Monday, December 21, 2015

WAZIRI WA MAMBO YA NJE AKAGUA UJENZI WA MAHAKAMA YA UMOJA WA MATAIFA JIJINI ARUSHA

Mhe. Dkt. Augustine Mahiga, Waziri wa Mambo ya Nje, Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Kikanda na Kimataifa akipata maelekezo ya ziada kuhusu ujenzi wa Mahakama ya Umoja wa Mataifa kwenye eneo la Lakilaki Jijini Arusha. Aneyetoa maelezo ni Afisa Mambo ya Nje na Mwansheria Bw. Elisha Suku. Kushoto kwa Waziri Mahiga ni Nd. Hamdouny Mansour, Katibu Tawala Msaidizi upande wa miundombinu. 



Mhe. Dkt. Augustine Mahiga, Waziri wa Mambo ya Nje, Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Kikanda na Kimataifa na ujumbe wake wakiangalia eneo la eka 16 ambapo majengo manne ya Mahakama ya Umoja wa Mataifa yanajengwa. Ujenzi huo unatarajiwa kukamilika Mwezi Aprili mwaka 2016.
 Mhe. Dkt. Augustine Mahiga, Waziri wa Mambo ya Nje, Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Kikanda na Kimataifa akiwa na Mkuu wa Wilaya ya Arumeru mkoani Arusha Mhe. Wilson Nkhambaku baada ya kukagua eneo hilo na kuridhika na kasi ya ujenzi uliozingatia viwango vya kimataifa na vile vya Umoja we Mataifa. 

Mhe. Dkt. Augustine Mahiga, Waziri wa Mambo ya Nje, Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Kikanda na Kimataifa akiwa na ujumbe wake baada ya kumaliza ukaguzi wa ujenzi wa Mahakama ya Umoja wa Mataifa jijini Arusha. 




TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI  
Serikali imeridhishwa na maendeleo na kasi ya ujenzi wa Mahakama ya Kimataifa ya Umoja wa Mataifa ya Masalia ya kesi za Mauaji ya Kimbari ya Rwanda (Mechanism for International Criminal Tribunals (MICT) katika eneo la Lakilaki jijini Arusha, uliozinduliwa rasmi Julai mosi mwaka huu.

Akikagua ujenzi huo na kupokea taarifa kutoka kwa wakandarasi na wasimamizi wa ujenzi wa majengo hayo, Waziri wa Mambo ya Nje, Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Kikanda na Kimataifa Mheshimiwa Dkt. Augustine Mahiga, amesisitiza kuwa ujenzi huo uzingatie viwango vya kimataifa ili kuhakikisha usalama wa nyaraka na ushahidi utakaohifadhiwa kwenye majengo hayo.

Alieleza kuwa ahadi ya Serikali iko palepale kushirikiana na Umoja wa Mataifa na kuhakikisha kuwa miundombinu muhimu kama vile barabara, umeme na maji vinapatikana kwenye eneo hilo ambapo ujenzi unaendelea kwa kasi ya kuridhisha.

“Nimefurahishwa na maendeleo ya ujenzi huu kwani hii ilikua kazi yangu ya mwisho nilipokuwa mwakilishi wa kudumu wa Tanzania kule Umoja wa Mataifa, kutetea mahakama hii ijengwe hapa Arusha.

Akifafanua miundombinu iliyowekwa na Serikali ya Mkoa wa Arusha, Katibu Tawala Msaidizi upande wa miundombinu Nd. Hamdouny Mansour alisema kuwa kwa upande wa upatikanaji wa maji, mkoa umefanikisha upatikanaji wa bomba maalum linaloleta maji kwenye eneo la ujenzi mojakwamoja bila kuathiri upatikanaji wa maji maeneo mengine pembezoni ili kutimiza azma hiyo ya Serikali.

Ujenzi huo wa Mahakama unaosimamiwa na Umoja wa Mataifa unatarajiwa kuwa na majengo makuu manne; jengo la mahakama, jengo la uhifadhi wa nyaraka, jengo la ulinzi na jengo la ofisi za Umoja wa Mataifa. Msimamizi wa ujenzi wa Umoja wa Mataifa alielezea teknolojia ya kisasa itakayotumika kujenga jengo la kuhifanyia nyaraka haitahitaji kutumia viyoyozi ili kuhifadhi uhasilia wa nyaraka.

