Wednesday, December 27, 2023

UMOJA WA MABALOZI WA AFRIKA WAKABIDHI MSAADA HANANG

Umoja wa Mabalozi wa nchi za Afrika wanaoziwakilisha nchi zao Tanzania wamekabidhi msaada wa mifuko 1,000 ya saruji kwa ajili ya kusaidia ujenzi wa nyumba kwa wananchi waliokumbwa na mafuruko na maporomoko ya udongo katika eneo la Katesh Wilayani Hanang mkoa wa Manyara.

Akikabidhi msaada huo kwa Serikali, Kiongozi wa Mabalozi hao na Balozi wa Visiwa vya Comoro nchini, Mhe. Dkt. Ahamada El Badaoui Mohamed amesema kundi la Mabalozi wa nchi za Afrika wanaowakilisha nchi zao Tanzania lina mabalozi 24 ambao wameonesha kuguswa na mafuriko yaliyotokea Katesh na kuona ni vyema kuwasaidia wananchi hao pamoja na Serikali kwa ujumla kwa kuchangia mifuko 1,000 ya saruji.

Dkt. El Badaoui Mohamed amesema umoja wa Mabalozi wa Afrika nchini wameguswa na mafuriko yaliyotokea Katesh na kwa umoja wao wamechangia  mifuko 1,000 ya saruji kwa ajili ya kuwasaidia wananchi wa eneo la Katesh ili kurejesha makazi ya wananchi hao.

“Tunaendelea kuomba Mungu awajalie subira na kwa wale waliopoteza maisha wapumzike kwa amani. Kadhalika, kwa waliosalia basi msaada huo utawasaidia kujenga makazi yao na kuendelea na maisha kama ilivyokuwa awali,” alisema Dkt. El Badaoui Mohamed  

Kwa upande wake Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk (Mb.) aliyepokea msaada huo kwa niaba ya Serikali amewashukuru mabalozi hao kwa umoja wao na kwa msaada huo ambao utasaidia kurejesha makazi ya wananchi wa Katesh.

Balozi Mbarouk aliongeza kuwa baada ya kupokelewa utaratibu utafanyika kwa kushirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu, Idara ya Maafa ili mifuko hiyo iwasilishwe katika Kijiji cha Katesh, Wilayani Hanang.

“Tunashukuru sana kwa msaada huu, baada ya kutokea kwa maafa yale sote tunajua Serikali imekuwa ikifanya juhudi kubwa kuhakikisha maisha ya watu yanarejea katika hali ya kawaida. Msaada huu utasaidia katika ujezi wa nyumba zilizoathiriwa na mafuriko hayo,” alisema Mhe. Balozi Mbarouk.

Balozi Mbaorouk amesema msaada huo ni uthibitisho kwamba uhusiano kati ya Balozi zote zilizopo nchini hususan Balozi za Afrika ni mzuri na kwa msaada huo wameonesha ushirikiano mkubwa na Serikali ya Tanzania.  

Tarehe 02 Disemba 2023 eneo la Katesh, Wilaya ya Hanang mkoani Manyara, lilikumbwa na mafuriko kutokana na mvua kubwa iliyonyesha na kusababisha vifo vya watu 89, kujeruhi wakazi wa eneo hilo na kuharibu makazi na mazao yao 

Msaada huo walioukabidhi kwa Serikali ni utekelezaji wa ahadi waliyoitoa, tarehe 7 Disemba 2023, wakati Waziri wa Mambo ya Nje  na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. January Makamba alipokutana na Jumuiya ya wana diplomasia nchini ili kuwapa taarifa rasmi ya Serikali juu ya tukio hilo na hatua zilizochukuliwa na Serikali baada ya kutokea kwa maporomoko ya tope kutoka mlima Hanang kufuatia mvua kubwa iliyonyesha Mkoani Manyara tarehe 02 Disemba, 2023.

