Friday, March 14, 2025

TANZANIA NA IRELAND ZAADHIMISHA SIKU YA Mtakatifu PATRICK, WAZIRI PINDI CHANA AAHIDI KUENDELEZA USHIRIKIANO

Waziri wa Maliasili na Utalii, Balozi Dkt. Pindi Chana



Tanzania na Ireland zimeungana kuadhimisha Siku ya Mtakatifu Patrick, katika hafla iliyofanyika  Ubalozi wa Ireland, jijini Dar es Salaam.

Akizungumza katika hafla hiyo, Waziri wa Maliasili na Utalii, Balozi Dkt. Pindi Chana, aliahidi kuwa Serikali ya Tanzania itaendelea kuimarisha ushirikiano na Ireland hasa ikizingatiwa kuwa nchini hizo zimekuwa na ushirikiano wa karibu kwa miaka mingi kupitia sekta za biashara, elimu, ujenzi wa uwezo, ulinzi wa kijamii, utalii, kilimo, ufugaji, pamoja na utawala bora.

Mhe. Chana alieleza kuwa Siku ya Mtakatifu Patrick ni Siku muhimu kwa Ireland na Tanzania inatumia siku hiyo kuendelea kuimarisha ushirikiano na uhusiano na Ireland.

Kwa upande wake, Waziri wa Mambo ya Nje na Biashara wa Ireland anayeshughulikia masuala ya Ushirikiano wa Kimataifa, Maendeleo, na Diaspora, Mhe. Neale Richmond, alisema maadhimisho ya Siku ya Mtakatifu Patrick ni tukio muhimu kwa Ireland, na kufanyika kwa hafla hiyo nchini kunatoa nafasi ya Nchi hiyo kuonyesha utamaduni wao na kuimarisha ushirikiano na Tanzania kupitia sanaa na muziki.

Sherehe hiyo ilihudhuriwa na viongozi mbalimbali wa Tanzania, akiwemo Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Cosato David Chumi (Mb), aliyemwakilisha Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Mahmoud Thabit Kombo (Mb).

Viongozi wengine ni Balozi wa Tanzania nchini Uingereza ambaye pia anawakilisha Ireland Mhe. Mbelwa Kairuki, Mkurugenzi wa Idara ya Ulaya na Amerika katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki na Mkurugenzi wa Idara ya Biashara ya Kimataifa na Diplomasia ya Uchumi, Balozi John Ulanga.

Hafla hiyo pia ilihudhuriwa na wanadiplomasia walioko nchini na wadau mbalimbali.
 
 
Waziri wa Mambo ya Nje na Biashara wa Ireland anayeshughulikia masuala ya Ushirikiano wa Kimataifa, Maendeleo, na Diaspora, Mhe. Neale Richmond
 
 
Waziri wa Maliasili na Utalii, Balozi Dkt. Pindi Chana (kushoto),Waziri wa Mambo ya Nje na Biashara wa Ireland anayeshughulikia masuala ya Ushirikiano wa Kimataifa, Maendeleo, na Diaspora, Mhe. Neale Richmond (katikati) na Balozi wa Ireland nchini Mhe. Balozi Nicola Brennan (kulia).
 
 
 

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Cosato Chumi (kulia), Balozi wa Tanzania nchini Uingereza anayeiwakilisha Ireland pia Mhe. Balozi Mbelwa Kairuki (katikati) pamoja na Mkurugenzi idara ya Ulaya na Marekani katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Swahiba Mndeme (kulia)
 
 
Balozi wa Tanzania nchini Uingereza anayeiwakilisha Ireland pia Mhe. Balozi Mbelwa Kairuki (kulia) pamoja na Mkurugenzi wa Idara ya Biashara ya Kimataifa na Diplomasia ya Uchumi, Balozi John Ulanga katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki.
 

