Friday, March 5, 2021

TANZANIA NA BURUNDI ZAKUBALIANA KUIMARISHA USHIRIKIANO


Tanzania na Burundi zimekubaliana kuimarisha ushirikiano kwa kusimamia kikamilifu utekelezaji wa makubaliano yaliyofikiwa kwenye Mkutano wa Sita wa Tume ya Pamoja ya Kudumu kati ya nchi hizo ulimalizika mkoani Kigoma tarehe 5 Machi 2021.

Makubaliano yaliyofikiwa yamejikita kwenye maeneo kuimarisha sekta za siasa na mahusiano ya kidiplomasia, ulinzi na usalama, maendeleo ya miundombinu, ushirikiano katika sekta ya uchumi na kijamii.

 Akizungumza wakati wa Mkutano huo, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamagamba John Kabudi amesema kuwa Tanzania imedhamiria kukuza uchumi wa watu wake kupitia jitihada mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi na nchi nyingine ikiwemo Burundi.

Ameongeza kuwa, Tanzania chini ya uongozi wa Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imekuwa ikitekeleza  mikakati mbalimbali ya kujenga uchumi na kuinua maisha ya watanzania. Alisema katika kipindi cha miaka mitano iliyopita, Serikali imeendelea kuwekeza na kuboresha sekta mbalimbali pamoja na kujenga miradi mikubwa ya kimkakati ukiwemo mradi wa Bwawa la kufua Umeme la Nyerere litakalozalisha Megawati 2,115 na ujenzi wa Reli ya kisasa kutoka Dar es Salaam hadi Mwanza yenye urefu wa kilomita 1,219.

Alisisitiza mbali na jitihada hizo, upo umuhimu mkubwa wa Tanzania kushirikiana na nchi nyingine ikiwemo Burundi ili mafanikio haya yawe na tija zaidi kwa wananchi. “Tanzania chini ya uongozi wa Mhe. Rais Magufuli imeendelea kuwekeza kwenye miradi ya kimkakati ili kukuza uchumi wa wananchi wake. itihada hizi haziwezi kufanikiwa kama Tanzania haitashirikiana na nchi nyingine na kama Tanzania haitawahimiza wananchi wake kuvuka mipaka na kufanya biashara na wenzao wan chi nyingine. Ni kwa msingi huo Mkutano huu wa Tume ya Pamoja ya kudumu una umuhimu mkubwa kwa nchi zetu mbili hususan kuingia makubaliano ya ushirikiano katika sekta mbalimbali” alisisitiza.

Kadhalika alisema kuwa maeneo ya ushirikiano yaliyokubalika kwenye mkutano huo ni sehemu tu ya maeneo mengi muhimu ambayo Tanzania na Burundi zitaendelea kuyaibua kadri ushirikiano huo unavyoendelea.

“Kuna maeneo mengi sana ambayo nchi zetu zinaweza kushirikiana, ni dhahiri mpaka sasa hatujaweza kuzitumia fursa zote zilizopo. Tumeanza na sekta za ulinzi na usalama; biashara na uwekezaji, uendelezaji wa miundombinu ya uchukuzi inayounganisha nchi hizi pamoja na masuala ya kijamii na tutaendelea kuvumbua maeneo mengine mapya ya ushirikiano kadri tunavyoimarisha ushirikiano huu” alisema Prof. Kabudi.

Prof. Kabudi alitumia fursa hiyo kuzihimiza sekta zinazohusika na usimamizi wa miradi ya kikanda ya miundombinu  inayotekelezwa na Serikali za Tanzania na Burundi chini ya uratibu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki ukiwemo  mradi wa ujenzi wa Barabara ya Kabingo-Kasulu-Manyovu (260km) na Barabara ya Rumonge-Gitaza (45km)  na ujenzi wa Kituo cha Huduma kwa Pamoja Mpakani (OSBP) cha Manyovu/Mugina kutekeleza kikamilifu ili kuharakisha maendeleo ya wananchi wa Tanzania na Burundi.

