Thursday, January 21, 2021

KAIMU KATIBU MKUU AKUTANA NA BALOZI WA VITNAM


Kaimu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Stephen Mbundi amekutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa Vietnam nchini Mhe. Nguyen Nam Tien ofisini kwake jijini Dodoma.

Katika mazungumzo yao viongozi hao wamesisitiza umuhimu wa kuendelea kuimarisha mahusiano ya kidiplomasia yaliyopo kati ya Tanzania na Vietnam na kuona jinsi Tanzania inavyoweza kujifunza na kunufaika na utaalam na uwekezaji kutoka Vietnam

Akizungumza katika kikao hicho, Kaimu Katibu Mkuu Balozi Mbundi ameelezea kuridhishwa na namna wawekezaji wa kutoka Vietnam wanavyoendesha shughuli zao nchini huku wakifuata sheria za nchi na kulipa kodi kwa wakati na hivyo kusaidia jitihada za Serikali ya Awamu Tano ya kukuza uchumi wa Nchi.

Pia ameelezea matarajio ya Tanzania katika kunufaika zaidi na mahusiano mazuri na Vietnam hususan katika maeneo ya matumizi ya teknolojia katika Kilimo na Uvuvi .

Naye Balozi Tien amesema Vietnam iko tayari kushirikiana na Tanzania katika maeneo hayo ili kuhakikisha maliasili zilizopo Tanzania zinainufaisha nchi na wananchi wake.

Amesema kwa sasa Ubalozi unafanya mazungumzo na wawekezaji wa nchini kwao ili kuona namna watakavyoshirikiana na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kuanzisha mazungumzo na Jumuiya ya Wafanyabiashara na Viwanda Tanzania (TCCIA) ili kuwaita wawekezaji wa Vietnam kuja kuwekeza nchini katika viwanda vya kuzalisha korosho nchini hasa ikizingatiwa kuwa Vietnam ni nchi ya pili kwa ununuzi wa Korosho za Tanzania.

Kaimu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Stephen P. Mbundi akisalimiana na Balozi wa Viet Nam nchini Tanzania Mhe. Nguyen Nam Tien alipowasili katika Ofisi za Wizara jijini Dodoma. Wawili hao wamezungumzia masuala mbalimbali ya ushirikiano ikiwemo biashara na uwekezaji baina ya Nchi hizi mbili.
Kaimu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Stephen P. Mbundi (kulia) akimsikiliza Balozi wa Viet Nam nchini Tanzania Mhe. Nguyen Nam Tien (kushoto) wakiwa katika mazungumzo yalifanyika katika Ofisi za Wazara jijini Dodoma.

Kaimu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Stephen P. Mbundi akielezea jambo wakati wa mazungumzo na Balozi wa Viet Nam nchini Tanzania Mhe. Nguyen Nam Tien.

Kaimu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Stephen P. Mbundi akiwa kwenye mazungumzo na Balozi wa Viet Nam nchini Tanzania Mhe. Nguyen Nam Tien (hayupo pichani)

Kaimu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Stephen P. Mbundi (kulia) na Balozi wa Viet Nam nchini Tanzania Mhe. Nguyen Nam Tien (kushoto) wakiwa katika mazungumzo yalifanyika katika Ofisi za Wazara jijini Dodoma.

Kaimu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Stephen P. Mbundi (kulia) na Balozi wa Viet Nam nchini Tanzania Mhe. Nguyen Nam Tien wakiwa katika picha ya pamoja na Maafisa kutoka Ubalozi wa Viet Nam na Wizarani mara baada ya mazungumzo. 





ACTING PS MET WITH VIETNAM AMBASSADOR IN THE CAPITAL DODOMA

The Acting Permanent Secretary in the Ministry of Foreign Affairs and East African Cooperation Ambassador Stephen Mbundi has met with the Vietnamese Ambassador to Tanzania Hon Nguyen Nam Tien in the capital Dodoma.