Kwa upande wa wakandarasi wanaojenga ambao ni kampuni kutoka India walielezea changamoto iliyopo kwenye ujenzi huo ni kutekeleza mpango wa kupanda mti aina ya mshita-acacia, utakaomaanisha haki ambayo kihistoria na jadi za kiafrika ilipatikana kwa mazungumzo kwenye mabaraza ya kijiji. Mti huo wa mshita au Tree of Justice utapandwa ndani katikati ya majengo hayo manne.

Serikali kupitia Hazina ilinunua eneo hilo la Lakilaki lenye ekari 431 na kukabidhiwa Wizara ya Mambo ya Nje ambapo limetengwa mahsusi kwa ajili ya ujenzi wa taasisi mbalimbali za kimataifa. Taasisi nyingine zinazotarajiwa kujengwa kwenye eneo hilo ni African Union Advisory Board on Corruption (AUABC), African Institute of International Law (AIIL) na African Court on Human and Peoples' Rights (ACHPR).

Ujenzi wa majengo haya ya awali kwenye eneo la Lakilaki unatarajiwa kukamilika mwezi Aprili mwakani. Ujenzi huo ulizinduliwa rasmi Julai mwaka huu wa 2015 na Rais wa Awamu ya Nne Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete.

MWISHO.
Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali kwa Umma,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa,

20 Desemba, 2015

Friday, December 18, 2015

Dkt. Mahiga afanya mahojiano maalum na BBC kuhusu Burundi

Waziri wa Mambo ya Nje, Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Kikanda na Kimataifa, Mhe. Dkt. Augustine Mahiga akijibu maswali kuhusu hali ya kisiasa nchini Burundi wakati wa mahojiano maalum na Mwandishi wa Habari kutoka Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC), Bw. Leonard Mubali. Kulia ni Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali, Bi. Mindi Kasiga akinukuu mahojiano hayo. Mahojiano hayo yatarushwa  tarehe 18 Desemba, 2015 saa 3:00 usiku kupitia kipindi cha Dira ya Dunia kinachorushwa na  Kituo cha Star TV
Mahojiano yakiendelea.
Mhe.Dkt. Mahiga akiagana na Bw. Mubali  baada ya kumaliza  mahojiano hayo.


TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI


ZIARA YA WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI, KIKANDA NA KIMATAIFA, MHE. DKT. AUGUSTINE MAHIGA
 MKOANI ARUSHA
 
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Kikanda na Kimataifa, Mhe. Dkt. Augustine Mahiga atafanya ziara ya kikazi ya siku mbili mkoani Arusha kuanzia kesho Jumamosi tarehe 19 Desemba 2015.

Atakapokuwa mkoani Arusha, Balozi Mahiga atafanya mazungumzo na Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), Dkt. Richard Sezibera. Mazungumzo yao yatahusu namna ya kutatua mgogoro wa kisiasa nchini Burundi.

Aidha, Mhe. Waziri atatembelea eneo la Lakilaki ambalo limetengwa na Serikali kwa ajili ya ujenzi wa ofisi za taasisi za kimataifa. Ujenzi unaoendelea hivi sasa kwenye eneo hilo ni jengo la ofisi la taasisi ya Mechanism for Crime Tribunals (MICT) inayorithi shughuli za Mahakama ya Kimataifa ya Mauaji ya Kimbari ya Rwanda (ICTR) ambayo itakamilisha shughuli zake tarehe 31 Desemba 2015.

Mhe. Waziri pia atatembelea Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Arusha (AICC) kuonana na uongozi wa Kituo hicho  kwa madhumuni ya kufahamiana. AICC ni moja ya taasisi zilizo chini ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Kikanda na Kimataifa.

Mhe. Waziri atarejea jijini Dar es Salaam siku ya Jumapili tarehe 20 Desemba 2015.

Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa,
Dar es Salaam
18 Desemba, 2015

Balozi Mulamula akutana kwa mazungumzo na Balozi wa India nchini

Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Kikanda na Kimataifa, Balozi Liberata Mulamula (kulia), akizungumza na Balozi wa India hapa nchini, Mhe. Sandeep Arya katika mazungumza yao yalijikita katika kukuza ushirikiano kati ya Tanzania na India katika sekta mbalimbali za kiuchumi, biashara, afya na elimu. Mazungumzo hayo yalifanyika tarehe 18 Desemba, 2015.
Balozi Arya naye akizungumza na Balozi Mulamula
Mazungumzo yakiendelea

Picha na Reginald Philip

Thursday, December 17, 2015

WANAWAKE NA WATOTO WA KIKE BADO WAPO NYUMA KATIKA MATUMIZI YA TEHAMA

Balozi Tuvako Manongi, Mwakilishi wa Kudumu wa   Tanzania katika Umoja wa Mataifa  akizungumza wakati wa Mkutano wa Ngazi ya Juu wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa kuhusu Teknolojia ya  Habari na Mawasiliano kwa Maendeleo. Mkutano huo wa siku mbili umefanyika hapa Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa jijini New York, Marekani
Na  Mwandishi Maalum,  New York

Wanawake na watoto wa kike wanaelezwa kama kundi ambalo bado  halijanufaika ipasavyo na  matumizi ya   Teknolojia ya Habari na Mawasiliano ( TEHAMA)

Na kwa sababu  hiyo, wito umetolewa  kwa nchi Wanahama wa Umoja wa Mataifa, Asasi za Kiraia naTaasisi za Kimataifa   kuhakikisha kwamba panakuwep  na mikakati na mipango ya  ziada yenye lengo la  kupunguza pengo la matumizi ya TEHAMA kati ya wanawake na wanaume.

Hayo yamejiri wakati wa  Mkutano wa siku mbili  wa Ngazi ya Juu wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa   uliokuwa ukitathmini utekelezaji   wa Teknolojia na  Habari na Mawasiliano kwa Maendeleo, ikiwa ni miaka kumi tangu mchakato wa kuhakisha kuwa  jamii inapata fursa ya  kupata na kutumia TEHAMA ambayo itakuwa   ni jumuishi na yenye gharama nafuu.

Wajumbe wa  mkutano huu walikuwa ni   Mawaziri  wanaohusika na masuala ya teknolojia ya habari na mawasiliano. Katibu Mkuu wa  Umoja wa Mataifa  Ban Ki Moon, na Rais wa Baraza kuu la Umoja wa Mataifa, Bw. Monges Lykketofts ni baadhi ya viongozi wakuu waliozungumza wakati wa ufunguzi wa mkutano huu.

Ujumbe wa Tanzania  umeongozwa na Balozi Tuvako Manongi, Mwakilishi wa  Kudumu wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa.

Katika hotuba yake mbele ya  wajumbe wa Mkutano, Balozi Manongi,  amesema Serikali inalichukulia kwa  umuhimu wa kipekee  suala   upatikanaji, uboreshaji, usambazaji na  matumizi ya TEHAMA kwa  wananchi wake.

Akasema katika kuhakikisha kuwa TEHAMA  inakwenda na wakati na inawafikia wananchi wengi na kwa gharama nafuu, serikali imekuwa ikishirikiana na kufanya kazi kwa karibu na wadau mbalimbali wa ndani na nje.  

Akasema kama  ilivyo kwa   nchi nyingine zinazoendelea, Tanzania ingependa kuona panakuwapo na ushirikiano zaidi na wenye tija baina ya mataifa yaliyoendelea  na yanayoedelea hususani katika eneo la    uwezeshawaji wa kiteknolojia,raslimali fedha na mafunzo.

Balozi Manongi, na kama  iliyokuwa  kwa wazungumzaji wengine, amesema   ingawa matumizi ya TEHAMA yamekuwa na manufaa makubwa kwa mwanadamu katika Nyanja mbalimbali, lakini pia pamekuwapo na changamoto kadhaa zitokanazo na matumizi mabaya.

Baadhi ya  changamoto hizo ni matumizi  yasiyo sahihi ya mitandao, ukiwamo uhalifu wa  mitandao , ugaidi, uingiliaji wa masuala binafsi ya mtu, ukiukwaji wa maadili,  usambazaji wa matamshi ya chuki na  misimamo mikali.

Akabainisha pia kuwa pamezuka tabia sugu  ( addiction) ya
matumizi ya TEHAMA kiasi  cha kudhoofisha mahusiano miongoni mwa familia na jamii kwa ujumla.


Kama hiyo haitoshi matumizi sugu ya TEHAMA  yamezalisha tatizo jingine la watu kujikuta wakipata magonjwa yasiyoambukiza kutokana na kwamba
wamekuwa wakitumia muda mwingi kwenye TEHAMA pasipo kuishughulisha   miili yao.


Mwakilishi  huyo wa Tanzania akasema panahitajika juhudi za   pamoja katika kuzikabili  changamoto hizo na nyingine  nyingi.

