Mazungumzo yakiendelea |
Wednesday, April 13, 2022
TANZANIA NA MOROCCO KUFUNGUA MILANGO YA USHIRIKIANO KATIKA MASUALA YA DIASPORA
BALOZI KATTANGA AKUTANA NA WAZIRI WA NCHI WA U.A.E
Na Mwandishi Wetu, Dar
Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Hussein Kattanga amekutana na kufanya mazungumzo na Waziri wa nchi Umoja wa Falme za Kiarabu (U.A.E) Mhe. Sheikh Shakhboot Nahyan Al Nahyan, Ikulu Jijini Dar es Salaam.
Balozi Kattanga amekutana na ugeni huo kwa niaba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Sulluhu Hassan. Viongozi hao pamoja na mambo mengine, wamejadili masuala mbalimbali ya kuimarisha ushirikiano baina ya Tanzania na Umoja wa Falme za Kiarabu (U.A.E) katika nyanja za biashara na uwekezaji pamoja na Ulinzi na Usalama.
Balozi Kattanga amemhakikishia Waziri huyo kuwa Tanzania inayo mazingira mazuri ya biashara na salama kuwekeza.
Kwa upande wake Waziri wa Nchi wa Umoja wa Falme za Kiarabu, Mhe. Sheikh Shakhboot Nahyan Al Nahyan ameishukuru Serikali ya Tanzania kwa ushirikiano ambao imekuwa ikiutoka kwa Umoja huo wakati wote.
Waziri wa Nchi wa Umoja wa Falme za Kiarabu, Mhe. Sheikh Shakhboot Nahyan Al Nahyan amewasili nchini leo kuja kushiriki Mkutano wa Tume ya Pamoja ya Kudumu kati ya Tanzania na Umoja wa Falme za Kiarabu.
Tuesday, April 12, 2022
WAZIRI MULAMULA ATETA NA MABALOZI WA UFARANSA, ITALIA NA USWISI
Na Mwandishi wetu, Dar
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula (Mb) amekutana kwa pamoja na kufanya mazungumzo na mabalozi wa Ufaransa, Italia na Uswisi.
Waziri Mulamula amekutana na Balozi wa Ufaransa nchini Mhe. Nabil Hajlaoui, Balozi wa Italia nchini Mhe. Marco Lombardi pamoja na Balozi wa Uswisi hapa nchini Mhe. Didier Chasot katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam.
Pamoja na mambo mengine, viongozi hao wamejadili namna ya kuimarisha ushirikiano baina ya Tanzania na nchi zao katika kupambana na mabadiliko ya tabia nchi na utunzaji wa mazingira.
Waziri Mulamula amewahakikishia mabalozi hao kuwa Serikali ipo tayari wakati wote kushirikiana na nchi zao katika utunzaji wa mazingira pamoja na mabadiliko ya tabia nchi.
“Serikali ya awamu ya sita imetoa kipaumbele katika utunzaji wa mazingira na kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi,” amesema Balozi Mulamula.
Nae Balozi wa Ufaransa nchini, Mhe. Hajlaoui kwa niaba ya mabalozi wengine, amesema wanafurahishwa na jitihada za Serikali ya Tanzania katika kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi pamoja na utunzaji wa mazingira.
Balozi wa Ufaransa nchini Mhe. Nabil Hajlaoui akimueleza jambo Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam |
Balozi wa Italia nchini Mhe. Marco Lombardi (mwenye suti ya kijivu) akifafanua jambo kwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula wakati wa mazungumzo yao |
Mazungumzo baina ya Waziri Mulalamula na Mabalozi yakiendelea katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam |
UONGOZI WA WIZARA WAWASISITIZA MABALOZI KUFANYA KAZI KWA BIDII, WELEDI
Mabalozi wakisikiliza na kufuatilia maelekezo ya Uongozi wa Wizara (hawapo pichani) |
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Balozi Joseph Sokoine katika picha ya pamoja na Mabalozi mara baada ya kumaliza kikao |
Monday, April 11, 2022
TANZANIA, UJERUMANI KUSHIRIKIANA KUBORESHA UTAMADUNI
Na Mwandishi wetu, Dar
Serikali ya Tanzania pamoja na Shirikisho la Ujerumani zimekubaliana kuongeza ushirikiano katika kuboresha Utamaduni na Malikale ili kuendelea kuhifadhi urithi wa historia ya nchi kwa faida ya kizazi kilichopo na kijacho.