The two leaders were discussing on ways to strengthening diplomatic relations existing between the two nations as well as attracting investors from Vietnam to come and invest in Tanzania.

Speaking at the meeting, the Acting Permanent Secretary Ambassador Mbundi expressed his appreciations over the role played by Vietnamese investor who are complying with the Tanzanian laws and paying the required taxes which contributes to the country’s economic development and its people.

He said he is optimistic that Tanzania and Vietnam will continue to prosper their cooperation for the mutual benefits of the two nations as well as Tanzania will continue learning and adopting technological advancement and skills from Vietnam in the areas of Agriculture and fishing.

On his side Hon. Ambassador Tien said Vietnam is eager to honour the diplomatic relations which has 55 years and will continue to support Tanzania especially in investing in the area of processing Tanzanian cashewnuts since Vietnam is the second country which buys Tanzanian cashewnuts

Friday, January 15, 2021

BALOZI MBUNDI AONGOZA MAJADILIANO BAINA YA TANZANIA NA POLAND


Mheshimiwa Balozi Stephene P. Mbundi (kulia), Kaimu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki akiwa na Balozi wa Poland nchini Tanzania  wa kwanza kulia)walipokutana kwa mazungumzo kwenye ofisi za Wizara jijini Dodoma.

Mheshimiwa Balozi  Mbundi, leo tarehe 15 Januari, 2021, ameongoza majadiliano baina ya Poland na Tanzania.

Mjadiliano hayo yaliyolenga kuimarisha ushirikiano hususan katika masuala ya biashara na  uwekezaji. Kwa upande wa Tanzania washiriki walikuwa ni Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Kilimo; Mjumbe kutoka Wizara ya Fedha na Mipango; Watendaji wa NFRA; na Watendaji wa TBA.

Kwa upande wa Poland, walioshiriki ni pamoja na  Mheshimiwa Krzysztof Buzalski Balozi wa Poland nchini Tanzania na Wawakilishi wa makampuni kutoka Poland ya Feerum S.A na Unia Spzo.o.

Mheshimiwa Balozi Stephene P. Mbundi, Kaimu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki akiwa patika picha ya pamoja na Balozi wa Poland nchini Mheshimiwa Krzysztof Buzalski 
Mheshimiwa Balozi Stephene P. Mbundi, Kaimu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki akifafanua jambo alipokutana kwa mazungumzo na Balozi wa Poland nchini Mheshimiwa Krzysztof Buzalski 
Sehemu ya wajumbe wakifuatilia mazungumo

Monday, January 11, 2021

RAIS NYUSI AWEKA JIWE LA MSINGI HOSPITALI YA RUFAA YA KANDA - CHATO

 Na Nelson Kessy, Chato

Rais wa Msumbiji, Mhe. Filipe Jacinto Nyusi amewasili nchini leo kwa ziara ya kikazi na kupokelewa na mwenyeji wake Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli katika uwanja wa ndege wa Geita - Chato na kisha kuweka jiwe la msingi la ujenzi wa hospitali ya Rufaa ya Kanda- Chato.

Akizungunza katika hafla hiyo ya uwekaji wa jiwe la msingi la ujenzi wa hospitali ya Rufaa ya Kanda-Chato, Rais Magufuli alimshukuru Rais Mhe. Filipe Nyusi kwa kumtembelea  Chato na kuongeza  kuwa  Msumbiji ni rafiki wa muda mrefu wa Tanzania na nchi hizo  zina makubaliano ya kushirikiana katika mambo mbalimbali ikiwemo biashara na uwekezaji.

"Biashara kati ya Tanzania na Msumbiji imeongezeka, hadi kufikia mwaka 2020 ilifikia shilingi bilioni 93.6, kuna makampuni ya Msumbiji yanafanya kazi hapa na baadhi ya makampuni ya Tanzania yanafanya kazi kule." Amesema Rais Magufuli.

