Friday, August 12, 2022

BALOZI FATMA ATETA NA UJUMBE WA SAUDI ARABIA

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika ya Mashariki, Balozi Fatma Rajab amekutana kwa mazungumzo na ujumbe wa wataalam kutoka Wizara ya Mazingira, Maji na Kilimo ya Saudi Arabia ambao upo nchini kwa ziara ya kikazi kuanzia tarehe 10 -13 Aug,2022. 

Ujumbe huo umeambatana na Balozi wa Tanzania nchini Saudi Arabia, Mhe. Ali Mwadini. Aidha, ziara hiyo ni matokeo ya ziara iliyofanywa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula mwezi Machi 2022 nchini Saudi Arabia ambapo katika ziara hiyo ilikubaliwa kuwa wataalamu hao kufanya ziara nchini Tanzania kwa lengo la kujionea fursa mbalimbali za uwekezaji hapa nchini katika sekta za kilimo na ufugaji. 

Pamoja na mambo mengine, wataalam hao wamekutana na wadau kutoka Chemba ya Wafanyabiashara wa Viwanda na Kilimo Tanzania (TCCIA), Kituo cha Taifa cha Uwekezaji (TIC), Wizara ya Uchumi wa Buluu, Mamlaka ya Kukuza Uwekezaji Zanzibar (ZIPA), Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Nchini (TAWA), Kampuni ya Ranchi za Taifa (NARCO) pamoja na Taasisi ya Kuendeleza Kilimo Ukanda wa Nyanda za Juu Kusini (SAGCOT).

Maeneo mengine ambayo ujumbe huo unatarajiwa kutembelea ni pamoja na kiwanda cha Tanchoice kilichopo Kibaha mkoani Pwani na Ranchi ya Mbogo ili kiujionea fursa za uwekeji katika maeneo hayo.

Naibu Katibu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika ya Mashariki, Balozi Fatma Rajab akipokea zawadi kutoka kwa kiongozi wa ujumbe wa wataalamu kutoka Saudi Arabia, Mhandishi Abdulaziz Bin Abdulrahman Al-Huwaish katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam


Naibu Katibu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika ya Mashariki, Balozi Fatma Rajab katika picha ya pamoja na kiongozi wa ujumbe wa wataalamu kutoka Saudi Arabia, Mhandishi Abdulaziz Bin Abdulrahman Al-Huwaish katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam

Naibu Katibu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika ya Mashariki, Balozi Fatma Rajab katika picha ya pamoja na Balozi wa Tanzania nchini Saudi Arabia, Mhe. Ali Mwadini,  Mkurugenzi wa Idara ya Mashariki ya Kati, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Hemed Mgaza na Ujumbe wa wataalamu kutoka Saudi Arabia katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam




Wednesday, August 10, 2022

SERIKALI KUSHIRIKIANA NA CCBRT KUBORESHA DIPLOMASIA YA AFYA

Na Waandishi wetu, Dar

Serikali kupitia Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki imeahidi kushirikiana na Hospitali ya CCBRT kuboresha mazingira ya utoaji wa huduma za afya nchini kupitia utekelezaji wa Diplomasia ya Afya.

Ahadi hiyo imetolewa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushiikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula (Mb.), alipofanya ziara ya kutembelea Hospitali hiyo kwa lengo la kujionea shughuli na huduma mbalimbali zinazotolewa hospitalini hapo leo Jijini Dar es Salaam 

Pamoja na mambo mengine, Waziri Mulamula ameupongeza Uongozi wa Hospitali hiyo kwa kazi nzuri wanayoifanya ya kuwahudumia watanzania hasa kuwapa akina mama tumaini la maisha hususan wanaopatwa na changamoto ya ugonjwa wa fistula.

“Wizara ninayoisimamia ni mtambuka na mchango wake umekuwa mkubwa ambapo nyinyi ni wadau wetu, tutashirikiana na Balozi zetu nje kuona ni jinsi gani tutapata wadau/washirika wa maendeleo watakaosaidia katika kuboresha sekta ya afya hususan hapa CCBRT,” amesema Waziri Mulamula.

Kwa upande wake Afisa Mtendaji Mkuu wa CCBT, Brenda Msangi amesema kuwa pamoja na jitihada ambazo Serikali imekuwa ikizichukua kuboresha sekta ya afya nchini, hospitali hiyo pia inajitahidi kuboresha huduma zake na mazingira yake kwa ujumla ili kuweza kuwahudumia wagonjwa wengi zaidi.

“Tunajitahidi kuwahudumia watanzania kadri tuwezavyo ila tunakabiliwa na baadhi ya changamoto za msaada wa utoaji wa huduma, vifaa tiba pamoja na kuwajengea uwezo wataalamu wetu ili kuweza kuboresha huduma zaidi,” amesema Bibi. Msangi.

Julai 05, 2022 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye hafla ya uzinduzi wa jengo la kutolea huduma ya afya ya mama na mtoto katika hospitali ya CCBRT alisema kuwa mikakati ya kuboresha huduma kwa akina mama wajawazito na watoto wachanga, Serikali kupitia Wizara ya afya kwa kushirikiana na vyama vya kitaaluma vya madaktari bingwa wa magonjwa ya kina mama na uzazi wameanzisha mfumo wa kupitia takwimu za vifo vya kina mama na watoto wakati wa kujifungua lengo likiwa ni kuboresha zaidi huduma katika sekta ya afya.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushiikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula akioneshwa baadhi ya viungo bandia vinavyotengenezwa katika hospitali ya CCBRT na Afisa Mtendaji Mkuu wa CCBT, Bibi. Brenda Msangi. Balozi Mulamula alifanya ziara ya kutembelea hospitali hiyo kwa lengo la kujionea shughuli na huduma zinazotolewa hospitalini hapo leo Jijini Dar es Salaam.    

