Tuesday, April 21, 2015
Monday, April 20, 2015
Waziri Membe: Hakuna Mtanzania katika mauaji ya Wageni Afrika Kusini
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa Mhe. Benard K. Membe (Mb.) akizungumza na Waandishi wa Habari nchini kuhusiana machafuko yanayoendelea nchini Afrika ya Kusini. |
Waandishi wa Habari wakimsikiliza na kunukuu taarifa kutoka kwa Waziri Membe ambaye hayupo pichani |
Waziri Membe akiendelea kuzungumza na Waandishi wa Habari. |
Watumishi wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa nao wakimsikiliza Waziri Membe (Hayupo pichani) |
Mwandishi wa Habari mkongwe Bw. Jackton Manyerere akiuliza swali kwa Mhe. Membe |
Mwandishi wa Habari kutoka Gazeti la Mawio Bi. Pendo Omary naye akiuliza swali kwa Waziri Membe. |
Waziri Membe akijibu Maswali yaliyo ulizwa na Waandishi wa Habari |
Mazungumzo yakiendelea |
Picha na Reginald Philip
==============================
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABAR
Waziri Membe: Hakuna Mtanzania katika mauaji ya Wageni Afrika Kusini
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Mhe. Bernard Membe, amesema leo kuwa hakuna Mtanzania kati ya watu wanane waliouawa katika mashambulizi dhidi ya wageni huko Durban na Johannesburg nchini Afrika ya Kusini.
Mhe. Membe amewaambia waandishi wa habari jijini Dar es Salaam kuwa taarifa zilizosambazwa na baadhi ya vyombo vya habari kwamba Watanzania watatu wameuwawa katika mashambulizii hayo siyo za kweli.
"Nimehakikishiwa na Waziri wa Usalama wa Afrika kusini, David Mahlobo, asubuhi hii kuwa hakuna Mtanzania kati ya watu wanane waliouwawa, ambao ni raia wa Ethiopia, Zimbabwe, Malawi na Swaziland," ametaarifu Mhe. Waziri.
Amesema serikali ina taarifa kuwa kuna Watanzania watatu waliofariki dunia nchini Afrika Kusini, lakini hawakuuwawa katika mashambulizi ya wenyeji dhidi ya wageni.
"Watanzania hao ni Rashidi Jumanne, ambaye imetaarifiwa alipigwa risasi katika tukio la ujambazi, kilometa 90 nje ya mji wa Durban; mfungwa Athumani China Mapepe, aliyeripotiwa kuchomwa kisu gerezani wakati wa vurugu za wafungwa, na Ali Heshima Mohamed, ambaye alifariki hospitalini kutokana na ugonjwa wa TB," alieleza Mhe. Membe.
Mwili wa marehemu Mohamed ulirejeshwa nchini jana kwa mazishi. Mhe. Waziri alitaarifu kuwa kuna Watanzania 23 katika kambi iliyotayarishwa na serikali ya Afrika Kusini huko Durban kuhudumia wageni wanaokimbia mashambulizi hayo ya wenyeji, na kuwa utaratibu unafanywa kuwarejesha nyumbani raia 21 walioomba. "Wawili wamesema hawako tayari kurudi."
Mhe. Membe amesema taarifa ya Serikali ya Afrika Kusini inaonyesha kuwa hali ya utulivu imerejea Durban na Johannesburg katika saa 48 zilizopita kutokana na juhudi za Rais Jacob Zuma na kamati maalum ya mawaziri aliyoiteua kushughulikia mashambulizi hayo.
Mapema jana, Mhe. Membe alimwita Balozi wa Afrika Kusini nchini Tanzania, Mhe. Thamsanqa Dennis Mseleku, na kuelezea kukerwa kwa Serikali na mauaji ya wageni na akataka hatua madhubuti zichukuliwe kuhakikisha usalama wa Watanzania nchini Afrika Kusini.
Alisema Tanzania inaunga mkono taarifa iliyotolewa na Mwenyekiti wa Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (SADC), Rais Robert Mugabe wa Zimbabwe, ambayo imelaani vikali mashambulizi ya Waafrika kutoka nje ya Afrika Kusini. Hata hivyo, Rais Mugabe, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Umoja mwa Afrika (AU), amesifia hatua zinazochukuliwa na serikali ya Afrika Kusini kukomesha mashambulizi hayo na kurejesha utulivu.
Mhe. Membe aliwataka Watanzania waishio Afrika Kusini na kwingineko nje ya nchi, kujitambulisha kwenye Balozi zetu ili iwe rahisi kufuatilia usalama wao na kuwasaidia yatokeapo majanga.
"Hatuna takwimu sahihi za idadi ya Watanzania waishio Afrika kusini kwa sababu wengi wao wamekwenda huko kwa njia za panya," alisema. Inakadiriwa kuna Watanzania 10,000 waishio Johannesburg na Durban.
