Friday, January 31, 2014

Mhe. Membe akutana kwa mazungumzo na Waziri wa Mambo ya Nje wa Uturuki

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Mhe. Bernard K. Membe (Mb.) akisalimiana na Waziri wa Mambo ya Nje wa Uturuki, Mhe. Ahmed Davutoglu walipokutana Mjini Addis Ababa kwa mazungumzo kuhusu kuimarisha ushirikiano kati ya Tanzania na Uturuki. Mhe. Membe yupo Addis Ababa akimwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwenye Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika (AU) uliofanyika kuanzia tarehe 30 hadi 31 Januari, 2014.
Mhe. Membe (katikati) akiwa na Mwakilishi wa Kudumu wa Tanzania kwenye Umoja wa Mataifa, Mhe. Balozi Tuvako Manongi (kushoto) pamoja na Bw. Togolani Mavura, Msaidizi wa Waziri wakati wa mazungumzo na Waziri wa Mambo ya Nje wa Uturuki (hayupo pichani)
Mhe. Membe (kushoto) akimsikiliza Mhe. Davutoglu (wa pili kulia) wakati wa mazungumzo yao.
Mhe. Membe akifurahia jambo na Mhe. Davotoglu huku akiondoka baada ya mazungumzo yao.

Mhe. Membe ahutubia Mkutano kuhusu Amani DRC na Nchi za Maziwa Makuu

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Mhe. Bernard K. Membe (Mb.) akiwa katika moja ya Mikutano ya Umoja wa Afrika inayoendelea mjini Addis Ababa, Ethiopia. Mhe. Membe alihutubia Mkutano wa Tatu wa Ngazi ya Juu kuhusu Utaratibu wa Usimamizi wa masuala ya Amani, Usalama na Ushirikiano  katika  Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) na Nchi za Kanda ya Maziwa Makuu uliofanyika mjini Addis Ababa, Ethiopia tarehe 31 Januari, 2014 pembezoni mwa Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika (AU) unaoendelea mjini hapa.
Baadhi ya Wajumbe kutoka Tanzania wakiwa kwenye Mkutano kuhusu Nchi za Ukanda wa Maziwa Makuu (ICGLR) mjini Addis Ababa. Mwenye tai nyekundu ni Bw. Robert Kahendaguza, Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Ushirikiano wa Kikanda na Balozi David Kapya.
Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Bw. Jan Eliason akizungumza wakati wa Mkutano kuhusu DRC na Nchi za Kanda ya Maziwa Makuu (ICGLR) uliofanyika Addis Ababa.
Mjumbe wa Sudan akisaini Mkataba wa Kujiunga na Mpango wa Amani, Usalama na Ushirikiano ulio chini ya ICGLR
Mjumbe Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Bibi Mary Robinson naye pia alikuwepo katika mkutano huo.
Wajumbe wengine kutoka nchi wanachama wa ICGLR wakifuatilia mkutano.
===============================




Na Mwandishi Wetu, Addis Ababa

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Mhe. Bernard K. Membe (Mb.) ametoa rai kwa Nchi za Ukanda wa Maziwa Makuu (ICGLR) kuweka nia mpya ili kutimiza lengo la kupatikana kwa amani ya kudumu katika Nchi za Ukanda huo. 

Mhe. Membe aliyasema hayo wakati akihutubia Mkutano wa Tatu wa Ngazi ya Juu kuhusu Utaratibu wa Usimamizi wa masuala ya Amani, Usalama na Ushirikiano  katika  Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) na Nchi za Kanda ya Maziwa Makuu uliofanyika mjini Addis Ababa, Ethiopia pembezoni mwa Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika (AU) unaoendelea mjini hapa.

Waziri Membe alisema kuwa kumekuwa na hatua nzuri zilizofikiwa katika kutafuta amani ya kudumu DRC na katika Kanda kwa ujumla. Hatua hizo ni pamoja na kusambaratishwa kwa kikundi cha Waasi cha M23 huko Mashariki mwa DRC. Hata hivyo alisema bado kunahitajika jitihada na nia madhubuti ili kuhakikisha migogoro isiyoisha inamalizwa kabisa. 

