Wednesday, September 16, 2020

MAADHIMISHO YA TISA YA SIKU YA MARA YAFIKIA TAMATI WILAYANI BUTIAMA

Maadhimisho ya Tisa (9) ya Siku ya Mara (Mara Day) yaliyofanyika katika uwanja wa Maria Nyerere uliopo wilayani Butiama  Mkoa wa Mara yamehitimishwa tarehe 15 Septemba, 2020. Maadhimisho haya hufanyika kila mwaka, kwa mzunguko kati ya Tanzania na Kenya kwa lengo la kuhamasisha utunzaji na Ikolojia ya Bonde la Mto Mara kwa jamii inayolizunguka bonde hilo. Madhimisho ya Mwaka huu  yameongozwa na kauli mbiu "Ikolojia ya Mara iliyotunzwa - Ustawi wetu"

Kwa kutambua umuhimu na changamoto za Ikolojia ya Bonde la Mto Mara, Baraza la Kisekta la 10 la Mawaziri wa Bonde la Ziwa Victoria, lililofanyika Kigali, Rwanda mnamo Mei 4, 2012, liliazimia na kutangaza kuwa kila tarehe 15 Septemba kuwa "Siku ya Mara", kwa kuzingatia pia katika msimu huo kuna uhamaji mkubwa wa wanyamapori kutoka Hifadhi ya Serengeti ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwenda Pori la Akiba la Kitaifa la Maasai-Mara katika Jamhuri ya Kenya.

Kwa mujibu wa utaratibu uliowekwa na nchi hizi mbili Tanzania na Kenya maadhimisho ya 9 ya Mto Mara ya mwaka huu , yalipaswa kufanyika nchini Kenya, lakini kutokana na  changamoto ya Ugonjwa wa Homa Kali ya Mapafu (COVID-19) pande zote mbili zimekubaliana kufanya maadhimisho ya siku hiyo nchini mwao. 

Madhimisho ya mwaka huu yalienda sambamba na shughuli mbalimbali kama vile, semina ya masuala ya udongo na kilimo kwa wakazi wa mkoa wa Mara waliohudhuria katika uwanja wa Maria Nyerere, Butiama, maonesho ya bidhaa mbalimbali za wajasiliamali, maonesho ya mashamba darasa na kazi za sanaa na ubunifu. 

Akizungumza katika sherehe za maadhimisho hayo Mkuu wa Mkoa wa Mara Mhe. Adam Malima ambaye pia alikuwa  mgeni mashuhuri katika sehehe hizo amesema serikali inatambua umuhimu wa Bonde la Mto Mara katika Ustawi wa kijamii na kiuchumi kwa jamii ya pande zote mbili (Tanzania na Kenya) zinazolizunguka Bonde hilo. Sambamba na hilo Mhe. Malima amewahimiza wananchi kuendelea kutunza Ikolojia ya Bonde la Mto Mara kwa kufuata taratibu zilizowekwa na kushauriwa na Wataamu katika kundesha shughuli zao za kila siku kwenye mzingira yanayozunguka Bonde hilo.

Mwakilishi wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Bi. Judith Ngoda akizungumza na wananchi kwenye sherehe za madadhimisho hayo amepongeza utayari    na ushiriki wa hali ya juu wa wananchi katika kulitunza Bonde la Mto Mara na kuongeza kuwa juhudi, nguvu na umoja unaoonyeshwa na Serikali za nchi zote mbili za Tanzania na Kenya unadhihirisha ushirikiano na mshikamano uliopo katika kuhakikisha ustawi wa uchumi kwa jamii inayozunguka Bonde la Mto Mara unakuwa endelevu kupitia mazingira. 

Sherehe za Siku ya Mara zinaongozwa na malengo matatu yafuatayo: kujenga uelewa kwa wadau muhimu kuhusu umuhimu wa Bonde la Mto Mara na rasilimali zake; kutambua na kuhusisha mchango wa watendaji mbalimbali wa umma na binafsi katika usimamizi wa Rasilimali za Mto Mara, na kukuza ushirikiano wa umma na binafsi kama njia ya kuelekea katika usimamizi endelevu wa Maji ya Mto Mara na bionuwai.

   Moja Banda la Wadau walioshiriki katika maonesho ya Maadhimisho ya Tisa (9) ya Siku ya Mara yaliofanyika katika viwanja vya Maria Nyerere, wilayani Butiama Mkoa wa Mara tarehe 12 -15 Septemba, 2020. 

    Baadhi ya Wananchi wa kutoka sehemu mbalimbali za Mkoa wa Mara wakisikiliza mada kwenye moja ya Semina iliyokuwa ikitolewa kwenye Maadhimisho ya Siku ya Mara yaliofanyika katika viwanja vya Maria Nyerere, Wilayani Butiama Mkoa wa Mara tarehe 12 -15 Septemba, 2020. 

Sehemu ya wananchi waliojitokeza katika viwanja vya Maria Nyerere, wilayani Butiama kwenye sherehe za maadhimisho ya 9 ya Siku ya Mara wakifuatilia burudani iliyokuwa ikiendelea uwanjani hapo. 

