Friday, January 14, 2022

WAZIRI MULAMULA AWAHIMIZA MABALOZI KUTEKELEZA DIPLOMASIA YA UCHUMI

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Liberata Mulamula (Mb.) amewasisitiza mabalozi wa Tanzania wanaowakilisha nje ya nchi kuweka mpango kazi wa utekelezaji wa majukumu ya kidiplomasia wenye maslahi mapana kwa uchumi wa Taifa.

Mhe. Mulamula ameyasema hayo alipokutana kwa mazungumzo na Balozi wa Tanzania nchini Kuwait, Mhe. Said Shaibu Mussa aliyekuja kumuaga ofisisni kwake leo tarehe 14 Januari 2022 katika ofisi za Wizara, jijini Dodoma.

Mazungumzo baina ya wawili hao yalijikita katika kuangalia namna bora ya kuboresha utendaji wa ofisi za balozi za Tanzania sambamba na Wizara ili kuweza kutumia fursa zilipo kunufaisha Taifa.

“Nasisistiza balozi zetu kutekeleza majukumu kwa kuhakikisha fursa za kiuchumi zinawekewa msisistizo sambamba na mafanikio yanayopatikana yanatangazwa kikamilifu ili kuweza kuuhabarisha uuma namna ya kuzitumia fursa zinazopatikana”. Alisema Mhe. Waziri

Pia ameeleza umuhimu wa kufanya kazi kwa pamoja ili kuweza kufikia malengo tarajiwa katika sekta ambazo serikali ya Tanzania imeingia makubaliano ya ushirikiano na mataifa wanayowakilisha.

Naye Balozi Said Shaibu Mussa amemshukuru Mhe. Waziri kwa maelekezo ya kiteundaji aliyoyapata sambamba na kuahidi kufanya kazi kwa ubunifu katika majukumu hayo mapya ili kuongeza maeneo ya ushirikiano baina ya Tanzania na Kutwait.

Tanzania na Kuwaita zimekuwa zikishirikiana katika sekta za kilimo, afya, ujenzi wa miundombinu ya barabara na maji.

====================================

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Liberata Mulamula (kulia) amekutana kwa mazungumzo na Balozi wa Tanzania nchini Kuwait, Mhe. Said Shaibu Mussa alipokuja kumuaga ofisini kwake leo tarehe 14 Januari 2022 jijini Dodoma.

Mazungumzo yakiendelea. Kulia ni Msaidizi wa Waziri, Bw. Seif Kamtunda akifatilia mazungumzo.

Mhe. Waziri Mulamula akimkabidhi vitendea kazi Mhe. Said Mussa.



WAZIRI MULAMULA AMUAGA BALOZI WA MALAWI NCHINI

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Liberata Mulamula amekutana na Balozi wa Malawi nchini Mhe. Glad Chembe Munthali leo tarehe 14 Januari 2022 katika ofisi za Wizara jijini Dodoma .

Katika mazungumzo yao Mhe. Waziri Mulamula amempongeza Mhe. Munthali kwa kumaliza salama muda wake wa utumishi katika nafasi ya Balozi hapa nchini na amemtakia utumishi mwema katika majukumu mengine mapya atakayopangiwa.

"Serikali ya Tanzania itaendelea kutoa ushirikiano kwa Serikali ya Malawi kwakuwa ushirikiano wetu umejikita katika kuhakikisha maendeleo ya watu na Taifa yanapatikana katika pande zote mbili za ushirikiano'', alisema Waziri Mulamula.

Pia akaeleza miradi ya ushirikiano inayofanywa baina ya Tanzania na Malawi itaendelea kusimamiwa kwa karibu mpaka pale atakapoteuliwa mwakilishi mwingine kushika nafasi hiyo.

Naye Balozi Munthali alitumia nafasi hiyo kutoa shukurani zake pamoja na za Serikali ya Malawi akieleza kuwa miaka mitatu ya utumishi wake hapa nchini imekuwa ya mafanikio kufuatia ushirikiano uliotolewa na Serikali ya Tanzania katika kutekeleza majukumu yake.

"Tanzania kwangu ni nyumbani, sisi ni majirani na siku zote watu wetu wamekuwa na muingiliano kupitia shughuli za kiuchumi na kijamii", alisema Balozi Munthali

Pia, Mhe. Munthali alimpongeza Mhe. Waziri Mulamula kwa utaratibu mzuri uliowekwa na Wizara katika kuhakikisha taratibu zote za Mabalozi na Wawakilishi wa Kimataifa zinasimamiwa na kuruhusu utekelezaji wa majukumu yao.

Tanzania na Malawi zimekuwa zikishirikiana katika sekta ya ujenzi wa miundombinu, huduma za jamii, biashara na masoko. 

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Liberata Mulamula akizungumza na Balozi wa Malawi aliyemaliza muda wake hapa nchini Mhe.Glad Chembe Munthali. Viongozi hao wamekutana leo tarehe 14 Januari 2022 katika katika ofisi za Wizara jijini Dodoma .

Waziri Mulamula akimkabidhi zawadi ya picha Mhe. Munthali.
Picha ya Pamoja. Kulia ni Mkurugenzi Idara ya Afrika katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Naimi Azizi na kulia ni Afisa Mambo ya Nje, Bw. Ali Ubwa.

 

TANZANIA KUENDELEA KUSHIRIKIANA NA MISRI KATIKA KUBORESHA SEKTA YA AFYA

Serikali ya Tanzania imepokea tani 16 za Dawa, Vifaa Tiba na Vifaa Kinga ikiwa ni msaada wenye thamani ya shillingi milioni 864 kutoka Serikali ya Misri.

Akizungumza kwa niaba ya Serikali wakati wa hafla fupi ya kupokea shehena ya dawa hizo iliyofanyika hivi karibuni jijini Dar es Salaam, Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Prof.  Abel Makubi amesema Tanzania inaishukuru Serikali ya Misri kwa msaada huo muhimu kwa wananchi wa Tanzania na kwamba itandelea kuimarisha ushirikiano na Serikali ya Misri hususan katika kuboresha sekta ya afya na kuahidi kuusimamia kikamilifu msaada huo ili uwafikie walengwa kwa wakati.

Pia aliongeza kusema kuwa,  msaada huo umewasili wakati mwafaka ambao Tanzania inaendelea kuboresha sekta ya afya kwa kusogeza huduma za afya kwa wananchi pamoja na kuongeza upatikanaji wa Dawa na Vifaa Tiba katika maeneo ya mijini na vijijini.


Aidha, alipongeza ushirikiano wa kidiplomasia uliopo kati ya Tanzania na Misri ambao umekuwa wa manufaa makubwa tangu kuanzishwa kwake na kupongeza jitihada zinazofanywa na Mhe. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika kuboresha Sekta ya Afya nchini ambapo alisema msaada huo ni miongoni mwa matokeo ya ziara ya Mhe. Rais aliyoifanya nchini Misri mwezi Novemba, 2021.


"Kwa niaba ya Serikali ya Tanzania na pia kwa niaba ya Waziri wa Afya. Mhe. Ummy Mwalimu napokea msaada huu wa Dawa na Vifaa Tiba wenye thamani zaidi ya shilingi milioni 800 kutoka Serikali ya Misri. Kama Serikali, tunaendelea kuboresha na kusogeza huduma za afya kwa wananchi hivyo msaada huu utachangia jitihada hizo. Ninakuomba Mhe. Balozi ufikishe salamu zetu za shukrani kwa Mhe. Abdel Fattah Al-Sisi, Rais wa Misri kwa msaada huu ambao tumeupokea kwa dhati na utatimiza lengo lilokusudiwa la kuwasaidia wananchi wa Tanzania" alisema Dkt. Makubi.


Kwa upande wake, Balozi wa Misri hapa nchini. Mhe. Mohamed Gaber Mohamed Abulwafa amesema nchi yake itaendelea kushirikiana na Tanzania na inaunga mkono jitihada za Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi makini wa Mhe. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania za kuwaletea watanzania maendeleo kupitia sekta mbalimbali ikiwemo ya afya.


Kadhalika, Mhe. Balozi Abulwafa alieleza kuwa, mbali na ushirikiano wa Tanzania na Misri kwenye sekta ya afya, Nchi yake itaendelea kushirikiana na Tanzania katika kutoa fursa za mafunzo ya kuwajengea uwezo watu wa sekta ya afya na fani mbalimbali kwa watanzania.

Hafla hiyo ilihudhuriwa pia na Katibu Mkuu wa Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Dkt. Faraji Kasidi Mnyepe, Mganga Mkuu wa Serikali, Dkt. Aifelo Sichwale, Mfamasia Mkuu wa Serikali, Bw. Daudi Msasi, Kaimu Mkuu wa Itifaki katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bw. Celestine Kakele na Maafisa Waandamizi kutoka Serikalini.

 Balozi wa Misri hapa nchini, Mhe. Mohamed Gaber Mohamed Abulwafa (katikati) akimkabidhi Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Prof. Abel Makubi (wa pili kulia) msaada wa Dawa na Vifaa Tiba kutoka Serikali ya Misri. Wengine katika picha ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Dkt. Faraji Kasidi Mnyepe ( wa pili kushoto), Mganga Mkuu wa Serikali, Dkt. Aifelo Sichalwe (wa kwanza kushoto) na Mwambata Jeshi wa Ubalozi wa Misri, Brigedia Sherif Farag Mohamed (wa kwanza kulia). Hafla ya makabidhiano ya msaada huo imefanyika jijini dar es Salaam hivi karibuni.
Mhe. Balozi Abulwafa akimkabidhi Prof. Makubi huku viongozi wengine wakishuhudia. Kulia ni Kaimu Mkuu wa Itifaki na Mwakilishi wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bw. Celestine Kakele.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Prof. Abel Makubi kwa pamoja na Balozi wa Misri nchini, Mhe. Mohamed Gaber Mohamed Abulwafa wakisaini Hati ya Makabidhiano ya Dawa na Vifaa Tiba vilivyopokelewa nchini kutoka Misri
Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Prof. Abel Makubi kwa pamoja na Balozi wa Misri nchini, Mhe. Mohamed Gaber Mohamed Abulwafa wakibadilishana Hati ya Makabidhiano waliyosaini wakati wa mapokezi ya Dawa na Vifaa Tiba  kutoka Misri
Balozi wa Misri nchini, Mhe. Mohamed Gaber Mohamed Abulwafa akizungumza mara baada ya kukabidhi msaada wa Dawa na Vifaa Tiba  kkwa Serikali ya Tanzania
Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Prof. Abel Makubi akizungumza  kwa niaba ya Serikali mara baada ya kupokea msaada wa  Dawa na Vifaa Tiba  kutoka Misri
Viongozi wakiwa katika picha ya pamoja
Picha ya pamoja ya viongozi na wadau mbalimbali

Afisa Mambo ya Nje katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bibi Faith Masaka akibadilishana mawazo na Afisa kutoka Ubalozi wa Misri hapa nchini, Bw. Mahmoud Hamdy Khalifa wakati wa hafla ya makabidhiano ya Dawa na Vifaa Tiba kutoka Misri


























 

Thursday, January 13, 2022

WAZIRI MULAMULA APOKEA NAKALA ZA HATI ZA UTAMBULISHO KUTOKA KWA MABALOZI WATEULE WA SAUDI ARABIA, KOREA, INDONESIA NA MOROCCO NCHINI

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Liberata Mulamula (kulia) akipokea Nakala za Hati za Utambulisho kutoka kwa Balozi Mteule wa Ufalme wa Saudi Arabia, Mhe. Abdullah bin  Ali Alsheryan. Makabidhiano hayo yamefanyika katika ofisi za Wizara Jijini Dodoma. 
Mara baada ya makabidhiano viongozi hao walipata fursa ya kuzungumza juu ya kuendelea kuimarisha ushirikiano wa kidiplomasia uliopo baina ya mataifa hayo pamoja na kufungua maeneo mapya ya ushirikiano. 
Balozi Mulamula akimkaribisha Mhe.Abdullah bin  Ali Alsheryan katika ofisi za Wizara zilizopo mji wa Serikali, Mtumba Jijini Dodoma
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Liberata Mulamula (kulia) akipokea Nakala za Hati za Utambulisho kutoka kwa Balozi Mteule wa Jamhuri ya Korea, Mhe. Kim Sun Pyo. Makabidhiano hayo yamefanyika katika ofisi za Wizara Jijini Dodoma. 
Mara baada ya makabidhiano hayo Waziri Mulamula alimhakikishia Mhe.Kim Sun Pyo kuwa serikali ya Tanzania itampa ushirikiano wa kutosha katika kutekeleza majukumu yake mapya katika kipindi chake atakachohudumu nchini. Jamhuri ya Korea imekuwa ikishirikiana na Tanzania katika sekta za teknolojia ya mawasiliano, elimu, afya, utalii na ujenzi wa miundobinu.
Kutoka Kushoto ni Mkurugenzi wa Idara ya Asia na Australasia katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Ceasar Waitara na Afisa Mambo ya Nje, Bw. Halmeinsh Lunyumbu wakifuatilia mazungumzo. 

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Liberata Mulamula (kulia) akipokea Nakala za Hati za Utambulisho kutoka kwa Balozi Mteule wa Jamhuri ya Indonesia, Mhe. Triyogo Jatmiko. Makabidhiano hayo yamefanyika katika ofisi za Wizara Jijini Dodoma. 

Mhe. Balozi Mulamula na Mhe. Triyogo Jatmiko walijadili juu ya kuimarisha ushirikiano katika sekta za biashara na masoko, viwanda, elimu, utalii na kufungua fursa nyingine za kiuchumi kupitia ushirikiano imara wa kidiplomasia uliopo baina ya mataifa hayo.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Liberata Mulamula (kulia) akipokea Nakala za Hati za Utambulisho kutoka kwa Balozi Mteule wa Ufalme wa Morocco, Mhe.Zacharia El Guoumiri. Makabidhiano hayo yamefanyika katika ofisi za Wizara Jijini Dodoma. 

Mazungumzo baina ya Mhe.Balozi Mulamula na Mhe. Balozi Zacharia El Guoumiri yalijikita katika kuimarisha ushirikiano baiba ya Tanzania na Morocco hususani katika sekta za michezo, elimu, maendeleo ya jamii na kuinua ujasiliamali kwa lengo la kukuza viwanda ili kuweza kuwanufaisha wananchi mataifa yao. 

Mazungumzo yakiendelea, kulia ni Mkurugenzi wa Idara ya Afrika katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Naimi Azizi akifatilia mazungumzo hayo.

SADC YAKUBALIANA KUENDELEA KUISADIA MSUMBIJI KULINDA AMANI

Mkutano wa Dharura wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Asasi ya Ushirikiano katika Masuala ya Siasa, Ulinzi na Usalama ya Jumuiya ya SADC, Jamhuri ya Msumbiji na Nchi zinazochangia Vikosi katika Misheni ya SADC iliyoko nchini Msumbiji ulioanza jana tarehe 11 Januari 2022 nchini Malawi umemalizika leo tarehe 12 Januari 2022 ambapo Nchi wanachama wa SADC wamekubaliana kuendelea kuisaidia Jamhuri ya Msumbiji katika kuhakikisha Amani na usalama vinapatikana.  

Pamoja na mambo mengine, katika mkutano huo wa Wakuu wa Nchi na Serikali, wamekubaliana  kuendelea kujitolea kulinda amani na usalama nchini Msumbiji hasa katika Jimbo la Cabo Delgado licha ya nchi nyingi kuendelea kukabiliana na changamoto ya ugonjwa wa uviko 19.

Akifunga Mkutano huo leo, Rais wa Jamhuri ya Malawi na Mwenyekiti wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) Mhe. Lazarus Chakwera amewashukuru wakuuu wa Nchi na Serikali kwa Ushirikiano na umoja ambao nchi wanachama wa SADC wamekuwa wakionesha katika kuisaidia Jamhuri ya Msumbiji kupambana na ugaidi.

“Lazima tuungane kwa pamoja na kuhakikisha kuwa Jamhuri ya Msumbiji inakuwa na Amani na Usalama……hivyo basi ni jukumu letu sisi sote katika kuhakikisha wananchi wa Msumbiji wanakuwa na amani kwani bila amani hakuna maendeleo,” amesema Rais Chakwera.

Awali akisoma tamko la pamoja, Katibu Mendaji wa SADC Bw. Elias Magosi amesema Wakuu wa Nchi na Serikali wameipongeza SADC kwa dhamira yake isiyoyumba ya kusimamia na kutetea amani na usalama, na kwa kutumia rasilimali zake katika kushughulikia na kupambana na ugaidi katika jimbo la Cabo Delgado.

Mkutano huo pia umepongeza hatua ya mshikamano iliyooneshwa kwa ahadi za chakula zilizotolewa na Jamhuri ya Malawi, Afrika Kusini na Zimbabwe ili kupunguza matatizo yanayowakabili wakimbizi  katika Jimbo la Cabo Delgado nchini Msumbiji.

Rais wa Jamhuri ya Malawi na Mwenyekiti wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) Mhe. Lazarus Chakwera akifunga Mkutano wa Dharura wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Asasi ya Ushirikiano katika Masuala ya Siasa, Ulinzi na Usalama ya SADC, Jamhuri ya Msumbiji na Nchi zinazochangia Vikosi katika Misheni ya SADC Msumbiji 



Ujumbe wa Tanzania ukiongozwa na Makamu wa Rais Mhe. Dkt. Philip Mpango katika Mkutano wa Dharura wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Asasi ya Ushirikiano katika Masuala ya Siasa, Ulinzi na Usalama ya SADC, Jamhuri ya Msumbiji na Nchi zinazochangia Vikosi katika Misheni ya SADC Msumbiji 




Mkutano ukiendelea


Wakuu wa Nchi na Wawakilishi wa Wakuu wa nchi wakiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kumalizika kwa Mkutano wa Dharura wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Asasi ya Ushirikiano katika Masuala ya Siasa, Ulinzi na Usalama ya SADC, Jamhuri ya Msumbiji na Nchi zinazochangia Vikosi katika Misheni ya SADC Msumbiji 

Wednesday, January 12, 2022

BALOZI MBAROUK ATEMBELEA UBALOZI WA TANZANIA NCHINI MALAWI, KUKAGUA MALI ZA SERIKALI

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk ametembelea Ubalozi wa Tanzania nchini Malawi kwa lengo la kujionea utendaji kazi wa Ubalozi pamoja na kukagua mali za Serikali nchini humo.

Balozi Mbarouk mara baada ya kukagua mali za Serikali, aliushukuru Ubalozi kwa mapokezi mazuri na kusema kuwa kuna haja ya kuchukua hatua za makusudi kuendeleza kiwanja cha Serikali kwa kujenga jengo la Ubalozi na kitega uchumi. 

Kwa upande wake Balozi wa Tanzania nchini Malawi, Mhe. Benedicto Mashiba amemshukuru Mhe. Naibu wa Waziri – Nje kwa kutenga muda wa kutembelea Ofisi ya Ubalozi na kukagua mali za Serikali zilizopo Lilongwe, licha ya kuwa na ratiba ngumu ya Mkutano wa Dharura wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa SADC. 

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk akioneshwa kiwanja cha Serikali na Balozi wa Tanzania Nchini Malawi, Mhe. Benedicto Mashiba 

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk akikagua moja kati ya nyumba za Serikali zilizopo Lilongwe, nchini Malawi. Katika ukaguzi huo, Naibu Waziri ameambatana na Balozi wa Tanzania Nchini Malawi, Mhe. Benedicto Mashiba



Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk akisaini kitabu cha wageni mara baada ya kuwasili katika Ofisi za Ubalozi wa Tanzania Nchini Mawali na kupokelewa na Balozi wa Tanzania Nchini Malawi, Mhe. Benedicto Mashiba









BALOZI MBAROUK KATIKA MKUTANO WA DHARURA BARAZA LA MAWAZIRI SADC

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk ameshiriki katika Mkutano wa Dharura wa Baraza la Mawaziri wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) Jijini Lilongwe, nchini Malawi.

Mbali na Mkutano wa Dharura wa Wakuu wa Nchi na Serikali, pia  mkutano huo ulitanguliwa na kikao cha Kamati ya Fedha ya Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) kilichofanyika Jijini Lilongwe, nchini Malawi na kuhudhuriwa na Makatibu Wakuu wa Wizara mbalimbali kutoka nchi wanachama wa SADC. 

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk akishiriki katika Mkutano wa Dharura wa Baraza la Mawaziri wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) Jijini Lilongwe, nchini Malawi

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk katika Mkutano wa Dharura wa Baraza la Mawaziri wa SADC Jijini Lilongwe, nchini Malawi


Mkutano wa Baraza la Mawaziri wa SADC ukiendelea Jijini Lilongwe nchini Malawi
Mawaziri walioshiriki katika Mkutano wa Dharura wa Baraza la Mawaziri wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) wakiwa katika picha ya Pamoja mara baada ya kumalizika kwa mkutano wao uliofanyika Jijini Lilongwe, nchini Malawi 





BALOZI FATMA ASHIRIKI KIKAO KAMATI YA FEDHA SADC

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Fatma Rajab ameshiriki katika kikao cha Kamati ya Fedha ya SADC kilichofanyika Jijini Lilongwe, nchini Malawi. 

Kikao hicho kimetanguliwa na Mkutano wa Dharura wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Asasi ya Ushirikiano katika Masuala ya Siasa, Ulinzi na Usalama ya Jumuiya ya SADC, Jamhuri ya Msumbiji na Nchi zinazochangia Vikosi katika Misheni ya SADC iliyoko nchini Msumbiji ulioanza tarehe 11 Januari 2021 Lilongwe, Malawi.

Katika Mkutano wa Dharuar wa Wakuu wa Nchi na Serikali, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango alimwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan.

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Fatma Rajab katika kikao cha Kamati ya Fedha ya SADC kilichofanyika Jijini Lilongwe, nchini Malawi

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Fatma Rajab katika kikao cha Kamati ya Fedha ya SADC



Tuesday, January 11, 2022

DKT. MPANGO AMWAKILISHA RAIS SAMIA MKUTANO WA DHARURA MALAWI

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango amuwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan katika Mkutano wa Dharura Wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Asasi ya Ushirikiano katika Masuala ya Siasa, Ulinzi na Usalama ya Jumuiya ya SADC, Jamhuri ya Msumbiji na Nchi zinazochangia Vikosi katika Misheni ya SADC iliyoko nchini Msumbiji ulioanza leo tarehe 11 Januari 2022 Lilongwe, Malawi.

Awali akifungua Mkutano huo, Rais wa Afrika Kusini ambaye pia ni Mwenyekiti wa TROIKA Mhe. Cyril Ramaphosa amesisitiza umuhimu wa nchi wanachama kuiunga mkono Jamhuri ya Msumbiji katika Mapambano yake dhidi ya mashambulizi ya kigaidi yanayoikabili nchi hiyo hasa Katila jimbo la Cabo Delgado.

Aidha, Mhe. Ramaphosa ameongeza kuwa kuna umuhimu kwa SADC kushirikiana katika kuimarisha ulinzi na usalama ndani ya jumuiya hiyo.

Ujumbe wa Tanzania katika Mkutano huo wa dharura umeongozwa na Makamu wa Rais Dkt. Philip Mpango, Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk, Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Fatma M. Rajab, Kaimu Mkurugenzi Idara ya Ushirikiano wa Kikanda katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bw. Edward Komba pamoja na Maafisa wengine waandamizi wa Serikali.

 
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Philip Mpango akifuatilia Mkutano wa Dharura wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Asasi ya Ushirikiano katika Masuala ya Siasa, Ulinzi na Usalama ya Jumuiya ya SADC, Jamhuri ya Msumbiji na Nchi zinazochangia Vikosi katika Misheni ya SADC iliyoko nchini Msumbiji. Mkutano umefanyika Lilongwe Malawi. Kulia ni Naibu Waziri Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk.



Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Philip Mpango akiongoza ujumbe wa Tanzania katika ukumbi wa Mkutano wa Dharura wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Asasi ya Ushirikiano katika Masuala ya Siasa, Ulinzi na Usalama ya Jumuiya ya SADC, Jamhuri ya Msumbiji na Nchi zinazochangia Vikosi katika Misheni ya SADC iliyoko nchini Msumbiji leo Lilongwe, Malawi

Baadhi ya Ujumbe wa Tanzania, Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk na Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Fatma M. Rajab pamoja na Maafisa Waandamizi wa Serikali

Rais wa Jamhuri ya Malawi na Mwenyekiti wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) Mhe. Lazarus Chakwera akisalimiana na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Philip Mpango, pamoja na Waziri wa Mambo ya Nje na Bishara za Kimataifa wa Zimbabwe Balozi Frederick Shawa kabla ya kuanza kwa Mkutano wa Dharura wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Asasi ya Ushirikiano katika Masuala ya Siasa, Ulinzi na Usalama ya Jumuiya ya SADC, Jamhuri ya Msumbiji na Nchi zinazochangia Vikosi katika Misheni ya SADC iliyoko nchini Msumbiji. Mkutano umefanyika Lilongwe, Malawi.

Rais wa Jamhuri ya Malawi na Mwenyekiti wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) Mhe. Lazarus Chakwera akisalimiana na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Philip Mpango muda mfupi kabla ya kuanza kwa Mkutano wa Dharura wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Asasi ya Ushirikiano katika Masuala ya Siasa, Ulinzi na Usalama ya Jumuiya ya SADC, Jamhuri ya Msumbiji na Nchi zinazochangia Vikosi katika Misheni ya SADC iliyoko nchini Msumbiji, Lilongwe, Malawi
Wakuu wa Nchi na Wawakilishi wa Wakuu wa Nchi walioshiriki katika Mkutano wa Dharura wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Asasi ya Ushirikiano katika Masuala ya Siasa, Ulinzi na Usalama ya Jumuiya ya SADC, Jamhuri ya Msumbiji na Nchi zinazochangia Vikosi katika Misheni ya SADC iliyoko nchini Msumbiji wakiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kufunguliwa kwa Mkutano huo leo Lilongwe, Malawi

Friday, January 7, 2022

BALOZI SHIYO AWASILISHA HATI ZA UTAMBULISHO KWA RAIS WA ETHIOPIA

Balozi wa Tanzania nchini Ethiopia na Mwakilishi wa Kudumu katika Umoja wa Afrika na Kamisheni ya Umoja wa Mataifa ya Uchumi Afrika (UNECA) Mhe. Innocent Eugene Shiyo amewasilisha Hati za Utambulisho Januari, 5 2022 kwa Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Shirikisho la Ethiopia Mheshimiwa Sahle- Work Zewde Ikulu Ethiopia.