Akijibu swali, Mhe. Membe alisema Tanzania inapaswa kutumia utajiri mkubwa wa gesi asilia ilionao kuendeleza viwanda vidogo, vya kati na vikubwa vitakavyotengeneza ajira za kuvutia kwa vijana ili wasikimbilie nchi za nje na kuhatarisha maisha yao.
Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali kwa Umma,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa,
Dar es Salaam
20 Aprili, 2015.
Waziri wa Mambo ya nje akiwasili katika ukumbi wa mikutano wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNICC) kwaajili ya kuzungumza na waandishi wa habari, jijini Dar es Salaam |
Waziri Membe akiingia katika ukumbi wa Mkutano kwaajili ya kuzungumza na waandishi we habari (hawapo pichani). |
Waziri akizungumza na waandishi wa Habari |
Mazungumzo yakiendelea |
Waziri Membe akiongozana na Viongozi wa Wizara na baadhi ya Waandishi wa habari kuelekea nje ya Ukumbi wa Mikutano wa Julius Nyerere. |
Friday, April 17, 2015
Waziri Membe akabidhi Ujumbe Maalum wa Mhe. Rais kwenda kwa Sultani wa Oman
Makabidhiano yakiendelea huku Balozi wa Tanzania nchini Oman, Mhe. Ali Ahmed Saleh akishuhudia. |
Waziri Membe akiwa kwenye
mazungumzo na Mhe. Alawi bin Abdulla, Waziri wa Mambo ya Nje wa Oman. =========================================== |
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Ujumbe Maalum wa Mhe. Rais Jakaya Mrisho Kikwete kwenda kwa Sultan
Qaboos wa Oman
Mhe. Bernard K. Membe (Mb.) Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano
wa Kimataifa amekabidhi ujumbe maalum kutoka kwa Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete,
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwenda kwa Mhe. Sultani Qaboos bin Said
Al Said, Mtawala wa Oman.
Ujumbe huo maalum ulikabidhiwa kwa Mhe. Yousuf bin Alawi bin
Abdulla, Waziri wa Mambo ya Nje na mwenyeji wa ziara ya Waziri Membe nchini Oman,
kwenye ofisi za Wizara hiyo jijini Muscat, Oman Alhamisi Aprili 16, 2015.
Makabidhiano hayo ya kihistoria nchini hapa, yalishuhudiwa na Mhe.
Dkt. Mwinyihaji Makame, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Utawala Bora, Zanzibar ,
Mhe. Ali Ahmed Saleh, Balozi wa Tanzania Oman, na viongozi wengine wa nchi zote
mbili na waandishi wa habari.
Baada ya makabidhiano, viongozi hao wawili na ujumbe wao walitumia
fursa hiyo kuzungumzia masuala mbalimbali ya ushirikiano baina ya Tanzania na
Oman.
Viongozi hao waliahidi kukuza uhusiano na utamaduni wa nchi hizi
mbili ambao unafanana kwa sababu za kihistoria. Mhe. Membe alimuelezea mwenyeji
wake nia ya Serikali kujenga Ofisi za Ubalozi kwenye kiwanja chake hapa
Mascut kama sehemu ya utekelezaji wa mpango wa kuwa na majengo ya Tanzania
kwenye nchi mbalimbali duniani.
Aidha mradi mkubwa wa bandari ya Bagamoyo pia ulizungumzwa na
viongozi hao ambapo Serikali ya Oman ni mojawapo ya mdau wa mradi huo. Wahusika
wengine wa mradi wa Bandari ya Bagamoyo ni Serikali ya China na Tanzania.
Mhe. Yousuf bin Alawi bin Abdulla, Waziri wa Mambo ya Nje wa Omani
alimuhakikishia mgeni wake ushirikiano wa Serikali yake kwenye hatua zote hizi
muhimu za kuendeleza na kukuza uhusiano wa muda mrefu wa nchi hizi mbili.
-Mwisho-
Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa,
Dar es Salaam
17 Aprili 2015
Thursday, April 16, 2015
Serikali kuwarudisha nchini Watanzania waliopo Yemen
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Serikali kuwarudisha Watanzania waliopo Yemen
Mhe. Bernard K. Membe (Mb.), Waziri wa Mambo ya Nje na
Ushirikiano wa Kimataifa ametangaza hatua ya Serikali kuwarudisha Watanzania
waishio nchini Yemen, kufutia mapigano yanayoendelea nchini humu ya vita vya
wenyewe kwa wenyewe.
Akizunguza na Mhe. Ali Ahmed Saleh, Balozi wa Tanzania
nchini Oman siku ya Alhamis tarehe 16 Aprili 2015, Waziri Membe amesema ni
jukumu la Serikali kuhakikisha kuwa Watanzania hao ambao wengi wao ni
wanafunzi, wanarejea nyumbani salama.