Pia alitoa rai kwa watendaji wa Tanzania na Burundi kusimamia kikamilifu utelezaji wa makubaliano yaliyofikiwa ikiwa ni pamoja na kufanya tathmini ili mikutano ya tume iwe yenye tija.

Kwa upande wake, Waziri wa Mambo ya Nje wa Burundi na Mwenyekiti Mwenza wa Mkutano wa Sita wa Tume ya Pamoja ya Kudumu, Mhe. Balozi Albert Shingiro alisema nchi yake imedhamiria kutekeleza makubaliano yote yaliyofikiwa na kutaja mkutano wa sita kama mwanzo mzuri wa kuendeleza ushirikiano wa kindugu uliopo baina ya Tanzania na Burundi.

Mkutano wa Sita wa Tume ya Pamoja ya Kudumu kati ya Tanzania na Burundi umehitimishwa kwa kusainiwa kwa Makubaliano ya Ushirikiano kwenye maeneo matano ambayo ni Ushirikiano wa Kidiplomasia; Ulinzi na Usalama; Uendelezaji Miundombinu ya Usafirishaji; Elimu na Utamaduni na Biashara na Uwekezaji. Kadhalika Mkutano huo umeshuhudia kusainiwa kwa Mkataba wa Makubaliano ya Ushirikiano kati ya Chemba za Biashara za Tanzania na Burundi ukiwa na lengo la kuimarisha biashara baina ya nchi hizi mbili.

Mkutano wa Sita wa Tume ya Pamoja ambao umefanyika mjini Kigoma kuanzia tarehe 3 hadi 5 Machi 2021 umehudhuriwa na Mawaziri, Naibu Mawaziri, Makatibu Wakuu, Naibu Makatibu Wakuu na viongozi wengine waandamizi kutoka sekta mbalimbali za Tanzania na Burundi.



Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamagamba John Kabudi akizungumza kama Mwenyekiti wa Mkutano wa Sita wa Tume ya Pamoja ya Kudumu kati ya Tanzania na Burundi uliofanyika kwa ngazi ya Mawaziri mkoani Kigoma tarehe 5 Machi 2021. Wengine katika picha ni Waziri wa Mambo ya Nje Burundi na Mwenyekiti Mwenza wa Mkutano huo Mhe. Balozi Albert Shingiro ( wa pili kushoto), Mkuu wa Mkoa wa Kigoma Mhe. Thobias Andengenye (wa pili kutoka kulia), Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Brig. Gen. Wilbert Ibuge (kulia)  na Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje wa Burundi, Mhe. Isidore Ntirampeba (kushoto). Mkutano huo ulitanguliwa na Mkutano wa Wataalam ulifanyika tarehe 3 na 4 Machi 2021.

Waziri wa Mambo ya Nje wa Burundi, Mhe. Balozi Albert Shingiro akizungumza wakati wa Mkutano wa Sita wa Tume ya Pamoja ya Ushirikiano kati ya Tanzania na Burundi ulifanyika kwa ngazi ya mawaziri mkoani Kigoma tarehe 5 Machi 2021

Balozi Ibuge nae akizungumza wakati wa mkutano sita wa tume ya pamoja ya kudumu kati ya Tanzania na Burundi uliofanyika kwa ngazi ya Mawaziri 

Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Mhe. Thobias Andengenye akiwakaribisha Mkoani Kigoma Viongozi na Wajumbe walioshiriki Mkutano wa Sita wa Tume ya Pamoja ya Kudumu kati ya Tanzania na Burundi ulifanyika kwa ngazi ya mawaziri 

Mhe. Prof. Kabudi kwa pamoja na Mhe. Balozi Shingiro wakisaini Hati ya Makubaliano ya Ushirikiano kwenye maeneo kadhaa yaliyojadiliwa na kukubalika wakati wa mkutano wa sita wa tume ya pamoja ya kudumu kati ya Tannzania na Burundi

Mawaziri wakibadilishana Hati hizo baada ya kusaini

Rais wa Chama cha Wafanyabiashara, Wenye Viwanda na Wakulima Tanzania (TCCA), Bw. Paul Koyi kwa pamoja na Kaimu Rais wa Chama cha Wafanyabiasha cha Burundi, Bw. Tharcisse Havyarimana (kushoto) wakisaini Mkataba wa Makubaliano ya Ushirikiano kwenya masuala ya Biashara na Uwekezaji.

