudi aliongeza kuwa SADC wamefanya hivyo ili kuzuia kuenea kwa Covid-19  na kuwezesha utekelezaji  mikakati ya kitaifa ya kupambana na ugonjwa huo na kuwezesha upatikana wa bidhaa muhimu ili kuzuia usafirishaji usio wa lazima kwa abiria katika ukanda huo wa Afrika .

MKUTAO WA DHARURA WA SADC KUHUSU COVID - 19 WAFANYIKA DAR ES SALAAM KWA NJIA YA MTANDAO

Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Kanali. Wilbert Ibuge akiendesha Mkutano wa dharura kwa njia ya video ambao unawahusisha Maafisa Waandamizi wa Nchi Wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC), kuhusu mwenendo ya mlipuko wa ugonjwa wa virusi vya Corona (Covid-19), mkutano ambao umefanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa Julius Nyerere Jijini Dar es Salaam, Tanzania.



 Makatibu Wakuu wa Wizara mbalimbali kutoka Tanzania wakifuatilia Mkutano wa dharura kwa njia ya video ambao unawahusisha Maafisa Waandamizi Nchi Wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC), kuhusu mwenendo ya mlipuko wa ugonjwa wa virusi vya Corona (Covid-19), mkutano ambao umefanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa Julius Nyerere Jijini Dar es Salaam, Tanzania.
Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Kanali. Wilbert Ibuge akiendesha Mkutano wa dharura kwa njia ya video ambao unawahusisha Maafisa Waandamizi Nchi Wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC), kuhusu mwenendo ya mlipuko wa ugonjwa wa virusi vya Corona (Covid-19), mkutano ambao umefanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa Julius Nyerere Jijini Dar es Salaam, Tanzania, wengine ni Makatibu Wakuu na Maafisa kutoka Wizara mbalimbali.


Mkutano wa dharura kwa njia ya video ambao unawahusisha Maafisa Waandamizi Nchi Wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC), kuhusu mwenendo ya mlipuko wa ugonjwa wa virusi vya Corona (Covid-19), ukiendelea katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa Julius Nyerere Jijini Dar es Salaam, Tanzania

Wednesday, April 1, 2020

KAMPUNI YA JAPAN YASAIDIA TAASISI YA MIFUPA (MOI) MSAADA WA VIFAA TIBA VYA MILIONI 80.9


Kampuni ya EAA Co. Ltd ya nchini Japan bandia imetoa msaada wa viungo bandia vyenye thamani ya Shilingi milioni 80.9 kwa Taasisi ya Tiba ya Mifupa (MOI) leo Jijini Dar es Salaam.

Akipokea msaada huo, Mkurugenzi wa Tiba (MOI) Dkt. Samwel Swai amesema kuwa msaada huo utasaidia kwa kiasi kikubwa matibabu ya wagonjwa wenye ulemavu wa miguu naa mikono. 

Kwa upande wake Meneja wa Kampuni ya EAA Co. Ltd, Josiah Benedict amesema wameguswa na changamoto zinazowakabili watanzania ndiyo maana wameamua kuunga mkono jitihada za Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Dkt John Pombe Magufuli ya kuboresha huduma za afya hapa nchini.

Msaada huo unatokana na juhudi za Ubalozi wa Tanzania Japan kwa kushirikiana na Watanzania waishio nchini Japan.


Mkurugenzi wa Tiba (MOI) Dkt. Samwel Swai (kulia) akipokea baadhi ya vifaa kutoka kwa Meneja wa Kampuni ya EAA, Josiah Benedict leo katika viwanja vya (MOI) jijini Dar es Salaam  

Mkurugenzi wa Tiba (MOI) Dkt. Samwel Swai (kulia) akipokea baadhi ya vifaa kutoka kwa Meneja wa Kampuni ya EAA Josiah Benedict leo katika viwanja vya (MOI) jijini Dar es Salaam  

Mkurugenzi wa Tiba (MOI) Dkt. Samwel Swai akiwa katika picha ya pamoja na Meneja wa Kampuni ya EAA, Josiah Benedict pamoja na baadhi ya wafanyakazi wengine waliohudhuria warsha ya makabidhiano leo katika viwanja vya (MOI) jijini Dar es Salaam