Tuesday, August 2, 2022
Friday, July 29, 2022
TANZANIA, URUSI KUONGEZA MAENEO YA USHIRIKIANO
Serikali ya Tanzania na Urusi zimekubaliana kuongeza maeneo ya ushirikiano katika sekta za biashara na uwekezaji,utalii pamoja na utamaduni.
Makubaliano hayo yamefikiwa na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk alipokutana kwa mazungumzo na Balozi wa Urusi nchini, Mhe. Andrey Levonovish Avetsyan katika Ofisi ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam.
Balozi Mbarouk amesema kuwa Tanzania na Urusi zimekuwa na ushirikiano wa muda mrefu wa kihistoria ambao uliasisiwa na Waasisi wa Mataifa hayo mawili…….“ kutokana na uhusiano mzuri tulionao umechangia kuimarisha sekta ya utalii, elimu pamoja na afya,” alisema Balozi Mbarouk
Balozi Mbarouk aliongeza kuwa Tanzania na Urusi zitaendelea kujikita zaidi kufungua maeneo mapya ya ushirikiano katika sekta za biashara, uwekezaji, utalii na masuala mengine ya kiuchumi kwa maslahi mapana ya mataifa hayo.
Kwa upande wake Balozi wa Urusi nchini, Mhe. Andrey Levonovish Avetsyan ameishukuru Tanzania kwa ushirikiano ambao imekuwa ikimpatia tangu aliwasili na kuongeza kuwa Urusi itaendelea kushirikiana na Tanzania katika kukuza na kuendeleza ushirikiano wa kufanya kazi kwa pamoja kwa manufaa ya mataifa mawili.
“Naamini kuwa mimi ni kiungo cha kuimarisha na kuendeleza uhusiano baina ya Urusi na Tanzania…..tumekuwa tukishirikiana katia sekta mbalimbali ikiwemo biashara na uwekezaji, elimu na afya utalii na utamaduni naahidi kuwa Urusi itaendelea kushirikiana na Tanzania kwa maslahi mapana ya pande zote mbili,” Amesema Balozi Avetsyan
Balozi Avetsyan ameongeza kuwa katika mwaka huu Serikali ya Urusi imepanga kutoa fursa za masomo kwa wanafunzi wa kitanzania takribani 70.
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk katika picha ya pamoja na Balozi wa Urusi nchini, Mhe. Andrey Levonovish Avetsyan |
TANZANIA, USWISI KUENDELEZA USHIRIKIANO
Balozi wa Uswisi nchini Mhe. Didier Chassot akitoa hotuba yake katika hafla ya kuandimisha Siku ya Taifa ya Uswisi iliyofanyika jijini Dar es Salaam tarehe 28 Julai 2022 |
Hafla ya kuadhimisha Siku ya Taifa ya Uswisi iliyofanyika jijini Dar es Salaam tarehe 28 Julai 2022 ikiendelea. |
Thursday, July 28, 2022
WAZIRI MULAMULA AMUAGA BALOZI WA PAKISTAN NCHINI TANZANIA
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Liberata Mulamula (Mb) na Balozi wa Misri nchini Tanzania Mhe. Mohamed Gaber wakiwa katika picha ya pamoja |
WAZIRI MULAMULA ASHIRIKI MKUTANO WA BARAZA LA AMANI NA USALAMA LA UMOJA WA AFRIKA KUJADILI HALI YA AMANI NA USALAMA NCHINI SOMALIA
Mkutano wa 1094 wa Baraza la Amani na Usalama la Umoja wa Afrika uliofanyika kwa njia ya mtandao tarehe 27 Julai 2022 ukiwa unaendelea. |
Wednesday, July 27, 2022
BALOZI MULAMULA AFUNGUA MAFUNZO YA UANDISHI WA HABARI ZA KIDIPLOMASIA
Balozi Patrick Tsere (kushoto) akiwa na Balozi Mindi Masiga (kulia) wakimfuatilia Balozi Peter Kalaghe (hayupo pichani) akizungumza na waandishi wa habari katika mafunzo ya waandishi wa habari ya kuandika habari za kidiplomasia yaliyoandaliwa na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikianio wa Afrika Mashariki jijini Dar es Salaam |
Baadhi ya washiriki mafunzo ya uandishi wa habari za kidiplomasia kwa waandishi wa habari nchini wakimfuatilia Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula akifungua mafunzo ya waandishi wa habari yaliyoandaliwa na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki na kufanyika katika Chuo cha Diplomasia jijini Dar es Salaam |
Mkurugenzi wa Mawasiliano Serikalini Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Mindi Kasiga akizungumza wakati wa mafunzo kwa waandishi wa habari ya kuandika habari za kidiplomasia yaliyoandaliwa na Wizara na kufanyika katika Chuo cha Diplomasia cha Dar es Salaam |
Balozi Patrick Tsere akiongea na waandishi wa habari juu ya kuandika habari kwa kuzingatia uzalendo katika kulinda taswira ya Tanzania wakati wa mafunzo kwa waandishi wa habari kutoka vyombo mbalimbali vya habari nchini yanayofanyika katika Chuo cha diplomasia jijini Dar es Salaam |
Kaimu Mkurugenzi wa Sera na Mipango , Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Bw. Justine Kisoka akizungumza katika mafunzo ya waandishi wa habari yaliyoandaliwa na wizara na kufanyika katika chuo cha diplomasia jijini Dar es salaam |
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula (aliyekaa katikati) katika picha ya pamoja na waandishi wa habari nchini baada ya kufungua mafunzo ya uandishi wa habari za kidiplomasia kwa waandishi wa habari nchini |
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula amefungua mafunzo ya uandishi wa habari za kidiplomasia kwa waandishi wa habari nchini.
