Saturday, January 25, 2025

Rais wa Sierra Leone Awasili nchini














Rais wa Jamhuri ya Sierra Leone, Mheshimiwa Julius Maada Bio, amewasili jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kushiriki Mkutano wa Kilele wa Wakuu wa Nchi za Afrika kuhusu Nishati, unaotarajiwa kufanyika katika Kituo cha Mikutano cha  Kimataifa cha Julius Nyerere kuanzia tarehe 27 hadi 28 Januari 2025.


Katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere, Mheshimiwa Rais Bio amepokelewa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mheshimiwa Balozi Mahmoud Thabit Kombo.


Mheshimiwa Rais Bio ni Rais wa kwanza kuwasili nchini kwa ajili ya mkutano huo ambao jumla ya Marais 25 kutoka nchi za Afrika aanatarajiwa kuja nchini kushiriki mkutano huo.


Mkutano huu wa kihistoria unalenga kuimarisha juhudi za pamoja katika kukabiliana na changamoto na fursa za nishati barani Afrika, sambamba na kupitisha Azimio la Dar es Salaam, linalosisitiza dhamira ya Viongozi wa Nchi na Serikali za Afrika kuhakikisha upatikanaji wa nishati ya uhakika, nafuu, na endelevu barani Afrika.







 

RAIS SAMIA AVUNJA RIKODI, MKUTANO WA NISHATI.

Idadi ya Wakuu wa Nchi watakaoshiriki Mkutano wa Wakuu wa Nchi za Afrika kuhusu Nishati uliopangwa kufanyika nchini Januari 27 na 28, 2025 ni rikodi nyingine kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mahmoud Thabit Kombo amesema Wakuu wa Nchi 25 na Makamu wa Rais, Mawaziri Wakuu na Naibu Mawaziri Wakuu 10 inafanya idadi ya viongozi wa ngazi ya juu 35 ambao Tanzania tokea izaliwe haijawahi kupokea idadi kubwa ya viongozi kama hao katika tukio moja.

“Tulipokea Wakuu wa Nchi 19 wakati wa kifo cha Baba wa Taifa, Hayati Julius Kambarage Nyerere mwaka 1999 na Wakuu wa Nchi 15 wakati wa Mkutano wa Wakuu wa Nchi za Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) mwaka 2019, mkiangalia idadi ya Wakuu wa Nchi katika mkutano huu ni kubwa ukilinganisha na matukio hayo mawili yaliyopita” Balozi Kombo alisema. 

Alizitaja nchi ambazo Wakuu wa Nchi zao zimethibitisha kushiriki kuwa ni Pamoja na; Algeria, Comoro, Liberia, Lesotho, Botswana, Kenya, Ghana, Gabon, Sierra Leone, Ethiopia, Sudan, Malawi, Zambia, Somalia, Guine Bisau, Burundi, Mauritania, Kongo Brazzaville, Madagascar, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, Libya, Nigeria, Djibouti na Gabon. 

Makamu wa Rais watakaoshiriki ni kutoka Gambia na Benin. Mawaziri Wakuu kutoka Cote d’Ivoire, Uganda, São Tomé and Príncipe na Equatorial Guinea na Naibu Mawaziri Wakuu ni kutoka Eswatine na Namibia.

Waziri Kombo amesema mkutano huo ni mwendelezo wa matunda ya diplomasia ya Tanzania ambapo Serikali imejipanga kuhakikisha kuwa Tanzania inaendelea kutangazika barani Afrika na duniani kwa ujumla. 

Amesema mwaliko wa Rais Samia Suluhu Hassan kushiriki katika Mkutano wa Nchi 20 Tajiri zaidi duniani (G20) uliofanyika Brazil Novemba 2024 na Mkutano wa Jukwaa la Ushirikiano kati ya Afrika na China (FOCAC) na kupewa na nafasi ya kuzungumza kwa niaba ya Bara la Afrika ni kielelezo cha diplomasia ya Tanzania kuimarika duniani.

Ameendelea kueleza kuwa mikutano hiyo ina faida kubwa kwenye Uchumi wa nchi hususan sekta ya utalii na makundi mbalimbali ya wajasiriamali kama boda boda, hoteli na mama lishe.

Waziri Kombo amemalizia kwa kuwashukuru waandishi wa habari kwa kazi nzuri ya kuelimisha umma na kuwasihi kazi yao hiyo inahitajika zaidi katika mkutano huu mkubwa kuwahi kufanyika nchini.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo akisisitiza jambo wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu Mkutano wa Wakuu wa Nchi za Afrika wa Nishati utakaofanyika Januari 27-28, 2025.





