Friday, September 29, 2023

TANZANIA YANADI FURSA ZA UWEKEZAJI KATIKA SEKTA YA KILIMO KUPITIA MAONESHO YA KIMATAIFA YA KAHAWA NCHINI JAPAN

Balozi wa Tanzania nchini Japan, Mhe. Baraka Luvanda amewahamasisha wafanyabiashara na wawekezaji wa Japan kuja kuwekeza nchini kwenye zao la kahawa na mazao mengine ya kimkakati.


Rai hiyo ameitoa hivi karibuni wakati akifungua semina maalum iliyoandaliwa kwa ajili ya Tanzania ikiwa ni siku ya pili ya Maonesho ya Kimataifa ya Kahawa yaliyofanyika kwa siku tatu nchini Japan kuanzia tarehe 27 hadi 29 Septemba 2023.


Semina hiyo ilipata mwitikio mkubwa kwa kuhudhuriwa na wadau wa kahawa wapatao 80 wa ndani na nje ya Japan ambapo Tanzania ilitumia fursa hiyo kutangaza kahawa ya Tanzania na zoezi la uonjaji  wa sampuli za kahawa ya Tanzania kutoka kampuni 30 zilizopo nchini lilifanyika. Sampuli hizo ni za kahawa ya Arabica laini Arabica ngumu na kahawa ya Robusta.


Tanzania inasifika Japan kwa kutoa kahawa bora aina ya Arabica inayolimwa katika mikoa ya Kilimanjaro, Arusha, Manyara, Mara, Tanga, Morogoro, Njombe, Iringa, Katavi, Rukwa, Ruvuma, Kigoma, Songwe na Mbeya; na kahawa ya Robusta inayolimwa mkoani Kagera.


Mbali na kuinadi Tanzania pamoja na vivutio vyake nchini Japan, kahawa ya Tanzania ni miongoni mwa vivutio hivyo ambapo imeweza kujipatia umaarufu mkubwa kutokana na ladha ya kipekee na kupewa Jina la Kibiashara la Tanzania Kilimanjaro Coffee. Jina hili hutumika nchini Japan kwa kahawa zinazozalishwa Tanzania pekee, kwa kutambua kivutio kikubwa cha Mlima Kilimanjaro uliopo nchini Tanzania.


Kadhalika, Tanzania imeshiriki Maonesho hayo ya Kimataifa ya Kahawa kama mdau  mkubwa wa kahawa duniani ambapo kwa mwaka huu yametimiza miaka 20 tangu kuanzishwa kwake mwaka 2003. Maonesho ya mwaka huu, yameshirikisha makampuni na taasisi zinazohusika na kahawa zipatazo 250 kutoka nchi zinazozalisha kahawa duniani na kuhudhuriwa na wadau wa kahawa wapatao 45,000 wakiwemo, wazalishaji na wanunuzi.

Balozi wa Tanzania nchini Japan, Mhe. Baraka Luvanda (mwenye scarf ya bendera ya Tanzania) akifungua semina maalum iliyoandaliwa wakati wa Maonesho ya Kimataifa ya Kahawa yaliyofanyika kwa siku tatu nchini Japan kuanzia tarehe 27 hadi 29 Septemba 2023. Semina hiyo pamoja na mambo mengine ililega kutangaza fursa za uwekezaji zinazopatikana kwenye sekta ya kilimo hapa nchini ikiwemo kilimo cha kahawa

Washiriki wa Semina wakifuatilia hafla ya ufunguzi
Zoezi la uonjaji wa kahawa ya Tanzania likiendelea wakati wa maonesho ya kimataifa ya Kahawa yaliyofanyika Japan kuanzia tarehe 27 hadi 29 Septemba 2023
Balozi Luvanda katika picha ya pamoja na washiriki na wadau wa kahawa kutoka Tanzania na Japan

Picha ya pamoja

 

Thursday, September 28, 2023

WAZIRI BYABATO AKOSHWA NA MRADI WA MABADILIKO YA TABIANCHI WILAYANI MAGU


Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki anayesimamia masuala ya Afrika Mashariki Mhe. Stephen Byabato (Mb.) ameeleza kuridhishwa kwake na utekelezaji wa Mradi wa Kuhimili Mabadiliko ya Tabia Nchi katika Bonde la Ziwa Victoria (Adapting to Climate change in Lake Victoria Basin – ACC – LVB)kupitia Kamisheni ya Bonde la Ziwa Victoria (LVBC) unaotekelezwa katika kijiji cha Ng’haya, Wilayani Magu.

