Friday, November 27, 2015

Katibu Mkuu wa Mambo ya Nje amuaga Balozi wa Korea Kusini

Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Balozi Liberata Mulamula (kulia) akimkabidhi zawadi ya mchoro wa picha ya binti wa kimaasai na shati la kitenge alipokuwa akimuaga Balozi wa Jamhuri ya Korea Kusini, Mhe. Chung II ambaye amemaliza muda wake wa uwakilishi nchini. 
     
Balozi Mulamula akizungumza na Balozi Chung II .
Balozi Chung II naye akimweleza jambo Balozi Mulamula wakati wa mazungumzo yao.
Mkurugenzi wa Idara ya Asia na Australasia, Balozi Mbelwa Kairuki (kushoto) na Afisa Mambo ya Nje, Bw. Khatibu Makenga nao wakifuatilia kwa  mazungumzo kati ya  Balozi Mulamula na Balozi Chung II (hawapo pichani).  
Balozi Mulamula (kulia) na Balozi Chung II wakifurahia jambo kwa pamoja wakati wa mazungumzo yao
Mazungumzo yakiendelea
 Balozi Mulamula akiagana na Balozi wa Jamhuri ya Korea Kusini aliyemaliza muda wake wa uwakilishi hapa nchini Mhe. Chung II mara baada ya kumaliza mazungumzo

Picha na Reginald Philip 

=============================================


Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Balozi Liberata Mulamula amempongeza Balozi wa Jamhuri ya Korea Kusini hapa nchini, Mhe. Chung II kwa kuiwakilisha vyema nchi yake na kupelekea miradi mingi ya maendeleo ikiwemo ile ya miundombinu kukamilika.   
       
Balozi Mulamula alitoa pongezi hizo leo alipokutana na Balozi Chung II ambaye alifika Wizarani kwa lengo la kuaga baada ya kumaliza muda wake wa uwakilishi hapa nchini.

Balozi Mulamula alisema kuwa Jamhuri ya Korea Kusini imekuwa ni miongoni mwa nchi ambazo Tanzania inashirikiana nazo kwa karibu katika kutekeleza miradi ya maendeleo. Alieleza kuwa, nchi hiyo imeshiriki kikamilifu kutekeleza miradi  yenye manufaa makubwa kwa Tanzania  katika Sekta mbalimbali zikiwemo za kiuchumi, biashara na uboreshaji wa miundombinu. 

"Nakupongeza Mhe. Balozi kwa uwakilishi wako mzuri kwani katika kipindi chote ulichokuwepo nchini na kupitia Serikali yako umeweza kukamilisha miradi mikubwa ukiwemo ule wa Daraja la Kikwete lililojengwa katika Mto Malagarasi huko Kigoma” alisema Balozi Mulamula.

Aidha, alimhakikishia ushirikiano kutoka Wizarani na Serikalini kwa ujumla kwa Balozi mpya atakayeteuliwa na nchi hiyo kuja nchini.

Kwa upande wake, Balozi Chung II ambaye amekuwepo nchini kwa kipindi cha miaka mitatu aliishukuru Wizara na Serikali kwa ujumla kwa ushirikiano mzuri aliokuwa akiupata wakati wote wa uwakilishi wake. Pia aliahidi kuendelea kuitangaza Tanzania nchini kwake ili kuendeleza mahusiano mazuri yaliyopo kati ya nchi hizi mbili.

-Mwisho-





 
 

Thursday, November 26, 2015

Katibu Mkuu akutana kwa mazungumzo na Balozi wa Kuwait

Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa Balozi Liberata Mulamula (kulia), akizungumza na Balozi wa Kuwait nchini Mhe. Jasem Ibrahim Al-Najem alipokuja kumtembelea Wizarani. Mazungumzo hayo yalijikita katika kuimarisha mahusiano zaidi kati ya Tanzania na Kuwait katika sekta mbali mbali zikiwemo zile kiuchumi na biashara. Pia Balozi Jasem Ibrahim Al-Najem alitumia fursa hiyo kuipongeza Wizara na Watanzania kwa kumpata Rais wa Awamu ya Tano ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Mazungumzo yakiendelea huku Afisa Mambo ya Nje Bw. Tahiri Bakari (wa kwanza kulia) akisikiliza na kunukuu.