Zoezi la kurudisha Watanzania hao lilianza siku chache
zilizopita ambapo familia ya watu watano ilisaidiwa na kurudi nyumbani kupitia
Oman, wakati zoezi la kuwatambua na kuwaandikisha Watanzania likenddelea.
“Nimeruhusu matumizi ya fedha ya dharura ili kuhakikisha ndugu
zetu walioko kwenye hatari na machafuko ya Yemen wanarejeshwa salama nyumbani
mara moja” alisema Mhe. Membe.
Watanzania
hao ambao wengi wao hadi sasa wameshafika kwenye miji midogo ya Sarfat na
Al-Mazyouna kwenye mkoa wa Salala mpakani mwa Oman na Yemen, walituma maombi ya
dharura (distress call) kwenye Ofisi za Ubalozi Oman, kuelezea mazingira ya
hatari yanayowakabili, na kuomba kurudishwa nyumbani.
“Kulingana na maelekezo ya Waziri Membe, zoezi la
kuwarejesha Watanzania limeanza. Nimewapeleka maafisa wa ubalozi kule Salala ni
kilometa takriban elfu moja kutoka Muscut, ambapo watahakiki na kukabidhiwa
Watanzania wote sitini na nne (64) na wataruhusiwa kuingia nchini Oman na
kuelekea Tanzania” alimaliza Mhe. Ali Ahmed Saleh, Balozi wa Tanzania nchini
Oman.
Mgogoro wa Yemen unaoendelea baina ya maafisa wa polisi
waaminifu kwa aliyekuwa rais wa nchi hiyo, Ali Abdullah Saleh, na makundi ya
usalama yanayomuunga mkono rais wa sasa, Abed Rabbo Mansour Hadi, umeua mamia
ya watu na kujerui maelfu.
Mhe. Membe ametoa rai kwa Watanzania wote wenye ndugu au jamaa
nchini Yemen kuchukua tahadhari na kuwataarifu watafute msaada kupitia
Ubalozini Muscat ili kujihakikishia usalama wao. Aidha ametoa tahadhari kwa
Watanzania wanaotegemea kusafiri kwenda Yemen, kusitisha safari zao hadi hali ya
usalama itakaporejea.
-Mwisho-
Imetolewa
na:
Kitengo
cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara
ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa,
Dar es
Salaam
16
Aprili, 2015
Wednesday, April 15, 2015
Ziara ya Mhe. Membe Kuwait katika Picha
Msafara wa Mhe. Membe ukiingingia Mjini Kuwait kwa ziara ya siku moja kwa mwaliko wa Waziri wa Mambo ya Nje wa Kuwait. |
Mhe. Bernard Membe, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa akiwasili kwene hoteli ya Sheraton Jijini Kuwait kwa ziara ya siku moja nchini humo. |
Mhe. Membe na ujumbe wake wakimsikiliza Mhe. Balozi Najib na kuangalia picha mbalimbali za historia ya Mji wa Kuwait mara baada ya kuwasili nchini humo kwa ziara ya siku moja. |
Waziri Membe akifuatiwa na Balozi Najeb na ujumbe wake wakiingia kwenye Ofisi za Mfuko wa Maendeleo wa Kuwait kwa mazungumzo ya pamoja na viongozi wa mfuko huo tarehe 14 Aprili 2015. |
Bw. Peter Noni, Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Maendeleo Tanzania (TIB) akimuonyesha Mhe. Abdulwahab A. Al-Bader kazi zinazofanywa na benki yake kwa ajili ya miradi ya maendeleo nchini Tanzania. |
Mazungumzo yakiendelea |
Mhe. Membe akiagana na Mhe. Abdulwahab A. Al-Bader, mara baada ya mazungumzo hayo kumalizika. |
Msafara wa Waziri Membe ukielekea kwenye ofisi za Makamu wa Kwanza wa Waziri Mkuu na Waziri wa Mambo ya Nje wa Kuwait (jengo refu la kwanza kushoto) |
Waziri Membe akiwasili na mapokezi yakiendelea |
Waziri Membe akitambulisha ujumbe wake kwa Mhe. Sheikh Sabah Al-Khalid Al-Sabah, Naibu Waziri Mkuu ambaye pia ni Waziri wa Mambo ya Nje wa Kuwait mara baada ya kuwasili ofisini kwake kwa mkutano. |
Mazungumzo yakiendelea |
Ujumbe wa Mhe. Membe ulihudhuria pia chakula cha mchana pamoja na mwenyeji wake Mhe. Sheikh Sabah Al-Khalid Al-Sabah, Naibu Waziri Mkuu ambaye pia ni Waziri wa Mambo ya Nje wa Kuwait |
Waziri Membe akiagana na mwenyeji wake Mhe. Sheikh Sabah Al-Khalid Al-Sabah, Naibu Waziri Mkuu ambaye pia ni Waziri wa Mambo ya Nje wa Kuwait. |
Mhe. Membe akiagana na Balozi Najeb kwenye Uwanja wa Ndege wa Kuwait baada ya kukamilisha ziara yake nchini humo. |
Tanzania kufungua Ubalozi nchini Kuwait
Mazungumzo ya ushirikiano yakiendelea ======================================= |
TAARIFA
KWA VYOMBO VYA HABARI
Tanzania
kufungua Ubalozi nchini Kuwait
Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imepanga kufungua Ubalozi
nchini Kuwait kabla ya kumalizika kwa mwaka huu wa fedha wa
2014/2015.
Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa
Kimataifa, Mhe. Bernard K. Membe (Mb.) alipokutana na Mtukufu Sheikh Sabah Al-Khalid Al-Sabah, Naibu Waziri Mkuu ambaye pia ni Waziri wa
Mambo ya Nje wa Kuwait nchini Kuwait siku ya Jumanne tarehe 14 Aprili, 2015.
Katika mazungumzo yao viongozi hao wawili walisifu ushirikiano
uliopo baina ya nchi hizi mbili ambao ni wa kidugu na unalenga kuwanufaisha
wananchi wa nchi hizi.
“Kwa kufungua ofisi za Ubalozi, Kuwait ushirikiano huu wa kidugu
utaongezeka kwenye nyanja zote muhimu na utazaa matunda yatakayo wanufaisha
watu wetu, kwa nchi hizi mbili” alisisitiza Waziri Membe katika mazungumzo yake
na kiongozi huyo.
Kwa upande wa Kuwait, Serikali yao ilifungua ubalozi nchini
Tanzania Februari 2015 na Mhe. Jassem Ibrahim Al Najem kuwa Balozi wake wa
kwanza nchini Tanzania, mwenye makazi yake Jijini Dar es salaam.
Aidha, kwa sasa Tanzania inawakilishwa nchini Kuwait kupitia Ubalozi
wake uliopo Riyadh, Saudi Arabia.
Katika mkutano huo, Mtukufu Sabah Al-Khalid Al Sabah alisifu
jitihada za Tanzania kwenye kulinda na kuleta amani Barani Afrika hasusan
kwenye maeneo yenye migogoro. Alisema kuwa Serikali yake itaendelea
kushirikiana na Tanzania sio tu kwenye maeneo muhimu ya maendeleo lakini pia
hata kwenye ulinzi wa amani kwani ndio changamoto kubwa inayoikabili dunia kwa
sasa.
Kuhusu misaada Barani
Afrika, viongozi hao walijadili suala la uratibu wa misaada mbalimbali ya
Serikali ya Kuwait Barani humo ambapo waliangalia uwezekano wa kuanzisha kituo
maalum nchini Tanzania kwa ajili ya kusimamia shughuli za uratibu wa misaada
hiyo.
Kwa sasa Serikali ya Kuwait kupitia Mfuko wake wa Maendeleo –
Kuwait Fund- imetoa Dola za Kimarekani Bilioni moja kwenye Umoja wa Afrika kwa
ajili ya usalama wa chakula Barani Afrika.
Awali Waziri Membe alikutana na Mhe. Abdulwahab A. Al-Bader,
Mkurugenzi wa Mfuko wa Maendeleo wa Kuwait na kumshukuru kwa misaada mbalimbali
ya kimaendeleo wanayoendelea kuitoa nchini Tanzania na barani Afrika kwa
ujumla.
Aidha Waziri Membe alielezea kuwa maandalizi ya miradi mitano ya
umwagiliaji nchini Tanzania ambayo inayofadhiliwa na mfuko huo yamekamilika, na
kwamba sasa iko tayari kuanza. Aidha Waziri Membe na Mhe. Al-Bader walizungumzia
uwezekano wa mfuko huo kuikopesha Benki ya Uwekezaji Tanzania (TIB) ili iweze
kuendesha shughuli zake kikamilifu.
Waziri Membe yuko nchini Kuwait kwa ziara ya siku moja na
anatarajiwa kuondoka kesho kuelekea nchini Oman. Ujumbe wa Mhe. Membe nchini Kuwait unamjumuisha Bw. Peter Noni,
Mkurugenzi Mkuu wa Benki ya Uwekezaji Tanzania, Balozi Simba Yahya, Mkuregenzi
wa Idara ya Mashariki ya Kati katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa
na Bi. Mindi Kasiga, Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali, Wizara ya
Mambo ya Nje.
-Mwisho-
Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya
Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na
Ushirikiano wa Kimataifa, Dar es Salaam
15 Aprili 2015.
Subscribe to:
Posts (Atom)