Mkurugenzi wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mindi Kasiga akieleza jambo kwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushiikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula pamoja na Afisa Mtendaji Mkuu wa CCBT, Bibi. Brenda Msangi hospitalini hapo leo Jijini Dar es Salaam 

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushiikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula akiwa katika kikao na Afisa Mtendaji Mkuu wa CCBT, Bibi. Brenda Msangi wakati alipofanya ziara ya kutembelea hospitali hiyo kwa lengo la kujionea shughuli na huduma zinazotolewa hospitalini hapo leo Jijini Dar es Salaam  

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushiikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula akiongea na baadhi ya wagonjwa wakati alipofanya ziara ya kutembelea hospitali ya CCBRT kwa lengo la kujionea shughuli na huduma zinazotolewa hospitalini hapo leo Jijini Dar es Salaam

Afisa Mtendaji Mkuu wa CCBT, Bibi. Brenda Msangi akimueleza jambo Waziri wa Mambo ya Nje na Ushiikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula wakati Mhe. Mulamula alipofanya ziara ya kutembelea hospitali hiyo kwa lengo la kujionea shughuli na huduma zinazotolewa hospitalini hapo leo Jijini Dar es Salaam 

Mkurugenzi wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mindi Kasiga akiagana na Afisa Mtendaji Mkuu wa CCBT, Bibi. Brenda Msangi hospitalini hapo leo Jijini Dar es Salaam 




JITAHADA ZAIDI ZINAHITAJIKA KUTANGAZA KAZI ZA WIZARA NDANI NA NJE YA NCHI- BALOZI MINDI



Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Serikali Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Mindi Kasiga akiwasilisha mada ya Diplomasia ya Umma (Public Diplomacy) wakati wa mafunzo ya kuwajengea uwezo waandishi wa habari na utaalamu na ujuzi wa kuandika taarifa za kidiplomasia yaliyofanyika katika Chuo cha Diplomasia jijini Dar es Salaam.

Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Serikali Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Mindi Kasiga akizungumza wakati wa mafunzo ya kuwajengea uwezo waandishi wa habari na utaalamu na ujuzi wa kuandika taarifa za kidiplomasia yaliyofanyika katika Chuo cha Diplomasia jijini Dar es Salaam


Balozi Mindi Kasiga akizungumza wakati wa mafunzo ya kuwajengea uwezo waandishi wa habari na utaalamu na ujuzi wa kuandika taarifa za kidiplomasia yaliyofanyika hivi karibuni jijini Dar es Salaam
                                     
Mkurugenzi Msaidizi  Idara ya Ushirikiano wa Kimataifa, Bw. Songalieli Shila akiwasilisha mada ya Umuhimu wa Tanzania kuwa mwanachama wa Jumuiya za Kikanda na Kimataifa wakati wa mafunzo ya kuwajengea uwezo waandishi wa habari na utaalamu na ujuzi wa kuandika taarifa za kidiplomasia yaliyofanyika hivi karibuni jijini Dar es Salaam


Mkurugenzi Msaidizi  Idara ya Ushirikiano wa Kimataifa, Bw. Songalieli Shila akizungumza wakati wa mafunzo ya kuwajengea uwezo waandishi wa habari na utaalamu na ujuzi wa kuandika taarifa za kidiplomasia yaliyofanyika hivi karibuni jijini Dar es Salaam


 Mkurugenzi wa Biashara, Uwekezaji na Sekta za Uzalishaji, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki  Bw. Bernard Haule akiwasilisha mada ya Umuhimu wa Soko Huru la Biashara Barani Afrika iliyowasilishwa wakati wa mafunzo ya kuwajengea uwezo waandishi wa habari na utaalamu na ujuzi wa kuandika taarifa za kidiplomasia yaliyofanyika hivi karibuni jijini Dar es Salaam


Baadhi ya washiriki wa mafunzo ya kuwajengea uwezo waandishi wa habari na utaalamu na ujuzi wa kuandika taarifa za kidiplomasia yaliyofanyika hivi karibuni jijini Dar es Salaam wakifuatilia mafunzo hayo 


 Mkurugenzi Msaidizi  Idara ya Ushirikiano wa Kimataifa, Bw. Songalieli Shila akiwa na baadhi ya washiriki wa mafunzo  ya kuwajengea uwezo waandishi wa habari na utaalamu na ujuzi wa kuandika taarifa za kidiplomasia yaliyofanyika hivi karibuni jijini Dar es Salaam


Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Serikali Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Mindi Kasiga amesema kuwa kuwa jitahada zaidi zinahitajika kutangaza ndani na nje ya nchi kazi ambazo Wizara inazifanya.

Balozi Mindi ametoa kauli hiyo alipowasilisha mada ya Diplomasia ya Umma (Public Diplomacy) wakati wa mafunzo ya kuwajengea uwezo waandishi wa habari na utaalamu na ujuzi wa kuandika taarifa za kidiplomasia yaliyofanyika katika Chuo cha Diplomasia jijini Dar es Salaam.

Amesema kuwa licha ya Wizara kufanya kazi kubwa bado kazi hizo hazijapata fursa ya kutangazwa ipasavyo na kuna haja ya kuongeza jitihada zaidi ili kuhakikisha kazi hizo zinajulikana ndani na nje ya nchi.

Amesema waandishi wa habari ni wadau muhimu katika kufanikisha azma hiyo ya Wizara kwa kushirikiana na Kitengo cha Mawasiliano cha Wizara. Balozi Kasiga aliahidi kuwa Wizara itaendelea kuandaa mafunzo hayo ambayo pamoja na mambo mengine yatawezesha kuwepo na orodha ya waandishi wenye ujuzi wa kuandika taarifa za kidiplomasia ambao watatambulishwa katika Jumuiya ya wanadiplomasia nchini na hivyo kuendelea kufanya nao kazi kwa ufanisi zaidi kuitangaza diplomasia ya Tanzania ndani na nje ya mipaka ya nchi yetu.