 
Mkurugenzi idara ya Ulaya na Marekani katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Swahiba Mndeme (kulia) pamoja na Afisa Mambo ya Nje, Noel Mtafya (kushoto)
 
 





 
 




 
 

WAZIRI WA IRELAND ATEMBELEA BANDARI YA DAR ES SALAAM, AJADILI FURSA ZA BIASHARA NA UWEKEZAJI



Waziri wa Mambo ya Nje na Biashara wa Ireland anayeshughulikia masuala ya Ushirikiano wa Kimataifa, Maendeleo na Diaspora, Mhe. Neale Richmond



Waziri wa Mambo ya Nje na Biashara wa Ireland anayeshughulikia masuala ya Ushirikiano wa Kimataifa, Maendeleo na Diaspora, Mhe. Neale Richmond, ametembelea Bandari ya Dar es Salaam kwa lengo la kuimarisha ushirikiano wa kibiashara kati ya Tanzania na Ireland, hususan katika sekta ya usafirishaji wa bidhaa kupitia bandari hiyo.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Mhe. Richmond alieleza  nia ya Ireland ya kuimarisha uhusiano wa kiuchumi na Tanzania kwa kuhakikisha mifumo ya usafirishaji wa bidhaa inaboreshwa ili kuongeza kasi ya biashara kati ya mataifa hayo mawili.

Katika ziara hiyo, Mhe. Richmond alipata fursa ya kutembelea miundombinu ya bandari na kujionea shughuli za upokeaji na usafirishaji wa mizigo, pamoja na kujadiliana na wadau mbalimbali juu ya fursa za uwekezaji.

Aidha, Waziri Richmond alikutana na kuzungumza na viongozi wa Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA), wawakilishi wa sekta binafsi, na uongozi wa Shirika la Mpango wa Chakula Duniani (WFP), ambalo hutumia bandari hiyo kuhifadhi na kusafirisha chakula kwenda katika maeneo mbalimbali.

Mazungumzo hayo yalijikita katika uimarishaji wa njia bora za  usafirishaji wa bidhaa za kilimo na chakula, ili kuongeza tija kwa wafanyabiashara na wawekezaji wa pande zote mbili.

Katika ziara hiyo Mhe. Richmond aliambatana na  Balozi wa Tanzania nchini Uingereza, Mhe. Mbelwa Kairuki, Balozi wa Ireland nchini Tanzania, Mhe. Nicola Brennan na Mkurugenzi wa Idara ya Ulaya na Amerika- Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Swahiba Mndeme.

Ziara hii inaonesha nafasi muhimu ya Tanzania kama kitovu cha biashara na usafirishaji katika Ukanda wa Afrika Mashariki na inatarajiwa kusaidia kuvutia wawekezaji zaidi kutoka Ireland, huku serikali ikiendelea kuweka mazingira rafiki kwa biashara na uwekezaji.
 
 

Waziri wa Mambo ya Nje na Biashara wa Ireland anayeshughulikia masuala ya Ushirikiano wa Kimataifa, Maendeleo na Diaspora, Mhe. Neale Richmond (kushoto) pamoja na Balozi wa Ireland nchini Mhe. Nicola Brennan.

 


 

 

 










WAZIRI WA IRELAND ATEMBELEA KIWANDA CHA KERRY GROUP





Waziri wa Mambo ya Nje na Biashara wa Ireland anayeshughulikia Masuala ya Ushirikiano wa Kimataifa, Maendeleo na Diaspora, Mhe. Neale Richmond





Waziri wa Mambo ya Nje na Biashara wa Ireland anayeshughulikia Masuala ya Ushirikiano wa Kimataifa, Maendeleo na Diaspora, Mhe. Neale Richmond, ametembelea Kiwanda cha Kerry Group kilichopo jijini Dar es Salaam


Kampuni ya Kitaifa ya Kerry Group yenye makao yake nchini Ireland, imewekeza katika kiwanda hicho kama sehemu ya mkakati wake wa kupanua shughuli zake barani Afrika, hususani katika Ukanda wa Afrika Mashariki.