Ahadi hiyo imetolewa na Waziri wa Nchi katika Wizara ya Mambo ya Nje ya Shirikisho la Ujerumani Mhe. Katja Keul wakati alipokutana kwa mazungumzo na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam.
Balozi Mulamula amesema kuwa Ujerumani imekuwa na msaada mkubwa katika maendeleo ya kijamii, kitamaduni, kielemu na kiuchumi. “Kwa sasa tunaadhimisha miaka 60 ya ushirikiano wa kidiplomasia kati ya Tanzania na Ujerumani. ziara ya Mhe. Keul hapa nchini imelenga kuangala namna gani tunaweza kuongeza ushirikiano katika masuala ya utamaduni na malikale ambapo katika kutimiza hilo tayari mkataba wa ushirikiano wa kuendeleza makumbusho yetu ya taifa umesaini jana,” amesema Balozi Mulamula.
Nae Waziri Keul amesema kuwa Ujerumani na Tanzania zinaadhimisha miaka 60 ya ushirikiano na lengo kuu ni kuongeza ushirikiano katika masuala ya utamaduni na malikale kwa maslahi ya pande zote mbili.
“Katika kuhakikisha tunaongeza na kuboresha ushirikiano katika masuala ya utamaduni na malikale, tumesaini mkataba wa ushirikiano kati ya Makumbusho ya Taifa na Mfuko wa Utamaduni wa Ujerumani lengo kwa lengo la kuhakikisha malikale na uhifadhi wa historia zinalindwa na kusaidia jamii kisayansi, kielimu, kiutamaduni na kiuchumi,” amesema Mhe. Keul
Kwa mujibu wa Sera ya Malikale ya mwaka 2008, malikale hujumuisha rasilimali za urithi wa utamaduni zinazoshikika na zisizoshikika; zinazohamishika, na zisizohamishika, zilizo nchi kavu na majini ambazo zinadhihirisha mabadiliko ya kimaumbile, kifikra, zana, vyombo na mazingira aliyoishi na kutumia binadamu na zenye umri wa miaka mia moja (100). Malikale hizi zinajumuisha zana za mawe na chuma, vyombo vya usafiri, metali, miti na mifupa; visukuku vya binadamu, mimea na wanyama; michoro ya miambani; miji ya kihistoria, magofu ya majenzi.
Saturday, April 9, 2022
WAZIRI WA MAMBO YA NJE WA JAMHURI YA SHIRIKISHO LA UJERUMANI AWASILI NCHINI
Friday, April 8, 2022
BALOZI MULAMULA AKUTANA NA MWAKILISHI WA HESHIMA WA TANZANIA NCHINI CZECH
Na Mwandishi wetu, Dar
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula (Mb) amekutana kwa mazungumzo na Mwakilishi wa Heshima wa Tanzania nchini Czech Bw. Roman Grolig katika Ofisi ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam.
Katika mazungumzo yao, viongozi hao wamekubaliana kuimarisha uhusiano baina ya Tanzania na Jamhuri ya Czech katika sekta za biashara na uwekezaji, kilimo, elimu na teknolojia.
Balozi Mulamula aliwakaribisha wawekezaji kutoka Czech kuwekeza nchini pamoja na kutia mkazo wa kuimarisha zaidi ushirikiano kati ya Tanzania na Czech.
Kwa upande wake, Mwakilishi wa Heshima wa Tanzania nchini Czech, Bw. Grolig amesema ataendelea kuwahamasisha wafanyabiashara na wawekezaji kutoka Czech kuja kuwekeza Tanzania kwani ni sehemu salama ya kuwekeza.
