Tuesday, May 10, 2022

BALOZI SOKOINE ATETA NA BALOZI MALAWI, COMORO

Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Joseph Sokoine amekutana kwa mazungumzo Balozi wa Malawi nchini, Mhe. Andrew Kumwenda pamoja na Balozi wa Visiwa vya Comoro nchini Dkt. Ahamada El Badaoui leo katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam.

Awali akizungumza na Balozi wa Malawi nchini, Balozi Sokoine amemhakikishia ushirikiano wa Wizara na Serikali kwa ujumla wakati wote wa utekelezaji wa majukumu yake hapa nchini.  

Kwa Upande wake Balozi wa Malawi nchini, Mhe. Kumwenda ameishukuru Serikali kwa ushirikano inaompatia tangu alipowasili nchini na ameahidi kuendeleza uhusiano mzuri kati ya Tanzania na Malawi kwa maslahi ya pande zote mbili.

Katika tukio jingine, Balozi Sokoine amekutana kwa mazungumzo na Balozi wa Visiwa vya Comoro nchini, Dkt. Ahamada El Badaoui ambapo pamoja na mambo mengine, viongozi hao wamejadili masuala mbalimbali ya kuimarisha uhusiano baina ya Tanzania na Comoro.

Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Joseph Sokoine akizungumza na Balozi wa Malawi nchini, Mhe. Andrew Kumwenda katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam

Mazungumzo ya Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Joseph Sokoine na Balozi wa Malawi nchini, Mhe. Andrew Kumwenda yakiendelea katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam

Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Joseph Sokoine akizungumza na Balozi wa Visiwa vya Comoro nchini Dkt. Ahamada El Badaoui leo katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam

Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Joseph Sokoine akiagana na Balozi wa Visiwa vya Comoro nchini Dkt. Ahamada El Badaoui baada ya kumaliza mazungumzo yao  


TANZANIA YAJIVUNIA USHIRIKIANO IMARA NA UMOJA WA ULAYA

Na Mwandishi wetu, Dar

Serikali imesema inajivunia uhusiano na ushirikiano imara baina yake na Umoja wa Ulaya (EU) ambapo mpaka sasa zaidi ya kampuni 100 za nchi wanachama wa umoja huo zimewekeza Tanzania.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula alitoa kauli hiyo Jijini Dar es Salaam wakati wa maadhimisho ya Siku ya Umoja wa Ulaya iliyohudhuriwa na wageni mbalimbali wa ndani na nje ya nchi.

Balozi Mulamula alisema kuwa EU umesimama na Tanzania wakati wote na umeendelea kuunga mkono ajenda ya maendeleo.

“Serikali ya Tanzania inaushukuru Umoja wa Ulaya kwa uhusiano huu imara ambao umedumu kwa muda mrefu pamoja na msaada ambao umekuwa ukitolewa kwa miaka mingi. 

“Umoja wa Ulaya ni wadau wetu wakubwa wa maendeleo, wanagusa kila sekta, mwezi Februari, mwaka huu, Rais Samia Suluhu Hassan, alitembelea Umoja wa Ulaya Brussels na alikutana na wafanyabishara, tulipata ahadi ya kampuni nyingi zilionyesha nia ya kuja kuwekeza Tanzania.” alisema Balozi Mulamula

Alisema kuwa hadi sasa wana kampuni zaidi ya 100 kutoka nchi za Jumuiya ya Ulaya ambazo zimewekeza Tanzania.

Balozi Mulamula aliongeza kuwa wawekezaji wengi kutoka nchi za Jumuiya ya Umoja wa Ulaya zimeonyesha nia ya kuwekeza hapa nchini na wameridhishwa na mazingira ya biashara yaliyopo.

Nae Balozi wa Umoja wa Ulaya nchini, Mhe. Manfredo Fanti alisema wataendelea kushirikiana na Tanzania kuimarisha maendeleo katika sekta ya biashara na uwekezaji, utamaduni, uongozi kwa wanawake katika masuala ya siasa, elimu na afya kwa maslahi ya mataifa yote mawili.

“Tunaiona Tanzania ikiendelea kubadilika, mara kwa mara tunakutana na vijana na watu wenye vipaji wakitekeleza malengo na miradi yao, hivyo muundo wa kijamii unabadilika.