Mafunzo hayo ya siku mbili (tarehe 27-28/ Julai, 2022) yameandaliwa na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kupitia Kitengo chake cha Mawasiliano (GCU) yamewashirikisha waandishi wa habari kutoka vyombo mbalimbali vya habari vya hapa nchini ikiwemo mitandao ya kijamii ambapo walieleza jinsi walivyofaidika na mada za mafunzo hayo zilizowasilishwa na mabalozi wabobezi na Wakuu wa Idara na Vitengo wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki.

 

Waandishi wa habari waliohudhuria mafunzo hayo walipata nafasi ya kusikiliza mada za Utekelezaji wa diplomasia ya uchumi iliyowasilishwa na Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Sera na Mipango, Bw. Justin Kisoka; Uandishi wa taarifa za kidiplomasia iliyowasilishwa na Balozi Mstaafu Peter Kallaghe; Uzalendo katika kujenga na kulinda tasiwra ya Tanzania iliyowasilishwa na Balozi Mstaafu Patrick Tsere; Diplomasia ya Umma iliyowasilishwa na Mkurugenzi wa Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali (GCU), Balozi Mindi Kasiga; Umuhimu wa Tanzania kuwa mwanachama wa Jumuiya za Kikanda na Kimataifa iliyowasilishwa na Mkurugenzi Msaidizi kutoka Idara ya Ushirikiano wa Kimataifa, Bw. Songalieli Shila; na Umuhimu wa Soko Huru la Biashara Barani Afrika iliyowasilishwa na Mkurugenzi wa Biashara, Uwekezaji na Sekta za Uzalishaji, Bw. Bernard Haule.

Mada hizo zililenga kuwapatia waandishi wa habari ufahamu kuhusu majukumu, malengo na mikakati ya Wizara katika utekelezaji wa Sera ya Mambo ya Nje inayojikita katika diplomasia ya uchumi.

Wawasilishaji mada walitumia fursa hiyo kuwaelimisha waandishi wa habari hao kuhusu agenda za nchi katika Jumuiya ya Kimataifa zikiwemo kutumia Soko Huru la Biashara barani Afrika kwa manufaa ya kiuchumi.

Mafunzo hayo yalifunguliwa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula tarehe 27 Julai, 2022 ambapo aliwaeleza waandishi wa habari kuwa ni wadau muhimu na kuwaahidi kuwa Wizara itaendelea kuimarisha uhusiano na kundi hilo muhimu kwa kuwawekea mazingira mazuri ikiwa ni pamoja na kuwaandalia mafunzo ya mara kwa mara ili waweze kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi zaidi.

WAZIRI MULAMULA AMUAGA BALOZI WA CANADA BAADA YA KUMALIZA MUDA WA UWAKILISHI

Na Waandishi wetu, Dar

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula (Mb.), ameagana na Balozi wa Canada nchini Mhe. Pamela O'Donnell ambaye amemaliza muda wake wa uwakilishi hapa nchini walipokutana katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam.

Akizungumza na Balozi O'Donnell Waziri Mulamula ameelezea kuridhishwa kwake na utendaji kazi wake ambao umewezesha Serikali ya Tanzania na Canada kuendelea kuimarisha ushirikiano katika sekta za afya, elimu pamoja na biashara na uwekezaji.

Waziri Mulamula ameongeza kuwa ushirikiano uliopo kati ya Tanzania na Canada ni jambo lililochochewa na kazi nzuri iliyofanywa na Balozi O'Donnell wakati akitekeleza majukumu yake ya kibalozi hapa nchini.

“Katika kipindi chako umeiwakilisha vyema Canada na kuonesha mafanikio makubwa ambayo yamefikiwa na Tanzania na Canada. Kazi yako imechochea uboreshaji wa sekta za afya na elimu pamoja na kuchangia ukuaji wa sekta ya biashara uwekezaji katika nchi zetu, ni matumaini yangu kuwa utaendelea kuwa Balozi mwema kwa Tanzania nchini Canada na kokote uendako Duniani,” amesema Balozi Mulamula.

Kwa upande wake Balozi wa Canada nchini Mhe. Pamela O'Donnell amesema anajivunia uwepo wake Tanzania, amejifunza mengi ikiwemo ukarimu wa Watanzania na amewashukuru Watanzania kwa upendo mkubwa waliomuonesha katika kipindi chote cha uwakilishi wake nchini.

“Naishukuru Tanzania na watu wake kwa ukarimu na ushirikiano walionionesha wakati natekeleza majukumu yangu ya kibalozi hapa nchini, kwa kweli ni ngumu sana kuaga na kusema kwaheri lakini hakuna budi, siku zote nitakumbuka utu na ukarimu wa Watanzania,” amesema Mhe. Balozi O'Donnell.

Pamoja na mambo mengine, Balozi O'Donnell ameihakikishia Tanzania kuwa Canada itaendelea kushirikiana na Tanzania katika sekta ya gesi pamoja na biashara na uwekezaji kwa maslahi ya pande zote mbili.