Sehemu ya Mawaziri na Makatibu wakuu na Viongozi wengine kutoka Tanzania wakiwa kwenye Mkutano wa Sita wa Tume ya Pamoja ya Ushirikiano kati ya Tanzania na Burundi uliofanyika kwa ngazi ya mawaziri tarehe 5 Machi 2021.

Sehemu nyingine ya Makatibu Wakuu wakifuatilia matukio mbalimbali ya mkutano wa sita wa tume ya pamoja ya kudumu kati ya Tanzania na Burundi

Ujumbe wa Tanazania wakati wa mkutano
Mkurugenzi wa Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bw. Emmanuel Buhohela akitoa ratiba ya masuala mbalimbali yanayoendelea wakati wa mkutano wa sita wa Tume ya Pamoja ya Kudumu kati ya Tanzania na Burundi

Ujumbe wa Burundi

Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Afrika, Bw. Frank Mwega (kulia)  akiwa na Maafisa kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki walioshiriki Mkutano wa Sita wa Tume ya Pamoja ya Kudumu ya Ushirikiano kati ya Tanzania na Burundi

Mhe. Prof. Kabudi akimpatia Mhe. Balozi Shingiro zawadi ya picha ya michoro maarufu  ya Tingatinga zinazopatikana hapa nchini

Mhe. Prof. Kabudi akimbidhi Mhe. Balozi Shingiro Kamusi ya Kiswahili ili kumwezesha kuendelea kuongeza msamiati wa Kiswahili ikiwa ni Lugha iliyokubalika kufundishwa nchini Burundi.

Mhe. Balozi Shingiro akimkabidhi Mhe. Prof. Kabudi zawadi ya kikapu  kinachotambulisha utamaduni wa Burundi 

Makatibu Wakuu  nao wakipeana zawadi ambapo Balozi Ibuge anaonekana akimkabidhi Mhe. Ntirampeba zawazi ya Kamuzi ya Kiswahili

Mhe. Ntirampeba nae akikabidhi zawadi kwa Balozi Ibuge

Viongozi wa meza kuu wakiwa katika picha ya pamoja

Meza kuu wakiwa katika picha ya pamoja na Makatibu Wakuu na Naibu Makatibu Wakuu pamoja na Balozi wa Tanzania nchini Burundi, Mhe. Jillyy Maleko ( wa tatu kushoto waliosimama)

Meza kuu wakiwa katika picha ya pamoja na Sekretarieti ya maandalizi ya Mkutano wa Sita wa Tume ya Pamoja ya Kudumu ya Ushirikiano kati ya Tanzania na Burundi

Mhe. Prof. Kabudi kwa pamoja naMhe. Balozi Shingiro wakifurahia kikundi cha ngoma maarufu kama Mapigo Tisa cha mkoani Kigoma kilichotumbuiza wakati wa Mkutano wa Sita wa Tume ya Pamoja ya Kudumu kati ya Tanzania na Burundi













 

Wednesday, March 3, 2021

BALOZI BRIG. GEN. IBUGE AFUNGUA MKUTANO WA SITA WA TUME YA USHIRIKIANO KATI YA TANZANIA NA BURUNDI

Mkutano wa Sita wa Tume ya Pamoja ya Kudumu (JPC) kati ya Tanzania na Burundi umeanza rasmi mjini Kigoma, ukiwa na lengo la kujadili mambo mbalimbali ikiwemo namna ya kutumia fursa zilizopo baina ya nchi hizo katika kukuza uchumi.


Akifungua mkutano huo, Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Brigedia Jenerali Wilbert Ibuge amesema mkutano huo pamoja na mambo mengine utajadili masuala matano o ambayo ni pamoja na siasa na mahusiano ya kidiplomasia, ulinzi na usalama, maendeleo ya miundombinu, ushirikiano katika sekta ya uchumi na kijamii.