Naibu Waziri Byabato ameeleza hayo alipokuwa ziarani katika Kijiji cha Ng’haya Wilayani Magu tarehe 27 Septemba 2023 ikiwa ni muendelezo wa ziara yake ya kikazi katika Kanda ya Ziwa ambapo anatembelea na kuona ufanisi wa miradi mbalimbali ya Jumuiya ya Afrika Mashariki inayotekelezwa kupitia LVBC. 

Akipokea taarifa ya utelekezaji wa mradi huo uliogharimu kiasi cha Shilingi 656,785,965 iliyowasilishwa na Watendaji wa Wilaya ya Magu ambapo pia alipata nafasi ya kutembelea miradi hiyo ameleza namna alivyofarijika kuona mradi huo ulivyochangia ustawi wa kiuchumi kwa wananchi wa kijiji cha Ng’haya. 

“Nimefarijika sana na namna mradi huu ulivyowanufaisha wananchi kwa kuwaongezea kipato kupitia miradi iliyotajwa kwenye taarifa yenu ambayo pia muda mfupi ujao nitaenda kuitembelea. Natoa pongezi sana kwa Uongozi na safu nzima ya Watendaji wa Wilaya kwa namna mlivyosimamia utekelezaji wa mradi huu na kufikia malengo mliyojiwekea” Alieleza Naibu Waziri Mhe.Byabato

Utekelezaji wa Mradi huu wa kuhimili mabadiliko ya Tabianchi katika kijiji cha Ng’haya unalenga kupunguza athari za mabadiliko ya tabianchi kwa jamii inayoishi katika bonde la Ziwa Victoria kwa nchi za Burundi, Kenya, Rwanda, Tanzania na Uganda. Vilevile kujenga uwezo wa jamii inayoishi katika maeneo hayo kuweza kuhimili mabadiliko ya Tabianchi kwa kutumia teknolojia za uvunaji wa maji ya mvua, maji chini ya ardhi, kilimo kinachohimili mabadiliko ya Tabianchi, mbinu zinazozingatia mifumo ya ikolojia katika shughuli zao za kijamii na kiuchumi.

Shughuli zingine zinazotekelezwa Wilayani Magu kupitia mradi huo kwa lengo la kuongeza kipato kwa jamii kupitia kilimo cha kisasa cha bustani na mboga mboga (kupitia vitalu nyumba) vikundi vya ufugaji wakuku, kondoo, unenepeshaji wa ng’ombe, ushonaji nguo na ufugaji wa nyuki. 

Kwa upande wake mwakilishi wa Kamisheni ya Bonde la Ziwa Victoria Bw. Amos Ndoto ameeleza kuwa kwa tathmini iliyofanywa na Kamisheni hiyo imebainisha kuwa Tanzania ndio nchi iliyofanya vizuri zaidi katika utekelezaji wa mradi huo ukilinganisha na nchi wanachama wanaonufaika na mradi, hivyo kujiweka katika nafasi nzuri zaidi ya kuendelea kunufaika na mradi katika awamu inayofuata.

Katika hatua nyingine Naibu Waziri Byabato alipata fursa ya kutembelea Shule ya Sekondari Ng’haya, Wilayani Magu ambayo inatekeleza Kilimo bora kinachotumia mbinu za kuhimili mabadiliko ya tabianchi (Climate Smart Agriculture) kupitia mradi huo ambao umewawezesha katika ujenzi wa kitalu nyumba kimoja kinachotumika kutoa mafunzo ya kilimo bora kwa vitendo kwa wanafunzi. 