“Wawekezaji na wafanyabiashara kutoka Canada wamekuwa wakiridhishwa na mazingira ya biashara na uwekezaji na baadhi yao wameonesha nia ya dhati ya kuwekeza katika sekta ya gesi Tanzania,” ameongeza Balozi O'Donnell

Kadhalika, Balozi O’Donell amepongeza kazi nzuri inayofanywa na Serikali ya Tanzania ya kuimarisha ukuaji wa Uchumi, utoaji wa huduma bora za afya, elimu ya msingi bure kwa watanzania pamoja na kuboresha miundimbinu kwa maendeleo ya watanzania.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula  akizungumza na Balozi wa Canada nchini Mhe. Pamela O'Donnell katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam

Sehemu ya Maafisa kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, wakifuatilia kikao cha Waziri Mulamula na Balozi wa Canada nchini Mhe. Pamela O'Donnell katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam

Balozi wa Canada nchini Mhe. Pamela O'Donnell akimueleza jambo Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula  katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula  akimkabidhi zawadi ya picha Balozi wa Canada nchini Mhe. Pamela O'Donnell katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam


TAARIFA KWA UMMA

 






Tuesday, August 9, 2022

DKT. KIKWETE ASHUHUDIA UPIGAJI KURA, KENYA

Rais Mstaafu wa Tanzania na Kiongozi wa Timu ya waangalizi ya Uchaguzi  Mkuu wa Kenya, ya Jumuiya ya Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete na timu yake ya wajumbe 52 kutoka taasisi na mashirika ya kiraia ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki inashuhudia zoezi la upigaji kura la uchaguzi mkuu nchini Kenya lililoanza Leo mapema asubuhi.

Kabla ya uchaguzi huo  Dkt. Kikwete alikutana na wadau mbalimbali wakiwemo wagombea wa Urais kupitia chama cha Muungano wa Azimio la Umoja, Mhe. Raila Odinga na mgombea Urais wa chama cha UDA,vMhe. William Ruto.

Rais Mstaafu wa Tanzania na Kiongozi wa Timu ya waangalizi ya Uchaguzi  Mkuu wa Kenya, ukanda wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete katika mazungumzo na mgombea Urais wa chama cha UDA, William Ruto. Mazungumzo hayo yalifanyika hivi karibuni Jijini Nairobi

Rais Mstaafu wa Tanzania na Kiongozi wa Timu ya waangalizi ya Uchaguzi  Mkuu wa Kenya, ukanda wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete akizungumza na mgombea Urais wa chama cha Muungano wa Azimio la Umoja, Raila Odinga hivi karibuni Jijini Nairobi

Rais Mstaafu wa Tanzania na Kiongozi wa Timu ya waangalizi ya Uchaguzi  Mkuu wa Kenya, ukanda wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete katika picha ya pamoja na mgombea Urais wa chama cha Muungano wa Azimio la Umoja, Raila Odinga Jijini Nairobi

Rais Mstaafu wa Tanzania na Kiongozi wa Timu ya waangalizi ya Uchaguzi  Mkuu wa Kenya, ukanda wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete katika picha ya pamoja na mgombea Urais wa chama cha UDA, William Ruto Jijini Nairobi


Sunday, August 7, 2022

SERIKALI YAWAHAHIKISHIA WAWEKEZAJI MAZINGIRA SALAMA YA UWEKEZAJI NCHINI

Na Mwandishi Wetu, Pwani

Serikali imeendelea kuwahakikishia wawekezaji kuwa Tanzania ina mazingira rafiki na salama kwa uwekezaji na inaendelea kuweka mikakati mahususi ya kuimarisha na kuendeleza sekta ya viwanda ili kuongeza ajira kwa wananchi na kupunguza umaskini.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula (Mb) ameyasema hayo jana wakati aliposhiriki katika hafla ya utiaji saini mkataba wa uzalishaji mbolea na viuatilifu hai katika kiwanda cha kuzalisha bidhaa za kibiolojia Tanzania (Tanzania Biotech Products Ltd) Kibaha Mkoa wa Pwani.

Pamoja na mambo mengine, Balozi Mulamula amewahakiki wawekezaji kuwa Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan inaendelea kuweka mikakati mahsusi ya kuimarisha na kuendeleza sekta ya viwanda ili kuongeza ajira kwa wananchi na hivyo kuwapunguzia umaskini.

“Serikali inaendelea kuwalinda wawekezaji wote wanaoamua kuanzisha viwanda hapa nchini kwa kuwapatia vivutio maalumu ikiwa ni pamoja na kuweka mazingira wezeshi ya uwekezaji na biashara,” amesema Balozi Mulamula.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Idara ya Ushirikiano wa Kimataifa katika Wizara ya Kilimo ya Cuba, na Kiongozi wa Ujumbe wa Serikali ya Jamhuri ya Cuba, Bw. Orlando Diaz Rodriguez amesema kuwa Cuba imekuwa ikijivunia ushirikiano wake na Tanzania na kwamba wanaamini kuwa kusainiwa kwa mkataba huo ni ishara ya kuendeleza ushirikiano baina ya mataifa hayo ulidumu kwa miaka 60.

“Kuanzishwa kwa kiwanda hiki cha Labiofam ni Faraja kwetu sisi Cuba, kiwanda hiki ni nguzo ya ushirikiano baina ya Tanzania na Cuba…….pia ufanyaji kazi wa kiwanda hiki utasaidia sana kupunguza kasi ya Malaria nchini Tanzania,” amesema Bw. Rodriguez

Bw. Rodriguez ameongeza kuwa, Cuba itaendelea kushirikiana na Tanzania katika sekta za afya, elimu na kilimo  pamoja na kuhakikisha kuwa mataifa hayo mawili yanaimarisha misingi ya kidiplomasia baina yao.

Awali, Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Mhe. Aboubakari Kunenge amesema kuwa mkoa wa Pwani unaongoza kwa Viwanda ambapo kuna viwanda 1,453 na kati ya hivyo 87 ni viwanda vikubwa.