Akifungua mafunzo hayo ya siku mbili yanayofanyika katika Chuo cha Diplomasia jijini Dar es Salaam, Balozi Mulamula amewataka watendaji wa Wizara kuhakikisha wanaimarisha mahusiano kati ya wizara na vyombo vya habari.
'Tuwe pamoja siku zote tuendelee kushirikiana, vyombo vya habari ni wadau muhimu, tufanye kazi pamoja kwa manufaa ya nchi yetu,' alisema.
Amesema waandishi wa habari wanajukumu la kuilinda na kuitetea taswira ya Tanzania kupitia kazi zao na kuwataka waandishi wa habari nchini kuzingatia taswira ya nchi wakati wanatekeleza majukumu yao.
"Wanahabari, tuko hapa kuelimishana juu ya kuandika habari za kidiplomasia, niwaombe kwanza mhakikishe mnailinda taswira ya nchi, hii ni nchi yetu wote, ikiharibika taswira yake hata wewe uliyeandika pia utakutana na athari zake, hata uende wapi utajulikana kama Mtanzania. Mnapoandika mzingatie uzalendo na miiko ya taaluma ya uandishi wa habari," alisema Balozi Mulamula.
Pia aliongeza kusema mafunzo haya ambayo yatakuwa endelevu yanalenga pamoja na mambo mengine kutoa uelewa kuhusu masuala ya diplomasia ikiwemo Itifaki, Diplomasia ya Umma, Uzalendo na Mawasiliano ya kimkakati baina ya Tanzania na nchi zingine.
Kadhalika, aliwashukuru waandishi wa habari kote nchini kwa ushirikiano uliopo kati yao na wizara na kuwataka kuzingatia mafunzo yatakayotolewa kwao.
"Nawashukuru kwa ushirikiano na kuelimisha umma kuhusu umuhimu wa Wizara na Sera ya Mambo ya Nje inayosisitiza katika Diplomasia ya Uchumi. Nawaomba mzingatie mafunzo haya kwani yatakuwa na tija kubwa kwenu," alisisitiza Balozi Mulamula.
Awali akimkaribisha Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula, Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Serikali Waziri ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Mindi Kasiga alieleza kuwa mafunzo hayo yameandaliwa kwa ajili ya kuwajengea uwezo waandishi wa habari nchini katika eneo la kuandika habari za kidiplomasia.
Amesema mafunzo hayo yatakuwa endelevu kwani kufanya hivyo kutasaidia kuboresha uandishi na kuwa daraja kati ya Wizara na waandishi wa habari na hivyo kuwafikia wananchi wengi.
Mafunzo hayo yameandaliwa na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki yamewashirikisha waandishi wa habari kutoka vyombo mbalimbali vya habari vya hapa nchini.