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk (Mb.) akizungumza na Kiongozi wa Mabalozi na Balozi wa Visiwa vya Comoro nchini, Mhe. Dkt. Ahamada El Badaoui Mohamed katika Ofisi Ndogo za Wizara JIjini Dar es Salaam

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk (Mb.) akizungumza na Kiongozi wa Mabalozi na Balozi wa Visiwa vya Comoro nchini, Mhe. Dkt. Ahamada El Badaoui Mohamed katika Ofisi Ndogo za Wizara JIjini Dar es Salaam

Kiongozi wa Mabalozi na Balozi wa Visiwa vya Comoro nchini, Mhe. Dkt. Ahamada El Badaoui Mohamed akimueleza jamba Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk katika Ofisi Ndogo za Wizara JIjini Dar es Salaam

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk akiangalia nyaraka za msaada wa mifuko 1,000 ya saruji baada ya kukabidhiwa na Kiongozi wa Mabalozi na Balozi wa Visiwa vya Comoro nchini, Mhe. Dkt. Ahamada El Badaoui Mohamed. Kushoto ni Balozi wa Rwanda nchini, Mhe. Fatou Harerimana.

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk katika picha ya pamoja na Kiongozi wa Mabalozi na Balozi wa Visiwa vya Comoro nchini, Mhe. Dkt. Ahamada El Badaoui Mohamed, Balozi wa Rwanda nchini, Mhe. Fatou Harerimana pamoja Naibu Katibu MKuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Said Mussa Shaib






Thursday, December 21, 2023

TANZANIA YASAINI MKATABA MPYA WA UBIA NA NCHI ZA OACPS, EU

    Balozi wa Tanzania nchini Ubelgiji, Luxembourg na Mwakilishi kwenye Umoja wa Ulaya na Jumuiya  ya Nchi za Afrika, Caribbean na Pacific (OACPS) Mhe. Jestas Abuok Nyamanga, akisaini kwa niaba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mkataba Mpya wa Ubia baina ya Nchi za OACPS na Umoja wa Ulaya (Mkataba wa Samoa). Hafla ya kusaini Mkataba huo ilfanyika tarehe 19 Desemba 2023  katika Makao Makuu ya OACPS Brussels Ubelgiji. Wanaoshuhudia tukio hilo ni maafisa waandamizi kutoka Sekretarieti ya OACPS na Umoja wa Ulaya.

  

Balozi wa Tanzania nchini Ubelgiji, Luxembourg na Mwakilishi kwenye Umoja wa Ulaya na Jumuiya ya Nchi za Afrika, Caribbean na Pacific (OACPS) Mhe. Jestas Abuok Nyamanga, akisaini kwa niaba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mkataba Mpya wa Ubia baina ya Nchi za OACPS na Umoja wa Ulaya (Mkataba wa Samoa).


Mhe. Balozi Jestas Abuok Nyamanga (katikati) ameshika Mkataba Mpya wa Ubia baina ya Nchi Wanachama wa Jumuiya ya Afrika, Caribbean na Pacific (OACPS) na Umoja wa Ulaya baada ya kusainiwa katika hafla fupi iliyofanyika Makao Makuu ya Jumuiya ya Afrika Caribbean na Pacific, jijini Brussels Ubelgiji tarehe 19 Desemba 2023. Waliosimama pamoja naye ni wawakilishi kutoka Umoja wa Ulaya na OACPS.



Kaimu Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Nchi za Afrika, Caribbean na Pacific (OACPS) Dkt. Ibrahim Richard akimpa mkono kumpongeza Mhe. Balozi Jestas Abuok Nyamanga baada ya kusaini mkataba huo kwa niaba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mhe.Balozi Jestas Abuok Nyamanga katika picha ya pamoja na baadhi ya wafanyakazi wa Ubalozi wa Tanzania, Brussels baada ya kusaini Mkataba Mpya wa Ubia baina ya Jumuiya ya Nchi za Afrika, Caribbean na Pacific (OACPS) na Umoja wa Ulaya katika hafla iliyofanyika katika Makao Makuu ya OACPS Brussels tarehe 19 Desemba 2023. Aliyesimama kulia kwa Balozi Nyamanga ni Dkt. Ibrahim Richard Kaimu Katibu Mkuu wa OACPS.