“Upatikanaji wa nishati, maji na miundombinu imara ni mambo muhimu katika uwekezaji wa viwanda. Tatizo la maji na nishati halipo tena katika mkoa wa pwani hivyo nawasihi wawekezaji kujitokeza kwa wingi kuja kuwekeza Tanzania hususan Kibaha kwani maeneo ya kuwekeza yapo ya kutosha na mazingira ni mazuri,” amesema Mhe. Kunenge

Juni 29, 2022 Waziri wa Mambo ya Nje wa Cuba, Mhe. Bruno Rodriguez Parrilla akiwa chini kwa ziara ya kikazi ya siku mbili kufuatia mwaliko wa Mhe. Balozi Liberata Mulamula, aliahidi kuboresha utendaji wa kiwanda cha viuadudu kilichopo Kibaha, Pwani ili malengo ya uwekezaji pamoja na yale ya kudhibiti malaria yaweze kufikiwa.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula akiwasilisha hotuba yake katika hafla ya utiaji saini mkataba wa uzalishaji mbolea na viuatilifu hai katika kiwanda cha kuzalisha bidhaa za kibiolojia Tanzania (Tanzania Biotech Products Ltd) Kibaha Mkoa wa Pwani

Mkurugenzi wa Idara ya Ushirikiano wa Kimataifa katika Wizara ya Kilimo ya Cuba, na Kiongozi wa Ujumbe wa Serikali ya Jamhuri ya Cuba, Bw. Orlando Diaz Rodriguez akiwasilisha hotuba yake katika hafla ya utiaji saini mkataba wa uzalishaji mbolea na viuatilifu hai katika kiwanda cha kuzalisha bidhaa za kibiolojia Tanzania (Tanzania Biotech Products Ltd) Kibaha Mkoa wa Pwani

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula pamona na Naibu Waziri Wizara ya Uwekezaji Viwanda na Biashara Mhe. Exaud Kigahe wakishuhudia utiaji saini mkataba wa uzalishaji mbolea na viuatilifu hai katika kiwanda cha kuzalisha bidhaa za kibiolojia Tanzania (Tanzania Biotech Products Ltd) Kibaha Mkoa wa Pwani

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula pamona na Naibu Waziri Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara Mhe. Exaud Kigahe wakiwa katika picha ya pamoja na viongozi mbalimbali walioshiriki hafla ya utiaji saini mkataba wa uzalishaji mbolea na viuatilifu hai katika kiwanda cha kuzalisha bidhaa za kibiolojia Tanzania, Kibaha Mkoa wa Pwani


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula pamoja na viongozi mbalimbali wakipata maelezo kuhusu kiwanda cha kuzalisha bidhaa za kibiolojia Tanzania walipofanya ziara ya kutembelea kiwanda hicho Kibaha Mkoa wa Pwani


Thursday, August 4, 2022

WAZIRI MULAMULA AWAAGA MABALOZI WA SWEDEN, FINALAND

Na Waandishi wetu, Dar 

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula ameagana na mabalozi wa Sweden na Finland nchini, Mhe. Anders Sjöberg na Mhe. Riita Swan baada ya kumaliza muda wao wa utumishi nchini Tanzania.

Waziri Mulamula amewaaga mabalozi hao kwa nyakati tofauti leo katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam ambapo amempongeza Balozi wa Sweden Mhe. Sjöberg kwa kazi nzuri aliyoifanya ya kudumisha uhusiano kati ya nchi yake na Tanzania wakati wote wa uwakilishi hapa nchini.  

 Waziri Mulamula amempongeza Balozi wa Sweden kwa kazi nzuri aliyoifanya katika kuendeleza uhusiano baina ya Sweden na Tanzania ambapo Sweden imekuwa na mchango mkubwa katika miradi ya maendeleo vijijini, biashara na uwekezaji pamoja na elimu.

“Biashara kati ya nchi zetu mbili bado ipo chini, hivyo nimemhimiza Mhe. Sjöberg pamoja na kuwa amemaliza muda wake wa uwakilishi aendelee kuwasihi wafanyabiashara kutoka Sweden kuja kuwekeza Tanzania,” amesema Balozi Mulamula 

Waziri Mulamula amesema mbali na sekta za biashara na uwekezaji pamoja na elimu,Tanzania itaendelea kushirikiana na Sweden katika sekta za afya, nishati na utalii hasa katika kuitangaza filamu ya ‘The Royal Tour’. 

Kuhusu ushirikiano wa Tanzania na Finland, Balozi Mulamula ameongeza kuwa Finland na Tanzania ni marafiki wa muda mrefu na wa karibu ambapo kupitia ushirikiano huo Finland imekuwa ikiiunga mkono Tanzania kwa misaada katika mradi wa ukusanyaji wa kodi pamoja na mradi wa kuendeleza misitu.

Kwa upande wake Balozi wa Sweden Mhe. Sjöberg ameishukuru Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa ushirikiano iliompatia wakati wote alipokuwa nchini akitekeleza majukumu yake ya kibalozi.

“Naondoka baada ya kumaliza muda wangu wa uwakilishi hapa Tanzania lakini kwa jinsi nilivyofanya kazi na watanzania, Tanzania ni sawa na nyumbani…….nafarijika pia kuona masuala ya utawala bora, amani na usalama pamoja na uwezeshaji wa wanawake kiuchumi vikiwa vimeboreshwa kwa kiasi kikubwa,” amesema Balozi Sjöberg

Naye Balozi wa Finland, Mhe. Swan ameishukuru Serikali ya Tanzania kwa kumpa ushirikiano wa kutosha wakati wa kipindi chake cha uwakilishi hapa nchini.

Mhe. Swan ameelezea kufurahishwa na uhusiano mzuri uliopo baina ya Finland na Tanzania na amepongeza hatua mbalimbali ambazo Serikali ya Tanzania imeendelea kuzichukua katika kuimarisha diplomasia ya uchumi.