    Sehemu ya wananchi waliojitokeza katika viwanja vya Maria                                                                                            Nyerere, wilayani Butiama kwenye sherehe za maadhimisho ya    9 ya Siku ya Mara wakifuatilia hotubani iliyokuwa ikitolea   uwanjani hapo. 

    Mkuu wa Mkoa wa Mara Mhe. Adam Malima na Mgeni Rasmi                 wa sherehe za maadhimisho ya 9 ya Siku ya Mara akiongea na moja kati ya wadau walioshiriki katika maonesho yaliyofanyika katika viwanja vya Maria Nyerere, wilayani Butiama Mkoa wa Mara 


    Mkuu wa Mkoa wa Mara Mhe. Adam Malima na Mgeni Rasmi                                 
wa sherehe za maadhimisho ya 9 ya Siku ya Mara akisaini kitabu cha Wageni mara baada ya kuwasili katika viwanja vya Maria Nyerere, wilayani Butiama, Mkoa wa Mara                                                                              

   Wawakilishi wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Bw. Mgeta Sabe na Bi. Judith Ngoda wakifuatulia jambo wakati wa sherehe za maadhimisho ya 9 ya Siku ya Mara 

Bi. Judith Ngoda mwakilishi wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki  akitoa salam za Wizara kwa  Viongozi na Wananchi waliojitokeza kwenye Sherehe za Maadhimisho ya 9 ya Siku ya Mara.

Tuesday, September 15, 2020

NCHI 15 ZARUHUSIWA KULETA WAANGALIZI WA UCHAGUZI MKUU 2020

 Nchi 15 kupitia Balozi zao hapa nchini zimeruhusiwa kuleta waangalizi wa Kimataifa katika uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika mwezi Octoba, 2020 baada ya Balozi hizo kuwasilisha maombi na kufuata taratibu.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamagamba John Kabudi ameyasema hayo leo Jijini Dar es Salaam alipokutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa Umoja wa Ulaya Balozi Manfred Fanti na kuongeza kuwa uchaguzi wa mwaka huu kwa mara ya kwanza umekuwa tofauti na miaka iliyopita kwa kuwa unafanyika kwa kugharamiwa na fedha za ndani badala ya wahisani jambo ambalo baadhi ya watu walianza kuhofia kutokuwepo kwa waangalizi wa kimataifa katika uchaguzi.

"Huu ni uchaguzi mkuu ambao kwa mara ya kwanza kwa asilimia 100 tunaugharamia sisi wenyewe kama Serikali ya Tanzania, utaratibu wa uchaguzi chini ya sheria ya uchaguzi na chini ya utaratibu wa Kimataifa huwa tunakuwa na waangalizi wa uchaguzi na mwaka huu nchi hizo 15 kupitia balozi zao zimepata  kibali mara baada ya kufuata taratibu za kuomba kuleta waangalizi wa uchaguzi mkuu," Amesema Prof. Kabudi 

Mbali na Balozi wa Umoja wa Ulaya pia Prof. Kabudi amekutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa Italia hapa nchini Balozi Roberto Mengoni na baadae Balozi wa Poland Balozi Krzysztof Buzalski ambapo amewakabidhi vitabu vya sheria ya uchaguzi na kanuni za uchaguzi na miongozo mbalimbali inayohusu masuala ya uchaguzi ili kuwapa fursa ya kufahamu namna uchaguzi unavyoendeshwa hapa nchini hasusani baada ya uwepo wa malalamiko kutoka kwa baadhi ya vyama vya upinzani juu ya kuenguliwa kwa wagombea wao. 

Kwa upande wake Balozi wa Umoja wa Ulaya hapa nchini Balozi Manfred Fanti amesema Nchi za Umoja huo zimekuwa zikifuatilia kwa karibu mchakato wa kampeni za uchaguzi mkuu zinavyoendelea hapa nchini ambapo mpaka sasa wanaridhishwa na kampeni zinavyofanyika kwa uhuru na amani na sasa wanajiandaa na zoezi la uangalizi wa uchaguzi huo. 

Balozi wa Italia hapa nchini Mhe. Roberto Mengoni amesema amevutiwa na namna vyombo vya habari vimekuwa vikitoa nafasi kwa wagombea wote kwa uhuru na bila ya ubaguzi na kupongeza namna Watanzania wanavyojitokeza kwa wingi kusikiliza sera za wagombea mbali na tishio la corona na kwamba ana imani kuwa Kiongozi atakayechaguliwa atakuwa ametokana na utashi wa wananchi.

Mbali na masuala ya uchaguzi mkuu, Waziri Kabudi na Mabalozi hao wamejadili pia masuala ya kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia,maendeleo ya kiuchumi,biashara na uwekezaji katika sekta mbalimbali ikiwemo elimu,afya,maji na miundombinu.