Thursday, January 23, 2025

WIZARA YA MAMBO YA NJE YAPONGEZWA KWA KUCHUKUA HATUA ZA ZIADA ZA UKAMILISHWAJI MUSWADA WA SHERIA YA MAREKEBISHO YA SHERIA MBALIMBALI

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria imeipongeza Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa kutoa ushirikiano wa hali ya juu kwa Kamati hiyo na kuiwezesha kukamilisha Muswada kuhusu Mapendekezo ya Marekebisho  ya Sheria Mbalimbali ikiwemo mabadiliko ya Sheria ya Uhamiaji Sura ya 54 na Sheria ya Ardhi  Sura ya 113 ikiwa ni hatua muhimu ya kuwezesha utekelezaji  wa Hadhi Maalum kwa raia wa nchi nyingine wenye asili ya Tanzania (Tanzania Non-Citizen Diaspora).

 

Pongezi hizo zimetolewa na Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Dkt. Joseph Kizito Mhagama (Mb.), wakati wa kikao cha majumuisho kutokana na ziara ya mafunzo kwa Kamati katika nchi za Ethiopia na Comoro. Kikao hicho kilifanyika Bungeni, jijini Dodoma Januari 23, 2025.

 

Mhe. Dkt. Mhagama ameishukuru Serikali kupitia Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa jitihada za makusudi zilizochukuliwa  katika kuijengea uwezo Kamati hiyo kwa kuwawezesha kutembelea nchi hizo mbili zenye  idadi kubwa ya Diaspora inayosaidia katika ujenzi wa mataifa hayo. Mafunzo hayo yamesaidia Kamati kutekeleza ipasavyo majukumu yake katika mapitio ya mapendekezo ya marekebisho ya Sheria kutoa Hadhi Maalum kwa raia wa nchi nyingine wenye asili ya Tanzania kama ambavyo yamewasilishwa na Serikali.

 

Ameongeza kusema kuwa,  hatua ya Wizara inaashiria dhamira yake ya dhati katika kuhakikisha utekelezaji wa suala zima la Hadhi Maalum kwa raia wa nchi nyingine wenye asili ya Tanzania kwa maslahi mapana ya Taifa linafanikiwa.

 

“Nampongeza Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, na wewe Mhe. Waziri na Wizara kwa ujumla kwa kulipa suala hili uzito wa kipekee. Ushirikiano mliotupatia kama Kamati umetuwezesha kupiga hatua kubwa kwenye ukamilishaji wa Muswada ili kuwezesha kuendelea na hatua zinazofuata,” alisema Mhe. Dkt. Mhagama.

 

Kwa upande wake, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki ameishukuru  Kamati hiyo kwa kuendelea kutekeleza jukumu kubwa la kuisimamia Serikali katika utekelezaji wa masuala ya Utawala, Katiba na Sheria ambayo ni misingi mikuu ya utendaji katika Serikali.

 

Pia, ameihakikishia Kamati hiyo kuwa, Wizara kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wakiwemo Uhamiaji na NIDA itaendelea kutoa ushirikiano wowote utakaohitajika pamoja na kutekeleza maelekezo yote yaliyotolewa na  Kamati ili kuendelea kuboresha Muswada huo. 

 

Vilevile,  Mhe. Balozi Kombo alitumia nafasi hiyo kumshukuru Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, (Sera, Bunge na Uratibu), Mhe. William Lukuvi (Mb.), kwa uongozi, uratibu na ushirikiano wake binafsi pamoja na Ofisi yake huku akitambua umuhimu wa miongozo na mafunzo mbalimbali ambayo amekuwa akiyatoa kwa Kamati na Wizara ambayo yameleta tija katika suala zima la ukamilishaji wa muswada huo.

 

Katika kikao hicho, Mhe. Waziri Kombo aliambatana na Viongozi na Watendaji mbalimbali kutoka Wizarani akiwemo Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Cosato Chumi (Mb.), Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki anayeshughulikia masuala ya Afrika Mashariki, Mhe. Dennis Londo (Mb.), Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki anayeshughulikia masuala ya Afrika Mashariki, Balozi Stephen Mbundi na Naibu Katibu Mkuu, Balozi Said Shaib Mussa.

 

Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali (Na.2) wa Mwaka 2024 unaopendekeza marekebisho katika Sheria kuu nane zikiwemo Sheria ya Uhamiaji, Sura ya 54 na Sheria ya Ardhi, Sura ya 113, uliwasilishwa Bungeni na Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mhe. Hamza Said Johari (Mb.), mwezi Septemba 2024.