Alisema mafanikio ya mkutano huo yanategemea zaidi jitihada za pamoja kama watendaji katika kutekeleza masuala watakayokubaliana na kwamba kujadili kwa uhalisia na kufikia makubaliano yatakayotekelezeka ni moja ya lengo la mkutano huo.

“Katika mkutano huu tuwe tayari kusimamia na kushiriki kikamilifu katika utekelezaji wa makubaliano na kuweka utaratibu wa kufanya mapitio ya utekelezaji wa masuala tutakayokubaliana angalau mara moja kwa mwaka,”alisema Balozi Ibuge.

Alisema kwa upande wa Tanzania utawekwa utaratibu wa kufanya mapitio ya mara kwa mara ya makubaliano yote yaliyofikiwa kwani kwa kufanya hivyo mkutano huo utatimiza matarajio ya viongozi wakuu na wananchi wa mataifa hayo mawili.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimaendeleo wa Burundi, Mhe. Isidore Ntirampeba alisema wanaishukuru Serikali ya Tanzania kwa kuendelea kuunga mkono ombi lao la kujiunga na Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) na kuendelea kuwasemea kwenye majukwaa ya kimataifa ili waweze kuondolewa vikwazo vya kiuchumi walivyowekewa na Jumuiya ya Ulaya.

“Tumejidhatiti kuhakikisha tunawaonesha wale wote wanaoiwekea vikwazo nchi ya Burundi kuwa wakati umeabadilika, kwani sasa tunayo amani na utulivu na kwamba tupo kwenye juhudi kubwa za kuimarisha ushirikiano na nchi zote na washirika wa maendeleo wenye mapenzi mema na nchi yetu,”alisema Ntirampeba.

Mkutano huo ambao umefunguliwa leo kwa ngazi ya wataalam utafuatiwa na Mkutano wa Mawaziri wa Wizara za Mambo ya Nje za Burundi na Tanzania ambao wanatarajiwa kusaini makubaliano yaliyofikiwa na pande zote mbili kwa ajili ya utekelezaji.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Brig. Gen. Wilbert Ibuge akizungumza wakati wa ufunguzi rasmi wa Mkutano wa Sita wa Tume ya Pamoja ya Kudumu kati ya Tanzania na Burundi unaofanyika mjini Kigoma kuanzia tarehe 3 hadi 5 Machi 2021. Mkutano huu umeanza kwa ngazi ya wataalam na utamalizika kwa ngazi ya Mawaziri tarehe 5 Machi 2021. Kulia walioketi ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje wa Burundi, Mhe. Isidore Ntirampeba.

Makatibu Wakuu na Naibu Makatibu Wakuu kutoka Tanzania wakifuatilia ufunguzi wa Mkutano wa Sita wa Tume ya Pamoja ya Kudumu kati ya Tanzania na Burundi

Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje wa Burundi, Mhe. Isidore Ntirampeba naye akizungumza wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa Sita wa Tume ya Pamoja ya Kudumu kati ya Tanzania na Burundi unaofanyika mjini Kigoma

Balozi wa Tanzania nchini Burundi, Mhe. Dkt. Jilly Maleko (kulia)  akiwa na viongozi wengine kutoka Tanzania wanaoishiriki Mkutano wa Sita wa Tume ya Pamoja ya Kudumu kati ya Tanzania na Burundi ulioanza kufanyika  kwa ngazi ya wataalam.

Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Afrika katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bw. Frank Mwega akizungumza kuhusu ratiba ya mkutano wa ngazi ya wataalam.