Balozi wa Umoja wa Ulaya Balozi Manfred Fanti akimuelezea jambo Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Prof. Palamagamba John Kabudi walipokutana kwa mazungumzo leo jijini Dar es Salaam 


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Prof.   Kabudi akimkabidhi Balozi wa Italia nchini Balozi Roberto Mengoni vitabu vya sheria ya uchaguzi na kanuni za uchaguzi na miongozo mbalimbali inayohusu masuala ya uchaguzi      


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Prof. Palamagamba John Kabudi akimfafanulia jambo Balozi wa Poland hapa nchini, Balozi Krzysztof 




 

Monday, September 14, 2020

UMOJA WA ULAYA KUTOA BILIONI 70 KUSAIDIA MAPAMBANO YA COVID 19 -TANZANIA

 



Balozi wa Tanzania nchini Ubelgiji na mwakilishi wa Tanzania katika Umoja wa Ulaya Mhe. Jestas Abuok Nyamanga pichani kulia akisisitiza vipaumbele vya Tanzania na zile za nchi za OACPS kwa Rais wa Baraza la Umoja wa Ulaya Mhe. Charles Michel kushoto. Kulia mwa Balozi ni afisa Mwandamizi wa ubalozi Dkt Geofrey Kabakaki na Kushoto mwa Rais Michel ni Afisa wa EU anayeshughulikia masuala ya Tanzania kutoka makao makuu ya Umoja huo Bibi Christina Barrios.


Mhe. Balozi Jestas Nyamanga kuliaa akiwasilisha hati za utambulisho kwa Mkuu wa Itifaki wa Ofisi ya Rais wa Baraza la Umoja wa Ulaya


Thursday, September 10, 2020

Nchi za Ulaya Zahimizwa Kuondoa Vizuizi vya Kusafiri

Jumuiya ya nchi za Afrika, Carribean na Pacific (OACPS) imetoa wito kwa Umoja wa Ulaya kuondoa vizuizi vya kusafiri (travel bans) kwa baadhi ya nchi za OACPS hususan zile zilizoonesha kuwa salama zaidi dhidi ya maambukizi ya Ugonjwa wa Corona kama Tanzania. Wito huo ulitolewa katika kikao maalum cha mashauriano baina ya Jumuiya ya nchi za OACPS na nchi ya Ujerumani ambayo kwa sasa ni Rais wa Baraza la Umoja wa Ulaya.

Mashauriano hayo yaliyofanyika tarehe 9 Septemba 2020 katika Ofisi za Jumuiya ya OACPS, Brussels nchini Ubelgiji, yaliongozwa na Balozi wa Tanzania nchini Ubelgiji na Mwakilishi wa Tanzania katika Umoja wa Ulaya ambaye pia ni Mwenyekiti wa Mabalozi wa nchi za OACPS walioko Brussels, Mhe. Jestas Abuok Nyamanga na ujumbe wa Ujerumani uliongozwa na Waziri wa Masuala ya Ushirikiano wa Uchumi na Maendeleo wa Serikali ya Shirikisho la Ujerumani, Dkt. Gerd MÙLLER.

Katika kikao hicho wajumbe walisisitiza umuhimu wa Umoja wa Ulaya kuendelea kuunga mkono Shirika la Afya Duniani (WHO) katika kusimamia ithibati za tafiti za chanjo za ugonjwa wa Corona na Shirika hilo kuendelea kujengewa uwezo wa kusimamia utaratibu wa kuhakikisha kuwa chanjo itakayothibitika inawafikia mataifa yote kwa usawa na kwa gharama nafuu.

Kikao hicho kilijadili pia hatua mbalimbali zinazopaswa kuongeza msukumo kwa Umoja wa Ulaya katika kuzisaidia nchi za OACPS kukabiliana na athari za kiuchumi zinazotokana na ugonjwa wa Corona hususan katika sekta ya utalii na kilimo. Mikakati iliyojadiliwa ni pamoja na ile inayolenga kupunguza, kufuta au kubadilisha masharti ya ulipaji wa madeni ya nchi za Jumuiya ya OACPS na wito wa nchi za OACPS kuutaka Umoja wa Ulaya kusogeza mbele utekelezaji wa baadhi ya kanuni na taratibu mpya za biashara zilizopangwa kuanza kutumika mwanzoni mwa mwaka ujao ili kuzipa nafasi nchi za OACPS kujipanga zaidi kabla ya kuanza kutumia kanuni hizo.

Kupitia mashauriano hayo, pande zote mbili zilitathmini mwenendo wa majadiliano ya Mkataba mpya wa ubia wa Ushirikiano wa Kiuchumi baina ya nchi za Jumuiya ya OACPS na Umoja wa Ulaya yanayoendelea hivi sasa baada ya mkataba wa sasa kufikia kikomo mwezi Desemba 2020. Pande mbili zilijadili kwa kina namna ya kushirikiana katika maeneo yanayolenga kuongeza mnyororo wa thamani ya mazao ya kilimo, uwiano ulio sawa katika biashara na maendeleo ya teknolojia katika kukuza uchumi na maendeleo ya watu.

Kikao kilihitimishwa kwa Ujerumani kuonesha utayari wa kuyapa kipaumbele masuala yote yaliyojadiliwa katika kipindi cha uongozi wake wa Baraza la Umoja wa Ulaya na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki katika kipindi hiki ambacho inashika nafasi ya Rais wa Baraza la Mawaziri wa nchi 79 wanachama wa Jumuiya ya nchi za Afrika, Carribean na Pacific itaendelea kushirikiana na Umoja wa Ulaya na kufanya kazi kwa karibu na uongozi wa Ujerumani kwenye Baraza la Umoja huo wa Ulaya kusukuma ajenda zenye manufaa na maslahi kwa pande zote mbili. 

