Thursday, April 18, 2024

WIZARA YA MAMBO YA NJE YAJIVUNIA KUIMARIKA KWA DIPLOMASIA, MIAKA 60 YA MUUNGANO


Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk (Mb.) ametaja mafanikio ya Wizara katika kipindi cha miaka 60 ya Muungano wa Tanzania.

Mhe. Balozi Mbarouk ametaja mafanikio hayo jijini Dodoma Aprili 18, 2024 alipozungumza na waandishi wa habari kuelezea mafanikio ya Wizara katika kipindi cha miaka 60 ya Muungano wa Tanzania. 

Balozi Mbarouk amesema Wizara inajivunia kuendelea kuimarika kwa ushirikiano na uhusiano kati ya Tanzania na nchi mbalimbali duniani na hivyo kupata mafanikio katika sekta mbalimbali kupitia ushirikiano wa uwili na ujirani mwema baina yake na mataifa mengine, 

“Mafanikio haya yamepatikana kupitia ushirikiano uliopo ambao unatekelezwa kupitia taratibu maalum ikiwemo mikutano ya Tume za Ushirikiano wa Pamoja. Ushirikiano huu umeleta mafanikio kupitia kusainiwa Mikataba na Hati za Makubaliano (MoUs) ili kutekeleza maeneo mahsusi katika sekta mbalimbali za siasa, kiuchumi na kijamii,” alisema. 

Amesema kupitia mikutano hiyo Tanzania imenufaika na kuongezeka kwa biashara na uwekezaji ambapo bidhaa za kilimo, mifugo, matunda na mbogamboga zimepata masoko katika nchi mbalimbali. 

Amesema Tanzania imenufaika na fursa za mafunzo ya muda mrefu na mfupi yanayofadhiliwa na nchi mbalimbali ikiwemo Uingereza, Uturuki, Marekani, Misri, India, Indonesia, China, Hungary, Japan, New Zealand, Australia, Urusi, Ujerumani, Cuba, Korea, Yugoslavia, Uholanzi, Ubelgiji, Algeria, Sudan, Saudi Arabia, Thailand na Pakistan. 

Amesema Tanzania imefanikiwa kuwa sehemu ya kuanzishwa kwa jumuiya za kikanda kama Umoja wa Afrika; Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), Jumuiya ya Afrika Mashariki na Jumuiya ya Nchi zilizo katika Maziwa Makuu (ICGLR) na kupitia uanachama katika jumuiya hizo Tanzania imetekeleza programu katika sekta mtangamano za siasa, ulinzi na Usalama; Miundombinu; Biashara, Viwanda, Fedha na Uwekezaji. 

“Tanzania imekuwa sehemu ya utekelezaji wa dhana ya kutatua changamoto za kidunia kwa pamoja yaani Multilateralism, kuwa mbia anayeaminika na kukubalika katika maamuzi mbalimbali duniani hasa katika mashirika ya kimataifa hususan Umoja wa Mataifa na kuwa mbia kwenye vyombo mbalimbali ikiwemo Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa; Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa; Benki ya Dunia na Shirika la Biashara Duniani (WTO),” alisema. 

Ameongeza kuwa Tanzania imekuwa sehemu ya maamuzi katika maeneo ya mazingira na mabadiliko ya tabia nchi; ulinzi na usalama; utatuzi wa migogoro; maendeleo endelevu na utafutaji rasilimali kwa ajili ya maendeleo ambapo kupitia jukwaa hilo imepata fursa ya kutoa misimamo yake kwa masuala muhimu ikiwemo mgogoro wa Isarel na Palestina na suala la Sahara Magharibi na kuwa sehemu ya kuunga mkono Sera ya Kutofungamana na Upande wowote (NAM) na kuunga mkono ajenda ya msimamo wa Kundi la 77 na China katika majukwaa ya Kimataifa kwa maslahi mapana ya Taifa. 

Amesema Tanzania inajivunia mchango wake katika juhudi za kulinda Amani Duniani na hivyo kutekeleza malengo ya Sera Mpya ya Mambo ya Nje na moja ya malengo mahsusi ya Umoja wa mataifa. 