Wednesday, December 20, 2023

BALOZI MBAROUK ASAINI KITABU CHA MAOMBOLEZO UBALOZI WA KUWAIT

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk (Mb.) amesaini kitabu cha maombolezo Ubalozi wa Kuwait Jijini Dar es Salaam kufuatia kifo cha Amir wa Kuwait, Sheikh Nawaf al-Ahmad Al-Sabah.

Kiongozi huyo alifariki tarehe 16 Disemba 2023 akiwa na umri wa miaka 86 ambapo aliongoza taifa hilo kwa miaka mitatu iliyopita. 

Balozi Mbarouk ametoa salamu za pole za Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa Balozi wa Kuwait nchini, Mhe. Mubarak Mohammed Alsehaijan ambapo amemuelezea kiongozi huyo atakumbukwa daima kama mwanadiplomasia na kiongozi imara aliyejitolea maisha yake katika masuala ya amani.

“Kiongozi huyo atakumbukwa kama kiongozi mahiri wa Kuwait aliyeimarisha ushirikiano wa karibu kati ya Kuwait na Tanzania,” alisema Balozi Mbarouk. 

“Kwa niaba ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, tunapenda kutoa salamu zetu za pole kwa wananchi wa Kuwait kwa kuondokewa na kiongozi bora na mpenda amani. Roho yake Ipumzike mahali pema peponi,” aliongeza Mhe. Balozi Mbarouk

Balozi Mbarouk aliongeza kuwa Daima Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania itamkumbuka Hayati Sheikh Nawaf al-Ahmad Al-Sabah kama kiongozi imara na aliyependa amani.


Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk akisalimiana na Balozi wa Kuwait nchini, Mhe. Mubarak Mohammed Alsehaijan baada ya kuwasili katika Ubalozi huo Jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kusaini kitabu cha maombolezo kufuatia kifo cha Amir wa Kuwait, Sheikh Nawaf al-Ahmad Al-Sabah kilichotekea tarehe 16 Disemba 2023


Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk akisaini kitabu cha maombolezo katika Ubalozi wa Kuwait Jijini Dar es Salaam kufuatia kifo cha Amir wa Kuwait, Sheikh Nawaf al-Ahmad Al-Sabah kilichotekea tarehe 16 Disemba 2023

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk akisaini kitabu cha maombolezo katika Ubalozi wa Kuwait Jijini Dar es Salaam kufuatia kifo cha Amir wa Kuwait, Sheikh Nawaf al-Ahmad Al-Sabah kilichotekea tarehe 16 Disemba 2023

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk akimfariji Balozi wa Kuwait nchini Mhe. Mubarak Mohammed Alsehaijan katika Ubalozi wa Kuwait Jijini Dar es Salaam kufuatia kifo cha Amir wa Kuwait, Sheikh Nawaf al-Ahmad Al-Sabah kilichotekea tarehe 16 Disemba 2023



Sunday, December 17, 2023

WAZIRI MAKAMBA ABAINISHA MAFANIKIO YA SERIKALI KWA MWAKA 2023 KUPITIA UTEKELEZAJI WA SERA YA MAMBO YA NJE

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. January Makamba (Mb.) ameainisha mafanikio yaliyopatikana kwa Taifa kutokana na utekelezaji wa Sera ya Mambo ya Nje yenye msisitizo katika Diplomasia ya Uchumi kuwa ni pamoja na kuimarika kwa ushirikiano baina ya Tanzania na nchi nyingine, kukua kwa biashara, uwekezaji na utalii na kuongezeka kwa ushawishi na sauti ya Tanzania katika majukwaa ya kikanda na kimataifa.

