Friday, September 8, 2023

AFRIKA INA ARDHI KUBWA YA KULISHA DUNIA, RAIS SAMIA

Rais wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan amezihimiza nchi za Afrika kushirikiana ili kukabiliana na aibu ya baa la njaa, kwakuwa bara hilo lina asilimia 65 ya ardhi inayofaa kwa kilimo duniani, asilimia 60 ya utajiri wa rasilimali na maziwa makubwa, nguvu kazi ya kutosha ya vijana na madini yanayoweza kuingizia fedha nyingi za kuwekeza katika kilimo barani humo.

Rais Samia ametoa kauli hiyo alipohutubia Mkutano wa Jukwaa la Mifumo ya Chakula ngazi ya Marais uliofanyika jijini Dar Es Salaam tarehe 07 Septemba 2023.

Mhe. Rais Samia amesikitishwa na hali ya Afrika ya kuwa Bara la walalamikaji badala ya kuweka mikakati na kutafuta mbinu za kujiiletea mapinduzi ya kijani. Alisema watu takribani milioni 283 barani Afrika wana lala na njaa kila siku, wengine wanapata utapia mlo na baadhi yao kufariki kwa kukosa chakula, jambo ambalo amelitaja ni la aibu na halikubaliki kwa dunia ya leo.

Mhe. Rais Samia amezitaka nchi za Afrika kuzigeuza changamoto zinazoikabili dunia kuwa fursa kwao, kwa kuwekeza zaidi katika kilimo, hususan kwa kuwawezesha vijana na kuwatatulia matatizo yao. Matatizo hayo yanayowakabili vijana ni pamoja na ukosefu wa taarifa sahihi, ardhi, mitaji, athari za mabadiliko ya tabianchi na kuibuka kwa magonjwa duniani.

Dkt. Samia amebainisha kuwa ili kufikia malengo ya usalama wa chakula barani Afrika, nchi za Afrika hazina budi kutathmini vipaumbele vyake na kutunga sera zinazoendena na mahitaji ya sasa ya dunia.

Alisema ni muhimu kwa nchi za Afrika kutekeleza ahadi ilizojiwekea ambazo zimebainishwa katika Progaramu ya Maendeleo ya Kilimo ya Umoja wa Afrika ya Mwaka 2003, Azimio la Malabo la mwaka 2014 kuhusu kuongeza kasi ya ukuaji wa sekta ya kilimo na mikakati mingine kuhusu kilimo.

Miongozo ya maazimio hayo yanaelekeza nchi za Afrika kuongeza bajeti ya kilimo hadi asilimia 10, kukuza sekta ya kilimo kwa asilimia 6, kuimarisha ukuaji jumuishi wa sekta ya kilimo, kuhamasisha na kushirikisha sekta binafsi katika kilimo, kutoa fursa za ajira kwa vijana angalau kwa asilimia 30 katika minyororo ya uongezaji thamani katika mifumo ya kilimo na kuongeza biashara ya bidhaa na huduma za kilimo barani Afrika.

Mhe. Rais alieleza kuwa Tanzania inatekeleza maazimio hayo kwa kuongeza bajeti ya sekta ya kilimo, kutekeleza agenda Namba 1030 ya kuongeza ukuaji wa sekta ya kilimo kwa asilimia 10 ifikapo mwaka 2030, kuingia katika masoko ya chakula ya kikanda na ya kimataifa ili kukidhi mahitaji ya chakula katika nchi mbalimbali.

Aidha, alieleza kuwa ili kuchochea sekta ya kilimo nchini, Serikali inatekeleza programu mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuwawezesha vijana na wanawake kupitia mpango wa Jenga Kesho iliyo bora (BBT) ambayo imezinduliwa na kutekelezwa katika mikoa mbalimbali nchini.

Rais Samia ambaye aliungana na Rais wa Kenya, Mhe. William Ruto, Rais wa Burundi, Mhe. Evariste Ndayishimiye na Rais wa Senegal, Mhe. Macky  Sall na Rais wa Zanzibar, Mhe. Dkt. Hussein Mwinyi aliahidi kuwa Afrika ipo tayari kuzalisha chakula cha kutosha na kuacha kutegemea bidhaa hiyo muhimu kutoka nje. 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akihutubia Mkutano wa Jukwaa la Mifumo ya Chakula uliofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere jijini Dar Es Salaam

Washiriki mbalimbali wakifuatilia Mkutano wa Jukwaa la Mifumo ya Chakula uliofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere jijini Dar Es Salaam
Washiriki wakiwa wamesimama kwa ajili ya kuimba Wimbo wa Taifa wakati wa Mkutano wa Jukwaa la Mifumo ya Chakula uliofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere jijini Dar Es Salaam
Viongozi mbalimbali akiwemo Rais wa Zanzibar, Mhe. Dkt. Hussein Mwinyi (kushoto) na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. January Makamba (wa pili kutoka kushoto) wakifuatilia Mkutano wa Jukwaa la Mifumo ya Chakula uliofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere jijini Dar Es Salaam
Rais wa awamu ya nne wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete na Rais wa Zanzibar, Mhe. Hussein Mwinyi wakiteta jambo wakati wa Mkutano wa Jukwaa la Mifumo ya Chakula uliofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere jijini Dar Es Salaam

Wakifuatilia Mkutano wa Jukwaa la Mifumo ya Chakula uliofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere jijini Dar Es Salaam


Mkurugenzi wa Kitengo cha Mawasiliano katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mindi Kasiga akifuatilia Mkutano wa Jukwaa la Mifumo ya Chakula uliofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere jijini Dar Es Salaam

Wanadiplomasia mbalimbali wakifuatilia Mkutano wa Jukwaa la Mifumo ya Chakula uliofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere jijini Dar Es Salaam






No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.