Amesema pia Tanzania imekuwa ikishiriki kulinda Amani kupitia Misheni za Kikanda ikiwemo Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) na Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC); Umoja wa Afrika na Umoja wa Mataifa na baadhi ya maeneo ambayo Tanzania imechangia walinda amani ni pamoja na Lebanon; Darfur; Abyei; Liberia; Sudan Kusini; Sudan; DRC; Msumbiji na Afrika ya Kati na kuongeza kuwa Tanzania imeshiriki kikamilifu katika utatuzi wa migogoro kwa njia ya mazungumzo na diplomasia kwenye nchi na maeneo mbalimbali ikiwemo, Darfur; Cambodia; Sudan Kusini; Burundi na Kenya. 

Amesema Tanzania kuwa mwenyeji wa Taasisi za Kimataifa kama ishara ya kuaminika na kukubalika na nchi nyingine. Tanzania imeendelea kufungua Balozi na Ofisi za Uwakilishi katika nchi mbalimbali za kimkakati ikiwa ni sehemu ya kuimarisha utekelezaji wa Sera ya Mambo ya Nje hususan Diplomasia ya Uchumi. 

Amesema Serikali ya Awamu ya Sita imefungua Balozi mpya mbili za Vienna, Austria na Jakata, Indonesia na Konseli Kuu mbili za Lugumbashi na Guangzhou, China ambapo ufunguzi wa Balozi hizo unaifanya Tanzania kuwa na Balozi na Ofisi za Uwakilishi 45 na Konseli Kuu TANO huku ikiwa ni mwenyeji wa nchi na mashirika ya kimataifa zaidi ya 90 zikiwemo Konseli Kuu ambazo baadhi yake zipo Zanzibar kama vile China, Oman, India na Umoja wa Falme za Kiarabu. 

Amesema Tanzania imefanikiwa kutoa viongozi mahiri kuongoza taasisi za kikanda na kimataifa ikiwa ni ishara ya kuaminiwa na mataifa mengine na kutaja baadhi ya nafasi hizo kuwa ni uteuzi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kuwa Mwenyekiti Mwenza wa Mkutano wa Kilele wa Matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia Barani Afrika utakaofanyika Paris, Ufaransa mwezi Mei 2024. 

Amesema Tanzania pia ilitoa Rais wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa ambapo Dkt. Salim Ahmed Salim aliongoza Vikao Vinne vya Baraza hilo mwaka 1979 na 1980 na Dkt. Salim Ahmed Salim alihudumu kama Katibu Mkuu wa Umoja wa Afrika (OAU). Watanzania wengine ni Dkt. Asha-Rose Migiro kuwa Naibu Katibu Mkuu wa kwanza kutoka Afrika; Balozi Getrude Mongela kuwa Rais wa Bunge la Afrika; Dkt. Stergomena Tax kuwa katibu Mtendaji wa SADC; Balozi Juma Mwapachu katibu Mkuu wa EAC; Mhe. Balozi Liberata Mulamula (Mb.), Katibu Mtendaji wa Jumuiya ya Nchi za Ukanda wa Maziwa Makuu (ICGLR); Profesa Anna Tibaijuka kuwa Naibu Katibu Mkuu na Mkuu wa Shirika la Maendeleo ya Makazi la Umoja wa Mataifa (UN-HABITAT) na Mkuu wa Ofisi za Umoja wa Mataifa Nairobi (UNON), Bi. Joyce Msuya, Naibu Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Mazingira la Umoja wa Mataifa (UNEP) na Spika wa Bunge la Tanzania Mhe. Dkt. Tulia Ackson (Mb.) kuchaguliwa kuwa Rais wa Umoja wa Mabunge Duniani (IPU). Dkt. Tulia ni mwanamke wa kwanza kutoka barani Afrika kushika wadhifa huo. 

Amesema Tanzania imechangia katika juhudi za kubidhaisha Kiswahili ndani na nje ya nchi na kutoa ushawishi wa matumizi yake kama nyenzo ya diplomasia, usuluhishi wa migogoro; ukombozi na uhuru katika nchi za bara la Afrika. 