Mhe. Makamba  ameanisha mafanikio hayo kwenye mkutano wake na waandishi wa habari uliofanyika jijini Dar es Salaam tarehe 17 Desemba 2023 wakati akitoa Tathmini ya Mafanikio ya  Wizara katika Kueneza, Kukuza na Kupanua Diplomasia ya Tanzania Kimataifa  kwa mwaka 2023  pamoja na kutoa Mwelekeo na Matarajio ya Wizara kwa Mwaka 2024.

Mhe. Makamba amesema kuwa, Diplomasia ya Tanzania chini ya uongozi imara wa Mwanadiplomasia namba moja, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuimarika katika nyanja mbalimbali ambapo kupitia uratibu wa Wizara na kwa kushirikiana na wadau mbalimbali, Tanzania katika kipindi cha mwaka 2023 imefanikiwa kuimarisha uhusiano  ya  uwili, kukuza biashara na uwekezaji, kuongeza ushawishi wa Tanzania katika masuala mtambuka yanayohitaji ushirikiano wa kimataifa,  kutafuta fedha kwa ajili ya kugharamia miradi ya kimkakati na kuongezeka kwa watalii.

Akifafanua kuhusu kuimarika kwa ushirikiano wa uwili kati ya Tanzania na nchi mbalimbali duniani na mashirika ya kimataifa, Mhe. Makamba amesema kupitia ziara mbalimbali zilizofanywa na Mhe. Rais Dkt. Samia, Viongozi Wakuu Serikalini na zile zilizofanywa na Marais na Wakuu wa Mashirika kutoka nje ya nchi hapa nchini zimeiwezesha Tanzania kunufaika kiuchumi kwa kuimarika zaidi kwa ushirikiano na nchi hizo pamoja na mashirika ya kikanda na kimataifa.

Kadhalika amesema kuimarika kwa ushirikiano huo kumeiwezesha Tanzania katika mwaka 2023 kuwa mwenyeji wa mikutano mikubwa ya kikanda na kimataifa ukiwemo Mkutano  wa Kimataifa kuhusu Mifumo ya Uzalishaji wa Chakula na Mkutano wa Kimataifa kuhusu masuala ya Rasilimali Watu.

Pia amesema Wizara imefanikiwa kuratibu Mikutano ya Tume ya Pamoja kati ya Tanzania na nchi mbalimbali zikiwemo Algeria, Comoro, Finland na Indonesia. Kupitia mikutano hiyo, Tanzania ilifanikiwa kujadili masuala mbalimbali ya kuimarisha ushirikiano katika sekta mbalimbali.

Kuhusu kukua kwa biashara na uwekezaji nchini, Mhe. Makamba amesema takwimu zinaonesha kwa kiasi kikubwa kazi imefanyika ambapo Mhe. Rais Dkt. Samia ameongoza ushiriki wa Tanzania kwenye makongamano mbalimbali ya biashara na uwekezaji  ikiwemo Kongamano la Biashara kati ya Tanzania na India, Kongamano la Biashara na Uwekezaji kati ya Tanzania na Zambia pamoja na kuelekeza kufanyika kwa makongamano mbalimbali likiwemo lile la Tanzania na Uholanzi na Tanzania na Ufaransa yaliyomshirikisha Mhe. Waziri Makamba.

“Kwenye kukuza biashara na uwekezaji kati ya Tanzania na nchini mbalimbali, takwimu zinaonesha kazi imefanyika kwa umahiri mkubwa. Mhe. Rais ameongoza kazi hii kama mwanadiplomasia namba moja na kushiriki kwenye makongamano ya biashara na uwekezaji kati ya Tanzania na India, Tanzania na Zambia lakini pia ameelekeza kufanyika kwa makongamano mengine ambayo tumeshiriki baadhi yetu sisi, Tanzania na Uholanzi, Tanzania na Ufaransa na Tanzania na Ungereza” amesisitiza Mhe. Makamba.

Mhe. Makamba pia amesema kuwa, Tanzania imefanikiwa kupanua  masoko ya bidhaa zake mbalimbali duniani ikiwemo kupatikana kwa soko la Mbaazi na Korosho nchini India na Vietnam na Mkonge  nchini China na Brazil na Maparachichi nchini China na nchi za Ulaya. Amesema kupanuka kwa masoko ya bidhaa hizo kutaongeza uzalishaji, ajira na kipato na hatimaye kuchangia maendeleo ya Taifa.

