Sunday, July 30, 2023

TANZANIA NA ALGERIA KUIMARISHA DIPLOMASIA YA UCHUMI


Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Watu wa Algeria zimesisitiza umuhimu wa kukuza diplomasia ya uchumi wakati wa hafla ya ufunguzi wa Mkutano wa Tano wa Tume ya Pamoja ya Kudumu ya Ushirikiano (JPC) kati ya Nchi hizo mbili ngazi ya Maafisa Waandamizi unaoendelea jijini Algiers, Algeria.

Mkutano huo ni maandalizi ya Mkutano Ngazi ya Mawaziri utakaofanyika tarehe 1 Agosti 2023 nchini humo ambapo ujumbe wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania unatarajiwa kuongozwa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Stergomena Tax (Mb.).

Ujumbe wa Tanzania katika ngazi ya Maafisa Waandamizi umeongozwa na Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Dkt. Samwel Shelukindo. Viongozi wengine walioshiriki mkutano huo ni: Naibu Makatibu Wakuu kutoka sekta za Elimu, Sayansi na Teknolojia; Mambo ya Ndani ya Nchi, na Nishati.

Aidha, kwa upande wa Serikali ya Algeria, Mkutano huo ulifunguliwa na Mkurugenzi Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje, Balozi Selma Malika na kuhudhuriwa na Viongozi Waandamizi kutoka nchini humo.

Akifungua mkutano huo Balozi Shelukindo ameeleza kuwa ushirikiano uliopo kati ya Tanzania na Algeria ni wa kihistoria na uliojengwa katika misingi imara na waasisi wa mataifa hayo mawili, Hayati Mwl. Julius Kambarage Nyerere wa Tanzania na Hayati Ahmed Ben Bella.

Pia amesema Tanzania imejikita katika mageuzi ya kisekta hususan katika sekta za kilimo, utalii na taasisi za fedha ili kuiwezesha sekta binafsi kukuza uchumi wa Taifa. Pia inaendelea na ujenzi wa miundombinu ili kurahisisha mawasiliano kupitia usafiri wa barabara, reli, maji na anga.

‘’Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan imeweka msisitizo wa kuimarisha sekta za uzalishaji na kuweka mpango wa usimamizi katika masuala ya biashara, uwekezaji na uchumi wa viwanda,’’ Alisema Balozi Shelukindo.

Naye Balozi Selma Malika katika hotuba yake ameeleza kuwa mkutano huu wa tano unaonesha utayari wa pande zote mbili katika kukuza ushirikiano wenye tija kwa maslahi ya watu wake.

‘’Serikali ya Algeria itaendelea kuhuisha na kuimarisha ushirikiano na Serikali ya Tanzania katika masuala ya diplomasia, biashara, mafunzo ya kujenga uwezo na tafiti, ufadhili katika elimu ya juu na kuongeza maeneo mapya ya ushirikiano kila inapohitajika ili kujenga uchumi imara wa mataifa yetu,’’ alisema Balozi Selma Malika.

Aidha, kupitia mkutano huu Balozi Shelukindo amewasilisha salamu za pole kwa Serikali ya Algeria kufuatia tukio la janga la moto lililotokea katika mikoa ya Bejaia, Jijel, Bouira, Media, Skikda na Tiziozou ulilosababishwa na ongezeko la joto kali. 

Tanzania na Algeria zinashirikiana katika sekta za Biashara, viwanda, kilimo, miundombinu, nishati, madini, utalii, sanaa na utamaduni, elimu, sayansi na teknolojia, ulinzi na usalama, siasa na diplomasia, mawasiliano, uvuvi, uwekezaji na maendeleo ya jamii.


===============================================


Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Dkt. Samwel Shelukindo akihutubia wakati wa ufunguzi wa  Mkutano wa Tano wa Tume ya Pamoja ya Kudumu ya Ushirikiano (JPC) kati ya Tanzania na Algeria Ngazi ya Maafisa Waandamizi, uliofanyika tarehe 30 Julai, 2023 jijini Algiers, Algeria. Kushoto ni Mkurugenzi Idara ya Afrika katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Naimi Aziz akifatilia  ufunguzi huo.



Mkurugenzi Mkuu katika Wizara ya Mambo ya Nje ya Algeria, Balozi Selma Malika akihutubia wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa Tano wa Tume ya Pamoja ya Kudumu ya Ushirikiano (JPC) kati ya Tanzania na Algeria Ngazi ya Maafisa Waandamizi uliofanyika  tarehe 30 Julai, 2023 jijini Algiers, Algeria. Kushoto ni Balozi wa Algeria nchini Tanzania, Mhe. Ahmed Djellal akifuatilia ufunguzi huo.