Wazungumzaji wengi katika  mkutano huo  pamoja na  kubainisha  kuachwa nyuma kwa wanawake na watoto wakike  katiika matumizi ya TEHAMA, walieleza pia kwamba kundi jingine ambalo nalo halijanufaika   na  TEHAMA ni watu wenye ulemavu.

Pia ilielezwa wakati wa mkutano huo kuwa  ingawa asilimia 40 ya  idadi ya watu wote duniani wamepata fursa ya kutumia TEHAMA, bado kuna pengo kubwa baina ya watumiaji kati ya mataifa yanayoendelea na yale yaliyoendelea.

Halikadhalika imebainishwa kwamba kuna pengo  pia miongoni wa watumiaji hao kati ya wale wa mijini na vijijini lakini pia uwezo wa kipato nalo ni tatizo linalosababisha siyo kila mtu anakuwa na uweze wa kumudu gharama za matumizi ya TEHAMA.



Baadhi ya wazungumzaji
wengine walikwenda mbali Zaidi kwa kueleza kwamba TEHAMA ni  muhimu sana kwa utekelezaji wa  ajenda mpya ya maendeleo endelevu lakini pia
ni muundombinu  muhimu ambao hauna
tofauti na miundombinu mingine kama vile barabara. 

Wednesday, December 16, 2015

Waziri Mahiga afanya mazungumzo na Katibu Mtendaji wa SADC na Balozi wa Marekani nchini

Waziri wa Mambo ya Nje, Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Kikanda na Kimataifa, Mhe. Dkt. Augustine Mahiga akimkaribisha Katibu Mtendaji wa Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC), Mhe. Dkt. Stergomena Tax alipofika Wizarani kwa ajili ya kumpongeza kwa kuteuliwa katika wadhifa huo na pia kumpatia taarifa fupi kuhusu muundo, majukumu na utendandaji wa Jumuiya ya SADC.Mazungumzo hayo yalifanyika Wizarani Jijini Dar es Salaam tarehe 16 Desemba, 2015.
Mhe. Dkt. Mahiga akimweleza jambo Dkt. Tax wakati wa mazungumzo yao.
Wajumbe waliofutana na Mhe. Dkt. Tax wakinukuu mazungumzo ya viongozi hao ambao hawaonekani pichani.
Mhe. Dkt. Tax akifafanua jambo kwa Mhe. Dkt. Mahiga.
Mkurugenzi wa Idara ya Ushirikiano wa Kikanda, Balozi Innocent Shiyo akiwa na Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali, Bi. Mindi Kasiga pamoja na Bw. Thobias Makoba, Msaidizi wa Waziri.
Mazungumzo yakiendelea

..........Mkutano na Balozi wa Marekani

Waziri wa Mambo ya Nje, Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Kikanda na Kimataifa, Mhe. Dkt. Augustine Mahiga akimkaribisha  Balozi wa Marekani hapa nchini, Mhe. Mark Childress alipofika Wizarani kwa lengo la kumpongeza  kwa kuteuliwa na Mhe. Rais kwenye wadhifa huo na pia kuzungumzia masuala ya ushirikiano kati ya Tanzania na Marekani.
Mhe. Dkt. Mahiga akizungumza na Balozi Childress ambapo alimhakikishia ushirikiano Balozi huyo.
Balozi Childress nae akizungumza.
Mkurugenzi wa Idara ya Ulaya na Amerika, Balozi Joseph Sokoine akiwa na Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali pamoja na Msaidizi wa Waziri, Bw. Thobias Makoba nao wakifuatilia mazungumzo kati ya Mhe. Dkt. Mahiga na Balozi Childress (hawapo pichani).
Maafisa kutoka Wizara ya Mambo ya Nje wakifuatilia mazungumzo
Mazungumzo yakiendelea
Picha na Reginald Philip

Wafanyabiashara wa Qatar wahimizwa kuwekeza Tanzania


Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Kikanda na Kimataifa, Balozi Liberata Mulamula amesema kuwa Serikali imeweka mazingira rafiki ya uwekezaji, hivyo alitoa wito kwa wafanyabiashara kutoka Qatar kutumia fursa lukuki za uwekezaji zinazopatikana hapa nchini. 


Balozi Mulamula aliyasema hayo kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Kikanda na Kimataifa katika hafla ya kuadhimisha Siku ya Taifa ya Qatar iliyofanyika kwenye Hoteli ya Hyatt Regence, Kilimanjaro jijini Dar es Salaam jana.