Balozi wa Tanzania nchini Ubelgiji, Mhe. Jestas Nyamanga akiongoza Mkutano maalum wa mashauriano  kati ya Jumuiya ya nchi za Afrika, Carribean na Pacific (OACPS) na ujumbe waUjerumani uliokuwa ukingozwa na Waziri wa Masuala ya Ushirikiano wa Uchumi na Maendeleo wa Serikali ya Shirikisho la Ujerumani, Dkt. Gerd MÙLLER ambayo kwa sasa nchi hiyo ni Rais wa Baraza la Umoja wa Ulaya

 Balozi wa Tanzania nchini Ubelgiji, Mhe. Jestas Nyamanga akiongoza Mkutano maalum wa mashauriano  kati ya Jumuiya ya nchi za Afrika, Carribean na Pacific (OACPS) na ujumbe wa Ujerumani uliokuwa ukingozwa na Waziri wa Masuala ya Ushirikiano wa Uchumi na Maendeleo wa Serikali ya Shirikisho la Ujerumani, Dkt. Gerd MÙLLER ambayo kwa sasa nchi hiyo ni Rais wa Baraza la Umoja wa Ulaya.



Mhe.Balozi Nyamanga kwa nafasi yake ya Mwenyeki wa Mabalozi wa OACPS akimtambulisha Waziri wa Ushirikiano wa Ujerumani Mhe. Dkt. Muller na timu yake katika Ukumbi wa OACPS.


Mhe. Balozi Nyamanga akimsindikiza Mgeni wake Mhe. Dkt.Muller nje ya ukumbi wa mkutano baada ya mkutano wa mashauriano kukamilika.

 




 

Tuesday, September 8, 2020

MAREKANI YAWATAKA WATANZANIA KUSHIRIKI UCHAGUZI, KUMCHAGUA KIONGOZI BORA

 Balozi wa Marekani hapa nchini Mhe. Dkt. Donald Wright amewataka Watanzania kushiriki kikamilifu katika uchaguzi mkuu utakaofanyika Octoba mwaka huu ili kumchagua kiongozi bora atakayeweza kutekeleza malengo yao kimaendeleo.

Dkt. Wright amesema hayo wakati alipokutana na kufanya mazungumzo na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Prof. Palamagamba John Kabudi leo jijini Dar es Salaam ambapo wamejadili masuala ya ushirikiano wa maendeleo baina ya Tanzania na Marekani pamoja na kugusia harakati za kampeni za uchaguzi mkuu unaoendelea hapa Nchini.

Katika mazungumzo hayo Prof. Kabudi akiwa ameambatana na Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Brigedia Jenerali Wilbert Ibuge amemhakikishia Balozi wa Marekani Dkt. Wright kuwa Tanzania ni sehemu salama ya kuwekeza hususani katika sekta za utalii,kilimo,na biashara na kumhakikishia kuwa uchaguzi mkuu wa mwaka huu utakuwa huru,haki na wa amani.

Prof. Kabudi ameongeza kuwa katika sekta ya utalii serikali ya awamu ya tano imedhibiti kwa kiasi kikubwa uwindaji haramu ikiwa ni pamoja na kupambana na ujangili jambo ambalo limeiwezesha serikali kuanzisha hifadhi za Taifa mpya nane ikiwa ni pamoja na kuimarisha hatua za usalama kwa watalii baada ya janga la corona kumalizika nchini.

Kwa upande wake Balozi wa Marekani hapa nchini Dkt. Donald Wright amemhakikishia Waziri kabudi kuwa atahamasisha wafanyabiashara na wawekezaji kuja nchini kuwekeza katika sekta za kilimo, biashara, huduma za afya na viwanda pamoja na kuhamasisha watalii kutoka marekani kuja nchini.

"Natumia fursa hii kuwasihi Watanzania kushiriki kikamilifu katika uchaguzi mkuu utakaofanyika Octoba mwaka huu ili kumchagua kiongozi bora atakayeweza kutekeleza malengo yao kimaendeleo," Amesema Dkt. Wright.

Balozi wa Marekani hapa nchini Mhe. Dkt. Donald Wright akimuelezea jambo Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Prof. Palamagamba John Kabudi walipokutana kwa mazungumzo leo jijini Dar es Salaam 

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Prof. Kabudi akimkabidhi Balozi wa Marekani hapa nchini Mhe. Dkt. Donald Wright moja ya nakala ya kitabu kinachoelezea masuala ya uchaguzi mkuu nchini Tanzania

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Prof. Kabudi akimkabidhi zawadi ya picha Balozi wa Marekani hapa nchini Mhe. Dkt. Donald Wright. Kulia mwa Waziri ni Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi, Brigedia Jenerali Wilbert Ibuge.

Monday, September 7, 2020

BALOZI IBUGE AKUTANA NA BALOZI WA CHINA NCHINI

Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Brigedia Jenerali Wilbert Ibuge amekutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa China nchini Mhe. Wang Ke ofisini kwake jijini Dodoma.