“Hii ni dhahiri kabisa kuwa Watanzania ndiyo waamuzi wa mustakabali wa jamii yao, Umoja wa Ulaya utaendelea kuunga mkono jitihada za mabadiliko katika jamii ya Watanzania kwa kuwa huo ndiyo ushirikiano na urafiki,”Balozi Fanti alisema.

Balozi Fanti pia aliipongeza Jumuiya ya Afrika Mashariki kwa kuongeza mwanachama mpya ambaye ni Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) kuwa jambo hilo ni jema linaongeza nguvu ya ushirikiano katika ukanda wa Afrika Mashariki.

Alisema Umoja wa Ulaya utaendelea kushirikiana na Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) katika kukuza na kuendeleza uchumi wa mataifa hayo kwa maslahi ya pande zote mbili.

Balozi wa Ufaransa nchini, Mhe. Nabil Hajlaoui ambaye alimuwakilisha Rais wa Umoja wa Ulaya katika maadhimisho hayo, alisema Jumuiya ya Ulaya imelenga pamoja na mambo mengine, kuendelea kuimarisha ushirikiano na Tanzania, kuongeza mshikamano, amani na uhuru pamoja kukuza demokrasia.   

Kwa Upande wake, Katibu Mkuu Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), Dkt. Peter Mathuki alisema Umoja wa Ulaya umekuwa mshirika mkuu wa nchi wanachama wa EAC kutokana na uhusiano mzuri na wa kishistoria uliojengewa misingi imara tangu 1975.

“EAC tunaishukuru Jumuiya ya Umoja wa Ulaya kwa misaada endelevu kwa miradi na programu za Jumuiya yetu ambazo zimekuwa zikiwanufaisha wananchi kwa miaka mingi,” Dk. Mathuki alisema.

Pia alizipongeza nchi wanachama wa Jumuiya Umoja wa Ulaya kwa umoja ambao umekuwa mfano wa kuigwa wa kiuchumi duniani kote.

Balozi wa Umoja wa Ulaya nchini, Mhe. Manfredo Fanti akiwasilisha hotuba yake wakati wa maadhimisho ya Siku ya Umoja wa Ulaya yaliyofanyika Jijini Dar es Salaam. Kulia ni Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, na Mgeni rasmi wamaadhimisho ya Siku ya Umoja wa Ulaya Balozi Liberata Mulamula akiwasilisha hotuba yake katika maadhimisho hayo yaliyofanyika Jijini Dar es Salaam

Balozi wa Ufaransa nchini, Mhe. Nabil Hajlaoui atoa salamu kwa niaba ya Rais wa Umoja wa Ulaya wakati wa maadhimisho ya Siku ya Umoja wa Ulaya

Katibu Mkuu Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), Dkt. Peter Mathuki akizungumza na wageni waalikwa katika maadhimisho ya Siku ya Umoja wa Ulaya 

Sehemu ya Washiriki wa maadhimisho ya Siku ya Umoja wa Ulaya

Baadhi ya Mabalozi wa nchi za Umoja wa Ulaya



UFARANSA YARIDHISHWA NA MAZINGIRA YA BIASHARA, UWEKEZAJI NCHINI

Na Mwandishi wetu, Dar 

Ufaransa imeonesha kuridhishwa na hatua zilizochukuliwa na zinazochukuliwa na Serikali ya Awamu ya Sita katika kuboresha mazingira ya biashara na uwekezaji nchini Tanzania.

Kauli hiyo imetolewa na Seneta wa Ufaransa anayeshughulikia masuala ya Wafaransa waishio Nje ya Ufaransa, Mhe. Olivier Cadic wakati alipokutana kwa mazungumzo na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula (Mb) katika Ofisi ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam.

Seneta, Cadic amesema kuwa kwa sasa mazingira ya kufanya biashara na uwekezaji nchini Tanzania yameboreshwa sana na yanashawishi wafanyabiashara wengi kuja kufanya biashara nchini.