Amesema Viongozi wa Tanzania katika awamu zote na sasa wakiongozwa na Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, Makamu wa Rais, Mhe. Dkt. Philip Isdor Mpango; Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt Hussein Ali Mwinyi; Waziri Mkuu, Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa (Mb.), Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. January Makamba (Mb.) wamekuwa wakifanya ziara za kimkakati katika nchi mbalimbali kwa lengo la kukuza na kuimarisha uhusiano baina ya Tanzania na nchi hizo. 

Amesema Wakuu wa Nchi waliotembelea Tanzania katika miaka ya hivi karibun ni pamoja na: Rais wa Uganda, Mhe. Yoweri Kaguta Museveni; Rais wa Rwanda, Mhe. Paul Kagame; Rais wa Burundi, Mhe. Everiste Ndayishimiye; Rais wa DRC, Mhe. Felix Tshisekedi; Rais wa Msumbiji, Mhe. Fillipe Nyusi; Rais wa Zambia, Mhe. Hakainde Hichilema; Rais wa Malawi, Mhe. Lazarous Chakwera; Rais wa Poland, Mhe. Andrzej Duda; Rais wa Ujerumani, Mhe. Frank-Walter Steinmeier; Rais wa Romania, Mhe. Klaus Werner Iohannis; Rais wa Hungary, Mhe. Katalin Novak; Rais wa Indonesia, Mhe. Joko Widodo; Makamu wa Rais wa Marekani, Mhe. Kamala Harris; Makamu wa Rais wa Cuba, Mhe. Salvador Valdes Mesa; Waziri Mkuu wa Ethiopia, Mhe. Abiy Ahmed na Naibu Waziri Mkuu wa China Mhe. Liu Guozhong na Rais wa Kenya, Mhe. William Ruto. 

Amesena Serikali imeimarisha ushiriki wa Watanzania waishio Nje ya Nchi na Raia wa Nchi nyingine Wenye Asili ya Tanzania katika maendeleo ya Taifa na kuchukua hatua za Kisera kwa kujumuisha masuala ya Diaspora katika mapitio ya Sera ya Mambo ya Nje ya Mwaka 2001 na imekamilisha mfumo wa kiditali wa kukusanya na kutunza taarifa za Diaspora ambapo mpaka sasa Diaspora wa Tanzania wapatao 1403 wamejiandikisha katika mfumo huo na hivyo kuiwezesha Serikali kupata takwimu sahihi za idadi ya Diaspora, mahali walipo, ujuzi na uzoefu walionao huku mfumo pia ukiwawezesha Diaspora kupata taarifa kuhusu fursa na huduma mbalimbali zinazotolewa na Serikali na sekta binafsi nchini. 

Amesema Serikali iko katika hatua za kukamilisha kutoa Hadhi Maalum (Special Status) kwa Raia wa Nchi Nyingine Wenye Asili ya Tanzania ili kuwezesha kuchangia ipasavyo katika maendeleo ya Taifa.


Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk (Mb) akiongea na waandishi wa habari kuhusu mafanikio ya Miaka 60 Muungano wa Tanzania katika kikao kilichofanyika jijini Dodoma.
Waandishi wa Habari wakimsikiliza Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk (Mb) alipokuwa akiongea nao kuhusu mafanikio ya Miaka 60 Muungano wa Tanzania katika kikao kilichofanyika jijini Dodoma.
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk (Mb) akisisitiza jambo wakati akiongea na waandishi wa habari kuhusu mafanikio ya Miaka 60 Muungano wa Tanzania katika kikao kilichofanyika jijini Dodoma.
Waandishi wa Habari wakimsikiliza Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk (Mb) hayupo pichani alipokuwa akiongea nao kuhusu mafanikio ya Miaka 60 Muungano wa Tanzania katika kikao kilichofanyika jijini Dodoma.