Rais Magufuli ameongeza kuwa Januari 9, 1967 Hayati Mwalimu Julius Nyerere alitembelea Wilaya ya Chato na kufungua kiwanda cha pamba kilichojengwa kwa shilingi milioni 2 ambacho kilikuwa na uwezo wa kuchakata marobota 20,000.

Aidha, Rais Magufuli amesema kuwa Mwalimu Nyerere alichangisha fedha na yeye binafsi kuchangia shilingi 2,000 kwa ajili ya kujenga bandari ya Nyamirembe ili iweze kusafirisha pamba kwenda Mwanza na Dar es Salaam kwa hiyo wa Rais Nyusi amefika eneo ambalo alifika Mwalimu Nyerere.

"Kwetu sisi tunaona hii ni zawadi kubwa kwa wewe kuja kuzindua hospitali hii ambayo ni kubwa na itahudumia pia nchi za jirani.Nawashukuru Wizara ya Afya na Wakandarasi, nitawabana Wizara ya Afya  ili hospitali hii ikamilike mara moja." Alisema Rais Magufuli

Kwa upande wake Rais Nyusi amempongeza Rais Magufuli kwa juhudim kubwa za kushughulikia maisha ya wananchi wa Tanzania kwa kuendelea kuboresha sekta pamoja na huduma za afya nchini.

"Nashukuru kwa Rais Magufuli kunipa nafasi ya kuweka jiwe la msingi kwa sababu Serikali inayoaangalia afya za wananchi hiyo ni Serikali inayopenda wananchi wake. Rais Magufuli anashughulikia sana maisha ya wananchi wa watanzania kwa kuangalia nyumba bora za kuishi, huduma za maji, chakula  na afya bora" amesema Rais Nyusi.

"Kwa hiyo hii ni zawadi kwetu  kwa kutupa nafasi ya kuweka jiwe la msingi katika hospitali hii kubwa, kule Msumbiji tumeanza (Program ya  presidential initiatives) ya kujenga hospitali kila wilaya hii ni zawadi kubwa kwetu ya  kutupa nafasi ya kuweka jiwe la msingi  katika afya ya wananchi," Ameongeza Rais Nyusi

Aidha, Rais Nyusi amesema kuwa mkoa wa Geita  ni tajiri kwa kuwa kuna kilimo cha mpunga,  madini ya dhahabu na uvuvi wa  samaki, hivyo kuwataka wananchi wa mkoa huo kufanyakazi kwa bidii.

Naye, Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dkt. Dorothy Gwajima amesema kuwa awamu ya kwanza ya ujenzi wa Hospitali ya Rufaa ya Kanda - Chato ilikadiriwa kutumia sh. bil.16, Serikali imeshatoa sh. bil.14 ambapo ujenzi umekamilika kwa asilimia 90 na makabidhiano yanatarajiwa kufanyika mwezi Machi, 2021.

Ameongeza kuwa awamu ya pili ya ujenzi  imeshaanza kwa jumla ya gharama ya shilingi bilioni 14 ambapo mpaka sasa Serikali imetoa shilingi bilioni 4.1 na utekelezaji wake umefikia asilimia 37.

"Hospitali ya Rufaa ya Kanda - Chato itakapokamilika itakuwa na uwezo wa kuhudumia wananchi zaidi ya milioni 14 ambapo kwa siku itakuwa na uwezo wa kuhudumia wagonjwa kati ya 700 - 1000." Amesema Dkt. Gwajima

Rais wa Msumbiji, Filipe Jacinto Nyusi yupo nchini kwa ziara ya siku moja ambapo atafanya mazungumzo na Rais Magufuli kuhusu namna ya kuboresha maisha  wananchi wetu  pamoja na usalama.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Pombe Joseph Magufuli akiteta jambo na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamagamba John Kabudi (Mb) muda mfupi kabla ya Rais wa Msumbiji, Mhe. Filipe Nyusi kuwasili katika uwanja wa ndege wa Geita - Chato