“Nimekuwa hapa nchi kwa zaidi ya miaka mitatu, mambo mengi yamebadilika kwa sasa nimefurahishwa na maboresho katika ukuaji na uboreshaji wa mazingira ya biashara na uwekezaji……naiona Tanzania ya mafanikio siku za karibuni,” amesema Balozi Swan.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula akizungumza na Balozi wa Sweden nchini, Mhe. Anders Sjöberg katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam wakati alipokuwa akimuaga baada ya kumaliza muda wake wa utumishi nchini

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula katika picha ya pamoja na Balozi wa Sweden nchini, Mhe. Anders Sjöberg. Wengine pichani ni Mkurugenzi wa Idara ya Ulaya na Amerika katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Swahiba Mndeme pamoja na Maafisa kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki 

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula akimkabidhi zawadi ya picha na Balozi wa Finland nchini, Mhe. Riita Swan baada ya kumaliza muda wao wa uwakilishi nchini

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula katika mazungumzo na Balozi wa Finland nchini, Mhe. Riita Swan baada ya kumaliza muda wao wa uwakilishi nchini

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula akiagana na Balozi wa Finland nchini, Mhe. Riita Swan baada ya kumaliza muda wao wa uwakilishi nchini



TANZANIA NA CHINA ZAAHIDI KUIMARISHA USHIRIKIANO

Na Mwandishi wetu, Dar

Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Jamhuri ya watu wa China zimeahidi kuendeleza ushirikiano wa kidiplomasia baina ya nchi hizo kwa kuzingatia misingi ya ushirikiano wa kirafiki kwa maslahi mapana ya mataifa yote mawili.

Rai hiyo imetolewa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula (Mb) alipokutana kwa mazungumzo na Balozi wa China nchini, Mhe. Chen Mingjian katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam.

Waziri Mulamula amesema katika mazungumzo yao wamejadili masuala mbalimbali, ikiwemo suala la namna ya kuimarisha misingi ya ushirikiano baina ya mataifa hayo.

"Tanzania tutaendelea kuzingatia kwa dhati kanuni ya kuwa na China moja, kuunga mkono kwa dhati msimamo halali wa China, kuunga mkono China katika kulinda maslahi yake ya msingi," amesema Waziri Mulamula

Kwa Upande wake Balozi wa China nchini, Mhe. Mingjian amesema kuwa Serikali yake wakati wote imekuwa rafiki mzuri kwa Serikali ya Tanzania na kwamba urafiki wa nchi hizo mbili umekuwa mfano mzuri wa kuigwa na China itaendelea kuheshimu na kuenzi urafiki huo.

"Tunathamini ushirikiano kati ya Tanzania na China, uhusiano huu umejengwa katika misingi imara na isiyotikisika…..China itaendelea kusisitiza dhamira yake ya kuimarisha uhusiano bora kati yake na Tanzania," amesema Balozi Mingjian.

Uhusiano kati ya Tanzania na China ulianza mapema miaka ya 1960 wakati nchi hizo mbili zilipoanzisha uhusiano wa kidiplomasia tarehe 9 Desemba 1961.


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula akizungumza na Balozi wa China nchini, Mhe. Chen Mingjian katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula katika picha ya pamoja na Balozi wa China nchini, Mhe. Chen Mingjian, Mkurugenzi wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini Balozi Mindi Kasiga pamoja na Afisa kutoka ubalozi wa China katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam



Wednesday, August 3, 2022

WAZIRI WA USAFIRISHAJI ZAMBIA AFANYA ZIARA BANDARI, TAZARA

Na Mwandishi Wetu, Dar

Waziri wa Uchukuzi na Usafirishaji wa Jamhuri ya Zambia Mhe. Frank Tayali amefanya ziara ya kutembelea Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA), Kampuni binafsi ya Kimataifa ya Kuhudumia Makontena Tanzania (TICTS) pamoja na Mamlaka ya Reli ya Tanzania na Zambia (Tazara) Jijini Dar es Salaam.

Katika ziara hiyo Mhe. Tayali aliambatana na mwenyeji wake Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Prof. Makame Mbarawa (Mb) ambapo pamoja na mambo mengine, viongozi hao wametembelea maeneo hayo ikiwa ni siku moja tu tangu Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan pamoja na Rais wa Jamhuri ya Zambia, Mhe. Hakainde Hichilema walipowaelekeza Mawaziri wa Sekta hiyo kushughulika changamoto zinazoikabilia miundombinu ya kiuchumi baina ya nchi hizo ikiwemo reli ya Tazara na Bomba la mafuta la Tazama.

Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi Prof. Makame Mbarawa amemhakikishia Waziri mwenzake kuwa Tanzania ipo tayari kushirikiana na Zambia katika kutafuta mikakati ya kuifufua reli ya Tazara na kuhakikisha kuwa wafanyabishara kutoka Tanzania na Zambia wananufaika na reli ya Tazara.

“Tanzania na Zambia ni washirika na ndugu hivyo sisi kama watanzania tupo hapa kuwahudumia na pia tupo tayari kushirikiana nanyi kuhakikisha kuwa uchumi wetu unakua……………. kupanua wigo wa biashara baina ya mataifa yetu,” amesema Prof. Mbarawa.

Nae Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Bandari Tanzania, Bw. Plasduce Mbossa amesema kuwa Zambia ni nchi moja wapo kati ya nchi zainazotumia Bandari ya Tanzania kwa asilimia kubwa ambapo Bandari inatambua mchango mkubwa wa wafanyabiashara kutoka Zambia wanavyotumia bandari ya Tanzania na kuwa Bandari inawaahidi ushirikiano katika kukuza na kuendeleza biashara baina ya Tanzania na Malawi.

