Friday, April 15, 2022

DIASPORA AWAVUTIA WATAFITI WA MALIGHAFI ZA UJENZI WA CHUO KIKUU CHA DAR ES SALAAM

Mtanzania anayeishi nchini Canada, ambaye ameonesha nia ya kuwekeza katika ujenzi wa miundombinu ya barabara nchini, Bw. Joseph Katallah amewavutia watafiti wa malighafi za ujenzi ambao ni wahadhiri katika fani za kemia, mazingira, sayansi na uhandisi wa raslimali za ujenzi kutoka Kampasi mbalimbali za Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM). 

Haya yamejiri leo terehe 14 Aprili 2022 wakati wa kikao kilichoongozwa na Kaimu Mkurugenzi wa Kitengo cha Diaspora katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bi. Tagie Daisy Mwakawago katika Ofisi ndogo ya Wizara jijini Dar es Salaaam. Kikao hicho kilitokana na ombi la watafiti hao kutaka kukutanishwa na Diaspora huyo ambaye ameleta teknolojia ya “geopolymer” inayoweza kutumika katika ujenzi wa barabara.

Watalaamu hao kutoka UDSM wamejikita katika kutafiti malighafi za udongo wa mfinyanzi (clay), miamba madini, hewa ya ukaa (CO2) na taka za viwandani na sekta ya kilimo ambazo wanazitumia kuzalisha bidhaa na vifaa mbalimbali vya ujenzi bila kuhusisha matumizi ya saruji (Portland cement). Teknolojia hiyo ambayo ni asili ya “geopolymer” imepata mapokezi mazuri miongoni mwa wataalamu wa sekta ya ujenzi kupitia uwekezaji wa Bw. Katallah, inatajwa kuwa ni rafiki wa mazingira, inazalisha bidhaa za bei nafuu, zinazodumu kwa muda mrefu zikiwa pia na uwezo wa kukabiliana na madhara ya chumvi na fangasi vinayoathiri majengo mengi yaliyojengwa kwa saruji.

Akizungumza katika kikao hicho kwa niaba ya timu ya watafiti wenzake, Dkt. Aldo Kitalika ambaye pia aliongoza ujumbe wa Wataalamu hao kwenye mazungumzo, alieleza jinsi alivyovutiwa na uzoefu na ujuzi wa Bw. Katallah katika sekta ya ujenzi na kueleza utayari wao wa kushirikiana naye kupitia tafiti ili kuongeza tija zaidi katika sekta ya ujenzi. 

“Tumevutiwa sana na teknolojia ya geopolymer ambayo kimsingi ni sehemu ya tafiti zetu tulizozifanya kwa kupima aina tofauti za malighafi za ujenzi ikiwemo udongo wa mfinyanzi (clay), madini ujenzi na taka za mimea kutoka maeneo mbalimbali ya nchi yetu kama vile mikoa ya Iringa, Njombe, Dodoma, Pwani, Manyara, Kilimanjaro, Mwanza, Ruvuma, Tanga, Morogoro na mingine mingi.” amesema Dkt. Kitalika.

Timu hiyo ya watafiti ilionesha wasilisho lenye bidhaa kifani (prototypes) kama vile matofali ya ujenzi wa aina mbalimbali, matofali yanayohimili joto kali (refractory bricks), vigae (tiles), vyungu vya maua, vyungu kwa ajili ya matumizi ya viwandani (crucibles), na meza za jikoni (kitchen counter tops).

Bw. Katallah amekuwa nchini kwa wiki kadhaa kwa madhumuni ya uwekezaji kwa kushirikiana na Kampuni ya Geopolymer Solutions LLC ya nchini Marekani inayomilikiwa na Bw. Rodney Zubrod, ambaye ni mbunifu wa teknolojia ya geopolymer.Teknolojia hiyo hutumia mabaki ya uchafu wa viwanda na migodi yenye kutengeneza alumina na vioo. Uchafu huo hujulikana kitaalamu kama matope mekundu.

