Friday, January 22, 2021

DKT. MWINYI: MAZINGIRA YA KISIASA ZANZIBAR YANATOA FURSA YA KUWALETEA WANANCHI MAENDELEO

 Na Mwandishi wetu, Zanzibar   

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi amesema Zanzibar iko salama na mazingira ya kisiasa yanatoa fursa ya kuwaletea wananchi wa Zanzibar maendeleo kutokana na uwepo wa Serikali ya umoja wa kitaifa.

Rais Mwinyi ameyasema hayo Ikulu ya Zanzibar wakati alipokutana na ufanya mazungumzo na uongozi wa juu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki ukiongozwa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamagamba John Kabudi na kuongeza kuwa uongozi wake unajipanga kutimiza ahadi alizotoa kwa wananchi.

Pia Rais Mwinyi ameongeza kuwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imetoa kipaumbele katika kuimarisha Uchumi wa Bahari kuu hasa Uchumi wa bluu kama chanzo mbadala cha mapato kitakachosaidia kukuza uchumi na kupunguza mzigo wa kodi kwa wananchi.

“Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar zimetoa kipaumbele katika kuimarisha Uchumi wa Bahari kuu hasa Uchumi wa bluu kama chanzo mbadala cha mapato kitakachosaidia kukuza uchumi,” Amesema Dkt. Mwinyi  

Katika tukio jingine, Uongozi wa Wizara ya Mambo ya Nje umekutana na kufanya mazungumzo na Makamu wa kwanza wa Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Mhe. Maalim Seif Sharif Hamad ambaye amesisitiza kuwa uchumi wa bluu ni muhimu sana kwa maendeleo ya Zanzibar hivyo ni muhimu kwa Serikali zote mbili (Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania) kulinda mipaka yake ya bahari ambapo pia ulinzi huo utasaidia kuzuia na kupambana na uingizwaji wa dawa za kulevya hapa nchini.

“Naamini kabisa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tukishirikiana katika kuimarisha ulinzi wa baharini itasaidia kupunguza uingizwaji wa dawa a kulevya hapa nchini,” Amesema Maalim Seif

Kwa upande wake Prof. Palamagamba John Kabudi ameupongeza uongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kwa hatua ulizozichukua katika kuhakikisha uwepo wa amani na utulivu visiwani humo na kwamba uwepo wa amani na utulivu utachangia kuleta maendeleo haraka kwa wananchi wa Zanzibar.

“Zanzibar imetulia na uchumi wake umezidi kuimarika sote ni mashahidi wa ongezeko la watalii hapa Zanzibar hii ni ishara ya kuwa na amani na utulivu, na jambo hili linachangia kukua kwa uchumi wa Zanzibar,” Amesema Prof. Kabudi

Mbali na kukutana na Rais wa Zanzibar na Makamu wa Kwanza wa Rais, pia Uongozi huo umekutana na kufanya mazungumzo na Makamu wa Pili wa Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla ambapo wamejadili masuala mbalimbali ya maendeleo yanayohusu Tanzania Bara na Zanzibar hususan yanayohusu Muungano.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamagamba John Kabudi katika ziara yake ameambatana na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. William Olenasha pamoja na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Balozi Brigedia Jenerali Wilbert Ibuge.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi akiongea na uongozi wa juu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, ukiongozwa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamagamba John Kabudi (Mb) Ikulu Zanzibar wakati wa ziara ya kikazi ya Prof. Kabudi Zanzibar. Prof. Kabudi ameambatana na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. William Olenasha pamoja na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Balozi Brigedia Jenerali Wilbert Ibuge.  


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi akiongea na viongozi wa juu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, (hawapo pichani) katika Ikulu ya Zanzibar  


Kikao cha Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi na uongozi wa juu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, kikiendelea katika Ikulu ya Zanzibar  


Makamu wa kwanza wa Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Mhe. Maalim Seif Sharif Hamad akimsikiliza Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamagamba John Kabudi wakati alipokuwa akimuelezea jambo wakati uongozi wa Wizara ulipomtembelea Mhe. Seif kwa zaiara ya kikazi mjini Zanzibar


Kikao cha Makamu wa kwanza wa Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Mhe. Maalim Seif Sharif Hamad na uongozi wa juu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kikiendelea katika Ikulu ya Zanzibar  



No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.