Mradi huu ni wa Majaribio wa Kikanda wa Kuhimili Mabadiliko ya Tabianchi katika Bonde la Ziwa Victoria unatekelezwa katika Nchi 5, ambazo ni; Tanzania, Kenya, Uganda, Burundi na Rwanda. Mradi huu ni ulikuwa ni wa miaka 3, ambapo ulianza kutekelezwa mwaka 2019 hadi 2022 kwa ufadhili wa Adaptation Fund (AF)/UNEP) chini ya uratibu wa Kamisheni ya Bonde la Ziwa Victoria (LVBC). Kwa upande wa Tanzania mradi huu unatekelezwa katika kijiji cha Ng’haya, Wilayani Magu.
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki anayesimamia masuala ya Afrika Mashariki Mhe. Stephen Byabato (Mb.) akisaini kitabu cha wageni alipowasili Ofisi ya Mkuu wa Wilaya Magu
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki anayesimamia masuala ya Afrika Mashariki Mhe. Stephen Byabato akielekeza jambo kwa Viongozi na Watendaji wa Wilaya ya Magu (hawapo pichani) alipokuwa ziarani wilayani humo
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki anayesimamia masuala ya Afrika Mashariki Mhe. Stephen Byabato akitazama moja ya miundombinu ya utekelezaji wa Mradi wa Kuhimili Mabadiliko ya Tabia Nchi katika Bonde la Ziwa unaotekelezwa katika kijiji cha Ng’haya, Magu
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki anayesimamia masuala ya Afrika Mashariki Mhe. Stephen Byabato akimsikiliza mratibu wa Mradi wa Kuhimili Mabadiliko ya Tabia Nchi katika Bonde la Ziwa Bw. Ngussa Buyamba
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki anayesimamia masuala ya Afrika Mashariki Mhe. Stephen Byabato akiwasili kwenye moja ya mradi wa Kuhimili Mabadiliko ya Tabia Nchi katika Bonde la Ziwa katika kijiji cha Ng’haya, wilayani Magu
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki anayesimamia masuala ya Afrika Mashariki Mhe. Stephen Byabato akielekeza jambo alipotembelea mradi wa Kuhimili Mabadiliko ya Tabia Nchi katika Bonde la Ziwa katika kijiji cha Ng’haya, wilayani Magu
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki anayesimamia masuala ya Afrika Mashariki Mhe. Stephen Byabato akizungumza na Mkuu wa Shule ya Sekondari ya Ng’haya, wilayani Magu Bi.Glory Sulungu Daudi alipotembelea shule hiyo kwa lengo la kujionea mradi wa Kilimo bora kinachotumia mbinu za kuhimili mabadiliko ya tabianchi
 Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki anayesimamia masuala ya Afrika Mashariki Mhe. Stephen Byabato akizungumza na wanafunzi wa Sekondari ya Ng’haya, wilayani Magu
Picha ya pamoja
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki anayesimamia masuala ya Afrika Mashariki Mhe. Stephen Byabato akiwa picha ya pamoja na wanafunzi wa Sekondari ya Ng’haya, wilayani Magu.
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki anayesimamia masuala ya Afrika Mashariki Mhe. Stephen Byabato akipanda mti kwenye Shule ya Sekondari ya Ng’haya, wilayani Magu 

Wednesday, September 27, 2023

TANZANIA YASHIRIKI KWENYE MAONESHO YA KIMATAIFA YA KAHAWA NCHINI JAPAN,

TANZANIA YASHIRIKI KWENYE MAONESHO YA KIMATAIFA YA KAHAWA NCHINI JAPAN,

Mheshimiwa Baraka Luvanda, Balozi wa Tanzania nchini Japan ameungana na mabalozi pamoja na viongozi mbalimbali wa nchi zinazozalisha kahawa duniani, kwenye hafla ya ufunguzi wa Maonesho ya 20 ya Kimataifa ya Kahawa nchini Japan (2023 Japan Specialty Coffee Conference & Exhibition) iliyofanyika jijini Tokyo, Japan tarehe 27 Septemba 2023 

Uzinduzi huo umeenda sanjari na Maadhimisho ya Miaka 20 ya Maonesho hayo tangu kuanzishwa kwake mwaka 2003.