Kutoka kulia ni Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Nishati, Bw. Athumani Mbuttuka na Balozi wa Tanzania nchini Algeria, Mhe. Mej. Jen. (Mst) Jacob Kingu wakifuatilia Mkutano wa Tano wa Tume ya Pamoja ya Kudumu ya Ushirikiano (JPC) kati ya Tanzania na Algeria Ngazi ya Maafisa Waandamizi unaofanyika tarehe 30 Julai, 2023 jijini Algiers, Algeria.


Maafisa Waandamizi kutoka Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa wakifatilia mkutano.


Kutoka kushoto ni Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Dkt. Isaac Kazi na Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. James Mdoe wakifuatilia Mkutano wa Tano wa Tume ya Pamoja ya Kudumu ya Ushirikiano (JPC) kati ya Tanzania na Algeria Ngazi ya Maafisa Waandamizi unaofanyika tarehe 30 Julai, 2023 jijini Algiers, Algeria.


Kushoto ni Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Afrika katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mshariki, Bi. Lilian Mukasa akifuatilia Mkutano wa Tano wa JPC kati ya Tanzania na Algeria unaofanyika jijini Algiers, Algeria.


Sehemu nyingine ya ujumbe wa Tanzania


Mkutano ukiendelea.

Ujumbe wa Tanzania

Ujumbe wa Tanzania
Ujumbe wa Algeria ukifuatilia hafla ya ufunguzi wa mkutano huo.

Sehemu nyingine ya ujumbe wa Algeria.


Friday, July 28, 2023

TANZANIA YAPONGEZWA KWA MAGEUZI MAKUBWA SEKTA YA AFYA

Serikali ya Tanzania imepongezwa kwa kufanya mageuzi makubwa katika Sekta ya Afya pamoja na kutoa ushirikiano kwa mashirika ya kimataifa hususan Shirika la Afya Duniani (WHO). 

Pongezi hizo zimetolewa na Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Afya Duniani (WHO) nchini, Dkt. Charles Sagoe-Moses wakati wa kuwasilisha Hati za Utambulisho kwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Stergomena Tax (Mb.) katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam tarehe 28 julai 2023.

"Ninaipongeza Serikali ya Tanzania kwa ushirikiano wenu ambao mmekuwa mkiutoa kwa Shirika la Afya Duniani, hakika tunaahidi kuendelea kufanya kazi kwa bidii na ushirikiano katika kuhakikisha kuwa tunaboresha na kuimarisha misingi ya sekta ya afya hapa Tanzania,” amesema Dkt. Sagoe-Moses

Dkt. Sagoe-Moses ameongeza kuwa juhudi za Serikali ya Tanzania katika kukabiliana na magonjwa ya mbalimbali hususan yale ya mlipuko ni nzuri na zinaridhisha, mfano mzuri ni jinsi Tanzania ilivyopambana na homa ya Marburg katika mkoa wa Kagera. 

“WHO tutaendelea kushirikiana na Serikali ya Tanzania katika kukinga na kutibu magonjwa mbalimbali ili kuhakikisha kuwa afya za watanzania zinakuwa bora wakati wote,” aliongeza Dkt. Sagoe-Moses.

Naye Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dkt. Stergomena Tax amemhakikishia ushirikiano wa kutosha kutoka kwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa utekelezaji wa majukumu yake hapa nchini.

Dkt. Tax amesema kuwa Tanzania itaendelea kufanya kazi na WHO ili kuhakikisha kuwa inaboresha na kuimarisha mifumo ya afya na Sekta ya afya kwa ujumla pamoja na kuwajengea uwezo wataalam wa sekta ya afya ili kuwawezesha kukabiliana na kudhibiti magonjwa mbalimbali yanayoibuka katika jamii.  

“Tanzania na Shirika la Afya Duniani zimekuwa zikishirikiana katika kuimarisha na kuboresha sekta ya afya nchini, mchango wa WHO ni mkubwa na umeisadia Serikali kuboresha sekta ya afya na utekelezaji wa afua mbalimbali za mapambano dhidi ya magonjwa…..mfano mzuri tumekuwa tukishirikiana katika kutokomeza Malaria, Uviko 19 na magonjwa mengine kama vile HIV, ” alisema Dkt. Tax.