MHE. RAIS SAMIA ATUNUKIWA SHAHADA YA HESHIMA YA UDAKTARI NCHINI UTURUKI


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt Samia Suluhu ametunukiwa Shahada ya Heshima ya Udaktari (Honoris Causa) katika Uchumi na Chuo Kikuu cha Ankara cha nchini Uturuki ikiwa ni ishara ya kutambua mchango wake katika kuboresha maisha ya watanzania kupitia mageuzi mbalimbali pamoja na kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi na nchi mbaimbali duniani ikiwemo Uturuki.


Akizungumza kupokea tuzo hiyo kwenye hafla iliyofanyika katika Chuo hicho jijini Ankara leo tarehe 18 Aprili 2024, Mhe. Rais Samia amelishukuru Baraza la Chuo kwa kumpatia heshima hiyo kubwa kwake na kwa Watanzania wake kwa waume na  kukipongeza Chuo hicho kwa kuendelea kutoa elimu yenye ubora na kuiweka Uturuki kuwa miongoni mwa nchi zinazotoa elimu ya juu bora duniani.

 

“Nilipopokea taarifa kuhusu kutunukiwa shahada hii nilijiuliza, wametumia vigezo gani hadi kufikia uamuzi huu, Waziri wangu wa Mambo ya Nje alinipatia orodha yenye vigezo hivyo nikakubali, nawashukuru sana” alisema Rais Dkt. Samia

 

Mhe. Rais Samia amesema Tanzania itaendelea kushirikiana na Uturuki katika kufikia malengo yake ya kukuza  uchumi kupitia ushirikiano katika sekta mbalimbali ikiwemo biashara, kilimo, uwekezaji na ushirikiano baina ya watu wa nchi hizi mbili.

 

Baraza la Chuo Kikuu cha Ankara kwa kauli moja liliamua kumtunukia Mhe. Rais Dkt. Samia Shahada hiyo ya heshima, kwa kutambua Uongozi wake wa kipekee ambao umeleta mageuzi makubwa ya kijamii, kisiasa, na kiuchumi nchini Tanzania. Mageuzi  hayo yameboresha ustawi wa Watanzania; na kuimarisha sifa ya Tanzania ulimwenguni; na yamekuza mahusiano ya kibiashara, kiuchumi na kisiasa kati ya Tanzania na nchi nyingine, ikiwemo Uturuki.


Hafla ya kukabidhiwa tuzo hiyo imeongozwa na Prof. Necdet Ãœnüvar, Mkuu wa Chuo, na kushuhudiwa na Wahadhiri  na wanafunzi wa Chuo hicho pamoja na viongozi mbalimbali kutoka Serikali ya Tanzania na Uturuki akiwemo Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. January Makamba, Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji, Waziri wa Uchukuzi, Mhe. Prof. Makame Mbarawa, Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar, Mhe. Lela Muhammed Mussa.

Shahada hii ni ya pili kwa Mhe. Rais Samia kutunukiwa kutoka ugenini ambapo Shahada ya kwanza ya aina hiyo alitunukiwa na Chuo Kikuu cha Jawaharlal Nehru cha nchini India mwezi Oktoba 2023.

Mkuu wa Chuo Kikuu cha Ankara cha nchini Uturuki,  Prof. Necdet Ãœnüvar, akimtunuku Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Shahada ya Heshima ya Udaktari (Honoris Causa) katika Uchumi katika hafla iliyofanyika Chuoni hapo tarehe 18 Aprili 2024 wakati wa ziara ya kitaifa ya Mhe. Rais Samia nchini humo.
Mhe. Rais Dkt. Samia akiwa katika picha ya pamoja na Prof. Ünüvar pamoja na Waziri anayeshughulikia masuala ya Familia na Huduma za Jamii wa Uturuki, Mhe.Mahinur Ozdemir Goktas mara baada ya kutunukiwa Shahada ya Heshima ya Udaktari katika Uchumi na Chuo Kikuu cha Ankara

Mhe. Rais Dkt. Samia akifuwa ukumbini kabla ya kutunukiwa Shahada ya Heshima ya Udaktari katika Uchumi na Chuo Kikuu cha Ankara. Kutoka kulia ni Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. January Makamba akifuatiwa na Prof.Ünüvar pamoja na Mhe. Waziri Mahinur



Taratibu mbalimbali zikiendelea kabla ya Mhe. Rais Samia kutunukiwa Shahada yake ya Udaktari. Pichani ni viongozi wakiwa wamesimama kwa heshima ya nyimbo za mataifa yao

Mhe. Rais Dkt. Samia akiwa katika picha ya pamoja na Mkuu wa Chuo cha Ankara, Wakufunzi na Viongozi mbalimbali

 

Wednesday, April 17, 2024

MHE. RAIS SAMIA AWASILI NCHINI UTURUKI KWA ZIARA YA KITAIFA

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan amewasili katika jijini Ankara, Uturuki leo tarehe 17 Aprili 2024 kuanza ziara yake ya kitaifa ya siku nne inayofanyika  kufuatia mwaliko wa Rais wa Jamhuri ya Uturuki, Mhe. Recep Tayyip Erdogan.

 

Mara baada ya kuwasili Mhe. Rais Samia alilakiwa na Waziri anayeshughulikia masuala ya Huduma za Jamii na Familia, Mhe. Mahinur Ozdemir GoktaÅŸ.

 

Akiwa nchini Uturuki, Mhe. Rais Samia atapokelewa rasmi na mwenyeji wake Mhe. Rais Erdogan katika Ikulu ya nchi hiyo jijini Ankara tarehe 18 Aprili 2024. Viongozi hao pamoja na mambo mengine watashiriki mazungumzo rasmi na dhifa ya kitaifa iliyoandaliwa na Mhe. Rais Erdogan kwa heshima ya Mhe. Rais Samia.

 

Siku hiyohiyo Mhe. Rais Samia atatunukiwa Shahada ya Heshima ya Udaktari katika Uchumi na Chuo Kikuu cha Ankara kutokana na chuo hicho kutambua uongozi wake wa kipekee ambao umeleta mageuzi makubwa ya kijamii, kisiasa na kiuchumi ambayo yameboresha ustawi wa Wtanzania na kuimarisha sifa ya Tanzania ulimwenguni pamoja na kukuza uhusiano wa kibiashara, kiuchumi na kisiasa kati ya Tanzania na nchi nyingine ikiwemo Uturuki.

 

Mhe. Rais Samia ataondoka Ankara tarehe 19 Aprili 2024 kuelekea Istanbul, mji mkuu wa kibiashara wa Uturuki kwa ajili ya kufungua rasmi  Kongamano la Biashara na Uwekezaji kati ya Tanzania na Uturuki ambalo litahudhuriwa pia na Makamu wa Rais wa Uturuki, Mhe. Cevdet Yılmaz.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akisalimiana na Waziri anayeshughulikia masuala ya Familia na Huduma za Jamii wa Uturuki, Mhe.Mahinur Ozdemir Goktas mara baada ya kuwasili nchini Uturuki kwa ajili ya kuanza ziara ya kitaifa itakayofanyika kuanzia tarehe 17 hadi 21 Aprili 2024

Mhe. Rais Samia akisalimiana na Balozi wa Tanzania nchini Uturuki, Mhe. Iddi Bakari mara baada ya kuwasili nchni humo kwa ziara ya kitaifa. Wanaoshuhudia ni pamoja na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. January Makamba (wa nne kushoto) pamoja Balozi wa Uturuki nchini Mhe. Dkt. Mehmet Gulluoglu (kulia)

Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan akiwa katika mazungumzo na Mhe. Mahinur mara baada ya kuwasili nchini Uturuki kwa ziara ya kitaifa






 

WAZIRI MAKAMBA AKUTANA KWA MAZUNGUMZO NA MWENYEKITI WA UMOJA WA URAFIKI WA WABUNGE WA TANZANIA NA UTURUKI

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. January Makamba amekutana kwa mazungumzo na Mbunge wa Bunge la Uturuki na Mwenyekiti wa Umoja wa Urafiki wa Wabunge wa Tanzania na nchi hiyo, Mhe. Zeki Korkutata.