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Pombe Joseph Magufuli na mgeni wake Rais wa Msumbiji Mhe. Filipe Nyusi wakipita katikati ya gadi ya heshima mara baada ya Rais Nyusi kuwasili nchini


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Pombe Joseph Magufuli na mgeni wake, Rais wa Msumbiji Mhe. Filipe Nyusi wakipata maelezo kuhusu ujenzi wa hospitali ya Rufaa ya Kanda - Chato kutoka kwa Katibu Mkuu, Wizara ya Afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto, Prof. Mabula Mchembe


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Pombe Joseph Magufuli na mgeni wake, Rais wa Msumbiji Mhe. Filipe Nyusi wakimsikiliza maelezo ya Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto, Dkt. Dorothy Gwajima wakati walipofanya ziara katika Hospitali ya Rufaa ya Kanda - Chato


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Pombe Joseph Magufuli na mgeni wake Rais wa Msumbiji Mhe. Filipe Nyusi wakiweka rasmi jiwe la msingi katika Hospitali ya Rufaa ya Kanda - Chato


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Pombe Joseph Magufuli akihutubia hadhara ya wananchi (hawapo pichani) mara baada ya kuweka jiwe la msingi katika Hospitali ya Rufaa ya Kanda - Chato


Rais wa Msumbiji Mhe. Filipe Nyusi akihutubia hadhara ya wananchi (hawapo pichani) mara baada ya kuweka jiwe la msingi katika Hospitali ya Rufaa ya Kanda - Chato

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Pombe Joseph Magufuli pamoja na Rais wa Msumbiji Mhe. Filipe Nyusi wakiwaaga wananchi (hawapo pichani) mara baada ya kuweka jiwe la msingi katika Hospitali ya Rufaa ya Kanda - Chato



 

Sunday, January 10, 2021

RAIS WA MSUMBIJI FILIPE NYUSI KUFANYA ZIARA YA KIKAZI NCHINI TANZANIA

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamagamba John Kabudi (Mb) akiongea na waandishi wa Habari Chato mkoani Geita (Hawapo pichani) kuhusu ziara ya siku mbili ya Rais wa Jamhuri ya Msumbiji hapa nchini,  Mhe. Filipe Jacinto Nyusi. Kulia ni Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Brigedia Jenerali, Wilbert Ibuge, na kushoto ni Mkuu wa Mkoa wa Geita, Mhandisi Robert Luhumbi. Picha na Nelson Kessy


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamagamba John Kabudi (Mb) akiongea na waandishi wa Habari Chato mkoani Geita kuhusu ziara ya siku mbili ya Rais wa Jamhuri ya Msumbiji hapa nchini,  Mhe. Filipe Jacinto Nyusi. Kulia ni Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Brigedia Jenerali, Wilbert Ibuge, na kushoto ni Mkuu wa Mkoa wa Geita, Mhandisi Robert Luhumbi. Picha na Nelson Kessy




Na Nelson Kessy, Chato

Rais wa Jamhuri ya Msumbiji,  Mhe. Filipe Jacinto Nyusi anatarajia kufanya ziara ya kikazi ya siku mbili hapa nchini Tanzania kuanzia tarehe 11 - 12 Januari 2021 kwa mwaliko wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Joseph Magufuli.

Akithibitisha juu ya ziara hiyo, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamagamba John Kabudi (Mb) amesema kuwa Mhe. Nyusi atawasili nchini kwa ziara ya kikazi ya siku mbili na kupokelewa na mwenyeji wake Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Joseph Magufuli katika uwanja wa ndege wa Geita - Chato.

"Ziara hii ya Rais Nyusi ni ziara ya kindugu ambayo ilipangwa kufanyika muda mrefu lakini haikuweza kufanyika mapema, kutokana na kutokana na sababu mbalimbali, hususan Uchaguzi Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania uliofanyika Oktoba 28, 2020," Amesema Prof. Kabudi.