WAZIRI MULAMULA ATOA WITO KWA AFRIKA KUTHAMINI MCHANGO WA WANAWAKE KATIKA KUJENGA UCHUMI
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Liberata Mulamula akipokelewa na Waandaaji wa Mkutano wa Uchumi wa Wanawake Afrika alipowasili katika mkutano uliofanyika jijini Dar es Salaam. Tarehe 26 Julai 2022 |
Sehemu ya washiriki wa Mkutano wa Uchumi wa Wanawake Afrika wakifualia mjadala ulikokuwa ukiendelea |
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Liberata Mulamula akiwa katika picha ya pamoja waandaaji na baadhi ya washiriki wa Mkutano wa Uchumi wa Wanawake Afrika uliofanyika jijini Dar es Salaam |
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Liberata Mulamula (Mb) akisisitiza jambo wakati wa akifungua Mkutano wa Uchumi wa Wanawake Afrika (Pan-African Women Economic Summit 2022) uliofanyika jijini Dar es Salaam |
Tuesday, July 26, 2022
BALOZI FATMA RAJAB AFANYA MAZUNGUMZO NA UJUMBE WA SERIKALI YA OMAN
Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika
Mashariki, Balozi Fatma Rajab amekutana kwa mazungumzo na Ujumbe wa Serikali ya
Oman leo tarehe 26 Julai 2022 katika ofisi za Wizara jijini
Dodoma.
Mazungumzo
yao yalijikita katika kuimarisha ushirikiano wa kihistoria uliopo baina ya
Tanzania na Oman kwakuwa nchi hizo zinashirikiana katika sekta za
biashara, kilimo, uwekezaji, utalii, afya, elimu, ujenzi wa miundombinu,madini
na uvuvi.
Ujumbe huo
upo nchini kwa ziara ya siku 6 na unaongozwa na Katibu Mkuu Wizara ya
Mambo ya Nje wa Oman, Mhe. Mohammed Bin Nasser Al Wahaibi ambaye ameambana na
viongozi wengine wa Serikali ya Oman.
Pamoja na
Balozi Fatma Rajab, ujumbe huo pia umefanya mazungumzo na Mkuu wa Mkoa wa
Dodoma, Mhe. Antony Mtaka pamoja na uongozi wa jiji la Dodoma ambapo, ulipata
wasaa wa kutembelea kiwanja kilichotolewa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania kwa ajili ya kujenga ofisi za Ubalozi wa Oman.
Aidha,
tarehe 24 Julai 2022 ujumbe huo ulikutana na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar
ambapo ulifanya mazungumzo na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la
Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi.
Ziara ya
ujumbe huu ni matokeo ya ziara ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe.
Samia Suluhu Hassan nchini Oman.
Hivyo,
ujumbe huu upo nchini kufanya ufuatiliaji wa masuala ya utekelezaji katika
maeneo mbalimbali ya ushirikiano yaliyokubaliwa wakati wa ziara hiyo na
kuangalia namna ya kuhuisha mikutano ya Tume ya Pamoja ya Ushirikiano baina ya
nchi hizo mbili.
=====================================
Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Fatma Rajab akizungumza na Katibu Mkuu Mambo ya Nje wa Oman, Mhe. Mohammed Bin Nasser Al Wahaibi leo tarehe 26 Julai 2022 katika ofisi za Wizara jijini Dodoma. |
Kutoka kushoto ni Balozi wa Tanzania nchini Oman, Mhe. Abdallah Kilima, mjumbe kutoka Serikali ya Oman na Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Mashariki ya Kati, Bw. Leonce Bilauri wakifuatilia mazungumzo. |
Ujumbe uliombatana na Mhe. Wahaibi ukifuatilia mazungumzo. |
Picha ya pamoja. |
Balozi Fatma Rajab akimkaribisha Mhe. Wahaibi na ujumbe wake. |
WAZIRI MULAMULA AWAKUMBUSHA WASHIRIKA WA MAENDELEO KUTO ELEKEZA MIRADI UPANDE MMOJA WA NCHI
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Liberata Mulamula akimsikiliza Balozi wa Autria nchini Tanzania Mhe. Christian Fellner mwenye makazi yake jijini Nairobi, Kenya walipokutana kwa mazungumzo yaliyofanyika katika Ofisi ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam. |
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Liberata Mulamula (wa tatu kushoto) Balozi wa Autria nchini Tanzania Mhe. Christian Fellner (wa pili kushoto) Balozi Swaiba Mndeme Mkurugenzi wa Idara ya Ulaya na America (wa tatu kulia) wakiwa katika picha ya pamoja na Maafisa kutoka Wizarani na Ubalozi wa Autria. |
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Liberata Mulamula (Mb) akifafanua jambo wakati wa mazungumzo na Balozi wa Autria nchini Tanzania Mhe. Christian Fellnermwenye makazi yake jijini Nairobi, Kenya yaliyofanyika katika Ofisi ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam. |
Monday, July 25, 2022
WIZARA YA MAMBO YA NJE YAWANOA WANAHABARI JUU YA MIKAKATI, MALENGO YA SADC
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki imeahidi kuendelea kushirikiana na vyombo vya habari katika kuielimisha jamii juu ya mikakati ya Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) ili waweze kutumia fursa mbalimbali za kiuchumi kwa maslahi mapana ya Taifa.