Umoja wa watafiti hao unaundwa na Dkt. Aldo Kitalika (DUCE), Dkt. Makungu Madirisha (Mwalimu Nyerere, Mlimani), Bw. Said Abeid (MRI, Dodoma), Dkt. Regina Mtei (Mwalimu Nyerere, Mlimani), Dkt. Petro Mabeyo (DUCE), Dkt. Silvia Mushi (DUCE) na Dkt. Elianaso Elimbinzi (MUCE). 

Mazungumzo hayo ni sehemu ya muendelezo wa utekelezaji wa mikakati ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kupitia Kitengo cha Diaspora ya kuhamasisha Diaspora wenye malengo ya kuwekeza katika sekta mbalimbali nchini ili kutekeleza diplomasia ya uchumi.


Kaimu Mkurugenzi wa Kitengo cha Diaspora katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Bi. Tagie Daisy Mwakawago akisitiza jambo kwenye kikao kilichoratibiwa na Wizara baina ya Bw. Joseph Katallah (Mwekezaji, Mtanzania anayeishi nchini Canada na ) na timu ya watafiti kutoka UDSM kilichofanyika katika ofisi ndogo ya Wizara jijini Dar es Salaaam.
Timu ya watafiti kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam wakifuatalia mada iliyokuwa ikitolewa na Daipora (Mtanzania anayeishi nchini Canada) Bw. Joseph Katallah (hayuko pichani) kwenye mazungumzo yaliyofanyika katika ofisi ndogo ya Wizara jijini Dar es Salaaam.
Mazungumzo yakiendelea
Bw. Joseph Katallah Mtanzania anayeishi nchini Canada akifafanua jambo wakati wa mazungumzo na Timu ya watafiti kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (hawapo pichani) yaliyofanyika katika ofisi ndogo ya Wizara jijini Dar es Salaaam.
Kaimu Mkurugenzi wa Kitengo cha Diaspora katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Bi. Tagie Daisy Mwakawago (watano kushoto) na Bw. Joseph Katallah (wane kulia) Mtanzania anayeishi nchini Canada na Timu ya watafiti kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam wakiwa katika picha ya pamoja. Waengine (wapili na watatu kulia) ni Maafisa wa Kitengo cha Diaspora
Dkt. Madirisha Makungu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam akisisitiza jambo wakati wa mazungumzo baina ya timu ya watafiti ya UDSM na Bw. Joseph Katallah yaliyofanyika katika ofisi ndogo ya Wizara jijini Dar es Salaaam.

Thursday, April 14, 2022

Balozi Mbega Awataka Wafanyabiashara wa India kuwekeza Tanzania

Balozi wa Tanzania nchini India, Mhe. Anisa Mbega ametoa wito kwa wafanyabiashara wa nchi hiyo kuja kuwekeza Tanzania kwenye sekta mbalimbali za uwekezaji.       


Alitoa wito huo katika kongamano kubwa la biashara na uwekezaji (Tanzania India Trade Conference) lililofanyika katika jiji la Chennai, India tarehe 11 na 12 Aprili 2022.


Kongamano hilo lililoandaliwa kwa ushirikiano kati ya Ubalozi wa Tanzania nchini India na Taasisi ya Uchumi na Biashara ya India (Indian Economic Trade Organization) lilitoa fursa kwa taasisi mbalimbali zinazohusika na masuala ya uwekezaji na biashara ikiwepo Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC), Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TANTRADE), na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kuwasilisha mada kuhusu fursa za uwekezaji zinazopatikana nchini.


Balozi Mbega alisema licha ya India kuwekeza nchini mtaji wa kiasi cha Dola za Marekani Bilioni 3.7 na kuifanya nchi hiyo kuwa ya tano kwa uwekezaji, lakini bado nchi hiyo ina fursa kubwa ya kuongeza uwekezaji wake nchini.


Kongamano hilo lilihudhuriwa na wafanyabiashara na wawekezaji takribani 110 ambapo waliweza kufahamishwa fursa za biashara kwa bidhaa za mazao ya kilimo, mifugo na uvuvi na fursa za uwekezaji katika sekta za Miundombinu, Madini, Ujenzi wa majumba, viwanda vya madawa, mitambo ya viwandani, nguo, Elimu na Afya.