“Tunayashukuru Majeshi ya Ulinzi ya DRC kwa msaada wa Vikosi vya Kulinda Amani vya Umoja wa Mataifa (MUNOSCO) na kile cha FIB ambapo tumeshuhudia kusambaratishwa kwa Kikundi cha M23, tunapongeza pia jitihada za Rais wa Uganda, Mhe. Yoweri Museveni ambaye pia ni msuluhishi wa mgogoro huo kufuatia kusainiwa kwa Azimio la Amani kati ya Serikali ya DRC na M23 hapo tarehe 12 Desemba, 2013”, alisema Mhe. Membe.

Mhe. Membe aliongeza kuwa umefika wakati sasa kwa watu na nchi za Ukanda wa Maziwa Makuu  kusema inatosha kwa migogoro isiyoisha ili kuwawezesha kuwekeza nguvu na vipaji vyao katika maendeleo ya kiuchumi na kijamii.

Aidha, kwa namna ya pekee, Waziri Membe alimpongeza Mjumbe Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa katika Nchi za Ukanda wa Maziwa Makuu, Mhe. Bibi Mary Robinson na Kamati yake ya Ufundi (TSC) kwa kazi nzuri waliyoifanya mwaka 2013. Kamati hiyo ya Ufundi imefanikiwa kutoa Mpango Kazi kwa ajili ya kutekeleza Mpango wa Amani, Usalama na Ushirikiano wa Kanda.

 “Nimeridhishwa na kazi inayofanywa na Kamati hiyo ya Ufundi  kwa kutoa Mpango Kazi ambao unajitosheleza kwa ajili ya kuutekeleza  Mpango wa Amani. Hivyo, tumekutana hapa kuridhia mpango huo ili kila mmoja wetu aweke nia mpya ya kutekeleza yale yote tuliyowahi kukubaliana chini ya Mpango wa Amani” alisisitiza Waziri Membe.

Aidha, wakati wa Mkutano huo nchi za Kenya na Sudan zilisaini rasmi Mkataba wa kujiunga na Mpango wa Amani, Usalama na Ushirikiano wa Kanda ya Maziwa Makuu  ( Peace, Security and Cooperation Framework).

Mkutano huo ulihudhuriwa pia na Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Bw. Jan Eliasson.

-Mwisho-


Tanzania na Colombia zajidili namna ya kuboresha ushirikiano wa kiuchumi.


Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Mhe. Balozi Rajabu Gamaha (kulia) akibadilishana mawazo na Mkurugenzi wa Asia, Afrika na Oceania kutoka Wizara ya Mambo ya Nje ya Colombia, Bibi Sandra Salamanca. katika kikao hicho, viongozi hao walijadili namna Tanzania na Colombia zitakavyoweza kushirikiana ili kutumia fursa zinazopatikana katika nchi hizo kwa madhumuni ya kuinua kipato cha wananchi wao.


Bibi Salamanca (kulia) akisisitiza jambo huku Balozi wa Colombia nchini Tanzania mwenye makao yake Nairobi, Kenya Mhe. Maria Lugenia Correa akisikiliza kwa makini.

Mkurugenzi wa Ulaya na Amerika katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Balozi Dora Msechu akifafanua jambo katika kikao hicho huku Bw. Graison Ishengoma, Afisa Mambo ya Nje akinukuu masuala muhimu ya mazungumzo. 



Picha ya pamoja, wa tatu kutoka kulia ni Naibu Katibu Mkuu ambapo kulia kwake ni Mratibu wa Masuala ya Afrika, Mashariki ya Kati na Asia ya Kati kutoka Wizara ya Mambo ya Nje ya Colombia, Balozi Betty Escorcia.



Picha na Reginald Philip Kisaka.

Ubalozi wa China watoa msaada kwa waathirika wa mafuriko


Balozi wa China nchini Tanzania, Mhe. Lu Youping akikabidhi msaada wa vifaa mbalimbali kwa Mkurugenzi wa Idara ya Maafa, Ofisi ya Waziri Mkuu, Leteni Jenerali Sylivester Rioba. Msaada huo ambao unathamani ya Shilingi milioni 32 umetolewa kwa ajili ya watu walioathirika na mafuriko mkoani Morogoro.