Maonesho ya Kimataifa ya Kahawa Japan yameandaliwa na Taasisi ya Kahawa ya Japan (Specialty Coffee Association of Japan – SCAJ) na kushirikisha makampuni na taasisi zinazohusika na kahawa zipatazo 250 kutoka nchi zinazozalisha kahawa duniani. Maonesho haya yanatarajiwa kuhitimishwa tarehe 29 Septemba 2023; na kuhudhuriwa na wadau wa kahawa wapatao 45,000 wakiwemo, wazalishaji, wanunuzi na wasafirishaji wa zao hilo.

Tanzania inawakilishwa na Bodi ya Kahawa Tanzania (Tanzania Coffee Board) ambayo, imeshiriki pamoja na wawakilishi wa vyama vya ushirika na makampuni ya Kitanzania yanayohusika na uzalishaji, usafirishaji, uuzaji na ufungashaji wa kahawa yakiwemo, Kagera Cooperative Union (KCU),  Kampuni ya Kaderes Peasants Development (KPD), Kampuni ya Kamal Agro, Kampuni ya TANJA, Kampuni ya Ubumwe na Kampuni ya Interbulk Packaging.

Aidha, katika maonesho hayo, Tanzania ina banda maalum la kuonesha bidhaa za kahawa zinazozalishwa Tanzania, zinajumuisha kahawa iliyochakatwa katika hatua za awali (green coffee) kutoka mikoa mbalimbali ya Tanzania. Pia, kupitia maonesho hayo inaoneshwa na kutangazwa kahawa iliyo tayari kwa ajili ya matumizi ikiwemo, kahawa mumunyifu (instant coffee) inayozalishwa na viwanda vikubwa vya kukaanga kahawa nchini Tanzania vya Amimza, Afri Café na Tanica.

Vilevile, siku ya pili ya maonesho hayo tarehe 28 Septemba 2023,  Tanzania itapata fursa ya kufanya semina maalum kuhusu kahawa ya Tanzania itakayoambatana na zoezi la uonjaji wa sampuli za kahawa za Tanzania (Tanzania Coffee Seminar and Cupping Session) kwa makampuni yapatayo 80 ya ukaangaji (coffee roasters) na usafirishaji kahawa ya nchini Japan. Katika tukio hilo, sampuli za kahawa za wazalishaji na makampuni ya Tanzania yapatayo 30 zitaoneshwa, kutangazwa na kuonjwa kwenye siku hiyo iliyotengwa maalum kwa ajili ya kuitangaza kahawa ya Tanzania. Sampuli hizo ni za kahawa ya Arabica laini (full washed), Arabica ngumu (naturals) na kahawa ya Robusta.

Maonesho haya, ni fursa adhimu katika kukuza soko la kahawa ya Tanzania nchini Japan ambayo ni kahawa pendwa iliyopewa jina maarufu la kibiashara la “Tanzania Kilimanjaro Coffee”.  Jina hili hutumika nchini Japan, kwa kahawa zinazozalishwa Tanzania pekee, kwa kutambua kivutio kikubwa cha Mlima Kilimanjaro uliopo nchini Tanzania.

Tanzania inasifika Japan kwa kutoa kahawa bora aina ya Arabica (Arabica laini - full washed na Arabica ngumu - natural) inayolimwa katika mikoa ya Kilimanjaro, Arusha, Manyara, Mara, Tanga, Morogoro, Njombe, Iringa, Katavi, Rukwa, Ruvuma, Kigoma, Songwe na Mbeya; na kahawa ya Robusta inayolimwa mkoani Kagera.