 

Katika mazungumzo yao ambayo yamefanyika tarehe 16 Aprili 2024 jijini Ankara, ikiwa ni sehemu ya kukamilisha maandalizi ya ziara ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan inayotarajiwa kufanyika nchini humo kuanzia tarehe 17 hadi 21 Aprili 2024 viongozi hao wamejadili maeneo muhimu ya ushirikiano ambayo pia yatajadiliwa kwa uzito wa juu wakati wa ziara hiyo.

 

Mhe. Makamba amesema miongoni mwa masuala muhimu nchi hizi mbili zitayapa kipaumbele kupitia ziara hii, ni  pamoja na kufanyika haraka kwa mkutano wa Tume ya Pamoja ya Ushirikiano kwenye masuala ya Uchumi baina ya Tanzania na Uturuki.

 

Amesema kupitia tume hii nchi hizi mbili zitapata fursa ya kujadili kwa kina sekta za ushirikiano wa kimkakati baina yake na kuandaa mikakati ya utekelezaji wa makubaliano yote yatakayofikiwa wakati wa ziara hii ya kihistoria.

 

Mhe. Makamba amesema kuwa, Uturuki ni nchi muhimu wakati huu  ambapo  Tanzania imejikita katika kukuza uchumi wake kupitia ushirikiano na nchi mbalimbali na kwamba ana imani kwamba Tanzania itanufaika kupitia sekta ambazo nchi hiyo imepiga hatua za kiuchumi na kimaendeleo kama viwanda, usafirishaji, utalii na nishati.

 

Amesema Kngamano la Biashara na Uwekezaji litakalofanyika wakati wa ziara ya Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan litakuwa ni chachu ya kuongeza kasi zaidi ya kukuza urari na ujazo wa biashara baina ya nchi hizi mbili.

 

Vile vile amesema wakati wa ziara hiyo hati nane za ushrikiano kwenye sekta za kimkakati ikiwemo Elimu, Uwekezaji na ushirikiano katika masuala ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu  zitasainiwa.

 

Pia alitumia fursa hiyo kumkaribisha Mhe. Korkutata kutembelea Tanzania hususan Bungeni ili kujionea utendaji wa shughuli za Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.  

Kwa upande wake, Mhe. Korkutata amesema Uturuki inathamini ushirikiano uliopo baina yake na Tanzania na kwamba ziara ya Mhe. Rais Samia ni ishara kuwa nchi hizi mbili zimedhamiria kuupeleka ushirikiano huo katika hatua nyingine ya juu kwa manufaa ya wananchi wa pande hizi mbili.

 

Mhe. Mhe. Makamba yupo nchini Uturuki kwa ajili ya kukamilisha maandalizi ya ziara ya kitaifa ya Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan ambapo mbali na kukutana na Mhe. Korkutata pamoja na kutembelea Bunge la Uturuki, Mhe. Makamba pia amekutana kwa mazungumzo na mwenyeji wake, Waziri wa Mambo ya Nje wa nchi hiyo, Mhe. Hakan Fidan.


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. January Makamba akizungumza na Mbunge na Mwenyekiti wa Umoja wa Urafiki wa Wabunge wa Tanzania na Uturuki Mhe. Zeki Korkutata (hayupo pichani) ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya ziara ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan nchini humo
Mhe. Korkutata naye akizungumza. Kushoto ni Balozi wa Tanzania nchini Uturuki, Mhe. Iddi Bakari na kulia ni Mkalimani wa Mhe. Korkutata
Mazungumzo yakiendelea

Mazungumzo yakiendelea



Mazungumzo yakiendelea. Wa pili kulia ni Mkurugenzi wa Idara ya Ulaya na Amerika katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Swahiba Mndeme
Mkuu wa Utawala katika Ubalozi wa Tanzania nchini Uturuki, Bw. Mashaka Chikoli (kushoto) pamoja na Afisa Mambo ya Nje, Bi. Clementina Msafiri wakifuatilia mazungumzo.

Mhe. Waziri Makamba akipokea zawadi kutoka kwa Mhe. Korkutata