Balozi wa China (katikati) akishikana mikono na Luteni Generali Rioba na Mwakilishi wa Mkuu wa Mkoa wa Morogoro ambaye ni Mkuu wa Wilaya ya Mvomero, Mhe. Athony Mtaka wakati wa hafla ya kukabidhi msaada iliyofanyika katika Ubalozi wa China. nyuma yao lori aina ya fuso likiwa limejazwa baadhi ya bidhaa za msaada huo.


Balozi wa China akikabidhi stakabadhi za vifaa vya msaada kwa Leteni Jenerali Rioba huku Mkuu wa Wilaya ya Mvomero akishuhudia.

Wanahabari nao hawakuwa mbali kushuhudia hafla ya makabidhiano.

Balozi wa China, Mhe. Lu Youping akitoa hotuba fupi.

Mkurugenzi wa Idara ya Maafa, Ofisi ya Waziri Mkuu akitoa hotuba ya kushukuru msaada uliotolewa na Balozi wa China.


Mkurugenzi wa Idara ya Asia na Australasia katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Balozi Mberwa Kairuki akisalimiana na Luteni Jenerali Rioba mara baada ya hafla ya kukabidhi msaada kukamilika.



Picha na Reginald Philip Kisaka
                                   




Thursday, January 30, 2014

Mkutano wa Wakuu wa Nchi wa AU wafunguliwa leo Addis Ababa



Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Mhe. Bernard K. Membe (Mb.) akimwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete kwenye Mkutano wa  Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika (AU) ambao  umefunguliwa  rasmi  leo tarehe 30 Januari, 2014 mjini Addis Ababa, Ethiopia.
Mwenyekiti wa Kamisheni  ya Umoja wa Afrika (AU), Mhe. Dkt. Nkosazana Dlamini-Zuma akisoma hotuba ya ufunguzi wa Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja huo mjini Addis Ababa, tarehe 30 Januari, 2014. Katika hotuba yake Dkt. Dlamini-Zuma alisisitiza umuhimu wa matumizi ya Lugha ya Kiswahili kwani ni moja ya lugha kubwa Barani Afrika.
Jopo la Marais Wastaafu wakiwa kwenye mkutano huo. Kutoka kushoto ni Mhe. Olusegun Obasanjo, Rais Mstaafu wa Nigeria, Mhe. Thabo Mbeki, Rais  Mstaafu wa Afrika Kusini na Mhe. Festus Mogae, Rais Mstaafu wa Botswana.

Rais Mpya wa Madagascar, Mhe. Henry Rajaonarimampianina akitoa hotuba yake ya shukrani kwa nchi za Afrika kwa michango yao iliyopelekea uchaguzi wa amani na demokrasia nchini Madagascar na pia kwa  Madagascar kurejea AU.
Waziri Mkuu wa Ethiopia, Mhe. hailemariam Dessalegn akitoa hotuba kama Mwenyekiti wa AU  anayemaliza muda wake kabla ya kukabidhi nafasi hiyo kwa Rais wa Mauritania, Mhe. Mohamed Ould Abdel Aziz.
Rais wa Mauritania, Mhe. Mohamed Ould Abdel Aziz  akitoa hotuba kama Mwenyekiti Mpya wa Umoja wa Afrika kwa kipindi cha mwaka mmoja hadi Januari 2015.
Picha ya Pamoja ya Viongozi wa AU.
Mhe. Membe akiongozana na Rais wa Zimbabwe, Mhe. Robert Mugabe mara baada ya hafla ya ufunguzi wa Mkutano wa Wakuu wa Nchi wa AU
Mhe. Membe akiteta jambo na Rais wa Afrika Kusini, Mhe. Jacob Zuma nje ya Ukumbi wa Mikutano wa AU.