“Tumepata wasaa mzuri wa kujadili fursa za biashara na uwekezaji ambazo zinapatikana nchini Tanzania ambapo wafanyabiashara na wawekezaji kutoka Ufaransa wanaweza kuja kuwekeza……kwangu mimi imekuwa fursa ya kuona mazingira haya ya uwekezaji ambayo yanapatikana hapa Tanzania,” 

“Serikali ya Tanzania imejiwekea mazingira rafiki ya biashara na uwekezaji kwa sasa, haya ni mabadiliko makubwa ambayo yataendeleza urafiki wa Tanzania na mataifa mbalimbali ikiwemo Ufaransa. Kwangu mimi imekuwa fursa kubwa ya kujionea mazingira haya mazuri ya biashara na nitawaelezea wafanyabioashara na wawekezaji kutoka Ufaransa kuja kuwekeza hapa,” amesema Seneta Cadic 

Kwa Upande wake Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula amesema kuwa ziara ya Seneta Olivier Cadic hapa nchini ni matunda ya ziara ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan aliyoifanya nchini Ufaransa hivyo Seneta Olivier amekuja nchini kuangalia maeneo ambayo wanaweza kuhamasisha wafanyabiashara na wawekezaji kutoka Ufaransa kuja kuwekeza Tanzania katika sekta za Uchukuzi, Nishati, Utalii, Elimu na Kilimo.

“Seneta amefurahishwa na juhudi zinazofanywa na Serikali ya Awamu ya Sita katika kuboresha zaidi na kuendeleza mazingira bora ya biashara nchini,” amesema Balozi Mulamula

Balozi Mulamula pamoja na mambo mengine, amemhakikishia Seneta Cadic kuwa Serikali bado inaendelea kuboresha mazingira ya biashara na uwekezaji ikiwa ni pamoja na kuondoa vikwazo vilivyokuwa vinahatarisha ukuaji wa biashara kati ya Tanzania na mataifa mengine.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula akisalimiana na Balozi wa Ufaransa nchini, Mhe. Nabil Hajlaoui katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula akizungumza na Seneta wa Ufaransa anayeshughulikia masuala ya Wafaransa waishio Nje ya Ufaransa, Mhe. Olivier Cadic katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam

Seneta wa Ufaransa anayeshughulikia masuala ya Wafaransa waishio Nje ya Ufaransa, Mhe. Olivier Cadic akimueleza jambo Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam



Mazungumzo ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula na Seneta wa Ufaransa anayeshughulikia masuala ya Wafaransa waishio Nje ya Ufaransa, Mhe. Olivier Cadic yakiendelea katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula akiagana na Seneta wa Ufaransa anayeshughulikia masuala ya Wafaransa waishio Nje ya Ufaransa, Mhe. Olivier Cadic yakiendelea katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam



Monday, May 9, 2022

BALOZI WA TANZANIA NCHINI ETHIOPIA AWASILISHA HATI ZA UTAMBULISHO UNECA

Mhe. Innocent Eugene Shiyo, Balozi wa Tanzania nchini Ethiopia na Mwakilishi wa Kudumu wa Tanzania kwenye Kamisheni Umoja wa Mataifa ya Uchumi Afrika (UNECA) amewasilisha Hati  za Utambulisho kwa Mhe.Dkt. Vera Songwe, Katibu Mtendaji wa Kamisheni Umoja wa Mataifa ya Uchumi Afrika (UNECA).

Wakati wa hafla hiyo, Mhe. Dkt. Vera Songwe alimpongeza Balozi Shiyo kwa kuteuliwa na Mhe. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuwa Mwakilishi wa Kudumu wa Tanzania kwenye Kamisheni ya Umoja wa Mataifa ya Uchumi Afrika (UNECA) yenye Makao Makuu Jijini Addis Ababa, Ethiopia na amemkaribisha na kumtakia heri katika utekelezaji wa majukumu yake.

Wakati wa mazungumzo yao, Balozi Shiyo na Dkt. Vera Songwe wamekubaliana kuendeleza ushirikiano mzuri uliopo kati ya Tanzania na UNECA katika masuala ya kipaumbele ikiwemo utekelezaji wa Malengo ya Maendeleo Endelevu, Mpango wa Maendeleo wa Afrika wa Agenda 2063 na juhudi za kukwamua uchumi dhidi ya madhara ya UVIKO-19.