Kwa upande wake Waziri wa Uchukuzi na Usafirishaji wa Zambia, Mhe. Tayali amesema Tazara ni nyenzo muhimu katika kuinua uchumi wa mataifa yote mawili, hivyo kufufuliwa kwa reli ya Tazara kutasaidia kuinua uchumi wa mataifa yote hususan kwa wafanyabiashara na wawekezaji. 

“Zambia tutafanya kazi kwa bidii kwa kushirikiana na Serikali ya Tanzania katika kutafuta mikakati mbalimbali ya kuifufua Tazara ili kuendelea kunufaisha watanzania na wazambia kwani bila kufanya hivyo maendeleo ya mataifa hayo yatadhorora,” amesema Mhe. Tayali

Aidha, viongozi hao wamewaagiza Makatibu Wakuu wa Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi kutoka Tanzania na Zambia kushirikiana na Uongozi wa Tazara kuunda Kamati ya kufuatilia mikakati ya ufufuaji wa Reli ya Tazara mapema iwezekananyo ili kuanza kutekeleza maagizo ya viongozi wakuu wa nchi yaliyotolewa jana tarehe 2 Aug, 2022 wakati wa Ziara rasmi ya kikazi ya Rais wa Jamhuri ya Zambia nchini Tanzania jana. 

Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Prof. Makame Mbarawa (kulia) na mgeni wake Waziri wa Uchukuzi na Usafirishaji wa Jamhuri ya Zambia Mhe. Frank Tayali (kushoto) wakichukua dondoo walipofanya ziara katika Mamlaka ya Bandari Tanzania. Mhe. Tayali ametembelea bandari ya Tanzania kwa lengo la kujionea jinsi bandari hiyo inavyotekeleza majukumu yake

Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Prof. Makame Mbarawa na mgeni wake Waziri wa Uchukuzi na Usafirishaji wa Jamhuri ya Zambia Mhe. Frank Tayali wakimsikiliza Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Reli ya Tanzania na Zambia (Tazara) Mhandisi Bruno Tching'andu (aliyesimama) alipokuwa akieleza jinsi Tazara inavyotekeleza majukumu yake


Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Prof. Makame Mbarawa na mgeni wake Waziri wa Uchukuzi na Usafirishaji wa Jamhuri ya Zambia Mhe. Frank Tayali wakipata taarifa fupi kuhusu Kampuni binafsi ya Kimataifa ya Kuhudumia Makontena Tanzania (TICTS) inavyotekeleza majukumu yake wakati walipotembelea ofisi za TICTS Jijini Dar es Salaam

Kikao cha Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Prof. Makame Mbarawa na mgeni wake Waziri wa Uchukuzi na Usafirishaji wa Jamhuri ya Zambia Mhe. Frank Tayali kikiendelea katika Ofisi za Tazara Jijini Dar es Salaam



Tuesday, August 2, 2022

RAIS SAMIA, HICHILEMA WAKUBALIANA KUBORESHA UHUSIANO

Na Mwandishi wetu, Dar 

RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Zambia, Mhe. Hakainde Hichilema wamekutana na kufanya mazungumzo kuhusu kufufua ushirikiano baina ya nchi hizo ambao ulikuwa umelegalega.

Mazungumzo hayo yamefanyika Ikulu Jijini Dar es salaam ambapo Mhe. Hichilema alikuja kwa ziara rasmi ya kiserikali ya siku moja.

Rais Samia amesema kuwa Tanzania na Zambia ni nchi ambazo zilikuwa karibu zikiwa na urafiki na undugu ambao ulianzishwa na waasisi wa mataifa hayo Hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere kwa upande wa Tanzania na Hayati Keneth Kaunda wa Zambia.

“Wazee hawa ndio walioshirikiana kuleta ukombozi kusini mwa bara la Afrika lakini kwa upande wao katika nchi zetu mbili wakatuanzishia mambo ambayo walitaka yadumu milele na yatuunganishe,” amesema Rais Samia.

Rais Samia ameongeza kuwa katika kurudisha undugu wameangalia maeneo yote ambayo yatachochea kurudi huko kwa kuangalia uhusiano wa kisiasa na kuongoza wananchi wao katika kuelewana vyema.

Mbali na hayo Rais Samia amesema wamejadili masuala ya usalama wa nchi hizo na kuangalia changamoto za kiusalama zinazokabili ukanda wao ikiwemo ugaidi na kukubaliana kushirikiana.

Wawili hao walizungumzia pia masuala ya uchumi ambapo walikubaliana kufufua upya miundombinu ya kiuchumi baina ya nchi hizo ikiwemo reli ya TAZARA na Bomba la mafuta la TAZAMA.

Rais Samia alisema wamekubaliana kuboresha reli ya TAZARA kwa kuijenga kwa kiwango cha kisasa (SGR) ili kuendana na mahitaji ya sasa ya kidunia.

“Tumekubaliana tuboreshe TAZARA kama tunaifanyia marekebisho reli iliyopo lakini tukakubaliana kwamba kwa dunia ya leo reli ni SGR, kwahiyo tutakuwa na mradi wa pamoja tutafute pesa kwa pamoja kupitia PPP pengine na marafiki waliotujengea reli hiyo tuone jinsi tutakavyoboresha kwa kiwango cha SGR,” amesema Rais Samia.

Kuhusu Bomba la mafuta la TAZAMA marais hao wamekubaliana kuwa lililopo ni dogo ikilinganishwa na mahitaji na hivyo kuona haja ya kujenga lingine kubwa kwani kwa sasa bomba la TAZAMA halifanyi kazi kama ilivyokusudiwa kutokana na mabadilko ya sera za Nishati za Zambia.