Aidha, Prof. Kabudi ameongeza kuwa, ziara ya Mhe Nyusi, ni kwa ajili ya kuendeleza na kuimarisha mahusiano ya nchi zetu mbili katika maeneo anuwai, yakiwemo yale ya kidiplomasia, kiuchumi, kisiasa na kijamii; kama yalivyoasisiwa na vyama vya ukombozi vya nchi zetu, yaani, chama cha TANU na Chama cha Afro-Shirazi na baadaye Chama cha Mapinduzi (CCM) kwa upande wa Tanzania na kile cha FRELIMO kwa upande wa Msumbiji. Mtakumbuka, mahusiano haya yaliyotukuka, yaliasisiwa na viongozi waanzilishi wa nchi zetu huru, yaani Hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere kwa upande wa Tanzania na Hayati Dkt. Eduardo Tshivambo Mondlane kwa upande wa Msumbiji.

"Uhusiano huo pia umeendelea baada ya Msumbiji kupata uhuru wake kupitia mapambano ya silaha mwaka 1975, ambapo, kama nyote mnavyofahamu, kuanzia Rais wa Kwanza wa Msumbiji Huru, Hayati Samora Moises Machel, na wengine wote waliomfuatia hadi leo, na Marais wa Tanzania baada ya Hayati Baba wa Taifa hadi leo, wote wameendelea kuimarisha mahusiano hayo na undugu wa Watanzania na Watu wa Msumbiji ambao kwa hakika ni ndugu wa damu," Ameongeza Prof. Kabudi

Prof. Kabudi ameeleza kuwa, licha ya uhusiano wa Kihistoria na Kidiplomasia kati ya nchi zetu mbili, uhusiano wa Kiuchumi nao umeendelea kuimarika. Tanzania inafanya biashara na Msumbiji kupitia mazao ya chakula na biashara pamoja na bidhaa za viwandani. Kwa mfano, takwimu kutoka Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) zinaonesha kuwa jumla ya mauzo ya Nje (Export) kati ya nchi hizi mbili zilifikia Shilingi za Kitanzania Bilioni 76.4 kwa mwaka 2018 na Shilingi za Tanzania Bilioni 93.5 kwa mwaka 2019.

Kuhusu uwekezaji, hadi sasa makampuni makubwa ya Kitanzania yaliyowekeza mitaji mikubwa nchini Msumbiji ni pamoja Bakheresa (Azam), Mohammed Enterprises, Quality Foam (Magodoro Dodoma), n.k. Vilevile kuna Watanzania wanaomiliki kampuni za usafirishaji wa abiria na mizigo pamoja na biashara za kati na ndogondogo nchini Msumbiji.

"Licha ya changamoto ya Ugonjwa wa Homa Kali ya Mapafu (COVID 19) SADC imeendelea kuwezesha na kusimamia biashara miongoni mwa nchi wanachama. Wakati wa ziara hii viongozi wetu watabadilishana mawazo ya namna ya kuendelea kuwezesha ufanyaji wa biashara," Ameongeza Prof. Kabudi

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Geita, Mhandisi Robert Luhumbi amewataka wananchi wa Geita kujitokeza kwa wingi na kumpokea mgeni wakati atakapokuwa amewasili katika uwanja wa ndege wa Geita - Chato.

"Nawasihi wananchi wa Geita kujitokeza na kumpokea mgeni wetu, kwani hii ni fursa kwa mkoa wetu, tunapaswa kuitumia fursa hii vizuri" Amesema Mhandisi Luhumbi.

Friday, January 8, 2021

HABARI KTK PICHA WANG Yi AKUTANA, KUFANYA MAZUNGUMZO NA JPM

Mjumbe wa Baraza la Taifa na Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamuhuri ya Watu wa China, mhe. Wangi Yi ameendelea na ziara yake leo kwa kutembelea eneo la Mwalo wa Chato na kukutana na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli pamoja na kuongea na vyombo vya Habari vya nchini akiwa yeye na mwenyeji wake, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamagamba John Kabudi, (Mb).

Awali, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli ametoa wito kwa Watanzania kutumia uwepo wa soko la China katika kupeleka mazao ya kilimo yaliyoongezwa thamani.

Ametoa wito huo wilayani Chato wakati akizungumza na Waziri wa Mambo ya Nje wa China Wang Yi aliyepo nchini kwa ziara ya kikazi ambapo Rais Magufuli ameiomba serikali ya China kutumia ushirikiano na Tanzania kununua mazao ya kilimo hapa nchini.


Mjumbe wa Baraza la Taifa na Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamuhuri ya Watu wa China, mhe. Wangi Yi akiangalia jinsi bondo la samaki linavyotolewa na mmoja kati ya wavuvi wanaojishughulisha na shughuli za uvuvi katika Mwalo wa Chato mkoani Geita

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akimsikiliza Mjumbe wa Baraza la Taifa na Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamuhuri ya Watu wa China, mhe. Wangi Yi  wakati alipokuwa anaongea na waandishi wa Habari - Chato mkoani Geita

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akimkabidhi moja kati ya zawadi Mjumbe wa Baraza la Taifa na Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamuhuri ya Watu wa China, mhe. Wangi Yi 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akiwa katika picha ya pamoja na Mjumbe wa Baraza la Taifa na Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamuhuri ya Watu wa China, mhe. Wangi Yi, Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi pamoja na baadhi ya Mawaziri wakiongozwa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamagamba John Kabudi (Mb) 


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akiwa katika picha ya pamoja na Mjumbe wa Baraza la Taifa na Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamuhuri ya Watu wa China, mhe. Wangi Yi, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Kabudi, Balozi wa China Nchini Tanzania, Mhe. Wang Ke pamoja na Makatibu Wakuu wa Wizara mbalimbali

 

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Kabudi, (Mb) akiongea na Waandishi wa Habari (hawapo pichani)- Chato mkoani Geita 

Mjumbe wa Baraza la Taifa na Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamuhuri ya Watu wa China, mhe. Wangi Yi akiongea na Waandishi wa Habari (hawapo pichani) - Chato mkoani Geita 

 

Mjumbe wa Baraza la Taifa na Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamuhuri ya Watu wa China, mhe. Wangi Yi akiwaaga viongozi mbalimbali katika uwanja wa ndege wa Geita - Chato muda mfupi kabla ya kuondoka kwake



Mawaziri wakiongozwa na Prof. Kabudi wakimuaga Mjumbe wa Baraza la Taifa na Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamuhuri ya Watu wa China, mhe. Wangi Yi katika uwanja wa ndege wa Geita - Chato   


Ndege aliyokuja nayo Mjumbe wa Baraza la Taifa na Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamuhuri ya Watu wa China, mhe. Wangi Yi ikiondoka 



















Thursday, January 7, 2021

WANGI YI AWASILI NCHINI, KUZINDUA VETA

Mjumbe wa Baraza la Taifa na Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamuhuri ya Watu wa China, mhe. Wangi Yi ameanza ziara yake ya kikazi ya kikazi nchini Tanzania.

Mhe. Wangi Yi amewasili majira ya saa 11 jioni katika uwanja wa ndege wa Geita - Chato na kupokelewa na mwenyeji wake Mhe. Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamagamba John Kabudi, (Mb).

Mara baada ya kuwasili, Mhe. Wang Yi ameshiriki katika uzinduzi wa chuo cha Veta kilichopo Chato mkoani Geita, ambapo ujenzi wa chuo hicho umegharamiwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Akizungumza wakati akimkaribisha Mhe. Wang Yi katika uzinduzi wa chuo hicho, Waziri wa Elimu Sayansi na Teknolojia, Mhe. Prof. Joyce Ndalichako amesema Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeweka umuhimu mkubwa katika Elimu ya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi, ili kufanikisha kujenga uchumi wa viwanda, na kufikia Dira ya Maendeleo ya Taifa ya 2025.

