Wednesday, April 17, 2024

WAZIRI MAKAMBA AKUTANA KWA MAZUNGUMZO NA MWENYEKITI WA UMOJA WA URAFIKI WA WABUNGE WA TANZANIA NA UTURUKI

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. January Makamba amekutana kwa mazungumzo na Mbunge wa Bunge la Uturuki na Mwenyekiti wa Umoja wa Urafiki wa Wabunge wa Tanzania na nchi hiyo, Mhe. Zeki Korkutata.

 

Katika mazungumzo yao ambayo yamefanyika tarehe 16 Aprili 2024 jijini Ankara, ikiwa ni sehemu ya kukamilisha maandalizi ya ziara ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan inayotarajiwa kufanyika nchini humo kuanzia tarehe 17 hadi 21 Aprili 2024 viongozi hao wamejadili maeneo muhimu ya ushirikiano ambayo pia yatajadiliwa kwa uzito wa juu wakati wa ziara hiyo.

 

Mhe. Makamba amesema miongoni mwa masuala muhimu nchi hizi mbili zitayapa kipaumbele kupitia ziara hii, ni  pamoja na kufanyika haraka kwa mkutano wa Tume ya Pamoja ya Ushirikiano kwenye masuala ya Uchumi baina ya Tanzania na Uturuki.

 

Amesema kupitia tume hii nchi hizi mbili zitapata fursa ya kujadili kwa kina sekta za ushirikiano wa kimkakati baina yake na kuandaa mikakati ya utekelezaji wa makubaliano yote yatakayofikiwa wakati wa ziara hii ya kihistoria.

 

Mhe. Makamba amesema kuwa, Uturuki ni nchi muhimu wakati huu  ambapo  Tanzania imejikita katika kukuza uchumi wake kupitia ushirikiano na nchi mbalimbali na kwamba ana imani kwamba Tanzania itanufaika kupitia sekta ambazo nchi hiyo imepiga hatua za kiuchumi na kimaendeleo kama viwanda, usafirishaji, utalii na nishati.

 

Amesema Kngamano la Biashara na Uwekezaji litakalofanyika wakati wa ziara ya Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan litakuwa ni chachu ya kuongeza kasi zaidi ya kukuza urari na ujazo wa biashara baina ya nchi hizi mbili.

 

Vile vile amesema wakati wa ziara hiyo hati nane za ushrikiano kwenye sekta za kimkakati ikiwemo Elimu, Uwekezaji na ushirikiano katika masuala ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu  zitasainiwa.

 

Pia alitumia fursa hiyo kumkaribisha Mhe. Korkutata kutembelea Tanzania hususan Bungeni ili kujionea utendaji wa shughuli za Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.  

Kwa upande wake, Mhe. Korkutata amesema Uturuki inathamini ushirikiano uliopo baina yake na Tanzania na kwamba ziara ya Mhe. Rais Samia ni ishara kuwa nchi hizi mbili zimedhamiria kuupeleka ushirikiano huo katika hatua nyingine ya juu kwa manufaa ya wananchi wa pande hizi mbili.

 

Mhe. Mhe. Makamba yupo nchini Uturuki kwa ajili ya kukamilisha maandalizi ya ziara ya kitaifa ya Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan ambapo mbali na kukutana na Mhe. Korkutata pamoja na kutembelea Bunge la Uturuki, Mhe. Makamba pia amekutana kwa mazungumzo na mwenyeji wake, Waziri wa Mambo ya Nje wa nchi hiyo, Mhe. Hakan Fidan.


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. January Makamba akizungumza na Mbunge na Mwenyekiti wa Umoja wa Urafiki wa Wabunge wa Tanzania na Uturuki Mhe. Zeki Korkutata (hayupo pichani) ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya ziara ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan nchini humo
Mhe. Korkutata naye akizungumza. Kushoto ni Balozi wa Tanzania nchini Uturuki, Mhe. Iddi Bakari na kulia ni Mkalimani wa Mhe. Korkutata
Mazungumzo yakiendelea

Mazungumzo yakiendelea



Mazungumzo yakiendelea. Wa pili kulia ni Mkurugenzi wa Idara ya Ulaya na Amerika katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Swahiba Mndeme
Mkuu wa Utawala katika Ubalozi wa Tanzania nchini Uturuki, Bw. Mashaka Chikoli (kushoto) pamoja na Afisa Mambo ya Nje, Bi. Clementina Msafiri wakifuatilia mazungumzo.

Mhe. Waziri Makamba akipokea zawadi kutoka kwa Mhe. Korkutata




 

No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.