“Jamhuri ya Czech imedhamiria kuongeza ushirikiano na Tanzania na katika kutimiza azma hiyo, wafanyabiashara na wawekezaji wameonesha nia ya kuwekeza katika viwanda vya kutengeneza ndege ndogondogo Pamoja na magari makubwa hapa Tanzania,” amesema Bw. Grolig
Pia ameongeza kuwa kwa sasa Czech ipo katika mchakato wa kuanzisha safari za ndege za moja kwa moja hapa nchini Tanzania ili kuwawezesha wawekezaji na wafanyabiashara kusafiri kwa urahisi kuja Tanzania kutafuta fursa za uwekezaji,” amesema Bw. Grolig.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula katika picha ya pamoja na Mwakilishi wa Heshima wa Tanzania nchini Czech Bw. Roman Grolig |
Thursday, April 7, 2022
BALOZI MULAMULA AZISIHI NCHI ZA EAC KUISHI KWA AMANI
Na Mwandishi wetu, Dar
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula amezisihi nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki kuishi kwa amani ili kuepukana na mauaji kama ya kimbari dhidi ya Watutsi yaliyotokea nchini Rwanda 1994.
Waziri Mulamula ametoa wito huo leo jijini Dar es Salaam katika kumbukizi ya miaka 28 ya mauaji ya Kimbari.
Balozi Mulamula ameongeza kuwa Tanzania inaungana na Rwanda kukumbuka tukio hilo baya lililoacha makovu kwa rai wa Rwanda.
"Tunashukuru na tunathamini hatua zilizochukuliwa na Rais wa Jamhuri ya Rwanda, Mhe. Paul Kagame kuijenga nchi na kuponya majeraha na makovu ya mauaji yale, ni tukio baya lilitokea, tunaomba lisijirudie tena katika nchi zetu,” amesema Balozi Mulamula.
Aidha balozi Mulamula ameongeza kuwa nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki zina mikataba inayotuongoza kuzuia mauaji na kuishi kwa amani.
Kwa upande wake Balozi wa Rwanda nchini Tanzania Mhe. Meja Jenerali Charles Karamba amesema wananchi wa Rwanda wanakumbuka tukio baya la kuuawa kwa ndugu zao lakini wanajivunia hatua zilizochukuliwa na viongozi wao na mafanikio yaliyopo leo nchini humo.
"Mauaji ya Kimbari yalituumiza sana kwa kupoteza ndugu zetu wasio na hatia lakini leo hii tunajivunia hapa tulipofika, kama taifa tumeendelea kujenga uzalendo na umoja,"amesema Balozi Karamba.
Nae Mratibu Mkaazi wa Shirika la Umoja wa Mataifa (UN), nchini Tanzania, Zlatan Millisic alisema shirika hilo linatoa pole kwa kumbukizi hiyo mbaya katika historia ya Rwanda na kusema leo kumbukizi hiyo imetumika kuelimisha dunia kuwa chuki ni mbaya.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula akiwasilisha hotuba yake katika kumbukizi ya mauaji ya Kimbari, leo Jijini Dar es Salaam |
Balozi wa Rwanda nchini Tanzania Mhe. Meja Jenerali Charles Karamba akihutubia Wanyarwanda paomja na wageni mbalimbali waliojitokeza katika kumbukizi ya miaka 28 ya mauaji ya Kimbari |
Balozi wa Comoro nchini, Mhe. Ahmed El Badaoui Mohamed Fakih akitoa hotuba yake katika kumbukizi ya miaka 28 ya mauaji ya Kimbari yaliyotokea nchini Rwanda mwaka 1994 |
Mratibu Mkazi wa Shughuli za Umoja wa Mataifa (UN) Bw. Zlatan Milišić akitoa salamu za UN katika kumbukimbizi ya miaka 28 ya mauaji ya Kimbari |