Kutokana na kongamano hilo, tayari wawekezaji mbalimbali wa India wameonesha nia ya kuwekeza nchini Tanzania ambapo kundi la kwanza la wawekezaji kwenye sekta ya ujenzi wa viwanda vya madawa ya binadamu na vifaa tiba kutoka India, linatarajiwa kutembelea Tanzania kuanzia tarehe 19 Aprili 2022 ili kukutana na wadau na kuanza taratibu za kuwekeza Tanzania.


Wafanyabiashara wengine walioshiriki Kongamano hilo wameonesha nia ya kushiriki maonesho ya 46 ya biashara ya kimataifa ya Dar es Salaam ambayo  yataanza tarehe 28 Juni hadi 13 Julai 2022. Ushiriki huo utawawezesha kukutana na wafanyabiashara na kuona bidhaa zinazozalishwa nchini Tanzania.


Kupitia kongamano hilo, wazalishaji wa bidhaa za Ngozi na korosho wa Tanzania wameunganishwa na wafanyabiashara wa India ambapo watapata fursa ya kuuza bidhaa hizo katika soko la India.


Sambamba na kongamano hilo, Ubalozi pia ulishiriki katika hafla ya uzinduzi wa ofisi ya uhamasishaji na uratibu wa biashara na uwekezaji inayojulikana kwa jina la INDIA TANZANIA TRADE COMMISSION (ITTC) iliyopo katika jengo laJJ Diamonds Mart No. 85, Barabara ya Gopathi Narayanas wani Chetty Chennai katika eneo la Thyagaraya Nagar ambalo ni kitovu cha biashara jijini Chennai. Ofisi hiyo itaongozwa na kusimamiwa na Dkt. J. Shrenik Naharkama Kamishna wabiashara wa ITTC.


Uwepo wa ITTC utasaidia kwa kiasi kikubwa upatikanaji wa haraka wa taarifa sahihi za biashara na uwekezaji zilizopo nchini Tanzania, kwa kuwa ITTC itakuwa na mawasiliano ya moja kwa moja na taasisi zinazosimamia masuala ya biashara na uwekezaji za nchini Tanzania.

Balozi wa Tanzania nchini India, Mhe Anisa Mbega akifungua Kongamano la biashara na uwekezaji kati ya Tanzania na India Jijini Chennai, India.


Baadhi ya washiriki wa Kongamano la biashara na uwekezaji kati ya Tanzania na India wakifuatilia matukio mbalimbali wakati wa kongamano hilo.

Mada kuhusu fursa zilizopo nchini Tanzania

Picha ya pamoja
Balozi wa Tanzania nchini India, Mhe Anisa Mbega akiweka Saini kitabu cha wageni alipowasili katika hafla ya ufunguzi rasmi wa ofisi ya uratibu wa biashara na uwekezaji  ITTC
Balozi wa Tanzania nchini India, Mhe. Anisa Mbega akikata utepe na kuwasha mshumaa kuashiria uzinduzi rasmi wa ofisi ya uratibu wabiashara na uwekezaji ITTC.

Balozi wa Tanzania nchini India, Mhe Anisa Mbega akiongoza kikao baada ya uzinduzi rasmi wa ofisi ya uratibu wa biashara na uwekezaji ITTC


Balozi wa Tanzania nchini India, Mhe Anisa Mbega akiwa katika picha ya pamoja na wadau wa masuala ya biashara na uwekezaji kutoka Tanzania na India katika hafla ya uzinduzi rasmi wa ofisi ya uratibu wabiashara na uwekezaji ITTC

Wednesday, April 13, 2022

MHESHIMIWA RAIS SAMIA AELEKEA NCHINI MAREKANI KWA ZIARA YA KIKAZI


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan akiagana na Makamu wa Rais Dkt. Philip Mpango katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) jijini Dar es salaam wakati akielekea nchini Marekani kwa ziara ya kikazi.

Akiwa nchini Marekani Mheshimiwa Rais Samia anatarajiwa kushiriki zoezi la uzinduzi wa Filamu ya Royal Tour unaotarajiwa kufanyika tarehe 18 Aprili 2022 New York. 