Uzinduzi wa Maonesho ya 20 ya Kimataifa ya Kahawa nchini Japan (2023 Japan Special Coffe Conference & Exhibition)
Washiriki wakiwa katika banda la Tanzania katika Maonesho ya 20 ya Kimataifa ya Kahawa nchini Japan (2023 Japan Special Coffe Conference & Exhibition)

Washirikiwakiwa katika banda la Tanzania katika Maonesho ya 20 ya Kimataifa ya Kahawa nchini Japan (2023 Japan Special Coffee Conference & Exhibition)

 

WAZIRI BYABATO AHIMIZA KASI NA UFANISI WA PROGRAMU NA MIRADI INAYOTEKELEZWA JIJINI MWANZA KUPITIA LVBC

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Stephen Byabato (Mb.) anayesimamia masuala ya Afrika Mashariki amewataka watendaji na wasimamizi wanaosimamia utekelezaji wa programu na miradi mbalimbali katika jiji la Mwanza kupitia Kamisheni ya Bonde la Ziwa Victoria (Lake Victoria Basin Commission –LVBC) kuhakikisha inatelezwa kwa kasi na ufanisi ili iwanufaishe wananchi wenye uhitaji. 

Naibu Waziri Byabato amebainisha hayo wakati akiendelea na ziara ya kikazi ya ukaguzi wa ufanisi wa programu na miradi mbalimbali inayotekelezwa katika maeneo mbalimbali ya Kanda ya Ziwa kupitia LVBC.

“Nitoe rai kwenu watendaji na wasimamizi wote wa miradi hii ya Jumuiya ya Afrika Mashariki inayotekelezwa katika Kanda ya Ziwa kupitia LVBC kuhakikisha sote kwa umoja wetu tunafanya kazi usiku na mchana kutimiza adhma ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan ya kuona Wananchi wa Tanzania wananufaika moja kwa moja na fursa zinazotokana na Jumuiya kijamii na kiuchumi. alisema Mhe. Byabato


Akiwa jijini Mwanza tarehe 26 Septemba 2023 Naibu Waziri Byabato ametembelea mradi wa ujenzi wa miundombinu ya majitaka na usafi wa mazingira chini ya programu ya pamoja ya usimamizi na uendelezaji wa Rasilimali za Maji (Lake Victoria Basin Integrated Water Resources Management Programme LVB – IWRMP) katika eneo la Pasiansi. Progamu hii inalenga kuchangia katika usimamizi endelevu wa rasilimali za maji ya Ziwa Victoria ili kuongeza ubora na upatikanaji wake kwa matumizi mbalimbali, ikihusisha usambazaji wa majisafi kwa kaya zilizopo maeneo ya milimani na ujenzi wa miundombinu ya majitaka na vyoo vya kisasa. Maeneo mengine yanayotarajia kunufaika na programu hiyo katika Jiji la Mwanza ni pamoja na Kitangiri, Mabatini, Kirumba na Nyamanoro. 


Sanjari na hayo kupitia utekelezaji wa mradi huu wa kupanua miundombinu ya majitaka katika Jiji la Mwanza wenye thamani ya shilingi bilioni 12.7 kutaweizesha Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Mwanza (MWAUWASA) kukarabati na kupanua mtandao wake wa majitaka kwa takriban 14.4km na kuunganisha kaya 1,600 kwenye mtandao huo. 

Programu na Miradi mingine aliyozitembelea Mhe. Byabato jijini Mwanza ni pamoja na; ujenzi wa Makao Makuu ya Kituo cha Uratibu wa Utafutaji wa Uokozi katika Ziwa Victoria (Maritime Rescue Coordination Centre – MRCC), Ukarabati wa Meli ya Utafiti ya Jumuiya (RV Jumuiya) iliyopo Ziwa Victoria katika Bandari ya Mwanza Kusini unaofanywa na Kampuni ya kitanzania ya Mundao Engineering na eneo la Machinjio lililopo eneo la Nyakato ikiwa ni sehemu ya Programu ya Usimamizi wa Mazingira katika Ziwa Victoria 

Katika hatua nyingine Wananchi wa Pasiansi kwa nyakati tofauti wameipongeza na kuishukuru Serikali kwa kuvutia utekelezaji wa mradi wa kupanua miundombinu ya majitaka katika Jiji la Mwanza ambao wameutaja kuleta mageuzi makubwa katika utunzaji wa mazingira na upatikanaji wa maji safi. 