Tanzania imekuwa ikishirikiana na WHO pamoja na wadau wengine wa ndani na nje ya nchi kuhakikisha kuwa inaboresha mifumo ya afya na Sekta ya afya ili kuijengea uwezo nchi na wataalam wake katika kutambua na kudhibiti magonjwa.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Stergomena Tax (Mb.) akipokea Hati za Utambulisho kutoka kwa Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Afya Duniani (WHO) nchini, Dkt. Charles Sagoe-Moses katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Stergomena Tax akizungumza na Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Afya Duniani (WHO) nchini, Dkt. Charles Sagoe-Moses katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Stergomena Tax akizungumza na Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Afya Duniani (WHO) nchini, Dkt. Charles Sagoe-Moses katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam

Mazungumzo ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Stergomena Tax na Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Afya Duniani (WHO) nchini, Dkt. Charles Sagoe-Moses yakiendelea katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Stergomena Tax katika picha ya pamoja na Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Afya Duniani (WHO) nchini, Dkt. Charles Sagoe-Moses  katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Stergomena Tax katika picha ya pamoja na Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Afya Duniani (WHO) nchini, Dkt. Charles Sagoe-Moses  pamoja na watumishi wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki na watumishi kutoka WHO 


Wednesday, July 26, 2023

MHE. MARIAM CHABI TALATA AREJEA BENIN

Makamu wa Rais wa Benin, Mheshimiwa Mariam Chabi Talata ameondoka nchini na kurejea Benin baada ya kumalizika kwa Mkutano wa Wakuu wa Nchi kuhusu Rasilimali Watu (Africa Human Capital Heads of State Summit) ulianza tarehe 25 na kumalizika tarehe 26 Julai 2023.

Katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere Dar es Salaam, Mhe. Mariam Chabi amesindikizwa na Waziri wa Maji, Mhe. Juma Aweso (Mb.), Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mhe. Albert Chalamila na viongozi mbalimbali waandamizi wa Serikali.

Makamu wa Rais wa Benin, Mheshimiwa Mariam Chabi Talata akiwasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere tayari kuondoka nchini Tanzania na kurejea Benin baada ya kumalizika kwa Mkutano wa Wakuu wa Nchi kuhusu Rasilimali Watu (Africa Human Capital Heads of State Summit) ulianza tarehe 25 na kumalizika tarehe 26 Julai 2023


Makamu wa Rais wa Benin, Mheshimiwa Mariam Chabi Talata akizungumza na Waziri wa Maji Mhe. Juma Aweso, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mhe. Albert Chalamila kabla ya kuondoka nchini na kurejea Benin baada ya kumalizika kwa Mkutano wa Wakuu wa Nchi kuhusu Rasilimali Watu (Africa Human Capital Heads of State Summit) ulianza tarehe 25 na kumalizika tarehe 26 Julai 2023










RAIS NYUSI AREJEA NCHINI MSUMBIJI

Rais wa Jamhuri ya Msumbiji, Mheshimiwa Filipe Jacinto Nyusi ameondoka nchini baada ya kumalizika kwa Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali kuhusu Rasilimali Watu (Africa Human Capital Heads of State Summit) uliofanyika jijini Dar es Salaam tarehe 25 na 26 Julai, 2023.

Katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere Dar es Salaam , Mhe. Rais Nyusi amesindikizwa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Stergomena Tax (Mb.), Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Mhe. Albert Chalamila na Balozi wa Tanzania nchini Msumbiji, Mhe. Faustine Kasike.

Rais wa Jamhuri ya Msumbiji, Mheshimiwa Filipe Jacinto Nyusi akisindikizwa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Stergomena Tax wakati wa kuondoka nchini na kurejea Msumbiji mara baada ya kumalizika kwa Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali kuhusu Rasilimali Watu (Africa Human Capital Heads of State Summit) uliofanyika jijini Dar es Salaam tarehe 25 na 26 Julai, 2023



Rais wa Jamhuri ya Msumbiji, Mheshimiwa Filipe Jacinto Nyusi akiagana na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Stergomena Tax wakati wa kuondoka nchini na kurejea Msumbiji baada ya kumalizika kwa Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali kuhusu Rasilimali Watu (Africa Human Capital Heads of State Summit)

Rais wa Jamhuri ya Msumbiji, Mheshimiwa Filipe Jacinto Nyusi akiagana na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Stergomena Tax wakati wa kuondoka nchini na kurejea Msumbiji baada ya kumalizika kwa Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali kuhusu Rasilimali Watu (Africa Human Capital Heads of State Summit)