TANZANIA, UAE ZASAINI MAKUBALIANO KUIMARISHA USHIRIKIANO

Na Mwandishi Wetu, Dar

Serikali ya Tanzania na Umoja wa Falme za Kiarabu (U.A.E), zimesaini Makubaliano ya Tume ya Kudumu ya Pamoja katika nyanja za forodha, elimu, kilimo, nishati, mawasiliano, ulinzi na usalama. 

Makubaliano hayo yamesainiwa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula na Waziri wa Nchi wa UAE, Shakhbout bin Nahyan Al Nahyan katika Mkutano wa Tume ya Kudumu ya Pamoja kati ya Tanzania na UAE leo Jijini Dar es Salaam

Akizungumza katika hafla hiyo iliyotanguliwa na kikao cha Makatibu Wakuu, Waziri Mulamula amesema kusainiwa kwa makubaliano hayo ni ishara tosha ya kunaimarika zaidi kwa ushirikiano baina ya mataifa hayo mawili.

"Kusainiwa kwa makubaliano hayo kunatoa fursa kati ya Serikali ya Tanzania na Umoja wa Falme za Kiarabu kuendeleza biashara na uwekezaji ,” amesema Balozi Mulamula 

Kwa upande wake Waziri wa nchi wa UAE Mhe. Sheikh Shakhboot Nahyan Al Nahyan amesema ni faraja kwa kwa kusainiwa kwa makubaliano hayo kwani wamesubiri kwa muda, na kilicho bakia ni utekelezaji wa maeneo waliyokubaliana kwa maslahi ya mataifa yote.

“Natumaini yale tuliyozielekeza chemba za biashara za pande zote mbili kuhakikisha kuwa zinashirikiana zaidi katika kuboresha zaidi mazingira ya bishara na uwekezaji kwa maslahi ya pande zote mbili,” amesema Mhe. Al Nahyan

"Baada ya kusainiwa kwa makubaliano haya tumedhamiria kuanza kuongeza maeneo ya ushirikiano baina yetu katika sekta za elimu, nishati, kilimo, biashara na mawasiliano,"amesema Al Nahyan.

Awali, akiwasilisha hotuba yeke, Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Fatma Rajab amesema kusainiwa kwa makubaliano ya Tume ya Kudumu ya pamoja kati ya Tanzania na UAE ni wazi kuwa ushirikiano baina ya Tanzania na UAE utazidi kuimarika zaidi.

“Pamoja na mambo mengine, kikao cha Makatibu Wakuu tumejadili na kukubaliana kuongeza ushirikiano katika nyanja za biashara na uwekezaji, mawasiliano, usafirishaji pamoja na ulinzi na usalama……kusainiwa kwa makubaliano haya kunaakisi ishara nzuri ya kuendeleza ushirikiano baina yetu,” amesema Balozi Fatma   

Naye Balozi wa Tanzania katika Umoja wa Nchi za Falme za Kiarabu (UAE) Balozi Mohammed Mtonga amebainisha fursa mbalimbali zinazopatika katika Falme za Kiarabu ikiwa ni pamoja na masoko ya matunda, nyama na korosho.

Mkutano wa Tume ya Kudumu ya Pamoja kati ya Tanzania na UAE ulifanyika mwaka 2016.



Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula akiwasilisha hotuba yake katika Mkutano wa Tume ya Kudumu ya Pamoja kati ya Tanzania na UAE leo Jijini Dar es Salaam

Waziri wa Nchi wa UAE, Shakhbout bin Nahyan Al Nahyan akiwasilisha hotuba yake katika Mkutano wa Tume ya Kudumu ya Pamoja kati ya Tanzania na UAE uliofanyika leo Jijini Dar es Salaam


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula akibadilisha mkataba wa makubaliano na Waziri wa Nchi wa UAE, Shakhbout bin Nahyan Al Nahyan mara baaya ya wawili hao kumaliza kusaini mikataba hiyo

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Fatma Rajab akibadilisha mkataba wa makubaliano na Balozi wa Umoja wa Falme za Kiarabu nchini Mhe. Khalifa Abdulrahman Mohamed Al-Marzooqi mara baada ya kusainiwa kwa makubaliano hayo katika kikao cha ngazi ya Makatibu Wakuu uliofanyika Jijini Dar es Salaam