Kuhusu utafutaji  fedha za kugharamia miradi ya maendeleo hapa nchini, Mhe. Waziri Makamba amesema jukumu hili limetekelezwa kikamilifu ambapo kupitia mawasiliano yaliyofanyika kati ya Tanzania na Mashirika mbalimbali ya kimataifa yanayotoa misaada na mikopo ikiwemo Benki ya Maendeleo ya Afrika, Mfuko wa Kuwait, Shirika la Fedha Duniani na mengine yamefanikisha upatikanaji wa fedha kwa ajili ya miradi ya maendeleo ikiwemo ujenzi wa Reli ya Kisasa.

Waziri Makamba amesema kutokana na kazi za nzuri inayofanywa na Mwanadiplomasia namba moja, Mhe. Rais Dkt. Samia sauti na ushawishi wa Tanzania katika masuala mtambuka imeendelea kusikika huku akitoa mfano wa Mkutano wa 28 wa Kimataifa wa Mambadiliko ya Tabianchi uliofanyika Umoja wa Falme za Kiarabu mwezi Desemba 2023 ambapo Mhe. Rais Dkt. Samia alifanikisha kufanyika kwa mkutano wa pembezoni kuhusu matumizi ya nishati safi ya kupikia ili kuepuka ukataji wa miti hovyo.

Kadhalika amesema kutokana na Diplomasia ya Tanzania kuimarika, Mhe. Rais Dkt. Samia ameteuliwa kwenye nafasi mbalimbali ikiwemo kuwa Championi wa Dunia kwenye masuala ya usawa wa kijinsia.

Pia Mhe. Makamba amesema kuwa, Tanzania kupitia Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki imefanikiwa kuimarisha ujirani mwema na nchi mbalimbali, jumuiya za kikanda na kudumisha amani na usalama katika kanda.

“Tanzania ni mwenyekiti ajaye wa Asasi ya Siasa, Ulinzi na Usalama ya Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) kupitia nafasi hii Tanzania itaendelea kutoa mchango wake katika kuimarisha amani na usalama katika kanda hii” amesema Mhe. Makamba.  

Akielezea mwelekeo na matarajio ya Wizara kwa mwaka 2024, Mhe. Makamba amesema Wizara itaendelea  kutekeleza  Sera ya Mambo ya Nje inayosisitiza katika Diplomasia ya Uchumi; Kukamilisha uandaaji wa Sera Mpya ya Mambo ya Nje ili iendane na mazingira ya sasa ya dunia; kukamilisha uratibu wa Hadhi Maalum kwa Diaspora; Kupanua uwakilishi wa Tanzania kwa kufungua Balozi mpya; Kuwa mwenyekiti wa Asasi ya Siasa, Ulinzi na Usalama ya SADC kwa kipindi cha mwaka mmoja; Kuratibu mikutano ya Tume za Pamoja za Ushirikiano na nchi mbalimbali; Kuandaa makongamano ya biashara kati ya Tanzania na nchi mbalimbali; Kuratibu na kuwa mwenyeji wa mikutano mbalimbali ya kikanda na kimataifa na kuratibu ziara za Mhe. Rais na Viongozi wengine wakuu wa Serikali.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. January Makamba (Mb.) ameainisha mafanikio yaliyopatikana kwa Taifa kutokana na utekelezaji wa Sera ya Mambo ya Nje yenye msisitizo katika Diplomasia ya Uchumi kwa waandishi wa Habari (Hawapo pichani) Jijini Dar es Salaam