“Hapo mwanzoni kabla ya kufikiwa na mradi huu sisi tunaoishi maeneo ya huku chini ya mlima tulikuwa tunaathiriwa sana na uchafu kutoka kwa wenzetu wanaoishi huko mlimani, tunaishukuru sana Serikali kwa kutekeleza mradi huu ambao umemaliza kabisa tatizo hilo, kwa sababu kila kaya imepata choo bora sambasamba na mifumo ya majitaka iliyo imara”. Alieleza Mzee William Mchomvu mkazi wa Pasiansi.

Hii ni ziara ya kwanza kwa Naibu Waziri Byabato toka ateuliwe na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kushika wadhifa wa Naibu Waziri anayesimamia masuala ya Afrika Mashariki katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki. Katika ziara hiyo Naibu Waziri Byabato ameambatana na Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Miundombinu ya Uchumi na Huduma za Jamii Mhandisi Abdillah Mataka katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki. 

Kamisheni ya Bonde la Ziwa Victoria yenye Makao Makuu yake mjini Kisumu, Kenya ilianzishwa na Nchi Wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki kwa Itifaki iliyosainiwa tarehe 29 Novemba, 2003. Jukumu la Kamisheni hiyo ni kuratibu usimamizi endelevu wa Bonde la Ziwa Victoria ikiwemo utekelezaji wa Miradi ya Mazingira, Miundombinu ya Kiuchumi na Kijamii katika Bonde la Ziwa Victoria kwa manufaa ya Nchi Wanachama hususan zinazopakana katika Bonde hilo ambazo ni Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jamhuri ya Burundi, Jamhuri ya Kenya, Jamhuri ya Rwanda na Jamhuri ya Uganda.

Kamisheni hii inaongozwa na Katibu Mtendaji ambapo kwa sasa nafasi hiyo inashikiliwa na Dkt. Masinde Bwire kutoka Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki anayesimamia masuala ya Afrika Mashariki Mhe. Stephen Byabato (Mb.) akisalimiana na watendaji mbalimbali wa Serikali wajitokeza kumpokea wakati akiwasili katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mwanza.
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki anayesimamia masuala ya Afrika Mashariki Mhe. Stephen Byabato (katikati) akiwasili katika eneo linalotarajia kujengwa Makao Makuu ya Kituo cha Uratibu wa Utafutaji wa Uokozi katika Ziwa Victoria (Maritime Rescue Coordination Centre – MRCC) jijini Mwanza.
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki anayesimamia masuala ya Afrika Mashariki Mhe. Stephen Byabato akisikiliza maelezo kuhusu mtambo wa usafishaji wa maji taka uliopo katika machinjio ya Nyakato jijini Mwanza
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki anayesimamia masuala ya Afrika Mashariki Mhe. Stephen Byabato akifuatilia maelezo kuhusu ukarabati wa Meli ya Utafiti ya Jumuiya (RV Jumuiya) unaoendelea Ziwa Victoria katika Bandari ya Mwanza Kusini
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki anayesimamia masuala ya Afrika Mashariki Mhe. Stephen Byabato akizungumza na Mzee William Mchomvu mkazi wa Pasiansi jijini Mwanza alipotembelea makazi yake kujione ufanisi wa mradi wa miundombinu ya majitaka na usafi wa mazingira
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki anayesimamia masuala ya Afrika Mashariki Mhe. Stephen Byabato akiwa katika ukaguzi wa mradi wa ujenzi wa miundombinu ya majitaka na usafi wa mazingira Pasiansi jijini Mwanza
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki anayesimamia masuala ya Afrika Mashariki Mhe. Stephen Byabato akiwasili katika Bandari ya Mwanza Kusini kuangalia Ukarabati wa Meli ya Utafiti ya Jumuiya (RV Jumuiya)
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki anayesimamia masuala ya Afrika Mashariki Mhe. Stephen Byabato akifurahia jambo na Kaptain Kwila Nkwama alipotembelea mradi wa ukarabati wa Meli ya Utafiti ya Jumuiya (RV Jumuiya)
Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Miundombinu ya Uchumi na Huduma za Jamii Mhandisi Abdillah Mataka (katikati) katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki akiwa kwenye Meli ya Utafiti ya Jumuiya (RV Jumuiya) inayoendelea na ukarabati
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki anayesimamia masuala ya Afrika Mashariki Mhe. Stephen Byabato akijadili jambo na watendaji mbalimbali wa Serikali walipotembelea eneo la ujenzi wa Makao Makuu ya Kituo cha Uratibu wa Utafutaji wa Uokozi katika Ziwa Victoria 