“Tanzania imeweka mazingira wezeshi ya uwekezaji katika sekta mbalimbali kama vile kilimo, madini, uchukuzi, elimu, afya, nishati, wanyamapori, mafuta na gesi, hivyo natoa wito kwa ndugu zetu wa Qatar watumie fursa ya uhusiano mzuri tulionao kuja kuwekeza nchini”, Balozi Mulamula alisema.  


Balozi Mulamula aliendelea kusema kuwa Serikali inaelekea katika uchumi wa gesi na ina matumani makubwa ya kufaidika na uzoefu wa mshirika wake Qatar ambayo ni mmoja wa wazalishaji wakubwa wa gesi duniani. 


Suala lingine ambalo Katibu Mkuu aliligusia ni umuhimu wa Tanzania na Qatar kuunganisha nguvu ili kutumia rasilimali fedha na ardhi zilizopo kuimarisha sekta ya kilimo kwa madhumuni ya kuodoa changamoto za usalama wa chakula kati ya nchi hizi mbili.


Kwa upande wake, Balozi wa Qatar nchini, Mhe. Abdulla Jassim Al Maadadi pamoja na mambo mengine, aliongelea suala la Qatar kuwa mwenyeji wa mashindano ya mpira wa miguu wa Kombe la Dunia kwa mwaka 2022. Alisema miradi mingi kwa ajili ya maandalizi ya mashindano hayo inatarajiwa kukamilika mwaka 2020.  Miradi hiyo ni pamoja na ujenzi wa barabara, mtandao wa reli, viwanja vya mpira, viwanja vya ndege na nyumba za makazi.


Alisema miradi hiyo ni mikubwa hivyo inahitaji wafanyakazi wengi kutoka sehemu mbalimbali duniani na aliahidi kuwa watu watakaokwenda kufanya kazi nchini humo, haki zao zitalindwa.



Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushikiano wa Afrika Mashariki, Kikanda na Kimataifa Balozi Liberata Mulamula akizungumza kwenye hafla ya kuadhimisha ya Siku ya Taifa la Qatar kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikano wa Afrika Mashariki, Kikanda na Kimataifa, Mhe. Balozi Augustine Mahiga. Katika maadhimisho hayo, Balozi Mulamula alisitiza umuhimu wa kuimarisha ushirikiano kati ya Tanzania na Qatar hususan katika sekta za kiuchumi na biashara.
Sehemu ya Mabalozi na wageni waalikwa wakimsikiliza Balozi Mulamula (hayupo pichani)
Balozi Mulamula akiendelea kuzungumza
Balozi wa Qatar nchini, Mhe. Abdallah Jassim Al-Maadadi naye akizungumza katika maadhimisho hayo.
Sehemu nyingine ya Mabalozi waliohdhuria hafla hiyo.
Sehemu ya watumishi wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Kikanda na Kimataifa, Bw. Hangi Mgaka (wa kwanza kulia), na Bw. Batholomeo Jungu (wa pili kutoka kulia) nao wakimsikiliza Balozi Al-Maadadi (hayupo), katika maadhimisho hayo.
Balozi Mulamula (wa pili kutoka kulia), Balozi wa Qatar nchini (wa tatu kutoka kulia), Balozi wa Demokrasia ya Kongo, Mhe. Juma Mpango (wa nne kutoka kushoto), Balozi wa Oman nchini, Mhe. Soud Ali Bin Mohamed Al Rugaishi (wa kwanza kushoto), Balozi wa Nchi za Falme za Kiarabu (UAE), Mhe. Abdulla Ibrahim Ghanim Al suwaidi (wa pili kutoka kushoto) wakishiriki tendo la kukata Keki ya maadhimisho ya Siku ya Taifa la Qatar.
Balozi Mulamula akizungumza na Balozi Al - Maadadi.
Balozi Mulamula akimtangaza mshindi wa bahati nasibu iliyochezeshwa hapo jana, mshindi huyo (hayupo pichani) alijishindia tiketi ya Ndege ya kuelekea Doha.
Balozi Mulamula akiwa katika picha ya pamoja na Balozi Al-Maadadi
Katibu Mkuu Balozi Mulamula akiwa katika picha ya pamoja na Mabalozi waliohudhuria maadhimisho hayo.


Picha na Reginald Philip