"Lengo letu ni kujenga angalau kituo kimoja cha umma cha mafunzo ya ufundi stadi katika kila wilaya," amesema Prof. Ndalichako  

Aidha, Prof. Ndalichako ameongeza kuwa lengo kubwa la Serikali ni kujenga vyuo vingi vya Veta kwa kutumia vyanzo vya mapato vya ndani na kwa ushirikiano na mataifa rafiki ambapo mpaka sasa Serikali ina vituo 41 vya umma vya mafunzo ya ufundi stadi nchini na vingine 29 vinaendelea kujengwa.

Pia Prof. Ndalichako amesema Serikali ya Tanzania iko tayari kupokea moja ya kati ya karakana 10 za mafunzo za Luban (Luban Workshops), ambazo China imedhamiria kuzijenga barani Afrika, ili kutoa mafunzo ya ufundi stadi kwa vijana wa ki-afrika. Karakana hiyo inaweza kuwa sehemu ya Kituo cha Mafunzo ya Ufundi Stadi cha Wilaya ya Chato ambacho tumekizindua leo.

Kwa upande wake Mjumbe wa Baraza la Taifa na Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamhuri ya Watu wa China Mhe. Wang Yi, amesema ili Taifa lolote liweze kupiga hatua za na kiteknolojia na kufikia malengo ya mapinduzi ya viwanda ni lazima taifa hilo liwe na vijana wenye ujuzi wa kitaaluma hivyo chuo cha Veta ni mojawapo ya maeneo ya kuwajengea vijana uwezo wa kitaaluma.

Mhe. Wang Yi ameongeza kuwa Serikali ya China ipo pamoja na Serikali ya Tanzania katika kuhakikisha vijana wanapata mafunzo ya kitaaluma katika vyuo vya Veta na kwa kudhihirisha hilo, China inachangia kiasi cha RB 1,000,000 za China sawa na fedha za kitanzania Shilingi 350 milioni kwa ajili ya kuendeleza chuo cha Veta - Chato.     

"Binafsi naomba kumpongeza Rais wa jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuwa mwanamapinduzi wa kweli kiuchumi na kitaaluma ambapo amefanikiwa kujenga idadi kubwa ya vyuo vya ufundi ili kuwajengea vijana uwezo wa kitaaluma jambo ambalo litachangia mapinduzi ya kiuchumi," Amesema Wang Yi.

China inasaidia Tanzania chuo cha VETA mkoani Kagera ambacho kina uwezo wa kuchukua wanafunzi 1,000 ambapo ujenzi wake unaendelea.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamagamba John Kabudi, (Mb) pamoja na mgeni wake Mjumbe wa Baraza la Taifa na Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamuhuri ya Watu wa China, mhe. Wangi Yi wakiangalia vikundi vya ngoma katika uwanja wa ndege wa Geita-Chato


Waziri wa Elimu Sayansi na Teknolojia, Mhe. Prof. Joyce Ndalichako, (Mb) pamoja na Mjumbe wa Baraza la Taifa na Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamuhuri ya Watu wa China, mhe. Wangi Yi wakizindua rasmi chuo cha VETA


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamagamba John Kabudi na Waziri wa Elimu Sayansi na Teknolojia, Mhe. Prof. Joyce Ndalichako pamoja na Mjumbe wa Baraza la Taifa na Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamuhuri ya Watu wa China, mhe. Wangi Yi wakizindua chuo cha VETA


Makatibu Wakuu, Mabalozi na viongozi waandamizi wa Serikali wakishuhudia uzinduzi wa chuo cha VETA Chato leo Mkoani Geita


Mjumbe wa Baraza la Taifa na Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamuhuri ya Watu wa China, mhe. Wangi Yi akimkabidhi Waziri wa Elimu Sayansi na Teknolojia, Prof. Joyce Ndalichako kiasi cha Shilingi milioni 350 kwa ajili ya kuendeleza chuo cha VETA. Chuo hicho kimejengwa kwa fedha za Serikali ya Tanzania. 