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. January Makamba (Mb.) ameainisha mafanikio yaliyopatikana kwa Taifa kutokana na utekelezaji wa Sera ya Mambo ya Nje yenye msisitizo katika Diplomasia ya Uchumi kwa waandishi wa Habari Jijini Dar es Salaam. Kushoto ni Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Balozi Dkt. Samwel Shelukindo.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. January Makamba (Mb.) ameainisha mafanikio yaliyopatikana kwa Taifa kutokana na utekelezaji wa Sera ya Mambo ya Nje yenye msisitizo katika Diplomasia ya Uchumi kwa waandishi wa Habari Jijini Dar es Salaam

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. January Makamba (Mb.) ameainisha mafanikio yaliyopatikana kwa Taifa kutokana na utekelezaji wa Sera ya Mambo ya Nje yenye msisitizo katika Diplomasia ya Uchumi kwa waandishi wa Habari  Jijini Dar es Salaam






Friday, December 15, 2023

TANZANIA YAIBUKA MSHINDI WA KWANZA MAONESHO YA JUAKALI YA JUMUIYA YA AFRIKA MASHARIKI

Mjasiriamali kutoka Tanzania ameibuka mshindi wa kwanza wa jumla kwenye Maonesho ya 23 ya Wajasiriamali Wadogo na wa Kati ya Jumuiya ya Afrika Mashariki maarufu kama Nguvu Kazi/Juakali yaliyomalizika jijini Bujumbura, Burundi tarehe 15 Desemba 2023.

 

Mshindi wa pili ametokea Kenya huku mshindi wa tatu akitokea Uganda.



Mjasiriamali huyo, Dkt. Herieth Mkangaa maarufu kama Mama batiki ambaye anamiliki Kampuni ya kutengeneza Batiki ya MoroBatiki ya mkoani Morogoro ametangazwa mshindi wakati wa ufungaji rasmi wa Maonesho hayo ambayo yamewashirikisha wajasiriamali 1,500 kutoka Nchi Wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki. 


Dkt. Mkangaa ni pia maarufu kwa kutengeneza vazi la batiki lililompatia umaarufu la “Suti ya Samia” ikiashiria mtindo wa nguo unaopendelewa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan. 


Akizungumza mara baada ya kupokea tuzo hiyo, Dkt. Mkanga amesema kuwa amefurahia ushindi huo ambao ni mkubwa kwake na kwa Tanzania na kwamba tuzo hiyo ni chachu kwake ya kuendelea kujituma zaidi na kutengeneza bidhaa nyingi na zenye ubora ili kulikamata soko la Afrika Mashariki, Afrika na Duniani kwa ujumla.

 

Pia amewahamasisha wajasiriamali kote nchini kujiamini na kuchangamkia fursa mbalimbali za biashara, masoko na uwekezaji zinazotangazwa na Serikali  ndani na nje ya nchi.


Wakati huohuo, Wajasiriamali wawili wenye ulemavu wa macho kutoka Zanzibar, Bw. Abdul Kadir Amini Ahmed na Bw. Khamis Khamis Haji wanaojishughulisha na utenegenezaji wa mikeka wamepongezwa na waandaji wa maonesho hayo kwa kufanikiwa kushiriki maonesho hayo kikamilifu licha ya hali ya ulemavu waliyo nayo huku jamii ikitakiwa kuiga mfano wao wa kujituma katika kazi badala ya kutegemea kuomba kusaidiwa.


Maonesho ya 23 ya Wajasiriamali Wadogo na wa Kati ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ambayo yamebeba Kaulimbiu isemayo “Kuunganisha Wajasiriamali Wadogo na wa Kati wa Afrika Mashariki kufanya biashara katika Eneo la Afrika Mashariki” hufanyika kila mwaka kwa utaratibu wa mzunguko kutoka nchi moja kwenda nchi nyingine ambapo maonesho ya 24 yanatarajiwa kufanyika nchini Sudan Kusini mwaka 2024. 