Tuesday, September 26, 2023

WAZIRI MAKAMBA AKUTANA NA BALOZI WA CANADA

 

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe.January Makamba (Mb.) akizungumza na Balozi wa Canada nchini Mhe. Kyle Nunas katika Ofisi ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam

Balozi wa Canada nchini Mhe. Kyle Nunas akizungumza na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. January Makamba katika Ofisi ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam


 

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe.January Makamba katika picha na Balozi wa Canada nchini Mhe. Kyle Nunas walipokutana katika Ofisi ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe.January Makamba na ujumbe wake katika picha ya pamoja na Balozi wa Canada nchini Mhe. Kyle Nunas na ujumbe wake walipokutana katika Ofisi ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam


 

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. January Makamba (Mb.) amekutana na kuzungumza na Balozi wa Canada nchini Mhe. Kyle Nunas katika Ofisi ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam.

Viongozi hao wamejadiliana njia za kuendelea kuimarisha uhusiano wa Kidiplomasia kati ya Tanzania na Canada.
 

Mhe. Balozi Nunas pia ameipongeza Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuwa mwenyeji wa mkutano wa Jukwaa la Chakula (AGRF) uliofanyika jijini Dar es Salaam mwezi Septemba 2023.

Saturday, September 16, 2023

NAIBU WAZIRI BYABATO AKUTANA NA WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA BIASHARA WA JAMAICA

Naibu Waziri Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Stephen Byabato (Mb.) akisalimiana na Waziri wa Mambo ya Nje na Biashara wa Jamaica Mhe. Kamina John Smith walipokuta pembezoni mwa Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Kundi la G77+ China unaofanyika jijini Havana nchini Cuba tarehe 16 Septemba 2023

 

Naibu Waziri Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Stephen Byabato (Mb.) akizungumza na Waziri wa Mambo ya Nje na Biashara wa Jamaica Mhe. Kamina John Smith walipokuta pembezoni mwa Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Kundi la G77+ China unaofanyika jijini Havana nchini Cuba tarehe 16 Septemba 2023

Naibu Waziri Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Stephen Byabato (Mb.) akizungumza na Waziri wa Mambo ya Nje na Biashara wa Jamaica Mhe. Kamina John Smith walipokuta pembezoni mwa Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Kundi la G77+ China unaofanyika jijini Havana nchini Cuba tarehe 16 Septemba 2023

 
Naibu Waziri Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Stephen Byabato (Mb.) katika picha na Waziri wa Mambo ya Nje na Biashara wa Jamaica Mhe. Kamina John Smith baada ya mazungumzo yao yaliyofanyika pembezoni mwa Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Kundi la G77+ China unaofanyika jijini Havana nchini Cuba tarehe 16 Septemba 2023

Naibu Waziri Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Stephen Byabato (Mb.) amekutana na kuzungumza na Waziri wa Mambo ya Nje na Biashara wa Jamaica Mhe. Kamina John Smith pembezoni mwa Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Kundi la G77+ China unaofanyika jijini Havana nchini Cuba.

Katika mazungumzo yao viongozi hao wameelezea kuridhishwa kwao na hali ya uhusiano wa kidiplomasia uliopo kati ya Tanzania na Jamaica na kuahidi kuendelea kushirikiana zaidi ili kuimarisha uhusiano huo.