Bw. Mwega akizungumza

Sehemu ya ujumbe kutoka Burundi unaoshiriki mkutano wa wataalam wakifuatilia ufunguzi wa mkutano wa Sita wa Tume ya Pamoja ya Kudumu kati ya Tanzania na Burundi

Sehemu nyingine ya ujumbe wa Burundi 

Ujumbe wa Burundi

Sehemu ya ujumbe wa Tanzania wanaoshiriki mkutano sita wa tume ya pamoja ya kudumu kwa ngazi ya wataalam

Ujumbe wa Tanzania

Sehemu nyingine ya ujumbe wa Tanzania wakati wa ufunguzi wa mkutano wa sita wa tume ya pamoja ya kudumu kati ya Tanzania na Burundi

Ujumbe wa Tanzania ukiwa kwenye mkutano

Sehemu ya ujumbe kutoka Tanzania wakifuatilia ufunguzi wa mkutano wa sita wa tume ya pamoja ya kudumu kati ya Tanzania na Burundi

Wajumbe wa Sekretarieti ya Mkutano 

Picha ya pamoja

 

Tuesday, March 2, 2021

MKUTANO WA SITA WA TUME YA PAMOJA KATI YA TANZANIA NA BURUNDI KUFANYIKA MKOANI KIGOMA

Tanzania na Burundi zimejipanga kuutumia Mkutano wa Sita wa Tume ya Pamoja ya Kudumu kama njia mojawapo ya kuhamasisha wananchi wa pande zote mbili kuchangamkia fursa mbalimbali za uchumi zinazopatikana katika nchi hizi ili kunufaika nazo.


Kauli hiyo imetolewa kwa pamoja na Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Brigedia Jenerali, Wilbert Ibuge na mwenzake kutoka Burundi, Mhe. Isidore Ntirampeba walipokutana na Waandishi wa Habari leo mjini Kigoma kwa ajili ya kuwajulisha kuhusu mkutano huo utakaofanyika mjini humo kuanzia tarehe 3 hadi 5 Machi 2021.


Balozi Ibuge alieleza kuwa, Tanzania na Burundi zimeendelea kuwa na ushirikiano wa kihistoria na kindugu kwa muda mrefu huku kila nchi ikinufaika kwa kiasi kikubwa na ushirikiano huo. Hata hivyo alieleza kuwa, bado upo umuhimu mkubwa wa kuendelea kuwahamasisha wananchi wa Tanzania na Burundi kuchangamkia fursa mbalimbali zinazopatikana kwenye nchi hizo ili ziwanufaishe kiuchumi. Fursa hizo ni pamoja na biashara na uwekezaji.


“Mikutano ya Tume za Pamoja za Kudumu pamoja na mambo mengine inaangalia namna ya kuhakikisha kila mwananchi kutoka nchi husika ananufaika na fursa zilizopo na jukumu letu ni kuendelea kuwahamasisha kuzichangamkia fursa hizo” alisema Balozi Ibuge.


Akizungumzia ukuaji wa sekta ya uchumi kati ya Tanzania na Burundi, Balozi Ibuge alisema pamoja na changamoto mbalimbali,  biashara kati ya Tanzania na Burundi imeendelea kukua mwaka hadi mwaka na kutoa mfano wa kipindi cha kuanzia mwaka 2015 hadi 2019 ambapo Tanzania na Burundi zilifanya biashara zenye thamani ya shilingi Bilioni 619.9 ukiwa ni  wastani wa Shilingi Bilioni 123.9 kwa mwaka.  Katika kiasi hicho, Tanzania iliuza nchini Burundi bidhaa zenye thamani ya shilingi bilioni 604.9 na Burundi iliuza Tanzania bidhaa zenye thamani ya Shilingi Bilioni 7.4.


Aidha, akizungumzia huduma ya wakimbizi, Balozi Ibuge alieleza kuwa, Tanzania imeendelea kuhifadhi wakimbizi kutoka Burundi huku Serikali ya Burundi ikiendelea kuwahimiza wakimbizi hao kurejea nchini kwao kwa hiari kutokana na kuimarika kwa hali ya amani na utulivu nchini humo.