Katika kikao hicho Katibu Mkuu, Balozi Ibuge na Balozi Wang Ke pamoja na mambo mengine wameongelea juu ya mapendekezo ya mabadiliko ya Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa kuhusu nafasi za uwakilishi wa kudumu kwa Bara la Afrika..

katika Kikao hicho Balozi Ibuge amesisitiza msimamo wa Tanzania kuunga mkono nia ya Bara la Afrika kuwa na nafasi mbili za uwakilishi wa kudumu katika Baraza hilo. Nchi za Afrika zinataka uwakilishi huo uwe na nguvu ikiwa ni pamoja na kupata nafasi moja ya kura ya Veto kama walivyokubaliana katika mkutano wa Ezulwini  na Azimio la Sirte la mwaka 1999. 

Balozi Ibuge pia amezungumzia kuhusu utekelezzaji wa mambo maalum ambayo yamo katika Hotuba ya Mhe. Rais Dkt. John Pombe Magufuli  aliyoitoa wakati wa kuzindua Bunge la 12. tarehe 13 Novemba 2020 jijini Dodoma, ambapo amemuomba Balozi Wang Ke kufikisha mambo yaliyomo katika hotuba hiyo kwa wawekezaji wa China ili kuwekeza nchini.

Balozi Ibuge amesema maono ya Mhe. Rais aliyoyasema katika hotuba yake ni utekelezaji wa moja ya kauli iliyowahi kutolewa na Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere kuwa "wakati wengine wanatembea Watanzania tunatakiwa tukimbie." ili kufikia maendeleo kwa haraka. 

Kwa Upande wake Balozi Wang Ke amemuhakikishia Balozi Ibuge, kwamba China iko pamoja na Bara la Afrika na kwamba wanaunga mkono  mapendekezo ya Bara la Afrika ya kuwa nafasi mbili za kudumu katika Baraza hilo.

Balozi Wang Ke ameelezea kufurahishwa na maono ya Mhe. Rais yaliyobainishwa katika Hotuba hiyo na kuahidi kuendelea kuisaidia Tanzania ili kufakisha maono hayo kwa vitendo na kuwaletea wananchi wa Tanzania maendeleo. 

Viongozi hao pia wamejadiliana na kubaliana kuendelea kuimarisha ushirikiano wa kimkakati na kindugu baina ya Tanzania na China kwa faida ya pande zote mbili.

Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi, Brigedia Jenerali Wilbert Ibuge akimkaribisha Balozi wa China nchini Mhe. Wang Ke alipokutana naye ofisini kwake jijini Dodoma.



Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi, Brigedia Jenerali Wilbert Ibuge akizungumza na Balozi wa China nchini Mhe. Wang Ke walipokutana ofisini kwake jijini Dodoma.


Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi, Brigedia Jenerali Wilbert Ibuge akisisitiza jambo wakati wa mazungumzo hayo walipokutana ofisini kwake jijini Dodoma.


Balozi Wang Ke akizungumza katika kikao hicho 






PROF. KABUDI AMUAGA BALOZI WA IRAN NCHINI TANZANIA

 Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamagamba John Kabudi amemuaga Balozi wa Iran nchini, Mhe. Mousa Ahmed Farhang ambaye amemaliza muda wake wa uwakilishi nchini.

Akiongea katika hafla ya kumuaga balozi wa Iran iliyofanyika leo jijini Dar es Salaam, Prof. Kabudi amempongeza Balozi Farhang kwa kazi nzuri aliyoifanya ya kudumisha uhusiano wa kidiplomasia kati ya nchi yake na Tanzania.

Pamoja na mambo mengine, Prof. Kabudi amemuahidi Balozi Farhang kuwa Tanzania itaendelea kushirikiana na Iran katika sekta za elimu, afya na utalii kwa maslahi mapana ya nchi zote mbili.

"Kwa niaba ya Serikali ya Tanzania nakuahidi ushirikiano kutoka kwetu, nakutakia kila la kheri katika maisha yako nje ya Tanzania na ni imani yangu kuwa utakuwa balozi mzuri wa Tanzania duniani," Amesema Prof. Kabudi

Kwa upande wake Balozi Farhang ameishukuru Serikali ya Tanzania kwa kumpa ushirikiano wa kutosha wakati wa kipindi chake cha uwakilishi hapa nchini.

Balozi Farhang ameelezea kufurahishwa na uhusiano mzuri uliopo baina ya Iran na Tanzania na amepongeza hatua mbalimbali ambazo Serikali ya Tanzania imeendelea kuzichukua katika kuimarisha diplomasia ya uchumi.

Balozi wa Iran Mhe. Mousa Ahmed Farhang akiongea na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamagamba John Kabudi wakati alipokuwa anamuaga baada ya kumaliza muda wa uwakilishi nchini 

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamagamba John Kabudi akimuelezea jambo Balozi wa Iran aliyemaliza muda wake wa uwakilishi nchini, Mhe. Mousa Ahmed Farhang  

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamagamba John Kabudi akimkabidhi zawadi ya picha ya Mlima Kilimanjaro, Balozi wa Iran aliyemaliza muda wake wa uwakilishi nchini, Mhe. Mousa Ahmed Farhang

Saturday, September 5, 2020

PROF. KABUDI, BALOZI IBUGE WASAINI KITABU CHA MAOMBOLEZO KUFUTIA KIFO CHA RAIS WA ZAMANI WA INDIA

 Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamagamba John Kabudi na Katibu Mkuu wa wizara hiyo Balozi Brigedia Jenerali Wilbert Ibuge wamesaini kitabu cha maombolezo Ubalozi wa India nchini kufuatia kifo cha Rais mstaafu wa Taifa hilo Shri Pranab Mukherjee kilichotokea tarehe 31 Agosti 2020.