Kiwanda cha Kerry Group kinajihusisha na uzalishaji wa viambato vya ladha kwa ajili ya masoko ya ndani na nje ya nchi na hivyo kuchangia ukuaji wa sekta ya uzalishaji wa chakula nchini.

Kiwanda hicho mbali ya kuongeza thamani ya mazao yanayozalishwa nchini kimetoa ajira kwa Watanzania, kuwezesha upatikanaji wa malighafi kwa gharama nafuu, ubunifu wa bidhaa na ushirikiano wa kibiashara na wadau wa ndani.

Akiwa Kiwanda hapo Mhe. Neale Richmond alibainisha kuwa Ireland ina nia ya kuimarisha zaidi uhusiano wa kiuchumi na Tanzania, huku akieleza kuwa uwekezaji wa Kerry Group ni kielelezo cha Nia hiyo na ni sehemu ya mafanikio yatokanayo na ushirikiano wa kibiashara kati ya mataifa haya mawili.

Aidha, Waziri Richmond alieleza kuwa Kerry Group imejikita kuleta maendeleo endelevu kwa kuzingatia utunzaji wa mazingira, jambo linaloendana na sera za kimataifa za uzalishaji wenye tija na rafiki kwa mazingira.

Alisema Ireland itaendelea kushirikiana na Tanzania ili kuhakikisha sekta ya viwanda inakua kwa kasi na kuleta manufaa kwa wananchi.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Balozi wa Tanzania nchini Uingereza ambaye pia anawakilisha Ireland Mhe. Mbelwa Kairuki, aliikipongeza Kiwanda cha Kerry Group kwa mchango wake katika sekta ya viwanda nchini na kuahidi kuendelea kutoa ushirikiano kwa kiwanda hicho.

Alisisitiza kuwa Serikali ya Tanzania itaendelea kuboresha mazingira ya biashara ili kuvutia wawekezaji zaidi kutoka Ireland na mataifa mengine.

Waziri Richmond yuko nchini kwa ziara ya kikazi ya siku Tatu kuanzia tarehe 14-16 Machi, 2025.
 
 
Waziri wa Mambo ya Nje na Biashara wa Ireland anayeshughulikia Masuala ya Ushirikiano wa Kimataifa, Maendeleo na Diaspora, Mhe. Neale Richmond (kulia) pamoja na Balozi wa Tanzania Nchini Uingereza ambaye pia anaiwakilisha Ireland, Mhe.Balozi Mbelwa Kairuki (kushoto)
 
 
 


 Balozi wa Tanzania nchini Ireland ambaye pia anaiwakilisha Ireland, Mhe. Balozi Mbelwa Kairuki (kushoto) pamoja na Mkurugenzi idara ya Ulaya na Marekani katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Swahiba Mndeme (kulia)
 

 Balozi wa Ireland nchini Mhe. Nicola Brennan 
 


 


 





TANZANIA NA IRELAND KUIMARISHA USHIRIKIANO WA KIUCHUMI NA MAENDELEO

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi  Mahmoud Thabit Kombo(Mb.)( kulia) na Waziri wa Mambo ya Nje na Biashara wa Ireland anayeshughulikia masuala ya ushirikiano wa Kimataifa, Maendeleo na Diaspora, Mhe. Neale Richmond. 

 


Tanzania na Ireland zimeazimia kuimarisha ushirikiano katika nyanja mbalimbali za maendeleo na uchumi ili kukuza uhusiano wa kidiplomasia, biashara, na uwekezaji kati ya Nchi hizo mbili.

Makubaliano hayo yamefikiwa wakati wa mazungumzo rasmi kati ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Mahmoud Thabit Kombo (Mb.) na Waziri wa Mambo ya Nje na Biashara wa Ireland anayeshughulikia masuala ya ushirikiano wa kimataifa, Maendeleo, na Diaspora, Mhe. Neale Richmond.

Mazungumzo hayo yamefanyika katika ofisi ndogo ya Wizara jijini Dar es Salaam, ambapo viongozi hao walijadili fursa na mikakati ya kuimarisha mahusiano ya pande mbili kwa manufaa ya kiuchumi na kijamii.