Kiswahili chazidi kupaa Umoja wa Afrika

Na Mwandishi wetu, Addis Ababa, 30/1/2014

Umoja wa Afrika umeitaja Lugha ya Kiswahili kuwa ndiyo lugha kubwa na rasmi Afrika na ndio Lugha inayofundishwa zaidi katika Vyuo Vikuu mbalimbali duniani kutoka Afrika.

Hayo yalisemwa na Mwenyekiti wa Kamisheni ya Umoja wa Afrika (AU), Dkt. Nkosazana Dlamini-Zuma wakati akifungua Mkutano wa 22 wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika mjini Addis Ababa, Ethiopia leo tarehe 30 Januari, 2013.

Dkt. Zuma katika hotuba yake ya kusisimua ambayo ilielezea maendeleo yaliyofikiwa Afrika katika kipindi cha miaka 50 iliyopita, changamoto mbalimbali zinazolikabili Bara hili na matarajio alisema kwamba katika kipindi hiki ni muhimu kuitumia Lugha ya Kiswahili kuiunganisha Afrika.

“Wajukuu zetu waliona ni kichekesho tulivyokuwa tukihangaika na  tafsiri za Lugha za Kiingereza, Kifaransa na Kireno wakati wa mikutano ya AU, na vile tulivyokuwa tukizozana kwamba chapisho la Kiingereza halifanani na lile la Kifaransa au Kiarabu, sasa tunayo Lugha yetu pamoja na hizo lugha nyingine huo ndio ustaarabu wa sasa” alisema Dkt. Dlamini-Zuma.

Akizungumzia maendeleo yaliyofikiwa Afrika katika kipindi cha miaka 50 iliyopita, Mhe. Dkt. Dlamini-Zuma alisema  kuwa Afrika sasa imepiga hatua kubwa katika maendeleo ambapo kwa sasa Afrika ndio msafirishaji mkubwa wa chakula nje na pia imekuwa kituo cha viwanda na kituo cha maarifa na hivyo kuleta manufaa kwa maliasili zilizopo ikiwemo mazao ya kilimo kama kichocheo cha mapinduzi ya viwanda.

“Rafiki zangu, kwa hakika Afrika imepiga hatua kubwa katika maendeleo, kutoka usafirishaji wa malighafi katika kipindi kilichopita na kuwa msafirishaji mkuu wa chakula nje, hii itasaidia maliasili iliyopo Afrika kubaki na kuwa kichocheo cha mapinduzi ya viwanda” alisema Dkt. Dlamini-Zuma. Aidha aliongeza kuwa, Kampuni nyingi za Afrika kuanzia zile za madini, fedha, chakula, vinywaji, utalii, madawa, uvuvi na Teknolojia ya Habari na Mawasiliano ni miongoni mwa zinazoongoza duniani katika sekta hizo.

Dkt. Dlamini-Zuma alieleza kuwa Afrika sasa ni ya tatu duniani kiuchumi. Hata hivyo alisisitiza bado kuna umuhimu kwa nchi za Afrika kuchangia katika maendeleo. Vile vile, alisema kwamba njia pekee ya kuleta amani ni kuwekeza kwa watu hususan kuwawezesha vijana na wanawake. ‘Afrika inahitaji mapinduzi katika ujuzi kwa kubadilisha mfumo wa elimu ili kuwaandaa vijana ambao ni wabunifu na wenye mawazo ya ujasiriamali ili kuleta maendeleo katika Bara lao’ alisema Dkt. Zuma.

Kuhusu hali ya amani na usalama huko, Sudan Kusini na Jamhuri ya Afrika ya Kati, Dkt. Dlamini-Zuma alielezea kusikitishwa kwake na hali katika nchi hizo na kusisitiza umuhimu wa nchi za Afrika kufanya kazi kwa pamoja ili kuleta amani ya kudumu katika nchi hizi. 

"Tunavyouanza mwaka 2014 mioyo yetu ipo na watu wa Sudan Kusini na  wale wa Jamhuri ya Afrika Kati hususan wanawake na watoto hivyo ni muhimu tufanye kazi kwa pamoja ili nchi hizi zipate amani ya kudumu na kutimiza lengo letu la kuzima kabisa mitutu ya bunduki katika Bara letu" alisisitiza Dkt. Dlamini-Zuma.