“Tanzania imeendelea kuhifadhi wakimbizi kutoka Burundi, hata hivyo kutokana na kuimarika kwa hali ya amani na usalama nchini kwao Serikali yao imeendelea kuwahimiza kurejea ili kwenda kushiriki katika shughuli za ujenzi wa Taifa lao. Itakumbukwa kuwa, zoezi la kuwawezesha wakimbizi hao kurejea kwa hiari Burundi limeendelea kuratibiwa na Kamati ya Utatu inayojumuisha Tanzania, Burundi na Shirika la Kimataifa la Kuhudumia Wakimbizi (UNHCR) ambapo kati ya mwezi Septemba 2017 na Februari 2021, jumla ya wakimbizi 113,488 wamerejea nchini Burundi kwa hiari” alifafanua Balozi Ibuge.


Kwa upande wake Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje kutoka Burundi, Mhe. Isidore Ntirampeba alisema tume ya pamoja ya ushirikiano ni nyenzo muhimu katika kuimarisha ushirikiano baina ya nchi na nchi kwani hutoa nafasi kwa nchi mbili kutathmini mafanikio yaliyofikiwa kupitia ushirikiano uliopo, kutafuta suluhu kwa changamoto mbalimbali na kuainisha hatua imara zaidi za kufikia malengo kusudiwa. Alieleza kuwa, mikutano hii ni fursa nzuri kwa pande zote mbili kujipanga na kuboresha utendaji kulingana na mabadiliko mbalimbali yanayotokea duniani na katika nchi yakiwemo yale ya kisera na kimazingira.


Kadhalika, alitumia fursa hiyo kuishukuru na kuipongeza Tanzania na kuitaja kama nchi ya kupigiwa mfano katika kuhudumia wakimbizi wakiwemo wale wa kutoka Burundi ambao wamekuwa wakipokelewa tangu mwaka 1972. Aliongeza kuwa, Burundi inajivunia mchango wa Tanzania kwenye ustawi wa nchi hiyo na kwamba nchi hiyo inavutiwa na uongozi imara wa Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambao unalenga kuwaletea wananchi wote maendeleo.


Mkutano wa Sita wa Tume ya Pamoja ya Kudumu kati ya Tanzania na Burundi ambao unafanyika miaka 15 baada ya Mkutano wa Tano uliofanyika jijini Dar es Salaam mwaka 2006 unalenga kuendeleza, kuimarisha na kudumisha uhusiano na ushirikiano uliopo kati ya Tanzania na Burundi. Mkutano huu ambao utaanza kwa ngazi ya wataalam kutoka Tanzania na Burundi tarehe 3 Machi 2021utahitimishwa na Mkutano wa Mawaziri kutoka nchi hizo tarehe 5 Machi 2021.

=================================================================



Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Brigedia Jenerali Wilbert Ibuge akizungumza na Waandishi wa Habari (hawapo pichani) kuhusu Mkutano wa Sita wa Tume ya Pamoja ya Kudumu kati ya Tanzania na Burundi utakaofanyika mkoani Kigoma kuanzia tarehe 3 hadi 5 Machi 2021. Kushoto ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Burundi, Mhe. Isidore Ntirampeba.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje wa Burundi, Mhe. Ntirampeba akiwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda na Biashara wa Tanzania, Prof. Riziki Shemdoe (katikati) pamoja na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji wa Tanzania, Mhandisi Nadhifa Kemikimba wakiwa kwenye Mkutano kati ya Balozi Ibuge na Waandishi wa Habari kuhusu Mkutano wa Sita wa Tume ya Pamoja ya Kudumu kati ya Tanzania na Burundi utakaofanyika mkoani Kigoma kuanzia tarehe 3 hadi 5 Machi 2021.

Katibu Tawala wa Mkoa wa Kigoma, Mhe. Rashid Mchata (kushoto) na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Dkt. Jim Yonazi  wakiwa kwenye Mkutano kati ya Balozi Ibuge na Waandishi wa Habari kuhusu Mkutano wa Sita wa Tume ya Pamoja ya Kudumu kati ya Tanzania na Burundi utakaofanyika mkoani Kigoma kuanzia tarehe 3 hadi 5 Machi 2021.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje wa Burundi, Mhe. Isidore Ntirampeba naye akizungumza  wakati wa mkutano na Waandishi wa Habari kuhusu Mkutano wa Sita wa Tume ya Pamoja ya Kudumu kati ya Tanzania na Burundi utakaofanyika mkoani Kigoma kuanzia tarehe 3 hadi 5 Machi 2021.