Akizungumza katika kikao hicho, Mhe. Kombo ameishukuru Serikali ya Ireland kwa ushirikiano wa muda mrefu na mchango wake katika sekta za elimu, biashara, uwekezaji, utalii, afya, jinsia, uwezeshaji wa wanawake, pamoja na mifugo.

Aidha, alimpongeza Mhe. Richmond kwa ziara yake rasmi nchini Tanzania tangu alipoteuliwa, akisisitiza kuwa ziara hiyo ni ishara ya juhudi za dhati za kuimarisha uhusiano kati ya mataifa haya mawili.

Mhe. Kombo amesisitiza umuhimu wa kuongeza kiwango cha biashara kati ya Tanzania na Ireland, akihimiza wawekezaji kutoka Ireland kuchangamkia fursa zilizopo nchini, hasa katika sekta za kilimo, utalii, nishati mbadala, teknolojia ya habari na mawasiliano (TEHAMA), viwanda, na miundombinu.

Pia, amebainisha kuwa kiwango cha biashara kati ya mataifa hayo bado ni kidogo, hivyo kuna haja ya kuweka mikakati madhubuti ya kuongeza biashara yenye uwiano sawa.

Katika sekta ya utalii, Waziri Kombo amependekeza kuimarishwa kwa juhudi za kutangaza vivutio vya Tanzania kwa soko la Ireland na kuboresha miundombinu ya usafiri ili kuvutia wageni zaidi.

Aidha, amependekeza kuanzishwa kwa mfumo wa mashauriano ya kisiasa kati ya Tanzania na Ireland ili kuimarisha zaidi uhusiano wa kidiplomasia na kuweka msingi wa ushirikiano wa karibu katika masuala ya kimataifa.

Kwa upande wake, Mhe. Richmond ameahidi kuimarisha mshikamano wa kiuchumi na kijamii kati ya mataifa haya mawili kwa manufaa ya pande zote. Akitilia mkazo mshikamano wa kiuchumi, utamaduni, na elimu na kusisisitiza umuhimu wa sekta ya elimu kama nyenzo ya maendeleo endelevu.

Aidha, amebainisha kuwa amani na usalama ni misingi muhimu kwa ustawi wa mataifa, akihimiza juhudi za pamoja katika kuhakikisha utulivu wa kisiasa na kijamii kwa maendeleo yenye usawa.
 
 
 

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi  Mahmoud Thabit Kombo(Mb.)( kulia) na Waziri wa Mambo ya Nje na Biashara wa Ireland anayeshughulikia masuala ya ushirikiano wa Kimataifa, Maendeleo na Diaspora, Mhe. Neale Richmond (kushoto)

 


Waziri wa Mambo ya Nje na Biashara wa Ireland anayeshughulikia masuala ya ushirikiano wa Kimataifa, Maendeleo na Diaspora, Mhe. Neale Richmond 
 




                                    Picha ya Pamoja.

Tuesday, March 11, 2025

Wanafunzi NDC watembelea Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki


Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Dkt. Samwel Shelukindo akizungumza wakati wa kuwakaribisha Wanafunzi wa kozi ya 13 kutoka Chuo cha Taifa cha Ulinzi (NDC) na Uongozi wa Chuo hicho Wizarani jijini Dodoma. 

Wanafunzi wa kozi ya 13 kutoka Chuo cha Taifa cha Ulinzi (NDC) na uongozi wa Chuo hicho umetembelea Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki.

Ziara hiyo ya mafunzo imelenga kutoa nafasi kwa Wanafunzi hao kujifunza kuhusu historia ya Wizara , Sera ya Mambo ya Nje na majukumu yanayotekelezwa na Wizara kwa wakati huu.

Akizungumza wakati wa kuwakaribisha Wanafunzi hao Wizarani Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Dkt. Samwel Shelukindo alielezea juu ya mabadiliko ya Sera ya Mambo ya Nje ya Mwaka 2001 ambayo alieleza kuwa yamefanyika ili kuiwezesha Sera hiyo kuendana na mahitaji ya wakati uliopo na huku ikikidhi mahitaji ya wakati ujao.