Rais wa Jamhuri ya Msumbiji, Mheshimiwa Filipe Jacinto Nyusi akiwaaga watanzania wakati wa kuondoka nchini na kurejea Msumbiji baada ya kumalizika kwa Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali kuhusu Rasilimali Watu (Africa Human Capital Heads of State Summit)

Rais wa Jamhuri ya Msumbiji, Mheshimiwa Filipe Jacinto Nyusi akiwaaga watanzania wakati wa kuondoka nchini na kurejea Msumbiji baada ya kumalizika kwa Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali kuhusu Rasilimali Watu (Africa Human Capital Heads of State Summit)

Viongozi mbalimbali wakiongozwa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Stergomena Tax wakimuaga Rais wa Jamhuri ya Msumbiji, Mheshimiwa Filipe Jacinto Nyusi


MHE. RAIS SAMIA AFUNGUA RASMI MKUTANO WA WAKUU WA NCHI ZA AFRIKA KUHUSU RASILIMALI WATU

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ametoa rai kwa nchi za Afrika kuwekeza zaidi katika kuboresha afya, elimu na lishe kwa watu wake ili kutengeneza rasilimali watu inayoweza kuchangia maendeleo na ukuaji wa uchumi barani Afrika.

 

Rai hiyo ameitoa jijini Dar es Salaam leo tarehe 26 Julai 2023 wakati akifungua rasmi Mkutano wa Wakuu wa Nchi za Afrika kuhusu Rasilimali Watu uliofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere.

 

Amesema Mkutano huu umetoa fursa kwa nchi za Afrika kujadili na kupanga mikakati mipya ya namna ya kutumia Rasilimali Watu ambayo Afrika imejaliwa kuwa nayo kama nyenzo muhimu katika kuchangia maendeleo na mafanikio ya Bara la Afrika.

 

Ameongeza kusema kwa upande wa Tanzania tayari mikakati mbalimbali imewekwa ya kuendeleza Rasilmali Watu ikiwemo kutenga fedha kwa ajili ya kuongeza afua za lishe na huduma za afya ya mama na mtoto ambapo amesema ameingia mkataba na Wakuu wa Mikoa kuhakikisha wanasimamia suala hili katika mikoa yao.

 

Amesema ifikapo mwaka 2050 Afrika itakuwa na asilimia 42 ya vijana duniani kote hivyo uwekezaji kwenye rasilimali watu yenye tija unahitajika ili kuwa na hatima nzuri. Amesema jitihada zaidi zinahitajika ili kuepuka kuzalisha vijana wasio na ujuzi, wasio ajirika na vijana wenye kujiingiza kwenye vitendo viovu vya kihalifu na uvunjifu wa amani.

 

Ameongeza kusema uwekezaji kwenye rasilimali watu unaanza tangu mtoto anapozaliwa kwa kumpatia lishe bora na chanjo stahiki ili kuondoa udumavu ambao husababisha upungufu wa uelewa na uwezo wa kusoma vizuri kwa watoto. Pia amesisitiza kuwekeza katika elimu ya awali ambayo ni msingi wa kuwaandaa watoto kimwili, kiakili, kihisia na kiubunifu.

 

Kadhalika ameeleza kuwa Tanzania inaendelea kuboresha utoaji huduma za jamii na kufanya maboresho ya miundombinu kama madarasa, vituo vya afya, kutoa mafunzo kwa wafanyakazi wa sekta ya elimu na afya na kutekeleza mpango wa elimu bure kwa shule za msingi hadi sekondari.

 

Awali akizungumza, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki amemshukuru Mhe. Rais Samia kwa kuridhia Tanzania kuwa mwenyeji wa Mkutano huo muhimu ambao amesema umehudhuriwa na zaidi ya Washiriki 2,500. Pia ameipongeza na kuishukuru Benki ya Dunia kwa kuandaa mkutano huo kwa kushirikiana na Serikali ya Tanzania.

 

Amesema Mkutano huo ni jukwaa kwa nchi za Afrika kupanga mikakati bora zaidi ya kuendeleza rasilimali watu kwa maendeleo endelevu ya Bara la Afrika.

