Friday, April 5, 2024

WAZIRI WA DERMARK AKUTANA NA DR. NCHEMBA, DR. JAFO NA PROF. MKUMBO


Kampuni za Denmark zimealikwa kuja kuwekeza nchini katika sekta za uchukuzi, nishati, madini, mazingira na uchumi wa buluu ambazo ni moja ya sekta za kipaumbele za Serikali ya Awamu ya Sita inayongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Mwaliko huo umetolewa wakati wa mikutano baina ya Waziri wa Ushirikiano wa Maendeleo na Masuala ya Hali ya Hewa wa Denmark, Mhe. Dan Jorgensen na Waziri wa Fedha, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, Mhe. Dkt. Selemani Jafo na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji, Mhe. Prof. Kitila Mkumbo iliyofanyika jijini Dodoma leo Aprili 5, 2024.

Waziri Nchemba alisema Serikali inajenga miundombinu ya reli ya kiwango cha kimataifa (SGR) ambapo Serikali ya Denmark imesaidia kipande cha kutoka Morogoro hadi Makutupora ambapo ujenzi wake umefikia zaidi ya asilimia 90. Alisema Serikali inakaribisha wawekezaji kuendesha reli hiyo ambapo itakapokamilika itaunganisha Tanzania na nchi za Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Burundi na Rwanda.

 

Dkt. Nchemba pia alizitaka kampuni za Denmark kuchangamkia fursa za ujenzi wa barabara ya mwendo kasi (express way) ya kutoka Dar Es Salaam hadi Dodoma ambayo pamoja na mambo mengine inalenga kupunguza msongamano wa magari katika barabara hiyo kuu nchini.

Kwa upande wake, Dkt. Jafo alisisitiza umuhimu wa Denmark kushirikiana na Tanzania katika programu za utunzaji wa mazingira ikiwemo uwekezaji katika sekta ya nishati jadidifu. Aliiomba Denmark kuunga mkono jitihada zinazofanywa na Serikali katika kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabianchi. Misaada inayohitajika, alisema kuwa ni pamoja na kujenga uwezo wa watumishi, misaada ya kiufundi na rasilimali mbalimbali zikiwemo fedha.

Prof. Mkumbo, kwa upande wake alisisitiza umuhimu wa kampuni za Denmark kuja kuwekeza katika viwanda vya kuongeza thamani (processing industries) hususan katika madini hadimu nchini. Alisema fursa katika sekta hiyo ni kubwa kwa kuwa Tanzania ina takribani aina 10 za madini hayo. 

Aliiomba Denmark kuunga mkono jitihada za Serikali za kuchochea sekta binafsi nchini ambayo mchango wake bado uko chini, licha ya umuhimu wake katika kuongeza ajira na kuondoa umasikini nchini. “Tunaomba kuungwa mkono katika misaada ya kiufundi, elimu ya ufundi, urasimishaji wa sekta binafsi, kuchochea uhai wa sekta binafsi ili tuweze kujenga uwezo wa watu wetu hasa vijana kuwa na mbinu za kujiajiri wenyewe”, Prof. Mkumbo alisema.

Waheshimiwa Mawaziri walihitimisha mazungumzo yao kwa kuishukuru Denmark kwa misaada inayoipatia Tanzania katika sekta mbalimbali. Ulitolewa mfano wa msaada wa Krone bilioni 1.95 uliotolewa na Denmark kwa ajili ya miradi ya maendeleo kwa kipindi cha mwaka 2014 hadi 2021.

Kwa upande wake, Mhe. Jorgensen alieleza kuwa Tanzania ni moja ya nchi za mwanzo kabisa barani Afrika kuanza ushirikiano wa kidiplomasia na Denmark katika miaka ya 1960. Hivyo, ameahidi kuendeleza ushirikiano huo kwa kuzingatia vipaumbele vitakavyobainishwa na pande zote mbili.

Waziri wa Fedha, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba (Mb.) akizungumza na Waziri wa Maendeleo na Mabadiliko ya Tabianchi wa Denmark, Mhe. Dan Jørgensen (hayupo pichani) alipomtembelea ofisini kwake jijini Dodoma tarehe 5 Aprili, 2024. Kushoto ni Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, Dkt. Natu Mwamba.

Ujumbe wa Tanzania ukifuatilia mazungumzo.

Mazungumzo yakiendelea.

Dkt. Mwigulu akimuaga Mhe. Dan Jørgensen.

Picha ya pamoja

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Mipango na Uwekezaji) Mhe. Prof. Kitila Mkumbo (Mb.) akizungumza na  Waziri wa Maendeleo na Mabadiliko ya Tabianchi wa Denmark, Mhe. Dan Jørgensen (hayupo pichani) alipomtembelea ofisini kwake jijini Dodoma tarehe 5 Aprili, 2024. Kushoto ni Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Dkt. Tausi Kida.

Waziri wa Maendeleo na Mabadiliko ya Tabianchi wa Denmark, Mhe. Dan Jørgensen akizungumza na Mhe. Prof. Mkumbo jijini Dodoma tarehe 5 Aprili, 2024. 

Picha ya pamoja.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais ( Muungano na Mazingira ), Mhe. Dkt. Selemani Jafo (wa pili kushoto) akizungumza na Waziri wa Maendeleo na Mabadiliko ya Tabianchi wa Denmark, Mhe. Dan Jørgensen (hayupo pichani) alipomtembelea ofisini kwake jijini Dodoma tarehe 5 Aprili, 2024. Wa pili kulia ni Balozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Denmark mwenye makazi yake nchini Sweden, Mhe. Grace Olotu.

Waziri wa Maendeleo na Mabadiliko ya Tabianchi wa Denmark, Mhe. Dan Jørgensen (wa tatu kulia) akizungumza na Mhe. Dkt. Jafo (hayupo pichani) alipomtembelea ofisini kwake jijini Dodoma tarehe 5 Aprili, 2024.

Picha ya pamoja.

No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.