 Akizungumza mara baada ya kusaini kitabu cha maombolezo katika ubalozi ubalozi wa India nchini, Jijini Dar es Salaam Prof. Kabudi ametoa pole kwa wananchi wote wa India na kuwasihi kuendelea kuwa watulivu na wastahimilivu wakati huu wa msiba wa kiongozi wao mstaafu.

 "Kusaini kitabu cha maombolezo ni ishara ya ushirikiano wetu, umoja wetu na undugu wetu na ndugu zetu wa India. Kifo cha Rais Shri Pranab Mukherjee kinawahusu pia watanzania kwa sababu Tanzania na India zina uhusiano mzuri, imara na wa muda mrefu ulianzishwa na baba wa Taifa Mwl. Julias Nyerere pamoja na Mahatma Gandhi,” amesema Prof. Kabudi

 Rais Shri Pranab Mukherjee ni miongoni mwa viongozi wa zamani wa India waliowahi kufanya kazi katika Serikali ya Waziri Mkuu wa Zamani Indira Gandhi aliyewahi kukabidhiwa nyadhifa mbali mbali ikiwemo Waziri katika Sekta tofauti.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamagamba John Kabudi akisaini kitabu cha maombolezo katika ubalozi wa India nchini Tanzani. Pembeni yake kulia ni Balozi wa India nchini Mhe. Shri Sanjiv Kohli  


Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Brigedia Jenerali Wilbert Ibuge akisaini kitabu cha maombolezo katika ubalozi wa India nchini Tanzania

 

Friday, September 4, 2020

TZ YAIHAKIKISHIA UINGEREZA NA JUMUIYA YA KIMATAIFA UCHAGUZI HURU, HAKI

Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki imeihakikishia Uingereza pamoja na Jumuiya ya Kimataifa kuwa uchaguzi mkuu unaotegemewa kufanyika mwezi Oktoba mwaka 2020 utafanyika kwa amani, uhuru na haki.

Kauli hiyo imetolewa leo jijini Dar es Salaam na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamagamba John Kabudi wakati akipokea nakala za hati za utambulisho za Balozi mteule wa Uingereza hapa nchini Mhe. David Concar   

Prof Kabudi amesema kuwa paamoja na mambo mengine, amemhakikishia balozi mteule wa Uingereza nchini Mhe. Concar kuwa mchakato wa uchaguzi nchini unaendelea vizuri sana ambapo mikutano ya kampeni imeanza kwa ngazi zote (ngazi ya uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani) na mpaka sasa kampeni zinaendea vizuri.

"kama ilivyoada ya watanzania nimemhakikishia kuwa uchaguzi huu utafanyika kwa amani na utulivu na mwisho wa siku maamuzi yatakayotolewa na watanzania ya kuamua nani awe diwani, nani awe mbunge na nani awe Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania yataheshimiwa na watanzania wote," Amesema Prof. Kabudi.

Kwa upande wake Balozi mteule Mhe.David Concar amesema kuwa katika maongezi yao mbali na kugusia suala la uchaguzi pia wameongelea namna ya kuimarisha mahusiano baina ya Tanzania na Uingereza na mazingira bora ya kuvutia zaidi wawekezaji kuja nchini,kukuza biashara hususani baada ya Uingereza kujitoa katika jumuiya ya Umoja wa Ulaya na pia kusaidia maendeleo katika maeneo ya afya,maji pamoja na elimu.

Katika hatua nyingine Prof. Kabudi amepokea nakala za hati za utambulisho za Balozi Mteule wa Pakistan hapa Nchini Mhe. Mohamed Saleem.

Katika mazungumzo hayo Prof. Kabudi amesema kutokana na Pakistan kupiga hatua kubwa ya kimaendeleo katika viwanda vya mbolea wamekubaliana kuangalia namna ya kushirikiana ili kujenga viwanda vingi vya mbolea hapa nchini pamoja na kufanya biashara ya moja kwa moja ya zao la chai badala ya kupitia katika masoko ya minada ya Afrika Mashariki.

Kwa upande wake Balozi wa Pakistan nchini, Mhe. Mohhamed Salim amesema atahakikisha kuwa Tanzania na Pakistan zinaendelea kuimarisha diplomasia ya uchumi kwa kuwawezesha wafanyabiashara na wawekezaji kutoka nchi zote mbili ili kuweza kunufaika na furza za kukuza uchumi.

Hafla ya mabalozi wateule kukabidhi hati za utambulisho pia ilihudhuriwa na Katibu Mkuu, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Brigedia Jenerali, Wilbert Ibuge.  