Waziri wa Viwanda, Biashara, Uchukuzi na Utalii wa Burundi, Mhe. Nijimbere Marie Chantal akimakibidhi tuzo Mshindi wa kwanza wa jumla wa Maonesho ya 23 ya Wajasiriamali wadogo na wa kati wa Jumuiya ya Afrika Mashariki kutoka Tanzania, Dkt. Herieth Mkangaa baada ya kuibuka mshindi kutokana na kuonesha bidhaa zenye ubora aina ya Batiki. Mshindi wa pili ametoka Kenya na mshindi wa tatu ametokea Uganda. Maonesho hayo ambayo yamefanyika jijini Bujumbura, Burundi kuanzia tarehe 05 hadi 15 Desemba 2023 yamewashirikisha Wajasiriamali 1,500 kutoka Nchi Wanachama wa Jumuiya hiyo.
Mgeni Rasmi ambaye pia ni Waziri wa Viwanda, Biashara, Uchukuzi na Utalii wa Burundi, Mhe. Nijimbere Marie Chantal akizungumza wakati wa hafla ya ufungaji wa Maonesho ya 23 ya Wajasiriamali Wadogo na wa Kati wa Jumuiya ya Afrika Mashariki yaliyofanyika jijini Bujumbura kuanzia tarehe 05 hadi 15 Desemba 2023
Mkurugenzi Msaidizi wa Idara ya Ajira na Ukuzaji Ujuzi kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Ajira, Vijana na Watu wenye Ulemavu, Bi. Kisa akizungumza kwa niaba ya ujumbe wa Tanzania kwenye hafala ya ufungaji wa Maonesho ya 23 ya Wajasiriamali Wadogo na wa Kati wa Jumuiya ya Afrika Mashariki yaliyofanyika jijini Bujumbura kuanzia tarehe 05 hadi 15 Desemba 2023
Mgeni Rasmi ambaye pia ni Waziri wa Viwanda, Biashara, Uchukuzi na Utalii wa Burundi, Mhe. Nijimbere Marie Chantal akiwa katika picha ya pamoja na Wajasiriamali wenye ulemavu wa macho kutoka Zanzibar. Wajasiriamali hao Bw. Khamis Khamis Haji (katikati) na Bw. AbdulKadir Amini Ahmed wamepongezwa na waandaaji wa maonesho hayo kwa kushiriki kikamilifu.
Mshindi wa Kwanza wa jumla na wa kwanza katika kundi la Tanzania wa Maonesho ya 23 ya Wajasiriamali Wadogo na wa Kati wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, Dkt. Herieth Mkangaa (katikati) akiwa na washindi wengine kutoka kundi la Tanzania ambao ni mshindi wa pili Bi. Aisha Rutta (kulia) kutoka Kampuni ya Komati ya Mkoani Pwani inayojishughulisha na utengenezaji wa bidhaa zinazotokana na Nazi na mshindi wa tatu Bi. Mwanahamisi Rashidi anayejishughulisha na utengenezaji wa  majiko kutoka  Umoja wa Wajasiriamali wa Tabora
Sehemu ya wadau mbalimbali walioshiriki hafla ya ufungaji wa maonesho hayo
Jukwaa kuu

Bi. Kisa akipokea zawadi ya mkeka mdogo kutoka kwa wajasiriamali wenye ulemavu wa macho kutoka Zanzibar

Naibu Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki anayeshughulikia masuala ya Fedha na Biashara, Bi. Annette Mutaawe akimkabidhi Mjumbe wa Sudan Kusini bendera ya Jumuiya ya Afrika Mashariki kama ishara ya kuikabidhi rasmi nchi hiyo jukumu la kuandaa Maonesho ya 24 ya Wajasiriamali Wadogo na wa Kati ya Jumuiya hiyo yatakayofanyika nchini humo mwaka 2024

Kikundi cha ngoma maarufu ya Burundi wakitumbuiza wakati wa hafla ya kufunga maonesho hayo
Wadau kutoka Tanzania wakishangilia baada ya kutangazwa kwa Mshindi wa kwanza wa jumla wa maonesho ya 23 ya wajasiriamali wadogo na wa kati wa Jumuiaya ya Afrika Mashariki, Dkt. Herieth  Mkangaa kutoka Tanzania
Shamrashamra za ushindi zikiendelea