Wednesday, January 6, 2021

PROF. KABUDI: WANGI YI KUWASILI TANZANIA KESHO

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamagamba John Kabudi (Mb) amesema kuwa Waziri wa Mambo ya Nje wa China mhe. Wangi Yi atawasili nchini Tanzania kesho kwa ziara ya kikazi ya siku mbili tarehe 7 na 8 Januari 2021.

Prof. Kabudi ametoa kauli hiyo wakati anaongea na waandishi wa Habari leo Wilayani Chato mkoani Geita, ambapo amesema kuwa Waziri Yi atakapokuwa nchini atafanya shughuli mbalimbali ikiwemo kuzindua Chuo cha Mafunzo na Ufundi Stadi (VETA) katika wilaya ya Chato mkoani Geita.

“Hapo kesho mara baada ya Mhe. Yi kuwasili hapa Chato, atazindua Chuo cha VETA cha wilaya ya Chato ambacho kimejengwa kwa fedha za watanzania,” alisema Prof. Kabudi.

Prof. Kabudi ameongeza kuwa “sababu ya kumuomba afungue chuo hicho ni utamaduni wetu wa kumpa heshima mgeni anapokuja hapa nchini kwetu, sambamba na kutambua elimu ya mafunzo na ufundi stadi ilivyopiga hatua huko nchini China.”

Pamoja na mambo mengine, Prof. Kabudi amesema kuwa  Serikali ya China itajenga Chuo cha Mafunzo na Ufundi Stadi (VETA) mkoani Kagera ikiwa ni namna ya kufikia lengo la  Serikali  ya Awamu ya Tano ya kujenga VETA kila Wilaya hapa nchini.

Waziri Kabudi ameongeza kuwa shughuli nyingine zitakazofanywa na Waziri wa Mambo ya Nje wa China, kuwa ni  mazungumzo na Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli, pamoja na kufanya  mazungumzo rasmi kati yake na ujumbe wake kutoka nchini China.

Aidha, shughuli nyingine atakazofanya Waziri Yi ni pamoja na kutembelea mwalo wa Chato ili kuona shughuli za uvuvi, ikizingatiwa kuwa ziwa Viktoria ni ziwa la pili kwa ukubwa dunia Pamoja na kusaini mkataba wa ujenzi wa reli ya kisasa (SGR) kipande cha tano kutoka Mwanza hadi Isaka chenye urefu wa km 341 ambapo kitagharimu kiasi cha Shilingi trilioni 3.0617

Waziri Kabudi ameogeza kuwa, Februari mwaka huu Serikali ya Tanzania inatarajia kuanzisha  safari za ndege za moja kwa moja kutoka Dar es Salaam hadi Guanzhou  nchini China ili kukuza sekta ya utalii. 

Historia ya mahusiano ya kidiplomasia kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya watu wa China ulianza mwaka 1965.


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamagamba John Kabudi (Mb) akiwaelezea waandishi wa Habari Chato mkoani Geita (Hawapo pichani) juu ya ziara ya Waziri wa Mambo ya Nje wa China Mhe. Wang Yi ambaye anatarajiwa kuwasili nchini Tarehe 7 Januari, 2021. 


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamagamba John Kabudi (Mb) akiongea na waandishi wa Habari Chato mkoani Geita (Hawapo pichani) juu ya ziara ya Waziri wa Mambo ya Nje wa China Mhe. Wang Yi. Kulia mwa Prof. Kabudi ni Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Brigedia Jenerali, Wilbert Ibuge, na kushoto mwa Waziri ni Balozi wa Tanzania nchini China, Mhe. Mbelwa Kairuki.


Mkutano ukiendelea