Balozi mteule wa Uingereza nchini Mhe. David Concar akiongea na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamagamba John Kabudi leo jijini Dar es Salaam

Balozi mteule wa Uingereza nchini Mhe. David Concar akimkabidhi nakala ya hati za utambulisho Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamagamba John Kabudi 


Balozi mteule wa Pakistan nchini, Mhe. Mohhamed Salim akimuelezea jambo Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamagamba John Kabudi  


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamagamba John Kabudi akipokea nakala ya hati za utambulisho kutoka kwa Balozi mteule wa Pakistan nchini, Mhe. Mohhamed Salim 



Katibu Mkuu, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Brigedia Jenerali, Wilbert Ibuge (kulia) akifuatilia maongeza mara baada ya Mabalozi wateue kuwasilisha hati za utambulisho kwa Waziri Prof. Kabudi  

Naibu Katibu Mkuu aongoza Ujumbe wa Tanzania kwenye majadiliano ya biashara baina ya EAC na Uingereza

Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Dkt. Mwinyi Talib Haji akifuatilia kikao cha  kuajadili namna bora ya kuendelea na majadiliao ya biashara baina ya Afrika Mashariki na Uingereza kilichokuwa kikiendelea kwa njia ya mtandao (Video Conference).

Dkt. Haji ameongoza ujumbe wa Tanzania kwenye kikoa cha Kanda cha Makatibu Wakuu wa Jamuiya ya Afrika Mashariki kujadili namna bora ya kuendelea na majadiliano ya biashara baina ya Jumuiya ya Afrika Mashariki na Uingereza.

Lengo la majadiliano baina ya Afrika Mashariki na Uingereza ni kuwa na Mkataba wa Biashara utakaowezesha Nchi Wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki kuuza bidhaa kwenye Soko la Uingereza na Uingereza kwenye Soko la Jumuiya ya Afrika Mashariki kuanzia tarehe 01 Januari, 2021.

Jumuiya ya Afrika Mashariki kwa muda mrefu imekuwa mshirika mzuri wa biashara kwa nchi ya Uingereza. Hata biashara hiyo biashara hiyo awali imekuwa ikifanyika kwa kufuata sheria, miongozo na taratibu za Umoja wa Ulaya. Kufauatia hatua ya Uingereza kujitoa katika Umoja wa Ulaya imeenda sera na mwongozo mpya utakao  ifanya nchi hiyo kuendelea kufanya biashara na Mataifa mbalimbali. 


Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Dkt. Mwinyi Talib Haji akiachangia  hoja wakati wa kikao.
Kikao kikiendelea 

Tanzania kuwania nafasi ya Ujumbe wa Mfuko wa Pamoja wa Mazao Duniani

Balozi wa Tanzania nchini Uholanzi, Mhe. Irene Kasyanju amemnadi mgombea wa Tanzania anayewania nafasi ya ujumbe kwenye Kamati ya Ushauri ya Mfuko wa Pamoja wa Mazao Duniani (Common Fund for Commodities – CFC) alipotembelea Ofisi za Mfuko huo zilizoko mjini Amsterdam, Uholanzi tarehe 02 Septemba, 2020.

Balozi Kasyanju alikwenda CFC kufanya mazungumzo na pia kumpongeza rasmi Mkurugenzi Mwendeshaji wa CFC, Mhe. Balozi Sheikh Mohammed Belal kwa kushika nafasi ya kuiongoza CFC kwa kipindi cha miaka minne, kazi aliyoianza rasmi mwezi Aprili 2020 baada ya kuchaguliwa kwa kauli moja kushika wadhifa huo wakati wa Mkutano Mkuu wa 31 wa Baraza la Uongozi la CFC uliofanyika tarehe 04 Desemba 2019. Katika mazungumzo yao Balozi Kasyanju alimhakikishia Mwenyeji wake huyo ushirikiano wa Tanzania kwa Taasisi yake na kutoa shukrani za dhati kufuatia mikopo yenye riba nafuu iliyotolewa kwa ajili ya kuboresha miradi mitatu inayoendelea hivi sasa nchini Tanzania.

Balozi Kasyanju aliitumia fursa hiyo sawia kumnadi mgombea wa Tanzania, Dkt. Jacqueline David Mkindi, ambaye ni Mkurugenzi Mtendaji wa “Tanzania Horticultural Association (TAHA)” iliyoko mjini Arusha. Balozi Kasyanju alimuelezea Dkt. Mkindi kuwa ni kiongozi mahiri na mchapa kazi na akadhihirisha kwamba endapo atachaguliwa kushika nafasi hiyo ataiwakilisha vema Tanzania kwa kuwa mshauri bora na makini kwa CFC na Nchi zote Wanachama wa CFC na hivyo kuleta mwamko mpya kwenye Taasisi hiyo muhimu.

CFC iliundwa mwaka 1989 kwa mujibu wa taratibu za Umoja wa Mataifa kwa lengo la kuboresha na kuleta maendeleo kwa jamii ya wakulima na wazalishaji wa bidhaa katika Nchi Zinazoendelea. Hivyo basi, CFC imejikita katika kutoa ufadhili wa mikopo kwa ajili ya miradi ya maendeleo kwa kutumia rasilimali zake zinazotokana na michango ya hiari ya Nchi Wanachama na Wafadhili.