Dkt, Vera Songwe ameeleza utayari wa UNECA kuisadia Tanzania kujenga na kuimarisha uwezo katika mikakati ya kukuza sekta za utalii,afya, kilimo,sekta binafsi, ukusanyaji wa mapato, utekelezaji wa Mkataba wa Eneo Huru la Biashara Afrika (AfCFTA), mapambano dhidi ya Mabadiliko ya Tabianchi na uwezeshaji Wanawake kwenye matumizi ya Teknolojia.

Kamisheni ya Umoja wa Mataifa ya Uchumi Afrika ilianzishwa mwaka 1958 kwa ajili ya kukuza maendeleo ya Kiuchumi na Kijamii katika nchi za Afrika, kukuza Mtangamano wa Kikanda na Ushirikiano wa Kimataifa kwa ajili ya maendeleo ya Afrika.

 Balozi wa Tanzania nchini Ethiopia na Mwakilishi wa Kudumu wa Tanzania kwenye Kamisheni Umoja wa Mataifa ya Uchumi Afrika, Mhe. Innocent Eugene Shiyo akiwasilisha Hati za Utambulisho kwa Katibu Mtendaji wa Kamisheni ya Umoja wa Mataifa ya Uchumi Afrika (UNECA), Mhe. Dkt. Vera Songwe. 

Mhe. Balozi Shiyo akiwa katika picha ya pamoja na Dkt. Songwe mara baada ya kuwasilisha Hati za Utambulisho

Friday, May 6, 2022

VACANCY ANNOUNCEMENT










 

BALOZI SOKOINE AKUTANA NA MJUMBE MAALUM WA SERIKALI YA CZECH


Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,  Balozi Joseph Sokoine akipokea ujumbe kutoka kwa Mjumbe Maalum wa Serikali ya Jamhuri ya Czech Balozi Miloslav Machalek alipokutana naye katika ofisi ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam tarehe 06 Mei, 2022. 

 

Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,  Balozi Joseph Sokoine akimsikiliza Balozi wa Jamhuri ya Czech mwenye makazi yake nchini Kenya Mhe. Martin Klepetko (katikati) walipokutana katika ofisi ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam tarehe 06 Mei, 2022 wakati Mjumbe Maalum wa Serikali ya Jamhuri ya Czech Balozi Miloslav Machalek (kushoto) alipowasilisha ujumbe wake kwa Katibu Mkuu.

Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,  Balozi Joseph Sokoine akizungumza na Balozi wa Jamhuri ya Czech mwenye makazi yake nchini Kenya Mhe. Martin Klepetko walipokutana katika ofisi ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam tarehe 06 Mei, 2022.  

Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,  Balozi Joseph Sokoine akizungumza na Balozi wa Jamhuri ya Czech mwenye makazi yake nchini Kenya Mhe. Martin Klepetko (katikati) walipokutana katika ofisi ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam tarehe 06 Mei, 2022. Pembeni ya Balozi Sokoine ni  Mkurugenzi wa Idara ya Amerika na Ulaya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Swahiba Mndeme akiwa na afisa dawati Bi Agness Kiama.


 


Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,  Balozi Joseph Sokoine amekutana na kufanya mazungumzo na Mjumbe Maalum wa Serikali ya Jamhuri ya Czech Balozi Miloslav Machalek katika mazungumzo yaliyofanyika katika ofisi ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam.

Mjumbe huyo maalum wa Serikali ya Czech Balozi Machalek amewasilisha andiko la Serikali ya nchi hiyo la kutaka kushirikiana na Tanzania katika maeneo ya usimamizi wa maji, kilimo,  afya, ICT na biashara.

Akizungumza katika kikao hicho Balozi Sokoine ameongelea kufurahishwa na wazo la kuihusisha Tanzania katika mradi huo ambao alisema kuwa utaimarisha uhusiano na ushirikiano kati ya Tanzania na Jamhuri ya Czech.  

Balozi Machalek amesema andiko aliloliwaasilisha katika kikao hiko ni mradi wa maendeleo ambao nchi yake unakusudia kuutekeleza katika nchi tano za Afrika za Tanzania, Tunisia, Kenya, Ghana na Ivory Coast.

