Wednesday, May 15, 2024

TANZANIA NA UFARANSA KUIMARISHA DIPLOMASIA YA UCHUMI

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. January Makamba amekutana kwa mazungumzo na Waziri wa Biashara, Uchumi, Nchi zinazozungumza Kifaransa na Wafaransa waishio nje ya nchi, Mhe. Frank Reister katika ofisi za Wizara jijini Paris, Ufaransa tarehe 15 Mei, 2024.

Mawaziri hao wamejadili kuhusu namna bora ya kuimarisha ushirikiano kwenye masuala ya biashara na uwekezaji ambapo, Mhe. Makamba ametumia fursa hiyo kuukaribisha Ujumbe wa Wafanyabiashara utakaongozwa na Jumuiya ya Wafanyabiashara wa Ufaransa (MEDEF) unaotarajia kushiriki kwenye Jukwaa la Biashara linalotarajia kufanyika kuanzia tarehe 27 hadi 29 Mei, 2024 jijini Dar es Salaam na Zanzibar. 

Aidha, kuelekea mashindano ya Kombe la Mataifa Afrika (CAN 2027), Mhe. Makamba amekaribisha makampuni ya Ufaransa kuja kuwekeza jijini Arusha kwenye nyanja mbalimbali ikiwemo nyumba za malazi na kumbi za mikutano. 

Tanzania inatarajia kuwa Mwenyeji mwenza wa Mashindano ya CAN 2027. Ufaransa kwa upande wao wameonesha nia ya kuwekeza ili kuwezesha Tanzania kuhudumia wageni watakaokuja wakati wa mashindano hayo.

Mhe. Riester pia amewakaribisha wafanyabiasha na wawekezaji wa Tanzania kuwekeza nchini Ufaransa kwa kuwa nchi hiyo imeweka mazingira mazuri ya uwekezaji.

Mhe. Waziri Makamba ameishukuru Serikali ya Ufaransa kwa kuendelea kuwa mshirika mzuri wa maendeleo nchini Tanzania kwa kufadhiri miradi mbalimbali ya maendeleo ikiwemo nishati, miundombinu ya usafirishaji, maji safi, kilimo na afya.


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. January Makamba akizungumza na Waziri wa Biashara za Nje, Uwekezaji, Nchi zinazozungumza Kifaransa na Wafaransa Waishio Nje ya Nchi, Mhe. Franck Riester katika ofisi za Wizara hiyo jijini Paris, Ufaransa tarehe 15 Mei, 2024. Kulia ni Mkurugenzi wa Idara ya Ushirikiano wa Kimataifa, Balozi Noel Kaganda. 

Kulia ni wa Waziri wa Biashara za Nje, Uwekezaji, Nchi zinazozungumza Kifaransa na Wafaransa Waishio Nje ya Nchi, Mhe. Franck Riester akizungumzia utekelezaji wa masuala mbalimbali ya biashara na uwekezaji ambayo kampuni za kifaransa zimewekeza nchini Tanzania.

Kutoka kulia, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. January Makamba, Balozi wa Tanzania nchini Ufaransa, Mhe. Ali Mwadini na Afisa Mambo ya Nje, Bw, Athuman Kikwete wakifatilia mazungumzo.

Mheshimiwa Waziri Makamba akisalimiana na Mheshimiwa Waziri Riester baada ya kuwasili ofisini kwake kwa mazungumzo.

Mheshimiwa Waziri Makamba akiteta jambo na Mheshimiwa Waziri Riester baada ya kuwasili ofisini za Wizara jijini Paris, Ufaransa.

Mheshimiwa Waziri Makamba akikaribishwa na Mheshimiwa Waziri Riester baada ya kuwasili ofisini za Wizara hiyo jijini Paris, Ufaransa

Mheshimiwa Waziri Makamba akisalimiana na maafisa walioambatana na  Mheshimiwa Waziri Riester katika mazungumzo.

Mazungumzo yakiendelea.

Picha ya pamoja.



No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.