Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria imeipongeza Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa kutoa ushirikiano wa hali ya juu kwa Kamati hiyo na kuiwezesha kukamilisha Muswada kuhusu Mapendekezo ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali ikiwemo mabadiliko ya Sheria ya Uhamiaji Sura ya 54 na Sheria ya Ardhi Sura ya 113 ikiwa ni hatua muhimu ya kuwezesha utekelezaji wa Hadhi Maalum kwa raia wa nchi nyingine wenye asili ya Tanzania (Tanzania Non-Citizen Diaspora).
Pongezi hizo zimetolewa na Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Dkt. Joseph Kizito Mhagama (Mb.), wakati wa kikao cha majumuisho kutokana na ziara ya mafunzo kwa Kamati katika nchi za Ethiopia na Comoro. Kikao hicho kilifanyika Bungeni, jijini Dodoma Januari 23, 2025.
Mhe. Dkt. Mhagama ameishukuru Serikali kupitia Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa jitihada za makusudi zilizochukuliwa katika kuijengea uwezo Kamati hiyo kwa kuwawezesha kutembelea nchi hizo mbili zenye idadi kubwa ya Diaspora inayosaidia katika ujenzi wa mataifa hayo. Mafunzo hayo yamesaidia Kamati kutekeleza ipasavyo majukumu yake katika mapitio ya mapendekezo ya marekebisho ya Sheria kutoa Hadhi Maalum kwa raia wa nchi nyingine wenye asili ya Tanzania kama ambavyo yamewasilishwa na Serikali.
Ameongeza kusema kuwa, hatua ya Wizara inaashiria dhamira yake ya dhati katika kuhakikisha utekelezaji wa suala zima la Hadhi Maalum kwa raia wa nchi nyingine wenye asili ya Tanzania kwa maslahi mapana ya Taifa linafanikiwa.
“Nampongeza Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, na wewe Mhe. Waziri na Wizara kwa ujumla kwa kulipa suala hili uzito wa kipekee. Ushirikiano mliotupatia kama Kamati umetuwezesha kupiga hatua kubwa kwenye ukamilishaji wa Muswada ili kuwezesha kuendelea na hatua zinazofuata,” alisema Mhe. Dkt. Mhagama.
Kwa upande wake, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki ameishukuru Kamati hiyo kwa kuendelea kutekeleza jukumu kubwa la kuisimamia Serikali katika utekelezaji wa masuala ya Utawala, Katiba na Sheria ambayo ni misingi mikuu ya utendaji katika Serikali.
Pia, ameihakikishia Kamati hiyo kuwa, Wizara kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wakiwemo Uhamiaji na NIDA itaendelea kutoa ushirikiano wowote utakaohitajika pamoja na kutekeleza maelekezo yote yaliyotolewa na Kamati ili kuendelea kuboresha Muswada huo.
Vilevile, Mhe. Balozi Kombo alitumia nafasi hiyo kumshukuru Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, (Sera, Bunge na Uratibu), Mhe. William Lukuvi (Mb.), kwa uongozi, uratibu na ushirikiano wake binafsi pamoja na Ofisi yake huku akitambua umuhimu wa miongozo na mafunzo mbalimbali ambayo amekuwa akiyatoa kwa Kamati na Wizara ambayo yameleta tija katika suala zima la ukamilishaji wa muswada huo.
Katika kikao hicho, Mhe. Waziri Kombo aliambatana na Viongozi na Watendaji mbalimbali kutoka Wizarani akiwemo Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Cosato Chumi (Mb.), Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki anayeshughulikia masuala ya Afrika Mashariki, Mhe. Dennis Londo (Mb.), Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki anayeshughulikia masuala ya Afrika Mashariki, Balozi Stephen Mbundi na Naibu Katibu Mkuu, Balozi Said Shaib Mussa.
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali (Na.2) wa Mwaka 2024 unaopendekeza marekebisho katika Sheria kuu nane zikiwemo Sheria ya Uhamiaji, Sura ya 54 na Sheria ya Ardhi, Sura ya 113, uliwasilishwa Bungeni na Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mhe. Hamza Said Johari (Mb.), mwezi Septemba 2024.
Muswada husika unatarajiwa kujadiliwa na Bunge katika Mkutano wa 18 wa Bunge hilo ambao umepangwa kufanyika kuanzia tarehe 28 Januari 2025.
Mhe. Waziri Kombo akisisitiza jambo wakati wa kikao kati ya Wizara na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria |
Mhe. Dkt. Kizito akisisitiza jambo wakati wa kikao hicho |
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge na Uratibu, Mhe. William Lukuvi (Mb.) akichangia hoja wakati wa kikao hicho ambacho alishiriki kama Mjumbe |
Mhe. Waziri Kombo akiwaonesha Wajumbe wa Kikao hicho Jarida la Wizara (Foreign Affairs Bulletin) ambalo limesheni taarifa mbalimbali kuhusu masuala ushirikiano baina ya Tanzania na mataifa mbalimbali |
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Cosato Chumi (Mb.) akitoa neno la shukrani wakati wa kikao na kamati ya bunge |
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki anayeshughulikia masuala ya Afrika Mashariki akijitambulisha wakati wa kikao na kamati ya Bunge |
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Said Shaib Mussa akijitambulisha kwa wajumbe wa kamati |
Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, Mhe. Florent Kyombo akichangia hoja wakati wa kikao |
Sehemu ya Waheshimiwa Wabunge ambao ni Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria |
Mkurugenzi wa Mawasiliano katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mindi Kasiga akijitambulisha kwa Wajume wa Kamati |
Mjumbe wa Kamati na Mbunge wa Bukene, Mhe. Selemani Zedi akichangia hoja |
Mjumbe wa Kamati, Mhe. Rashid Shangazi akichangia hoja |
Wajumbe wa Kamati ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria wakifuatilia kikao |
No comments:
Post a Comment
Note: Only a member of this blog may post a comment.