Balozi Machalek aliambatana na Balozi wa Jamhuri ya Czech nchini Tanzania  mwenye makazi yake nchini Kenya  Mhe. Martin Klepetko ambaye pia alitumia fursa hiyo kuzungumza na Balzoi Sokoine katika kuimarisha uhusiano na ushirikiano kati ya Tanzania na Jamhuri ya Czech.

Naye Balozi  wa Jamhuri ya Czech ameelezea nia ya Serikali ya Czech kushirikiana zaidi na Tanzania kupitia Nyanja za biashara na uwekezaji ili kukuza ushusiano na ushirikiano kwa faida  ya pande zote mbili na kuongeza kuwa ni matumaini yake kuwa uhusiano mzuri ulipo baina ya nchi hizo utaendelea kuimarika.

 


WAZIRI MULAMULA ASHIRIKI MKUTANO WA DHARURA WA BARAZA LA MAWAZIRI WA SADC

 

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula akizungumza katika Mkutano wa Dharura wa Baraza la Mawaziri wa  SADC uliofanyika kwa njia ya mtandao tarehe 06 Mei, 2022.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula (kushoto) akiwa na Mkurugenzi wa Idara ya Ushirikiano wa Kikanda Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Agnes Kayola (kulia ) wakifuatilia  Mkutano wa Dharura wa Baraza la Mawaziri wa  SADC uliofanyika kwa njia ya mtandao tarehe 06 Mei, 2022.

 

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula (wa kwanza kulia) akiwa na washiriki kutoka Idara ya Ushirikiano wa Kikanda Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki wakati wa  Mkutano wa Dharura wa Baraza la Mawaziri wa  SADC uliofanyika kwa njia ya mtandao tarehe 06 Mei, 2022.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula (wa pili kulia) na washiriki kutoka Idara ya Ushirikiano wa Kikanda wakiimba wimbo wa Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (SADC) baada ya kukamilika kwa  Mkutano wa Dharura wa Baraza la Mawaziri wa  SADC uliofanyika kwa njia ya mtandao tarehe 06 Mei, 2022.


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula (Mb) ameshiriki Mkutano wa Dharura wa Baraza la Mawaziri wa Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (SADC) uliofanyika kwa njia ya mtandao tarehe 06 Mei, 2022.

Akiongelea mkutano huo Mhe. Waziri amesema Mkutano huo umejadili masuala ya madhara yaliyotokana na mafuriko yaliyozikumba baadhi ya nchi wanachama wa jumuiya hiyo na Mkataba Cotnou ambao unaongelea ushirikiano kati ya nchi za Afrika, Pasifiki na Carebean na Jumuiya ya SADC ili kuhakikisha ushirikiano baina ya nchi unaimarika.

Akizungumza katika kikao hicho, Balozi Mulamula alitoa salamu za pole kwa nchi za Afrika Kusini, Msumbiji, Mauritius na Malawi kufuatia mafuriko makubwa yaliyozikumba nchi hizo na kusababisha vifo vya wananchi wake, hasara ya mali na miundombinu katika nchi  hizo.

‘‘Kupitia Mkutano huu nitoe pole nyingi kwa wananchi wa nchi wanachama wenzetu kutokana na mafuriko yaliyotokea katika nchi za Afrika Kusini, Msumbiji, Madagascar na Malawi, mafuriko ambayo yameziletea nchi hizo madhara makubwa kama vile vifo vya wananchi na uharibifu mkubwa wa mali na miundombinu,’’ alisema Balozi Mulamula.

Katika mkutano huo nchi wanachama kwa ujumla wao waliangalia madhara yaliyotokana na mafuriko hayo na namna ambavyo jumuiya hiyo inaweza kuzisaidia nchi zilizoathirika.

Mkutano huo uliokuwa chini ya uenyekiti wa Waziri wa Mambo ya Nje wa Malawi Mhe. Nansy Tembo uliridhia utoaji wa fedha kutoka katika Mfuko wa Maafa wa Jumuiya ya SADC kwa ajili ya kusaidia nchi hizo zilizoathiriwa na mafuriko hayo.

 

 

TANZANIA YASHIRIKI MAONESHO YA KILIMO YA MACFRUT 2022 ITALIA

Katika jitihada za kutekeleza Diplomasia ya Uchumi kwa vitendo, Tanzania kwa mara ya kwanza imeshiriki katika maonesho ya kimataifa ya kilimo yanayojulikana kama MACFRUT FIERA yanayoendelea mjini Rimini, nchini Italia.