Mawaziri, Mabalozi na Makatibu wakuu wakiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kumalizika kwa mkutano



TANZANIA NA MOROCCO KUFUNGUA MILANGO YA USHIRIKIANO KATIKA MASUALA YA DIASPORA

Nchi za Tanzania na Morocco zimeanza kuangazia namna ya kushirikiana katika masuala ya Diaspora. Haya yamejiri kwenye mazungumzo yaliyofanyika leo tarehe 13 Aprili 2022 baina ya Kaimu Mkurugenzi wa Kitengo cha Diaspora katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Bi. Tagie Daisy Mwakawago na Balozi wa Ufalme wa Morocco nchini Tanzania Mheshimiwa Zakaria El Guomiri katika Ofisi ndogo ya Wizara jijini Dar es Salaam. 

Katika hatua ya awali ya kuanzisha ushirikiano huo wamegusia kuanzisha jukwaa la pamoja litakalowakutanisha pamoja Diaspora wa Tanzania na Morocco ili waweze kubadilishana uzoefu, ujuzi na kunufaika na fursa zinazopatikana katika nchi zote mbili.

Bi. Mwakawago katika mazungumzo hayo amebainisha kuwa amevutiwa na hatua iliyofikiwa na Ufalme wa Morocco katika kushughulikia masuala ya Diaspora. “Nimevutiwa sana na namna mnavyofanya vizuri kwenye kushirikisha Diaspora wenu katika kuchangia pato la nchi. Natambua kuwa Daispora wenu wanachangia takribani asilimia 6 ya jumla ya pato la nchi ni hatua nzuri sana, bila shaka tukishirikiana vyema katika eneo hili itakuwa ni fursa nzuri kwetu kuendelea kujifunza na hatimaye nchi zetu zitanufaika zaidi kutokana na kuongezeka kwa uwigo wa fursa miongoni mwa Diaspora wetu” Alisema Bi. Tagie Daisy.


Kwa upande wake Balozi wa Morocco nchini Tanzania Mhe. Guomiri, amepongeza jitihada mbalimbali zinazoendelea kufanywa na Serikali ya Tanzania katika kutatua changamoto mbalimbali zinazowakabili Diaspora. Ameongeza kuwa jitihada hizo ndizo zilizomsukuma kufanya mazungumzo na Kaimu Mkurugenzi wa Diaspora Bi. Tagie Daisy ili aweze kutoa uzoefu na mchango wa mawazo ambao utasaisaidia zaidi Serikali kunufanika na mchango wa Diaspora katika kuendeleza uchumi wa nchi. “Morocco tumefanikiwa kutumia programu mbalimbali ambazo zimetusaidia kutuweka karibu na kuwaunganisha Diaspora wetu wapatao milioni 6 waliopo sehemu mbalimbali duniani. Hutua hii imetusaidia kuendelea kunufaika na mchango wao katika kukuza uchumi wa Nchi. Nimefurahi kupata fursa ya kuongea na Kaimu Mkurugenzi Bi. Tagie Daisy ambapo tumepata fursa ya kuangalia namna mbalimbali ya kushirikiana katika eneo hili” Amesema Balozi Guomiri. 