Katibu Tawala wa Mkoa wa Kigoma, Mhe. Rashid Mchata naye akizungumza wakati wa mkutano na Waandishi wa Habari kuhusu Mkutano wa Sita wa Tume ya Pamoja ya Kudumu kati ya Tanzania na Burundi utakaofanyika mkoani Kigoma kuanzia tarehe 3 hadi 5 Machi 2021

Balozi wa Tanzania nchini Burundi, Mhe. Dkt. Jily Maleko akifuatilia  Mkutano kati ya Balozi Ibuge na Waandishi wa Habari kuhusu Mkutano wa Sita wa Tume ya Pamoja ya Kudumu kati ya Tanzania na Burundi utakaofanyika mkoani Kigoma kuanzia tarehe 3 hadi 5 Machi 2021

Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Afrika katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bw. Frank Mwega akifuatia Mkutano kati ya Balozi Ibuge na Waandishi wa Habari kuhusu Mkutano wa Sita wa Tume ya Pamoja ya Kudumu kati ya Tanzania na Burundi utakaofanyika mkoani Kigoma kuanzia tarehe 3 hadi 5 Machi 2021

Sehemu ya wadau kutoka sekta mbalimbali za Tanzania na Burundi walioshiriki mkutano kati ya Baloiz Ibuge na Waandishi wa Habari kuhusu Mkutano wa Sita wa Tume ya Pamoja ya Kudumu kati ya Tanzania na Burundi utakaofanyika mkoani Kigoma kuanzia tarehe 3 hadi 5 Machi 2021

Sehemuu nyingine ya wadau

Sehemu ya wadau wakifuatilia mkutano

Wadau wa Mkutano wa Sita wa Tume ya Pamoja ya Kudumu kati ya Tanzania na Burundi

Mkutano ukiendelea



 

Monday, March 1, 2021

PROF. KABUDI APOKEA NAKALA ZA HATI ZA UTAMBULISHO ZA MABALOZI WATEULE

 

Na Mwandishi wetu, Dar es Salaam

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamagamba John Kabudi (Mb) amekutana na kupokea nakala za hati za utambulisho za mabalozi wateule hapa nchini pamoja na hati ya utambulisho ya Konseli Mkuu wa China Zanzibar.

Mabalozi waliowasilisha nakala za hati za utambulisho kwa Prof. Kaabudi katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam ni Balozi mteule wa Namibia, Mhe. Lebbius Tangeni Tobias na Balozi mteule wa Ireland mhe. Mary O’Neil, pamoja na Konseli Mkuu wa China Zanzibar Mhe. Zhang Zhisheng.

Awali akiongea mara baada ya kupokea nakala ya hati ya utambulisho wa Balozi mteule wa Namibia, Prof. Kabudi amesema kuwa Tanzania na Namibia zimekubaliana kuendeleza kuimarisha sekta ya biashara na uwekezaji, mifugo na uvuvi katika bahari kuu pamoja madini kwa maslahi ya mataifa yote mawili.

“Tanzania na Namibia tuna historia inayofanana iliyoanza tangu vita vya ukombozi wa uhuru wa Namibia….wote tulikuwa makoloni ya Wajerumani, hivyo tumekubaliana kuimarisha sekta za biashara na uwekezaji, na katika maeneo ya mazao ya mifugo, uvuvi, kilimo, na madini, ambapo katika maeneo hayo Tanzania tunayo mengi ya kujifunza kutoka Namibia hasa katika sekta ya mifugo na uvuvi katika bahari kuu,hivyo tukiimarisha maeneo hayo uchumi wan chi zetu mbili utazidi kukua na kuimarika” Amesema Prof. Kabudi

Kwa upande wake Balozi Mteule wa Namibia hapa nchini, Mhe. Lebbius Tangeni Tobias ameahidi kuendeleza ushirikiano wa kidiplomasia uliopo kati ya Tanzania na Namibia.

“Mimi kama mwakilishi wa Serikali ya Namibia nitajitahidi wakati wa utumishi wangu hapa Tanzania kuhakikisha kuwa uhusiano wetu sisi Namibia na Tanzania unazidi kuimarika kwa maslahi mapana ya wananchi wetu wote,” Amesema Mhe. Tobias     

Kadhalika, Prof. Kabudi amepokea nakala ya hati za utambulisho wa Balozi mteule wa Ireland hapa nchini, Mhe. Mary O’Neil ambapo mara baada ya kukabidhi hati za utambulisho Balozi Mteule ameahidi kuendeleza uhusiano mzuri uliopo baina ya Tanzania na Ireland.

“Ni furaha kwangu kuwepo hapa leo na kukabidhi nakala ya hati ya utambulisho wangu hapa nchini Tanzania, napenda kuahidi kwa kipindi nitakachokuwa hapa nitahakikisha kuwa uhusiano wetu wa kidiplomasia unakuwa na kuimarika kwa maslahi ya mataifa yetu,” Amesema Balozi O’Neil

Kwa upande wake Prof. Kabudi amesema kuwa mahusiano ya kibalozi kati ya Tanzania na Ireland yalianza tangu mwaka 1979 ambapo Ireland ilianzisha utaratibu wa kutoa ufadhili wa masomo katika vyuo vikuu vya Ireland kwa watanzania katika taaluma mbalimbali.

“Mbali na kutoe ufadhili wa elimu kwa Watanzania, tumeongelea masuala ya kuimarisha ufadhili wa masomo, biashara na uwekezaji hasa kwa kutumia teknolojia ya habari pamoja na kuimarisha uvuvi wa bahari kuu na katika kipindi chake cha uwakilishi hapa nchini tutaangalia maeneo mapya ya ushirikiano ili tuweze kuendele kuimarisha ushirikiano baina yetu na Ireland,” Amesema Prof. Kabudi.

Katika tukio jingine, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamagamba John Kabudi (Mb) amekutana na kupokea hati ya utambulisho wa Konseli Mkuu wa China Zanzibar Mhe. Zhang Zhisheng.

Prof. Kabudi amesema kuwa China imekuwa ikiisaidia sana Zanzibar tangu mapinduzi ya mwaka 1964, katika maeneo mbalimbali kama vile ujenzi wa barabara, ujenzi wa shule, ukarabati wa uwanja wa ndege, hospitali ya Mnazi mmoja pamoja na Abdallah Mzee………na “tumekubaliana kuwa tutaendelea kuimarisha mahusiano kati ya China na Tanzania – Zanzibar ikiwa sehemu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,” Amesema Prof. Kabudi   

Nae Konseli Mkuu wa China Zanzibar amesema kuwa China kama taifa lililoendelea wataendelea kushirikiana na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika kuhakikisha mahusiano ya China na Tanzania yanaimarika kijamii, kisiasa na kiuchumi.

“China inaunga mkono umoja, amani na mshikamano wa Tanzania, sisi tumekuwa marafiki wa muda mrefu na tutaendelea kusaidiana ili kuhakikisha kuwa mahusiano kati ya China na Tanzania yanazidi kuimarika hasa katika kipindi hiki cha uongozi wa Rais Magufuli na Rais Mwinyi,” Amesema Mhe. Zhisheng 

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamagamba John Kabudi (Mb) akipokea nakala ya hati za utambulisho kutoka kwa Balozi mteule  wa Namibia, Mhe. Lebbius Tangeni Tobias leo katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam


Balozi mteule wa Ireland mhe. Mary O’Neil akimkabidhi nakala ya hati za utambulisho Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamagamba John Kabudi (Mb) katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamagamba John Kabudi (Mb) akipokea hati za utambulisho kutoka Konseli Mkuu wa China Zanzibar Mhe. Zhang Zhisheng