Monday, October 29, 2018

Mwakilishi wa UN WOMEN awasilisha Hati za Utambulisho

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Dkt. Augustine Mahiga amepokea Hati za Utambulisho kutoka kwa Mwakilishi wa Shirika la Wanawake la Umoja wa Mataifa (UN WOMEN) Bi. Hodan Addou. Baada ya kupokea Hati hizo Dkt. Mahiga alitumia fursa hiyo kumkaribisha nchini na kumuhakikishia kumpatia Ushirikiano wa kutosha kwa kipindi chote cha utendaji kazi wake hapa nchini.  
Dkt. Mahiga akizungumza na Bi. Addou
Bi. Addou akimwelezea jambo Dkt. Mahiga



Italia yaiahidi Afrika Ushirikiano wa kiuchumi

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Italia yaiahidi Afrika Ushirikiano wa kiuchumi

Mawaziri wa Mambo ya Nje wa Italia na Afrika wameazimia kukuza na kuimarisha Ushirikiano katika nyanja mbalimbali, hususan biashara na uwekezaji kwa ajili ya maendeleo ya kweli barani Afrika.

Mawaziri hao walifikia azimio hilo wakati wa mkutano wa pili wa Mawaziri wa Mambo ya Nje wa Italia na Afrika uliofanyika Farnesina, Italia tarehe 25 Oktoba 2018 na kuhudhuriwa na Mawaziri wa zaidi ya nchi 40 akiwemo Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirkiano wa Afrika Mashariki wa Tanzania, Mhe.  Dkt. Augustine Mahiga (Mb).

Mawaziri hao walikutana kwa madhumuni ya kujadili kwa pamoja changamoto zinazohusu usalama, uhuru, amani, demokrasia na namna wadau wa Italia (wenye viwanda, Wafanyabiashara, wanazuoni na taasisi zisizo za kiserikali) watakavyoweza kushiriki katika kukuza uchumi barani Afrika hasa katika sekta ya uwekezaji na biashara.

Katika hotuba yake kwenye mkutano huo ambao ulifunguliwa na Rais wa Italia, Mhe. Sergio Mattarella,  Mhe Waziri Mahiga alisisitiza suala la amani kuwa ni muhimu kwa ajili ya maendeleo ya kiuchumi barani Afrika. Aidha, alieleza umuhimu wa Jumuiya za Kikanda katika kusuluhisha migogoro mbalimbali inayotokea kwenye Bara la Afrika. Katika hilo, alijulisha jitihada zinazofanywa na Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) na Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) katika kusuluhisha mgogoro nchini Burundi na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.

Sanjari na mkutano huo, Waziri Mahiga alipata fursa ya kufanya mazungumzo kwa nyakati tofauti na Waziri wa Mambo ya Nje wa Italia, Mhe Enzo Moavero na Rais wa Mfuko wa Kimataifa wa Ufadhili wa Maendeleo ya Kilimo (IFAD), Bw. Gilbert F. Houngbo.

Kwenye mazungumzo na Waziri wa Mambo ya Nje wa Italia, Viongozi hao walikubaliana kuwa, kuandaliwe Hati ya Makubaliano (MoU) kati ya Tanzania na Italia ya kufanya majadiliano ya mara kwa mara yenye lengo ya kukuza ushirikiano katika sekta mbalimbali ikiwemo biashara, uwekezaji, utalii, elimu na utamaduni.

Kuhusu mazungumzo na Rais wa IFAD, wawili hao walikubaliana kuimarisha ushirikiano wa Tanzania na Mfuko huo kwenye maeneo makuu mannne ambayo ni Huduma za kifedha kwa wakulima wadogo, kuwajengea uwezeo vijana ili waweze kufanya kilimo kama sehemu ya ajira, kuboresha sekta ya mifugo pamoja na masuala ya lishe bora.

Aidha, Rais wa IFAD alimuahidi Mhe Waziri kuwa mfuko huo utaendelea kushirikiana vizuri na serikali ya Tanzania hata kwenye miradi inayoendelea ikiwemo Programu ya Miundombinu ya masoko, uongezaji wa thamani na kuwawezesha wakulima wadogo wa vijijini kifedha (Marketing Infrastructure, Value Addition and Rural Finance-MIVRAF). Madhumuni ya programu hiyo ni kupunguza umasikini na kuharakisha ukuaji wa uchumi vijijini ili kuboresha kipato na usalama wa chakula kwa jamii ya watu wa vijijini.

Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,
Dar Es Salaam, Tanzania
29 Oktoba 2018

Sunday, October 28, 2018

UBALOZI WA TANZANIA, KOMORO WAADHIMISHA MIAKA19 YA KUMBUKUMBU YA MWALIMU NYERERE

Balozi wa Tanzania Visiwani Komoro Mhe. Sylvester M. Mabumba akihutubia kwenye Kongamano la Mwalimu Nyerere, ambapo Ubalozi wa Tanzania kwa kushirikiana na Diaspora ya Watanzania Visiwani Komoro (TADICO) pamoja na taasisi ya kijamii ya Komoro ijulikanayo kama Udjamaa wa Komori na Afrika Mashariki uliandaa Kongomano hilo la siku mbili kuanzia tarehe 26 – 27 Oktoba, 2018 kama sehemu ya kumenzi Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.

Watanzania waishio Visiwani Komoro wakimsikilisha Mhe. Mabumba hayupo pichani.


Watanzania waishio Visiwani Komoro wakiwa kayika picha ya pamoja mara baada ya kumalizika kwa ufunguzi wa Kongamano hilo



UBALOZI WA TANZANIA, KOMORO WAADHIMISHA MIAKA19 YA KUMBUKUMBU YA MWALIMU NYERERE
TAREHE 26 – 27 Octoba, 2018

Katika harakati za kuendeleza kukuza na kuhuisha kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere, Ubalozi wa Tanzania Visiwani Komoro kwa kushirikiana na Diaspora ya Watanzania Visiwani Komoro (TADICO) pamoja na taasisi ya kijamii ya Komoro ijulikanayo kama Udjamaa wa Komori na Afrika Mashariki uliandaa Kongomano la siku mbili kuanzia tarehe 26 – 27 Oktoba, 2018 kama sehemu ya kumenzi Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.
Kongomano hilo lilifanyika katika ukumbi wa Bunge la Taifa la Komoro ambapo mgeni rasmi alikuwa ni Waziri wa Elimu wa Komoro, Mhe. Salime Mohamed Abderemane. Aidha, kutoka Tanzania, Mhe. Pro. Mark Mwandosya alialikiwa kama mmoja ya watoa mada juu ya maisha ya Mwalimu Nyerere.
Wageni wengine mashuhuri walioshiriki katika Kongomano hilo ni pamoja na Mhe. Mohamed Msaidie, Waziri wa zamani wa Mambo ya Ndani wa Komoro, Mhe. Balozi Ahmed Thabeet, mmoja ya waazilishi wa Chama cha Ukombozi cha Komoro kujilikanacho kama MOLINACO. Aidha, Balozi wa Tanzania Visiwani Komoro, Mhe. Sylvester M. Mabumba naye pia aliweza kushiriki kikamilifu katika Kongomano hilo.
Hii ni mara ya kwanza kwa Ubalozi wa Tanzania Visiwani Komoro kusheherekea kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere Visiwani hapa. Lengo la Kongomano hilo ilikuwa ni kuelezea mchango wa Mwalimu Nyerere na Tanzania kwa ujumla katika harakati za ukombozi wa Visiwa vya Komoro kuanzia 1962 – 1975. Aidha, Kongomano hilo lililenga pia kuikurubisha Komoro katika ukanda wa Afrika Mashariki, kwa kuwa mda mrefu Visiwa hiyo vimeelekeza mahusiano yake katika nchi za Ulaya na Mashariki ya Kati.
Watoa mada mbalimbali waliweza kuelezea kwa kina mchango wa Mwalimu Nyerere katika harakati za ukombozi wa Visiwa vya Komoro na Afrika kwa ujumla. Prof. Mwandosya kwa upande wake alielezea mchango wa Mwalimu katika harakati zake za kudumisha umoja na kuwasihi wa Komoro kudumisha umoja wao hasa katika kipindi hiki ambapo nchi hiyo inapitia mageuzi makubwa ya kisiasa.
 Kongomano la kumuenzi Mwalimu Nyerere lilifana sana na imekuwa ni chachu kwa Wakomoro kuona umuhimu wa kudumisha mahusiano ya (Kusini-Kusini), South-South Cooperation. Ubalozi umedhimiria kuendeleza Kongomano la Mwalimu kwani imeonekana yanachangia sana kudumisha mahusiano mazuri yaliopo baina ya Tanzania na Komoro.