Maonesho hayo yanawakutanisha wazalishaji, wanunuzi na wauzaji wa bidhaa za kilimo cha mbogamboga na matunda, ufugaji wa kuku na mashine za kisasa zinazotumika katika kilimo. 

Akifungua maonesho hayo, Waziri wa Kilimo wa Italia, Mhe. Stefano Patuanelli, alisisitiza umuhimu wa ushirikiano katika sekta ya kilimo ikiwa ni pamoja na matumizi ya teknolojia ya kisasa katika kilimo ili kuongeza tija katika uzalishaji na usalama wa chakula. 

Ubalozi wa Tanzania nchini Italia kwa kushirikiana na Wizara ya Kilimo umevutia ushiriki wa sekta binafsi katika maonesho hayo ambayo tunda la mwaka huu ni parachichi. 

Balozi wa Tanzania nchini Italia, Mhe. Mahmoud Thabit Kombo, aliwasihi wafanyabiashara na wawekezaji kutoka nchini humo kuja kuwekeza Tanzania katika sekta ya kilimo na sekta nyinginezo.

“Nawahakikishia kuwa Tanzania imeboresha mazingira ya uwekezaji kwa kupunguza kero zilizokuwa hapo awali na kwamba, Watanzania wapo tayari kuwapokea,” alisema Balozi Kombo. 

Maonesho ya MACFRUT hufanyika kila mwaka. Awamu inayofuata ya maonesho (MACFRUT FIERA 2023) itafanyika mwezi Mei, 2023 katika mji wa Rimini. 

Balozi wa Tanzania nchini Italia, Mhe. Mahmoud Thabit Kombo akizungumza na washiriki kutoka Angola waliotembelea banda la Tanzania katika maonesho ya MACFRUT

Maafisa kutoka Ubalozi wa Tanzania nchini Italia wakizungumza na baadhi ya washiriki waliotembelea banda la Tanzania katika maonesho ya a MACFRUT 

Washiriki kutoka Tanzania wakiwa katika picha ya pamoja naBalozi wa Tanzania nchini Italia, Mhe. Mahmoud Thabit Kombo kwenye maonesho ya MACFRUT katika mji wa Rimini, Italia

Naibu Waziri Mkuu wa Uganda na mgeni rasmi katika kongamano maalum kwa ajili ya Afrika, Mhe. Rebecca Kadaga (katikati mwenye barakoa) akiungana na viongozi wengine kukata utepe kuashiria ufunguzi rasmi wa maonesho hayo uliofanyika tarehe 4 Mei 2022


Thursday, May 5, 2022

BALOZI SOKOINE ASHIRIKI MKUTANO WA MAKATIBU WAKUU SADC

Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Joseph Sokoine ameshiriki Mkutano wa Kamati ya Kudumu katika ngazi ya Makatibu Wakuu wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini Mwa Afrika (SADC) uliofanyika leo kwa njia ya mtandao.

Balozi Sokoine ameshiriki mkutano huo akiwa katika Ofisi ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya Mkutano wa Dharura wa Baraza la Mawaziri wa SADC unaotarajiwa kufanyika kwa njia ya mtandao tarehe 6 Mei 2022. 

Pamoja na masuala mengine, Makatibu Wakuu wamejadili athari za mafuriko yaliyotokea katika Ukanda wa SADC kwa kipindi cha Januari hadi Aprili 2022.

Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Joseph Sokoine akishiriki Mkutano wa Kamati ya Kudumu katika ngazi ya Makatibu Wakuu wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini Mwa Afrika (SADC) uliofanyika leo kwa njia ya mtandao katika Ofisi ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam


Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Joseph Sokoine akishiriki Mkutano wa Kamati ya Kudumu katika ngazi ya Makatibu Wakuu wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini Mwa Afrika (SADC) uliofanyika leo kwa njia ya mtandao katika Ofisi ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam. Kushoto ni Mkurugenzi wa Uhusiano wa Kikanda katika Wizara ya Mambo  ya Nje Ushirikiano wa Afrika Mashariki,  Balozi Agnes Kayola.