“Tumekubaliana bomba lile (TAZAMA) ni dogo sana kwahiyo kuna haja ya kujenga kubwa litakalopeleka mafuta kwa wingi na bandari ya Dar es Salaam na miundombinu iliyopo Tanzania iwasaidie kupunguza ughali wa mafuta katika nchi yao,” ameongeza Rais Samia

Kadhalika viongozi hao walijadili kuhusu biashara na uwekezaji ambapo pamoja na mambo mengine,  wameangalia vikwazo vya kikodi na visivyo vya kikodi na kukubaliana mamlaka zinazoshulika na kodi na forodha kukutana na kuangalia mambo ya kuondoa ili kuruhusu biashara baina ya nchi hizo kufanyika vizuri.

Rais Samia alisema wamewazungumzi pia wafanyabishara wadogowadogo wanaovuka mipaka na kubaini kuwa masharti wanayopewa ni makubwa kuanzia vibali vya kuingia hadi tozo.

“Tumeagiza Mawaziri wakae na kuangalia jinsi ya kusaidia biashara ziendelee bila matatizo,” amesema Rais Samia.

Vilevile wamejadili changamoto za madereva na kukubaliana taasisi za madereva za Zambia na Tanzania ziwekwe pamoja zizungumze na Serikali zote mbili na kuona ni jinsi gani changamoto zinazowakabili zinaondolewa.

Rais Samia ameongeza kuwa katika mazungumzo yao waligusia mambo ya kilimo ambapo wameona kuwa wote ni wazalishaji wa soya ambayo ina soko nje ya nchi zetu, na kwamba Zambia wapo vizuri katika uzalishaji wa mbegu.

“Tumekubaliana tusishindane lakini tuongezeane uwezo, wenzetu ni mabingwa wa uzalishaji wameendelea kidogo wana mbegu nzuri na tumezungumza kwamba linapokuja suala la mbegu mnatutoza sana akaniambia basi tuzungumze tuuziane kirafiki na kindugu.”

“Tumekubaliana kufanya kazi kwa pamoja na kama mmoja ana soko amwambie mwingine kuna soko hapa na sisi leo tumeofa soko la nyama, ng’ombe na kondoo tuna soko kubwa tumelipata Saudia Arabia tumewaalika wenzetu waje twende tukalitumie hilo soko,” amesema Rais Samia

Kwa upande wake Rais wa Jamhuri ya Zambia, Mhe. Hakainde Hichilema amesema viongozi wa nchi hizo mbili  ni kizazi ambacho kinatakiwa kuendeleza  urithi ulioachwa na waasisi  Keneth Kaunda na Julius Nyerere.

“Tumekubaliana na dada yangu Rais Samia kuendeleza urafiki wetu katika mambo mbalimbali kama vile masuala ya utamaduni kwa sababu ukienda maeneo kama Nakonde au Tunduma kuna familia ambazo shangazi anaishi upande wa Zambia na mjomba anaishi upande wa Tanzania kwa hiyo sisi ni ndugu.

“Tunaangalia pia namna ya kutumia umoja wetu kupitia majukwaa kama SADC, Nchi za ukanda wa Maziwa Makuu na Ukanda wa Jumuiya ya Afrika Mashariki hasa ikizingatiwa Tanzania ni nchi wanachama kote, sisi hatupo baadhi lakini tunaweza kufaidika na uwepo wa Tanzania kwenye umoja huo,” amesema Rais Hichilema 

Rais Hichilema ameongeza kuwa Zambia imepanga kuimarisha uhusiano na Tanzania na kufanya kazi kwa pamoja kwa maslahi mapana ya mataifa yote mawili.

Aidha, Mhe. Hichilema amesema kuwa Tanzania imefanikiwa kwenye sekta ya madini ambapo imewawezesha wachimbaji wadogo na kuwainua hadi kuwa wachimbaji wakubwa.

Katika hafla hiyo pia Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula (Mb.) pamoja na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa wa Zambia, Mhe. Stanley Kakubo  wamesaini mikataba mitatu ya ushirikiano katika sekta ya ulinzi na usalama pamoja na sanaa na utamaduni.

Akifafanua kuhusu ziara hiyo, Waziri Mulamula alisema mikataba miwili inahusu ulinzi na usalama ambapo nchi hizo zitashirikiana kwenye masuala ya kijeshi pamoja na mafunzo kwa maofisa wa ngazi za juu kwenye masuala ya ulinzi na usalama wakati mkataba wa tatu utahusu masuala ya sanaa na utamaduni.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan pamoja na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Zambia Mhe. Hakainde Hichilema wakisalimiana na viongozi mbalimbali waliofika kwenye mapokezi baada ya Mhe. Hichilema kuwasili katika uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) Jijini Dar es Salaam 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan pamoja na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Zambia Mhe. Hakainde Hichilema wakisalimiana na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula baada ya Mhe. Hichilema kuwasili katika uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) Jijini Dar es Salaam 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan akiwa amesimama pamoja na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Zambia, Mhe. Hakainde Hichilema wakati nyimbo za Taifa (Tanzania na Zambia) zikiimbwa mara baada ya kuwasili katika uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) Dar es Salaam

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan akizungumza na Wanahabari (hawapo pichani) katika ziara ya Rais wa Jamhuri ya Zambia, Mhe. Hakainde Hichilema Ikulu Jijini Dar es Salaam

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula pamoja na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa wa Zambia, Mhe. Stanley Kakubo  wakionesha mikataba waliyosaini. Mikataba hiyo ni ya ushirikiano katika sekta ya ulinzi na usalama pamoja na sanaa na utamaduni

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan akiagana na Rais wa Jamhuri ya Zambia, Mhe. Hakainde Hichilema mara baada ya kuhitimisha ziara yake ya siku moja Jijini Dar es Salaam

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan akiagana na Rais wa Jamhuri ya Zambia, Mhe. Hakainde Hichilema mara baada ya kuhitimisha ziara yake ya siku moja Jijini Dar es Salaam



TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI