Thursday, February 19, 2026

WAZIRI KOMBO AKUTANA NA BALOZI WA JAMHURI YA ZIMBABWE, HELEN BAWANGE DINGANI

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo (Kulia) akiwa na  Balozi wa Jamhuri ya Zimbabwe nchini Tanzania Mhe. Helen Bawange Dingani (Kushoto).


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mheshimiwa Balozi Mahmoud Thabit Kombo, alikutana na kufanya mazungumzo ya ngazi ya juu na Balozi wa Jamhuri ya Zimbabwe nchini Tanzania Mheshimiwa Helen Bawange Dingani.

Mazungumzo hayo yalifanyika tarehe 18 Februari 2026 katika ofisi ndogo za Wizara ya Mambo ya Nje jijini Dar es Salaam, Tanzania.

Mkutano huo ulijikita katika kuendeleza uhusiano wa pande mbili kwa kuangazia utambuzi wa vipaumbele vya pamoja, kuimarisha ushirikiano wa kidiplomasia, na kuchunguza njia za vitendo za ushirikiano.

Lengo kuu lilikuwa ni kujadili namna ya kuendeleza na kuimarisha zaidi ushirikiano ambao pande zote mbili zinauona, kuwa wa kimkakati katika mazingira ya kikanda yanayobadilika.

Pande zote mbili zilithibitisha tena dhamira yao ya kuendeleza mazungumzo ya pande mbili yaliyo imara na yenye kuleta matokeo chanya.

Ushirikiano huu unaashiria nia endelevu ya kuimarisha mahusiano kupitia diplomasia ya busara, huku ikisisitiza nafasi ya Tanzania kama jukwaa la ushirikiano wa kikanda na kimataifa.


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo (Kulia) akiwa na  Balozi wa Jamhuri ya Zimbabwe nchini Tanzania Mhe. Helen Bawange Dingani (Kushoto) wakati mazungumzo yakiendelea katika ofisi ndogo za Wizara Jijini Dar-es-Salaam.


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo


Balozi wa Jamhuri ya Zimbabwe nchini Tanzania Mhe. Helen Bawange Dingani




TANZANIA NA MSUMBIJI KUIMARISHA USHIRIKIANO KATIKA SEKTA YA AFYA

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo (Kulia) akiwa  na Balozi wa Msumbiji nchini  Tanzania Mhe. Ricardo Mtumbuida (Kushoto).


Serikali ya  Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Msumbiji zimeeleza dhamira ya kuimarisha zaidi ushirikiano wa pande mbili katika maeneo ya kimkakati, ikiwemo Sekta ya Afya ili kuleta maendeleo ya wananchi wake.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo na Balozi wa Msumbiji nchini Mhe. Ricardo Mtumbuida, wameeleza dhamira hiyo walipokutana na kufanya mazungumzo tarehe 18 Februari, 2026 katika ofisi ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam.

Mazungumzo hayo yalilenga kubainisha maeneo ya ushirikiano zaidi kati ya nchi hizo mbili kwa lengo la kuongeza ushirikiano katika Sekta ya afya, kukuza uchumi, na kujadili maandalizi ya Mkutano wa Tume ya Kudumu ya Pamoja unaotarajiwa kufanyika nchini mwaka huu.

Kwa upande wake Mhe. Balozi Kombo pia amewakaribisha wananchi wa Msumbiji kunufaika na huduma za Afya za kibingwa na kibobezi zinazopatikana nchini ikiwa ni sehemu ya kuendeleza mshikamano na ushirikiano wa kihistoria kati ya Tanzania na Msumbiji.

Naye Balozi wa Msumbiji nchini, Mhe. Ricardo Mtumbuida, ameishukuru Tanzania kwa ushirikiano wa kindugu unaoendelea kuipatia nchi yake, na kusisitiza azma ya Msumbiji ya kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia na kiuchumi na Tanzania ili kukuza ustawi wa wananchi wa mataifa yote mawili


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo 


Balozi wa Msumbiji nchini Mhe. Ricardo Mtumbuida


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo (Kulia) akiwa  na Balozi wa Msumbiji nchini  Tanzania Mhe. Ricardo Mtumbuida (Kushoto) wakati mazungumzo yakiendelea kwenye Ofisi ndogo za Wizara Jijini Dar-es-Salaam.