Picha na Reginald Philip

Azimio kuhusu watu wenye Ualibino lapitishwa kwa kauli moja


Mwakilishi wa Kudumu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa, Balozi Tuvako Manongi akiwasilisha mbele ya wajumbe wa Kamati ya Tatu ya Baraza Kuu la Umoja wa Matifa Azimio kihusu watu wenye ualibino. Azimio hilo lililipitishwa kwa kauli moja na wajumbe wa Kamati hiyo.
Sehemu ya Wajumbe wa Kamati ya Tatu ya Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa wakiwa katika mkutano wao siku ya jumanne ambapo pamoja na kupitisha Azimio kuhusu watu wenye ualibino, azimio lililoandaliwa kwa pamoja kati ya Tanzania na Malawi, pia Kamati hiyo ilipitisha maazimio mengine kadhaa yanayohusiana na masuala mtambuka kama yale ya haki za mtoto,haki za binadamu, maendeleo ya vijana, usawa na uwezeshaji wa wanawake na utokomezaji wa umaskini.

Na Mwandishi Maalum, New York

Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imewashukuru wajumbe wa Kamati ya Tatu ya Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa kwa kupitisha kwa kauli moja Azimio linalotaka pamoja na mambo mengine Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa kuwasilisha taarifa kuhusu watu wenye ualibino.

Azimio hilo na ambalo liliandaliwa kwa pamoja kati ya Wakilishi za Kudumu za Tanzania na Malawi katika Umoja wa Mataifa, limepitishwa siku ya Jumanne baada ya majadiliano ya kina na jumuishi yaliyowashilikisha nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa.
Akiwasilisha Azimio hilo mbele ya wajumbe wa Kamati hiyo ambayo inahusika na masuala ya Haki za Binadamu, Utamaduni na Maendeleo ya Jamii, Mwakilishi wa Kudumu wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa, Balozi Tuvako Manongi amesema
“Azimio hilo linalenga katika kuitaka jumuiya ya kimataifa kutambua na kutafuta ufumbuzi wa changamoto mbalimbali zinazowakabili watu wenye ualibino”

Akabainisha kwamba ni kwa kutambua changamoto hizo zikiwano za kielimu, kiafya na kiuchumi pamoja na hatari zinazowakabili kwa sababu tu ya kuwa na ualibino ndio maana Tanzania kwa kushirikiana na Malawi ziliamua kuanda na hatimaye kuwaalika nchi wanachama si tu kulijadili na kuboresha mapendekezo yaliyomo katika azimio hilo bali pia kuliunga mkono.

Balozi Tuvako Manongi akawaeleza wajumbe wa Kamati ya Tatu ya Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa kwamba, katika eneo la afya watu wenye ualibino wanakabiliwa na tatizo kubwa la kansa ya ngozi kutoka na hali hiyo. Tatizo alilosema linahitaji ushirikiano wa pamoja katika kuwasaidia.

“Azimio hili linalenga katika kuelezea pengo lililopo kuhusiana na changamoto zinazowakabili watu wenye ualibino hususani katika elimu, afya, na ajira . Matatizo yao na changamoto zao na kwa kuwa yanaingiliana yanahitaji ushiriano kati yetu sisi sote na ufumbuzi wa muda mrefu” akabinisha Balozi Manongi.

Na kuongeza kuwa hakuna matibabu au uponyaji kwa watu wenye ualibino lakini kuna baadhi ya nchi chache ambazo zimeweza kubuni sera za kijamii na za afya za kuwasaidia watu wenye ualibino. Na kwamba ushirikiano kati ya nchi hizo chache ambazo zina sera nzuri za afya na zile ambazo hazina uwezo mkubwa wa raslimali ni jambo ambalo Tanzania inapenda kupitia azimio hilo kuona ukiimarishwa na kuwa shirikishi.

“Tunawashukuru wale wote ambao wameshirikia katika majadiliano ya awali ya maandalizi ya Azimio hili kwa mchango wao wa mawazo lakini pia kwa kuliunga mkono Azimio hili. Hapashaka Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa atawasilisha taarifa yake kama alivyoombwa kupitia Azimio hili.

Kwa mujibu wa Azimio hilo,Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa anatakiwa kuwasilisha Taarifa kuhusu watu wenye ualibino wakati wa kipindi cha Baraza Kuu la 72 la Umoja wa Mataifa.

Katika miaka ya hivi karibuni tatizo na changamoto zinazowakabili watu wenye ualibino limekuwa likipewa uzito wa aina yake katika Jumuiya ya Kimataifa.

Mwaka jana Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa lilipitisha Azimio ambalo lilitamka kwamba Juni 13 ya kila mwaka inakuwa siku ya Kimataifa ya watu wenye ualibino. Na mwezi Machi mwaka huu Baraza la Haki za Binadamu liliteua mtaalamu wa kujitegemea kuhusu haki za binadamu za watu wenye ualibino.

Azimio lililoandaliwa na Tanzania na Malawi ni mwendelezo wa juhudi kutafuta namba bora na jumuishi za kuwasaidia na kuwaendeleza watu wenye ualibino.