 

Muswada husika unatarajiwa kujadiliwa na Bunge katika Mkutano wa 18 wa Bunge hilo ambao umepangwa kufanyika kuanzia tarehe 28 Januari 2025.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo (Mb.) akizungumza wakati wa Kikao cha Majuisho  baina ya Wizara na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria uliofanyika Bungeni jijini Dodoma Januari 23, 2025. Majumuisho hayo yalihusu Muswada kuhusu Mapendekezo ya Marekebisho  ya Sheria Mbalimbali ikiwemo mabadiliko ya Sheria ya Uhamiaji Sura ya 54 na Sheria ya Ardhi  Sura ya 113 ikiwa ni hatua muhimu ya kuwezesha utekelezaji  wa Hadhi Maalum kwa raia wa nchi nyingine wenye asili ya Tanzania (Tanzania Non-Citizen Diaspora). Pamoja na mambo mengine Kamati hiyo iliipongeza Wizara kwa mchango wake na ushirikiano katika kukamilisha Muswada huo.
Mhe. Waziri Kombo akisisitiza jambo wakati wa kikao kati ya Wizara na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria
Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Joseph Kizito Mhagama (Mb.) akizungumza wakati wa kikao baina ya Kamati hiyo na Uongozi wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
Mhe. Dkt. Kizito akisisitiza jambo wakati wa kikao hicho
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge na Uratibu, Mhe. William Lukuvi (Mb.) akichangia hoja wakati wa kikao hicho ambacho alishiriki kama Mjumbe
Mhe. Waziri Kombo akiwaonesha Wajumbe wa Kikao hicho Jarida la Wizara (Foreign Affairs Bulletin) ambalo limesheni taarifa mbalimbali kuhusu masuala ushirikiano baina ya Tanzania na mataifa mbalimbali
Viongozi Wakuu wa Wizara wakishiriki kikao hicho. Kutoka kulia ni Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Cosato Chumi (Mb.); Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki anayeshughulikia masuala ya Afrika Mashariki, Mhe. Dennis Londo (Mb.), Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Said Shaib Mussa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki anayeshughulikia masuala ya Afrika Mashariki, Balozi Stephen Mbundi
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Cosato Chumi (Mb.) akitoa neno la shukrani wakati wa kikao na kamati ya bunge
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki anayeshughulikia masuala ya Afrika Mashariki akijitambulisha wakati wa kikao na kamati ya Bunge
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Said Shaib Mussa  akijitambulisha kwa wajumbe wa kamati
Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki anayeshughulikia masuala ya Afrika Mashariki, Balozi Stephen Mbundi (kushoto) akiwa na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Said Shaib Mussa wakati wa kikao na kamati ya bunge
Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, Mhe. Florent Kyombo akichangia hoja wakati wa kikao
Sehemu ya Waheshimiwa Wabunge ambao ni Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria
Mjumbe wa Kamati hiyo, Mhe. Seif Khamis Gulamali akichangia hoja
Sehemu ya Menejimenti ya Wizara
Kikao kikiendelea
Mkurugenzi wa Mawasiliano katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mindi Kasiga akijitambulisha kwa Wajume wa Kamati
Sehemu nyingine ya wajumbe kutoka Wizarani na Uhamiaji wakishiriki kikao cha Kamati
Mjumbe wa Kamati na Mbunge wa Bukene, Mhe. Selemani Zedi akichangia hoja
Mjumbe wa Kamati, Mhe. Rashid Shangazi akichangia hoja
Wajumbe wa Kamati ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria wakifuatilia kikao
Mjumbe wa Kamati, Mhe. Edward Kisau akichangia hoja
Mjumbe wa Kamati, Mhe. Abeid Ramadhan akichangia hoja
Mjumbe wa Kamati, Mhe. Yahaya Massare akichangia hoja
Mjumbe wa Kamati, Mhe. Abdullah Ali Mwinyi akichangia hoja
Mjumbe wa Kamati akichangia jambo
Sehemu ya wajumbe kutoka Wizarani na Uhamiaji wakishiriki kikao
Mjumbe wa Kamati, Mhe. Aziza Ally akichangia jambo
Sehemu ya Wakurugenzi kutoka Wizarani
Sehemu nyingine ya Wakurugenzi kutoka Wizarani
Wajumbe wa Kamati ya Bunge
Wakurugenzi kutoka Wizarani
Sehemu ya Wajumbe kutoka Wizarani na Uhamiaji
Sehemu ya Wajumbe kutoka Wizarani
Mhe. Waziri Kombo akizungumza na Balozi Mbundi mara baada ya kikao na Kamati ya Bunge anayeshuhudia ni Mhe. Londo