Akizungumza katika kikao hicho Mhe. Byabato amemuelezea Mhe. Smith kuwa Tanzania inaridhishwa na uhusiano mzuri uliopo na kuongeza kuwa kuna haja ya kuhakikisha uhusiano huo wa kidplomasia unaimarishwa na kufikia hatua ya juu.

Amemuhakikishia utayari wa Serikali ya Tanzania kuanzisha Tume ya Kudumu ya Pamoja (JPC) na Jamaica katika maeneo yatakayozinufaisha pande zote mbili.

Pia amemuelezea nia ya Tanzania kupanua wigo wa maeneo ya ushirikiano na kuingiza sekta za uchumi wa buluu, biashara na uwekezaji.

Akizungumza katika kikao hicho Mhe. Smith alisema pamoja na uhusiano mzuri uliopo kati yake na Tanzania, Jamaica inaiomba Tanzania kuiunga mkono katika nafasi mbili inazogombea kimataifa katika Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia masuala ya Bahari (IMO) na Kamati ya Urithi wa Dunia iliyo chini ya UNESCO.

DKT. MWINYI AHUTUBIA MKUTANO WA NCHI ZA KUNDI LA G77+CHINA

 






Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dk. Hussein Ali Mwinyi akizungumza katika Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Kundi la G77+ China akimwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan jijini Havana Cuba tarehe 15 Septemba 2023


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dk. Hussein Ali Mwinyi akizungumza katika Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Kundi la G77+ China akizungumza jijini Havana Cuba tarehe 15 Septemba 2023

 



 


Washiriki wa Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Kundi la G77+ China katika picha ya pamoja jijini Havana Cuba tarehe 15 Septemba 2023


Washiriki wa Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Kundi la G77+ China katika picha ya pamoja jijini Havana Cuba tarehe 15 Septemba 2023




Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dk. Hussein Ali Mwinyi amehutubia Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Kundo la G77+ China akimwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.

 

Akihutubia katika Mkutano huo, Dkt. Mwinyi amesema Sayansi, Teknolojia na Ubunifu ni nguzo muhimu kwa nchi zinazoendelea kujiletea maendeleo ya kiuchumi na kuongeza kuwa nchi hizo zinaweza kuendelea kiuchumi kupitia maendeleo katika sekta muhimu za kilimo, nishati, elimu, afya, madini, maendeleo ya muindombinu, maji na mazingira.

Mhe. Rais Dkt. Mwinyi amekumbusha namna nchi zinazoendelea zilivyoathirika na janga la maradhi ya UVIKO-19, bidhaa kupanda bei, mizozo ya kisiasa na athari za mabadiliko ya tabia nchi na kuongeza kuwa baadhi ya changamoto zilisababisha kupanda kwa gharama za maisha na kudhoofisha jitahada za kujikwamua kiuchumi.

 

Mhe. Dkt. Mwinyi alikumbushia namna nchi zilizoendelea zilivyobanwa na teknolojia ya kutengeneza chanjo na kunyimwa msaada wa kiteknolojia ili zitengeneze chanjo zao na kusababisha kampuni za kutengeneza dawa za mataifa tajiri kupata faida kubwa kwa kuziuzia nchi zinazoendelea chanjo ya UVIKO-19.Ã¥

Mhe.Dkt. Mwinyi amezitanabaisha nchi za kundi la G77+China kuchukua changamoto hizo kama somo na zisibweteke kusubiri msaada kutoka mataifa yaliyoendelea. 

 

Mkutano huo unaofanyika jijini Havana nchini Cuba tarehe 15-16 Septemba 2023 unayakutanisha mataifa yanayoendelea unajadili changamoto zinazoikabili dunia baada ya kuathirika na janga la UVIKO-19 na migogoro inayoendelea duniani na vikwazo mbalimbali vya kiuchumi.  

 

Mkutano huo umejikita kutafuta namna bora ya kujenga ustahimilivu kupitia maendeleo ya sayansi na teknolojia na ubunifu ili kundi la G77+China liweze kufikia malengo yake kwa pamoja.

 

Kaulimbiu ya Mkutani inasema, “Changamoto za Maendeleo: Nafasi ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu”.