Ahadi hiyo imetolewa na Mkurugenzi wa Idara ya Ushirikiano wa Kikanda Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Agnes Kayola alipofungua mafunzo hayo kwa niaba ya Katibu Mkuu Balozi Joseph Sokoine.
Balozi Kayola amesema waandishi wa habari wana mchango mkubwa katika kuhakikisha watanzania wengi hasa vijana wanafahamu umuhimu wa SADC na kutumia vizuri fursa zinazopatikana katika jumuiya hiyo.
"Waandishi wa habari mna mchango mkubwa kuhakikisha kundi la vijana linafahamu ipasavyo umuhimu wa SADC ili waweze kushiriki na kuzitumia fursa zilizopo katika jumuiya hii ya kikanda kwa manufaa,"amesema Balozi Kayola.
Balozi Kayola ameongeza kuwa Tanzania inazo huduma nyingi ambazo zikitumika ipasavyo zitaweza kuwa na mchango mkubwa katika uchumi na kuwasihi waandishi hao wa habarinkuhakikisha wanatumia lugha ya Kiswahili ipasavyo katika kutoa taarifa zao.
“Tanzania itaendelea kutumia lugha yetu ya Kiswahili kama bidhaa, hivyo jukumu kubwa ambalo mnapaswa kulifahamu ni kuhakikisha mnakitumia Kiswahili ipasavyo katika kutoa taarifa zenu," ameongeza Balozi Kayola.
Pamoja na mambo mengine, Balozi Kayola ameeleza mikakati mbalimbali ya Serikali ya Tanzania katika SADC ikiwemo kuwaenzi viongozi waanzilishi akiwemo Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere.
Amesema wanahabari wana jukumu la kuifanya jamii ya Watanzania inafahamu majukumu, malengo na fursa zinazopatikana katika nchi wanachama wa Jumuiya ya SADC.
Awali Mkurugenzi wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mindi Kasiga aliwasihi waandishi wa habari pamoja na Maafisa Habari walioshiriki katika warsha hiyo kuhakikisha uelewa wanaoupata katika mafunzo hayo wanaielimisha jamii ya watanzania ili kuelewa mikakati na fursa za kiuchumi zinazopatika katika ukanda wa SADC.
“Vyombo vya Habari ni mhimili wa nne katika Serikali, hivyo nawasihi tujitahidi kuielimisha jamii yetu ili iweze kuchangamkia fursa mbalimbali zinazopatikana katika ukanda huo,” alisema Balozi Mindi.
Mafunzo ya waandishi wa habari nchini yameandaliwa na Wizara ya Mambo ya Nje kwa kushirikiana na Shirika la Maendeleo la Ujerumani (GIZ).
Mkurugenzi wa Idara ya Ushirikiano wa Kikanda Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Agnes Kayola akifungua mafunzo ya waandishi wa habari mjini Bagamoyo mkoani Pwani |
Mkurugenzi wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mindi Kasiga akiongea na washiriki wa mafunzo ya waandishi wa habari mjini Bagamoyo mkoani Pwani |
Balozi mstaafu Mhe. Dkt. Mohamed Omar akiwasilisha mada katika mafunzo ya waandishi wa habari mjini Bagamoyo mkoani Pwani |
Mkurugenzi wa Idara ya Ushirikiano wa Kikanda Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Agnes Kayola pamoja na Mkurugenzi wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mindi Kasiga wakifuatilia mafunzo ya waandishi wa habari mjini Bagamoyo mkoani Pwani |
Mwezeshaji wa masuala yanayohusu SADC, Bw. Chibamba Kanyama akizungumza na waandishi wa habari walioshiriki mafunzo mjini Bagamoyo Mkoani Pwani |
Sehemu ya waandishi wa habari wakifuatilia mafunzo mjini Bagamoyo Mkoani Pwani |
Viongozi kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki katika picha ya pamoja na washiriki wa mafunzo ya waandishi wa habari mjini Bagamoyo Mkoani Pwani |