Ushirikiano baina Tanzania na Morocco katika masuala ya Diaspora na kuanzishwa kwa jukwaa la kuwaleta pamoja Diaspora wa pande hizi mbili kuchochea ukuaji wa biashara na uwekezaji nchini. 
Bi. Tagie Daisy Mwakawago, Kaimu Mkurugenzi wa Kitengo cha Diaspora katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki akisalimiana na Mhe. Zakaria El Guomiri Balozi wa Ufalme wa Morocco nchini Tanzania walipokutana kwa mazungumzo katika Ofisi ndogo ya Wizara jijini Dar es Salaam
Kaimu Mkurugenzi wa Kitengo cha Diaspora katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Bi. Tagie Daisy Mwakawago akielezea jambo wakati wa mazungumzo na Balozi wa Ufalme wa Morocco nchini Tanzania Mhe. Zakaria El Guomiri yaliyofanyika katika Ofisi ndogo ya Wizara jijini Dar es Salaam.
Kaimu Mkurugenzi wa Kitengo cha Diaspora katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Bi. Tagie Daisy Mwakawago akisitiza jambo wakati wa mazungumzo na Balozi wa Ufalme wa Morocco nchini Tanzania Mhe. Zakaria El Guomiri yaliyofanyika katika Ofisi ndogo ya Wizara jijini Dar es Salaam.
Balozi wa Ufalme wa Morocco nchini Tanzania Mhe. Zakaria El Guomir akifafanua jambo wakati wa mazungumzo na Kaimu Mkurugenzi wa Kitengo cha Diaspora katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Bi. Tagie Daisy Mwakawago yaliyofanyika katika Ofisi ndogo ya Wizara jijini Dar es Salaam.
Mazungumzo yakiendelea
Kaimu Mkurugenzi wa Kitengo cha Diaspora katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Bi. Tagie Daisy Mwakawago (watatu kulia) na Balozi wa Ufalme wa Morocco nchini Tanzania Mhe. Zakaria El Guomir (watatu kushoto) wakiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya maafisa wa Ubalozi wa Morocco na Kitengo cha Diaspora.

BALOZI KATTANGA AKUTANA NA WAZIRI WA NCHI WA U.A.E

Na Mwandishi Wetu, Dar 

Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Hussein Kattanga amekutana na kufanya mazungumzo na Waziri wa nchi Umoja wa Falme za Kiarabu (U.A.E) Mhe. Sheikh Shakhboot Nahyan Al Nahyan, Ikulu Jijini Dar es Salaam.

Balozi Kattanga amekutana na ugeni huo kwa niaba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Sulluhu Hassan. Viongozi hao pamoja na mambo mengine, wamejadili masuala mbalimbali ya kuimarisha ushirikiano baina ya Tanzania na Umoja wa Falme za Kiarabu (U.A.E) katika nyanja za biashara na uwekezaji pamoja na Ulinzi na Usalama.

Balozi Kattanga amemhakikishia Waziri huyo kuwa Tanzania inayo mazingira mazuri ya biashara na salama kuwekeza. 

Kwa upande wake Waziri wa Nchi wa Umoja wa Falme za Kiarabu, Mhe. Sheikh Shakhboot Nahyan Al Nahyan ameishukuru Serikali ya Tanzania kwa ushirikiano ambao imekuwa ikiutoka kwa Umoja huo wakati wote.

Waziri wa Nchi wa Umoja wa Falme za Kiarabu, Mhe. Sheikh Shakhboot Nahyan Al Nahyan amewasili nchini leo kuja kushiriki Mkutano wa Tume ya Pamoja ya Kudumu kati ya Tanzania na Umoja wa Falme za Kiarabu.

Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Hussein Kattanga akimsikiliza Waziri wa nchi wa Umoja wa Falme za Kiarabu (U.A.E) Mhe. Sheikh Shakhboot Nahyan Al Nahyan, wakiwa katika mazungomzo yaliyofanyika Ikulu Jijini Dar es Salaam

Waziri wa nchi wa Umoja wa Falme za Kiarabu (U.A.E) Mhe. Sheikh Shakhboot Nahyan Al Nahyan, akieleza jambo wakati wa mazungumzo baina yake na Katibu Mkuu Kiongozi Balozi Hussein Kattanga, Ikulu Jijini Dar es Salaam

Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Hussein Kattanga akimueleza jambo Waziri wa nchi wa Umoja wa Falme za Kiarabu (U.A.E) Mhe. Sheikh Shakhboot Nahyan Al Nahyan (hayupo pichani), wakati wa mazungomzo yaliyofanyika Ikulu Jijini Dar es Salaam

Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Hussein Kattanga katika picha ya pamoja na Waziri wa nchi wa Umoja wa Falme za Kiarabu (U.A.E) Mhe. Sheikh Shakhboot Nahyan Al Nahyan na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula mara baada ya kumaliza mazungumzo yao yaliyofanyika Ikulu Jijini Dar es Salaam



Tuesday, April 12, 2022

WAZIRI MULAMULA ATETA NA MABALOZI WA UFARANSA, ITALIA NA USWISI

Na Mwandishi wetu, Dar

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula (Mb) amekutana kwa pamoja na kufanya mazungumzo na mabalozi wa Ufaransa, Italia na Uswisi.

