Wednesday, May 8, 2024

TANZANIA YAZINDUA KAMPENI YA MGOMBEA WA NAFASI YA MKURUGENZI WA SHIRIKA LA AFYA DUNIANI KANDA YA AFRIKA


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. January Makamba (Mb.) akizundua kampeni ya mgombea wa Tanzania katika nafasi ya Mkurugenzi wa Afrika katika Shirika la Afya Duniani (WHO) uliofanyika jijini Dar es Salaam.

Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imemtangaza Mgombea wa Nafasi ya Mkurugenzi wa Afrika katika Shirika la Afya Duniani (WHO) Mhe. Dkt. Faustine Ndugulile ambaye kwa sasa ni Mbunge wa Bunge la Tanzania wa Jimbo la Kigamboni jijini Dar es Salaam.

Akitambulisha sifa na uwezo binafsi wa mgombea huyo, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. January Makamba (Mb.) amesema kuwa Mhe. Ngugulile ni mgombea sahihi mwenye uwezo wa kazi na kufanya mageuzi na maboresho katika ya Sekta ya Afya.

Aidha, ameeleza kuwa Mhe. Ndugulile alipokuwa Naibu Waziri katika Wizara ya Afya aliweka kipaumbele cha kusimamia suala la kutunga, kusimamia sera na kuratibu mipango mbalimbali ya kitaifa na kimataifa ili kuhakikisha usimamizi wa sekta ya afya nchini unaimarika kwa ajili ya kujenga nguvu kazi imara ya Taifa.

“Kupatikana kwa nafasi hii kutaiwezesha Tanzania kuimarika zaidi katika utekelezaji wa Diplomasia ya Afya ambayo ni muhimu katika Diplomasia yetu kwa ujumla hususan katika usimamizi wa mipango, maarifa na rasilimali ulimwenguni.’’ Waziri Makamba.

Mbali na hayo Waziri Makamba ameeleza kuwa kufauatia jitihada mbalimbali za kidiplomasia zilizofanywa na Serikali kupitia Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikano wa Afrika Mashariki tayari mgombea wa Tanzania ameungwa mkono na Nchi 16 Wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) na nchi zingine 7 kutoka Afrika, hivyo kuipa Tanzania mtaji wa jumla ya kula 23 katika kinyang’anyiro cha kuwania nafaisi hiyo. 

Naye Waziri wa Afya, Mhe. Ummy Mwalimu akimwelezea mgombea huyo Mhe. Dkt. Ndugulile ameeleza kuwa akiwa Naibu Waziri katika Wizara ya Afya alifanya jitihada katika kuimarisha afya ya msingi kwa kuwezesha upatikanaji wa rasilimali fedha kutoka Serikalini na wadau wa maendeleo.

Ameongeza kuwa Mhe. Ndugulile alitoa mchango mkubwa kwenye usimamizi wa maboresho ya afya ya mama na mtoto na lishe na chanjo ambapo usimamizi huo umewezesha kupunguza kwa kiasi kikubwa vifo vya wajawazito na watoto.

“Akiwa Naibu Waziri, Mhe. Dkt. Ngugulile alikuwa msaidizi ambaye alitumia taaluma yake katika kushauri masuala ya afya kitaalam na hivyo kuwezesha utekelezaji wenye tija wa masuala mbalimbali katika Wizara yetu.’’ Waziri Ummy

Kwa upande wake Mhe. Ndugulile ameeleza vipaumbele vyake ambayo endapo atafanikiwa kushika nafasi hiyo atavisimamia, ambavyo ni pamoja na; afya ya mama na mtoto, kukabilina na magonjwa yasiyokuambukiza, afya ya msingi, ustahimilivu wa mazingira na mfumo endelevu wa afya, bima ya afya, uvumbuzi na utafiti na ubia na ushirikiano katika masuala ya afya.

Vilevile Dkt. Ndugulile amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan kwa kumthibitisha kuwa mgombea katika nafasi hiyo hadhimu pamoja Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki na Wizara ya Afya kwa kiliratibu suala hilo kwa mafaniko makubwa.

Uzinduzi wa nafasi hiyo ya mgombea umefanywa kwa ushirikiano kati ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki na Wizara ya Afya, ambapo umehudhuriwa na mabalozi Afrika wanaoziwakilisha Nchi zao hapa Nchini na Wakuu wa Mashirika ya Kimataifa yaliyopo nchini. 

Wagombea wote Watano wanaowania nafasi hiyo watapigiwa kura na Mawaziri wa Afya wa nchi za Afrika katika Mkutano unaotarajiwa kufanyika nchini Congo Brazaville mwezi Agosti 2024 ambao utahusisha jumla ya nchi 47 za Afrika.

Mhe. Dkt. Faustine Ndugulile mgombea wa Tanzania katika nafasi ya Mkurugenzi wa Afrika katika Shirika la Afya Duniani (WHO) akizungumza kwenye hafla ya uzinduzi wa kampeni ya kuwania nafasi hiyo iliyofanyika jijini Dar es Salaam
Sehemu ya mabalozi wa Afrika wanaoziwakilisha Nchi zao hapa Nchini na Wakuu wa Mashirika ya Kimataifa yaliyopo nchini wakifuatilia hafla ya uzinduzi wa kampeni ya mgombea wa Tanzania katika nafasi ya Mkurugenzi wa Afrika katika Shirika la Afya Duniani (WHO) iliofanyika jijini Dar es Salaam.
Waziri wa Afya Mhe. Ummy Mwalimu akizungumza kwenye hafla ya ufunguzi wa kampeni ya mgombea wa Tanzania katika nafasi ya Mkurugenzi wa Afrika katika Shirika la Afya Duniani (WHO) uliofanyika jijini Dar es Salaam.
Picha ya pamoja 
Sehemu ya Watendaji wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki wakifuatilia hafla ya uzinduzi wa kampeni ya mgombea wa Tanzania katika nafasi ya Mkurugenzi wa Afrika katika Shirika la Afya Duniani (WHO) iliofanyika jijini Dar es Salaam.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. January Makamba (Mb.) akizundua kampeni ya mgombea wa Tanzania katika nafasi ya Mkurugenzi wa Afrika katika Shirika la Afya Duniani (WHO) uliofanyika jijini Dar es Salaam.
Katibu Mkuu Wizari wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Dkt. Samwel Shelukindo wakifuatilia hafla ya uzinduzi wa kampeni ya mgombea wa Tanzania katika nafasi ya Mkurugenzi wa Afrika katika Shirika la Afya Duniani (WHO) iliofanyika jijini Dar es Salaam.
Sehemu ya Mabalozi wa Afrika wanaoziwakilisha Nchi zao hapa Nchini na Wakuu wa Mashirika ya Kimataifa yaliyopo nchini wakifuatilia hafla ya uzinduzi wa kampeni ya mgombea wa Tanzania katika nafasi ya Mkurugenzi wa Afrika katika Shirika la Afya Duniani (WHO) iliofanyika jijini Dar es Salaam.
Sehemu ya Watendaji  na Maafisa wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki wakifuatilia hafla ya uzinduzi wa kampeni ya mgombea wa Tanzania katika nafasi ya Mkurugenzi wa Afrika katika Shirika la Afya Duniani (WHO) iliofanyika jijini Dar es Salaam.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. January Makamba (Mb.) akizundua kampeni ya mgombea wa Tanzania katika nafasi ya Mkurugenzi wa Afrika katika Shirika la Afya Duniani (WHO) uliofanyika jijini Dar es Salaam.

No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.