Wednesday, May 9, 2012

Msimamo wa Tanzania kuhusu Sahara Magharibi




Mhe. Bernard K. Membe (MB), Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa akitoa msimamo wa Tanzania kuhusu suala la Sahara Magharibi na Morocco, wakati akiongea na waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam.  
 

Mhe. Bernard K. Membe (MB), Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa akitoa msimamo wa Tanzania kuhusu suala la Sahara Magharibi na Morocco, wakati akiongea na waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam.

 
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Mhe. Bernard K. Membe (MB), akijibu maswali mbalimbali yaliyoulizwa na waandishi wa habari kwenye ukumbi wa Mkutano wa Wizara ya Mambo ya Nje leo jijini Dar es Salaam.  Mwingine pichani ni Bw. Assah Mwambene, Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali -Wizarani.
 
 
 
 
Msimamo wa Tanzania kuhusu Sahara Magharibi
 
Tanzania imesema haijabadili msimamo wake katika kuwaunga mkono Watu wa Sahara Magharibi kuhusu haki yao ya kujitawala kutoka mikononi mwa Morocco.

Hayo yalisemwa na Mhe. Bernard K. Membe (Mb), Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa wakati akiongea na Waandishi wa vyombo mbalimbali vya habari leo jijini Dar es Salaam.

Aidha, Tanzania imeisihi Morocco irudi katika uanachama wa Umoja wa Afrika ili kuweza kuwa na mazungumzo ya pamoja baina yao, wananchi wa Sahara Magharibi na Umoja wa Mataifa kwa lengo la kutafuta suluhu ya kudumu kuhusu mgogoro huo.

“Tatizo hilo limekuwa kidonda ndugu haliwezi kupona kesho, kwa hiyo msimamo wa Tanzania ni huo. Tunataka kuwe na uhuru wa Sahara Magharibi na tunaomba pande zote, pamoja na Umoja wa Mataifa wamalize kwa haraka sana tatizo hili ili kuwe na kura ya maoni ya wananchi wenyewe kuamua ama kujitawala au kuwa sehemu ya Morocco,” alisema Mhe. Membe.

Mhe. Membe aliongeza kuwa, Tanzania itaheshimu maamuzi yoyote ya wananchi wa Sahara Magharibi kwa vile “tunaamini wataamua kujitawala wenyewe na siyo kuwa kama kile Kisiwa cha Mayote nchini Comoro”.  Wananchi wa Kisiwa hicho waliamua kuwa sehemu ya nchi ya Ufaransa, ingawa kipo Afrika.

Kuhusu tatizo la kumpata Mwenyekiti wa Kamisheni ya Umoja wa Afrika (AU), Mhe. Membe alisema Tanzania inaungana na Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC) kumuunga mkono mgombea kutoka Afrika Kusini kwenye nafasi hiyo Bi. Nkosazana Dlamini-Zuma dhidi ya mgombea anayetetea uenyekiti huo, Bw. Jean Ping.

Nchi Wanachama wa AU zinatarajiwa kupiga kura na hatimaye kumchagua Mwenyekiti wa Kamisheni hiyo mwezi wa Julai mwaka huu wakati wa Mkutano wa Wakuu wa Nchi mjini Lilongwe, nchini Malawi. 






No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.