Aidha, alimtangaza Bibi Binta Diop kuwa Mjumbe Maalum wa Amani na Usalama Afrika ambaye atakuwa na jukumu la kuhakikisha sauti za wanawake zinasikika katika masuala ya kujenga amani na utatuzi wa migogoro.

Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika pia ulishuhudia ubadilishanaji wa Uenyekiti wa Umoja wa Afrika kutoka kwa Waziri Mkuu wa Ethiopia, Mhe. Hailemariam Dessalegn kwenda  kwa   Rais wa Mauritania, Mhe. Mohamed Ould Abdel Aziz. Aidha, Mkutano huo ulimkaribisha  Rais mpya wa Madagascar, Mhe. Hery Rajaonarimampianina baada ya miaka minne ya kufutwa uanachama wa AU.

Akitoa hotuba yake kabla ya kukabidhi uenyekiti, Mhe. Dessalegn alizishukuru nchi zote za Afrika kwa ushirikiano na kusisitiza umuhimu wa kuweka vipaumbele vya maendeleo Barani Afrika katika Agenda ya Maendeleo ya Kimataifa baada ya mwaka 2015 na ile ya Malengo ya Maendeleo Endelevu.

Ujumbe wa Tanzania kwenye Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa AU uliongozwa na Mhe. Bernard K. Membe (Mb.), Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa ambaye alimwakilisha Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

-Mwisho-





Wednesday, January 29, 2014

Waziri Mkuu wa Finland ahutubia Wadau wa Maendeleo

Waziri Mkuu wa Finland akitoa mada katika kikao maaulum kilichofanyika katika Hoteli ya Hyatt Regency, Kilimanjaro. Kikao hicho kilijadili mbinu ambazo nchi za Afrika na Ulaya zikishirikiana kwa pamoja, zinaweza kuzitumia kukuza uchumi kwa faida ya wananchi wao. Katika mada yake Waziri Mkuu alisisitiza umuhimu wa kuimarisha Jumuiya za Kikanda kwa ajili ya kuleta maendeleo ya kiuchumi na utulivu wa kisiasa. Wazungumzaji wengine walisisitiza umuhimu wa Afrika na Ulaya kuwa na ushirikiano wenye uwiano sawa ambao utaleta maendeleo ya kiuchumi kwa pande zote mbili bila kudhulumiana. 





Wadau wakijadili fursa na changamoto za maendeleo katika nchi za Afrika na Ulaya.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bw. John Haule wa pili kushoto akisikiliza kwa makini michango mbalimbali kuhusu kuboresha ushirikiano wa kiuchumi baina ya nchi za Afrika na Ulaya.


Mjumbe akichangia mada.












Hafla ya Mapokezi Rasmi ya Waziri Mkuu wa Finland, Ikulu Dar es Salaam

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete aliyeketi kulia na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mhe. Sadik Meck Sadik wakijadili jambo wakati wakiwa wanamsubiri Waziri Mkuu wa Findland, Mhe. Jyrki Katainen kuwasili Ikulu, Dar es Salaam.

Rais Kikwete (kulia) akiongozana na Mgeni wake, Waziri Mkuu wa Findland kuelekea katika jukwaa maalum kwa ajili ya kupigiwa Nyimbo za Taifa na Mizinga 19 ya kumkaribisha rasmi Mhe. Waziri Mkuu nchini Tanzania. 

Rais Kikwete (kulia) na Mgeni wake, Waziri Mkuu wa Findland wakifurahia jambo huku wakielekea kwenye jukwaa maalum.

Rais Kikwete (kulia) pamoja na Mgeni wake, Waziri Mkuu wa Findland wakiwa wamesimama huku Nyimbo za Taifa za Mataifa yao zikiwa zinapigwa.


Mizinga 19 ikipigwa kwa ajili ya heshima ya Waziri Mkuu wa Findland.

Waziri Mkuu wa Findland anakagua gwaride.

Waziri Mkuu wa Findland akiwapungia viongozi na watu wengeine wakati alipokuwa anaingia Ikulu, Dar es Salaam.