Tanzania ni Mwanachama hai wa CFC na katika Taasisi hii inawakilishwa kwenye Baraza lake la Uongozi na Katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda na Biashara, kama Gavana; na Balozi wa Tanzania Nchini Uholanzi ambaye ni Gavana Msaidizi. Aidha, Tanzania imewahi kushika nafasi ya Mkurugenzi Mwendeshaji wa CFC na vile vile mjumbe wa Kamati ya Ushauri ya CFC zaidi ya miaka 10 iliyopita. Hivyo, ni wakati mwingine muafaka kwa Tanzania kushika nafasi kwenye CFC hasa baada ya kutambua kwamba Mkurugenzi Mwendeshaji huyu mpya ameingia na nguvu mpya za kuleta mageuzi kwenye Taasisi yake na kuifanya iwe yenye tija zaidi kwa Wanachama wake.

Balozi wa Tanzania nchini Uholanzi, Mhe. Irene Kasyanju akipokea Taarifa ya Mwaka 2019 ya Mfuko wa Pamoja wa Mazao Duniani (Common Fund for Commodities – CFC) kutoka kwa Mkurugenzi Mwendeshaji wa CFC, Mhe. Balozi Sheikh Mohammed Belal, baada ya mazungumzo yao.

Balozi Irene Kasyanju akimkabidhi Mhe. Balozi Belal vipeperushi na majarida 20 yanayotangaza Utalii wa Tanzania yaliyoandikwa kwa lugha ya Kiingereza na Kidachi kwa ajili ya kusambazwa kwa wadau.

Balozi Irene Kasyanju na Mhe. Balozi Belal wakiwa pamoja na wasaidizi wao Bi. Linda Mkony (kushoto), Mtumishi wa Ubalozi; na kulia ni Bw.Hector Besong, CFC Portfolio and Risk Manager.


 

Thursday, September 3, 2020

BALOZI WA TANZANIA NCHINI KENYA AWASILISHA HATI ZA UTAMBULISHO KWA RAIS KENYATTA

 Rais wa Jamhuri ya Kenya, Mhe. Uhuru Kenyatta amepokea hati za utambulisho za Balozi wa Tanzania nchini Kenya Mhe. Dkt. John Stephen Simbachawene.

Hafla ya kuwasilisha hati za utambulisho imefanyika Ikulu jijini Nairobi ambapo pamoja na mambo mengine, Rais Kenyatta amepokea hati za utambulisho za Balozi wa Tanzania nchini Kenya, Mhe. Balozi Simbachawene.   

Balozi Simbachawene amemhakikishia Rais Kenyatta kuwa ataendelea kuboresha mahusiano ya nchi hizo mbili za Tanzania na Kenya, kukuza biashara baina ya nchi hizo kwa kuboresha diplomasia ya uchumi kwa ujumla wake.  

Rais wa Kenya, Mhe. Uhuru Kenyatta akiwa tayari kupokea hati ya utambulisho kutoka kwa Balozi wa Tanzania nchini Kenya Mhe. Dkt. John Stephen Simbachawene 


Rais wa Kenya, Mhe. Uhuru Kenyatta akipokea hati za utambulisho kutoka kwa Balozi wa Tanzania nchini Kenya Mhe. Dkt. John Stephen Simbachawene

Wednesday, September 2, 2020

KATIBU MKUU WA MAMBO YA NJE AFANYA MAZUNGUMZO NA MRATIBU MKAZI WA UMOJA WA MATAIFA NCHINI

Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Brigedia Generali Wilbert A. Ibuge akizungumza na Mratibu Mkazi wa Umoja wa Mataifa nchini,
Bw. Zlatan MiliÅ¡ić
 alipomtembelea Ofisini kwake jijini Dodoma tarehe 2 Septemba 2020.

Katika mazungumzo yao walijadili masuala mbalimbali ya ushirikiano kati ya Tanzania na Shirika la Umoja wa Mataifa ambapo Balozi Ibuge alitoa shukrani kwa Shirika hilo kwa ushirikiano uliopo kati yake na Serikali hususan kwenye masuala mbalimbali ya maendeleo ya kiuchumi na kijamii. Kwa upande wake, Bw. 
MiliÅ¡ić aliipongeza Tanzania kwa kudumisha amani na utulivu ambao ni chanzo cha uchumi wa nchi kustawi. Pia aliipongeza kwa kuendelea kuchangia vikosi vya ulinzi wa amani kwenye mataifa mbalimbali  yenye  migogoro duniani na kuitakia Tanzania uchaguzi wa amani na utulivu hapo mwezi Oktoba 2020.

Ujumbe wa Wizara ukimjumuisha Bw. Hangi Mgaka, Katibu wa Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki na Bi. Prisca Mwanjesa, Afisa Mambo ya Nje wakifuatilia mazungumzo kati ya Balozi Ibuge na Mratibu Mkazi wa Umoja wa Mataifa nchini, Bw. MiliÅ¡ić (hawapo pichani)

Mazungumzo yakiendelea
Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Ibuge akiwa katika picha ya pamoja na Mratibu Mkazi wa Umoja wa Mataifa nchini, Bw. MiliÅ¡ić mara baada ya kukamilisha mazungumzo yao.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Ibuge akiagana na Mratibu Mkazi wa Umoja wa Mataifa hapa nchini, Bw. MiliÅ¡ić mara baada ya mazungumzo kati yao.