“Tunayo Sera ya Mambo ya Nje ambayo tulitengeneza mwaka 2001 lakini sera hiyo sasa tumeifanyia maboresho ili iweze kuendana na mabadiliko mbalimbali ambayo yametokea duniani" alisema Balozi Shelukindo.

Alisema maboresho hayo yataiwezesha Sera ya Mambo ya Nje kukidhi mahitaji ya wakati huu na wakati ujao.

Balozi Shelukindo pia alisisitiza kuwa pamoja na maboresho hayo bado Sera ya Mambo ya Nje ya Tanzania imeendelea kusimamia katika misingi yake ile ile ya ujirani mwema, kutokufungamana na upande wowote, kutokuonea wanyonge, kuwa na Afrika yenye Umoja, na kutekeleza malengo ya Maendeleo ya Umoja wa mataifa. 

Balozi Shelukindo ametumia nafasi hiyo kuihakikishia NDC kuwa Wizara itaendelea kushirikiana nao wakati wote ili kuhakikisha NDC inaendelea kuwa kituo bora cha mafunzo nchini na kutoa Wanafunzi mahiri kwa manufaa ya Taifa.

Akizungumza wakati wa utambulisho wa wanachuo hao Mkuu wa Chuo cha NDC Meja Jenerali Balozi Wilbert Ibuge alisema wanafunzi waliotembelea Wizarani ni wa kozi ya 13 kwa mwaka 2024/2025 ambapo 40 wanatoka Jeshini na katika Wizara, Idara na Taasisi za Umma nchini na Wengine 21 wanatoka katika nchi rafiki za Bangladesh, Botswana, Burundi-2, Ethiopia, Misri-2, India, Kenya-2, Malawi, Namibia,Nigeria,Rwanda-2, Sierra Leone, Afrika Kusini, Uganda, Zambia-2 na Zimbabwe.

Amesema ziara ya wanafunzi hao Wizarani imelenga kuwapatia wanachuo hao mafunzo kwa vitendo ikizingatiwa kuwa masuala ya mambo ya nje na sera ya mambo ya nje ni miongoni mwa masuala Makuu ambayo wanafundishwa chuoni hapo.

“Chuo chetu katika kozi hizo za Ulinzi na Strategia focus yetu kubwa ni kuhusu masuala ya ulinzi na mambo ya nje na hapa wamekubaliana Leo ili asilia kutoka kwa wahusika ambao wanatekeleza majukumu hayo kwa vitendo".

Mkuu wa Chuo cha Taifa cha Ulinzi (NDC) Meja Jenerali Balozi Wilbert Ibuge akizungumza wakati alipoongoza ujumbe wa chuo kutembelea Wizara ya  Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki jijini Dodoma.

Picha ya pamoja
Mkurugenzi wa Idara ya Ushirikiano wa Kimataifa (DMC) katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Noel Kaganda akiwasilisha mada  kwa Wanafunzi wa kozi ya 13 kutoka Chuo cha Taifa cha Ulinzi (NDC) na Uongozi wa Chuo hicho Wizarani jijini Dodoma
Sehemu ya Wanafunzi wa kozi ya 13 kutoka Chuo cha Taifa cha Ulinzi (NDC) 
Sehemu ya Wanafunzi wa kozi ya 13 kutoka Chuo cha Taifa cha Ulinzi (NDC) 

Sehemu ya Wanafunzi wa kozi ya 13 kutoka Chuo cha Taifa cha Ulinzi (NDC) 



Mkurugenzi wa Idara ya Diplomasia ya Uchumi katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi John Ulanga kiwasilisha mada  kwa Wanafunzi wa kozi ya 13 kutoka Chuo cha Taifa cha Ulinzi (NDC) na Uongozi wa Chuo hicho Wizarani jijini Dodoma