Katika mazungumzo yao, Mheshimiwa Rais Zewde alimkaribisha Balozi Shiyo nchini Ethiopia na kumpongeza kwa kuteuliwa kuiwakilisha Tanzania nchini Ethiopia. Aidha, alisifia mahusiano na ushirikiano mzuri uliopo kati ya Tanzania na Ethiopia uliojengwa na waasisi wa mataifa haya mawili, Hayati Baba wa Taifa, Julius Nyerere na Mfalme Haile Selassie, ambao walifanya kazi pamoja kuanzisha Umoja wa Afrika.
Aidha, Rais Zewde aliishukuru Tanzania kwa kuendelea kuunga mkono Ethiopia kwenye masuala mbalimbali ya kikanda na kimataifa ikiwemo kwenye suala la matumizi ya maji ya Mto Nile chini ya ushirikiano wa Nchi za Bonde la Mto Nile. 
Vilevile, Mheshimiwa Rais Zewde aliipongeza Tanzania kwa kuendelea kuunga mkono jitihada zinazofanywa na Serikali ya Ethiopia za kuhakikisha changamoto za usalama nchini Ethiopia zinapata ufumbuzi. Pia, amemuahidi Mhe. Balozi Shiyo ushirikiano wa kutosha katika kutekeleza majukumu yake wakati wote atakapokuwepo nchini Ethiopia. 
Kwa upande wake, Mhe. Balozi Shiyo aliishukuru Serikali ya Ethiopia kwa mapokezi na ukarimu alioupata tangu kuwasili kwake nchini Ethiopia tarehe 26 Novemba, 2021. Aidha, aliwasilisha Salamu za heri kutoka kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwenda kwa Mheshimiwa Sahle- Work Zewde, Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Shirikisho la Ethiopia.
Aidha, Mhe Balozi Shiyo alirejea mafanikio ya ziara ya Mhe. Rais Sahle-Work Zewde aliyoifanya nchini Tanzania mwezi Januari 2021 ambapo nchi zote mbili zilikubaliana kuimarisha ushirikiano kwenye maeneo mbalimbali ikiwemo biashara na uwekezaji, uchukuzi, nishati, mifugo na bidhaa za Ngozi, utalii, uhamiaji na ulinzi na usalama. 
Balozi Shiyo ameahidi kuendelea kufanya kazi kwa bidii ili kuimarsha ushirikiano kati ya nchi hizi mbili kwenye maeneo hayo na maeneo mengineyo yenye manufaa kwa pande zote mbili.  Balozi Shiyo pia ameongelea kuhusu suala la kuanza kufundisha lugha ya Kiswahili kwenye Chuo Kikuu cha Addis Ababa kupitia ushirikiano kati ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na Chuo Kikuu cha Addis Ababa.
Balozi Shiyo amemhakikishia Mheshimiwa Rais Zewde kwamba Tanzania itaendelea kuunga mkono Ethiopia kwenye jithada za kurejesha amani na usalama nchini humo. 
Balozi wa Tanzania nchini Ethiopia na Mwakilishi wa Kudumu katika Umoja wa Afrika na Kamisheni ya Umoja wa Mataifa ya Uchumi Afrika (UNECA) Mhe. Innocent Shiyo akiwasilisha hati za Utambulisho kwa Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Shirikisho la Ethiopia Mheshimiwa Sahle- Work Zewde

Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Shirikisho la Ethiopia Mheshimiwa Sahle- Work Zewde akimsikiliza Balozi wa Tanzania nchini Ethiopia na Mwakilishi wa Kudumu katika Umoja wa Afrika na Kamisheni ya Umoja wa Mataifa ya Uchumi Afrika (UNECA) Mhe. Innocent Shiyo mara baada ya kuwasilisha Hati za Utambulisho 

Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Shirikisho la Ethiopia Mheshimiwa Sahle- Work Zewde katika picha ya pamoja na Balozi wa Tanzania nchini Ethiopia na Mwakilishi wa Kudumu katika Umoja wa Afrika na Kamisheni ya Umoja wa Mataifa ya Uchumi Afrika (UNECA) Mhe. Innocent Shiyo  

Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Shirikisho la Ethiopia Mheshimiwa Sahle- Work Zewde na Balozi wa Tanzania nchini Ethiopia na Mwakilishi wa Kudumu katika Umoja wa Afrika na Kamisheni ya Umoja wa Mataifa ya Uchumi Afrika (UNECA) Mhe. Innocent Shiyo katika picha ya pamoja na baadhi ya maafisa waliohudhuria hafla ya kuwasilisha Hati za Utambulisho