Waziri Mulamula amekutana na Balozi wa Ufaransa nchini Mhe. Nabil Hajlaoui, Balozi wa Italia nchini Mhe.  Marco Lombardi pamoja na Balozi wa Uswisi hapa nchini Mhe. Didier Chasot katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam.

Pamoja na mambo mengine, viongozi hao wamejadili namna ya kuimarisha ushirikiano baina ya Tanzania na nchi zao katika kupambana na mabadiliko ya tabia nchi na utunzaji wa mazingira.

Waziri Mulamula amewahakikishia mabalozi hao kuwa Serikali ipo tayari wakati wote kushirikiana na nchi zao katika utunzaji wa mazingira pamoja na mabadiliko ya tabia nchi.

“Serikali ya awamu ya sita imetoa kipaumbele katika utunzaji wa mazingira na kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi,” amesema Balozi Mulamula.

Nae Balozi wa Ufaransa nchini, Mhe. Hajlaoui kwa niaba ya mabalozi wengine, amesema wanafurahishwa na jitihada za Serikali ya Tanzania katika kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi pamoja na utunzaji wa mazingira. 

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula akisalimiana na Balozi wa Ufaransa nchini Mhe. Nabil Hajlaoui, Balozi wa Italia nchini Mhe.  Marco Lombardi pamoja na Balozi wa Uswisi hapa nchini Mhe. Didier Chasot katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam

Balozi wa Ufaransa nchini Mhe. Nabil Hajlaoui akimueleza jambo Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam

Balozi wa Uswisi nchini Mhe. Didier Chasot (wa kwanza kushoto) akifafanua jambo kwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula walipokutana kwa mazungumzo katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam

Balozi wa Italia nchini Mhe. Marco Lombardi (mwenye suti ya kijivu) akifafanua jambo kwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula wakati wa mazungumzo yao

Mazungumzo baina ya Waziri Mulalamula na Mabalozi yakiendelea katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam 



Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Mulamula akiongea na Balozi wa Ufaransa nchini Mhe. Nabil Hajlaoui, Balozi wa Italia nchini Mhe.  Marco Lombardi pamoja na Balozi wa Uswisi hapa nchini Mhe. Didier Chasot 

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula katika picha ya pamoja na Balozi wa Ufaransa nchini Mhe. Nabil Hajlaoui, Balozi wa Italia nchini Mhe.  Marco Lombardi pamoja na Balozi wa Uswisi hapa nchini Mhe. Didier Chasot. Wengine ni Mkurugenzi wa Idara ya Ulaya na Amerika Balozi Swahiba Mndeme na Afisa kutoka Wizarani, Bibi Kisa Mwaseba.  



UONGOZI WA WIZARA WAWASISITIZA MABALOZI KUFANYA KAZI KWA BIDII, WELEDI



Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula pamoja na Katibu Mkuu wa Wizara Balozi Joseph Sokoine wakiongea na mabalozi wanne walioapishwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan tarehe 10 Aprili 2022, (hawapo pichani) katika Ofisi ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam

Mkurugenzi wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Balozi Mindi Kasiga, (wa kwanza kulia) Mkurugenzi wa Idara ya Ushirikiano wa Kimataifa (Multilateral Co-operation) Balozi Macocha Tembele (wa pili kulia), Balozi James Bwana ambaye atakuhudumu katika Idara ya Ushirikiano wa Kimataifa (Multilateral Co-operation) - (wa tatu kulia) pamoja na Balozi Noel Kaganda ambaye anahudumu katika Chou cha Ulinzi (NDC) wa kwanza kushoto kwa pamoja wakiwasikiliza viongozi wa Wizara (hawapo pichani) katika kikao kilichofanyika katika Ofisi ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam

Mabalozi wakisikiliza na kufuatilia maelekezo ya Uongozi wa Wizara (hawapo pichani)

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Balozi Joseph Sokoine katika picha ya pamoja na Mabalozi mara baada ya kumaliza kikao 

 

Monday, April 11, 2022

TANZANIA, UJERUMANI KUSHIRIKIANA KUBORESHA UTAMADUNI

Na Mwandishi wetu, Dar

Serikali ya Tanzania pamoja na Shirikisho la Ujerumani zimekubaliana kuongeza ushirikiano katika kuboresha Utamaduni na Malikale ili kuendelea kuhifadhi urithi wa historia ya nchi kwa faida ya kizazi kilichopo na kijacho.