 

Naye Makamu wa Rais wa Benki ya Dunia anayesimamia Kanda ya Mashariki na Kusini mwa Afrika, Bi. Victoria Kwakwa amesma Benki hiyo itaendelea kushirikiana na kuunga mkono jitihada mbalimbali zinazofanywa na Nchi za Afrika katika kuendeleza rasilimali watu ili hatimaye kuwa na maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

 

Mkutano huo ambao umehudhuriwa na Wakuu wa Nchi kutoka Nchi sita za Kenya, Madagascar, Sao Tome na Principe, Sierra Leone, Malawi na Msumbiji na wadau mbalimbali kutoka sekta binafsi naza umma umemalizika kwa kupitishwa kwa Azimio la Dar es Salaam ambalo limeainisha mikakati ya kuboresha maendeleo ya rasilimali watu barani Afrika.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akifungua rasmi Mkutano wa Wakuu wa Nchi wa Afrika Kuhusu Rasililmali Watu uliofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Julius Nyerere jijini Dar es Salaam tarehe 26 Julai 2023

Mhe. Rais Samia akihutubia mkutano
 
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Stergomena Tax akitoa neno la utangulizi wakati wa Mkutano wa Wakuu wa Nchi za Afrika kuhusu Rasilimali Watu kabla ya kumkaribisha Mhe. Rais Samia kufungua rasmi mkutano huo.
 
Rais wa Benki ya Dunia anayesimamia Kanda ya Mashariki na Kusini mwa Afrika, Bi. Victoria Kwakwa akizungumza wakati wa Mkutano wa Wakuu wa Nchi za Afrika kuhusu Rasilimali Watu
 
Marais kutoka Nchi za Afrika ni miongoni mwa viongozi waliohudhuria Mkutano wa Wakuu wa Nchi za Afrika kuhusu Rasilimali Watu. Kutoka kushoto ni Rais wa Kenya, Mhe. William Ruto, Rais wa Malawi, Mhe. Lazarus Chakwera na Rais wa Msumbiji, Mhe. Filipe Nyusi
 
Mhe. Rais Dkt. Samia (wa nne kushoto) akiwa na Marais walioshiriki Mkutano wa Wakuu wa Nchi za Afrika kuhusu Rasilimali Watu. Kutoka kushoto ni Mhe. Rais Ruto, Mhe. Rais Chakwera, Mhe. Rais Nyusi, Mhe. Rais Andry Rajoelina wa Madagascar, Mhe. Rais Carlos Vila Nova wa Sao Tome na Principe na Mhe. Rais Julius Maada Bio wa Sierra Leone

Mhe. Dkt. Tax akiteta jambo na Mhe. William Lukuvi

Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Dkt. Samwel Shelukindo akifurahia jambo kwa pamoja na Mkurugenzi wa Kitengo cha Mawasiliani Serikalini katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mindi Kasiga wakati wa Mkutano wa Wakuu wa Nchi za Afrika kuhusu Rasilimali Watu.

Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Fatma Mohammed Rajab akiwa na Balozi wa Tanzania nchini Malawi, Mhe. Agnes Kayola wakati wa Mkutano wa Wakuu wa Nchi za Afrika kuhusu Rasilimali Watu.
Mkutano ukiendelea
Wageni waalikwa wakishiriki Mkutano wa Wakuu wa Nchi za Afrika kuhusu Rasilimali Watu.

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mhe. Albert Chalamila akishiriki Mkutano wa Wakuu wa Nchi za Afrika kuhusu Rasilimali Watu.

Katibu Mkuu, Balozi Dkt. Shelukindo akisalimiana na Balozi wa Tanzania nchini Zambia, Mhe. Mathew Mkingule wakati wa Mkutano wa Wakuu wa Nchi za Afrika kuhusu Rasilimali Watu. Anayeshuhudia  katikati ni Balozi Kasiga

Balozi wa Afrika Kusini nchini, Mhe. Noluthando Mayende-Malepe akishiriki Mkutano wa Wakuu wa Nchi za Afrika kuhusu Rasilimali Watu.

Mkurugenzi wa Idara ya Ulaya na Amerika katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Swahiba Mndeme (kushoto) akiwa Mkurugenzi wa Idara ya Mashariki ya Kati, Balozi Mteule, Iman Njalikai wakati wa Mkutano wa Wakuu wa Nchi za Afrika kuhusu Rasilimali Watu.

Mkurugenzi wa Kitengo cha Diaspora katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikino wa Afrika Mashariki, Balozi James Bwana akishiriki  Mkutano wa Wakuu wa Nchi za Afrika kuhusu Rasilimali Watu.

Mkurugenzi wa Idara ya Asia na Australasia katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Caesar Waitara akishiriki Mkutano wa Wakuu wa Nchi za Afrika kuhusu Rasilimali Watu.

Picha ya pamoja

Picha ya pamoja

Picha ya pamoja