Mazungumzo Rasmi


Rais Kikwete akitambulisha ujumbe wake kwa Waziri Mkuu wa Findland hayupo pichani kabla ya kuanza mazungumzo rasmi Ikulu, Dar es Salaam.

Ujumbe wa Rais Kikwete katika mazungumzo rasmi, kushoto ni Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Mhe. Dkt. Mahadhi Juma Maalim (Mb).

Wajumbe wengine.

Ujumbe wa Tanzania (kulia) pamoja na ule wa Finland katika mazungumzo rasmi Ikulu, Dar es Salaam.

Mhe. Membe kumwakilisha Mhe. Rais Kikwete Mkutano wa Wakuu wa Nchi wa AU

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Mhe. Bbernard K. Membe (Mb) akiwa katika moja ya vikao vya Baraza la Mawaziri wa Umoja wa Afrika (AU) mjini Addis Ababa. Mhe. Membe atamwakilisha Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwenye Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika unaofanyika kuanzia tarehe 30 hadi 31 Januari, 2014 mjini hapa.

==========================


WAZIRI MEMBE KUMWAKILISHA MHE. RAIS KIKWETE MKUTANO WA WAKUU WA NCHI WA AU ADDIS ABABA.

Na Mwandishi wetu, Addis Ababa

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Mhe. Bernard K. Membe (Mb.) atamwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete kwenye Mkutano wa 22 wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika (AU) unaotarajiwa kuanza kesho Alhamisi tarehe 30 Januari, 2014 mjini Addis Ababa, Ethiopia.

Mkutano huo ulitanguliwa na Mkutano wa Baraza la Mawaziri wa AU uliofanyika tarehe 27 na 28 Januari, 2014 ambao Mhe. Membe aliongoza ujumbe wa Tanzania kwenye mkutano huo.

Kaulimbiu ya Mkutano wa mwaka huu ni “Kilimo na Usalama wa Chakula” unalenga kuweka mikakati madhubuti katika kuhakikisha kilimo kinakuwa mkombozi wa watu Barani Afrika kwa kuwainua kiuchumi na kuondokana na wasiwasi wa njaa unaolikabili Bara hili mara kwa mara.

Mkutano wa Wakuu wa nchi pia utapokea Ripoti mbalimbali ikiwemo ile ya Kamati ya Kimataifa ya Wakuu wa Nchi za Afrika kuhusu Mabadiliko ya Tabianchi (CAHOSCC) iliyokuwa chini ya Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mkutano huo wa Wakuu wa Nchi na Serikali unatarajiwa kumalizika tarehe 31 Januari, 2013.

-Mwisho-




Waziri Mkuu wa Findland awasili Tanzania kwa ziara ya kikazi ya siku mbili

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Mizengo Peter Pinda (Mb), mwenye tai nyekundu akiongozana na Waziri Mkuu wa Findland, Mhe. Jyrki Katainen ambaye amewasili nchini Tanzania usiku wa tarehe 29 Januari, 2014 kwa ziara ya kikazi ya siku mbili.


Waziri Mkuu wa Findland, Mhe. Jyrki Katainen wa kwanza kushoto akipeana mkono na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Mhe. Dkt. Mahadhi Juma Maalim (Mb) katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere alipowasili kwa ziara ya kikazi. Anayeangalia kulia ni Balozi wa Tanzania nchini Sweden, Mhe. Mohammed Mzale.


Mhe. Katainen akiendelea kusalimiana na viongozi waliojitokeza katika Uwanja wa Ndege kwa ajili ya kumlaki. Katika picha hii, Mhe. Waziri Mkuu anasalimiana na Mkurugenzi wa Idara ya Ulaya na Amerika katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa Balozi Dora Msechu.

Salamu zinaendelea, Bibi Victoria Mwakasege, Mkurugenzi Msaidizi katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa naye akisalimiana na Waziri Mkuu wa Findland

Mhe. Mizengo Peter Pinda, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aliyeketi kulia akibadilishana mawazo na mgeni wake Waziri Mkuu wa Findland alipowasili nchini usiku wa tarehe 29 Januari, 2014