Ahadi hiyo imetolewa na Waziri wa Nchi katika Wizara ya Mambo ya Nje ya Shirikisho la Ujerumani Mhe. Katja Keul wakati alipokutana kwa mazungumzo na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam.

Balozi Mulamula amesema kuwa Ujerumani imekuwa na msaada mkubwa katika maendeleo ya kijamii, kitamaduni, kielemu na kiuchumi. “Kwa sasa tunaadhimisha miaka 60 ya ushirikiano wa kidiplomasia kati ya Tanzania na Ujerumani. ziara ya Mhe. Keul hapa nchini imelenga kuangala namna gani tunaweza kuongeza ushirikiano katika masuala ya utamaduni na malikale ambapo katika kutimiza hilo tayari mkataba wa ushirikiano wa kuendeleza makumbusho yetu ya taifa umesaini jana,” amesema Balozi Mulamula.

Nae Waziri Keul amesema kuwa Ujerumani na Tanzania zinaadhimisha miaka 60 ya ushirikiano na lengo kuu ni kuongeza ushirikiano katika masuala ya utamaduni na malikale kwa maslahi ya pande zote mbili.

“Katika kuhakikisha tunaongeza na kuboresha ushirikiano katika masuala ya utamaduni na malikale, tumesaini mkataba wa ushirikiano kati ya Makumbusho ya Taifa na Mfuko wa Utamaduni wa Ujerumani lengo kwa lengo la kuhakikisha malikale na uhifadhi wa historia zinalindwa na kusaidia jamii kisayansi, kielimu, kiutamaduni na kiuchumi,” amesema Mhe. Keul 

Kwa mujibu wa Sera ya Malikale ya mwaka 2008, malikale hujumuisha rasilimali za urithi wa utamaduni zinazoshikika na zisizoshikika; zinazohamishika, na zisizohamishika, zilizo nchi kavu na majini ambazo zinadhihirisha mabadiliko ya kimaumbile, kifikra, zana, vyombo na mazingira aliyoishi na kutumia binadamu na zenye umri wa miaka mia moja (100). Malikale hizi zinajumuisha zana za mawe na chuma, vyombo vya usafiri, metali, miti na mifupa; visukuku vya binadamu, mimea na wanyama; michoro ya miambani; miji ya kihistoria, magofu ya majenzi.  

 Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula katika mazungumzo na Waziri wa Nchi katika Wizara ya Mambo ya Nje ya Shirikisho la Ujerumani Mhe. Katja Keul wakati katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam

Waziri wa Nchi katika Wizara ya Mambo ya Nje ya Shirikisho la Ujerumani Mhe. Katja Keul akimueleza jambo Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam

Mazungumzo baina ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula na Waziri wa Nchi katika Wizara ya Mambo ya Nje ya Shirikisho la Ujerumani Mhe. Katja Keul yakiendelea katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam

Mazungumzo baina ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula na Waziri wa Nchi katika Wizara ya Mambo ya Nje ya Shirikisho la Ujerumani Mhe. Katja Keul yakiendelea katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula katika picha ya pamoja na Waziri wa Nchi katika Wizara ya Mambo ya Nje ya Shirikisho la Ujerumani Mhe. Katja Keul. Wengine pichani ni Balozi wa Ujerumani nchini Mhe. Regina Hess, Balozi wa Tanzania nchini Ujerumani Mhe. Dkt. Abdalla Possi, Mkurugenzi wa Idara ya Ulaya na Amerika, Balozi Swahiba Mndeme pamoja na Maafisa kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na Maafisa walioambatana na Mhe. Keul katika ziara yake hapa nchini.