Wednesday, December 8, 2021

WAZIRI MULAMULA AKUTANA KWA MAZUNGUMZO NA VIONGOZI MBALIMBALI

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula leo tarehe 08 Disemba 2021 amekutana kwa nyakati tofauti na kufanya mazungumzo na Viongozi kutoka nchi mbalimbali ambao wapo nchini kwa ajili ya kushiriki maadhimisho ya miaka 60 ya Uhuru wa Tanzania Bara yatakayofanyika jijini Dar es Salaam tarehe 09 Desemba 2021.

Miongoni mwa Viongozi aliokutana nao ni pamoja na Rais Mstaafu wa Malawi, Mhe. Dkt. Joyce Banda, Waziri wa Mambo ya Nje wa Msumbiji, Mhe. Veronica Macamo, Waziri wa Mambo ya Nje wa Eswatini, Mhe. Seneta Thulisile Dladla na Waziri wa Mambo ya Nje wa Rwanda, Mhe. Dkt. Vicent Biruta.

Katika mazungumzo yao, Mhe. Balozi Mulamula amewakaribisha nchini  viongozi hao na kuwashukuru kwa kukubali mwaliko wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan wa kuja kushiriki maadhimisho hayo pamoja na wananchi wa Tanzania. Kadhalika, viongozi hao wamekubaliana kuimarisha ushirikiano kati ya nchi zao na Tanzania kwenye maeneo mbalimbali.

Rais Mstaafu wa Malawi, Mhe. Dkt. Joyce Banda akiwa katika mazungumzo na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula jijini Dar es Salaam


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula akizungumza na Waziri wa Mambo ya Nje wa Msumbiji, Mhe. Veronica Macamo katika Ofisi ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam  


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula akizungumza na Waziri wa Mambo ya Nje wa Eswatini, Mhe. Seneta Thulisile Dladla katika Ofisi ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula akizungumza na Waziri wa Mambo ya Nje wa Rwanda, Mhe. Dkt. Vicent Biruta katika Ofisi ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam. Kushoto ni Balozi wa Rwanda nchini Tanzania Mhe. Meja Jenerali Charles Karamba.    



TANZANIA YANADI BIDHAA ZA KILIMO NCHINI MAREKANI

Na Mwandishi Wetu,

Katika kusheherekea miaka 60 ya Uhuru wa Tanzania Bara na miaka 60 ya uhusiano kati ya Tanzania na Marekani, Serikali ya Tanzania kupitia Ubalozi wake nchini Marekani imefanya Kongamano kwa njia ya Mtandao kuhusu biashara ya bidhaa za Kilimo za Tanzania.

Mkutano huo umeandaliwa kwa kushirikiana na Taasisi za Kituo cha Kuendeleza Kilimo Kusini mwa Tanzania (SAGCOT), Baraza la Kilimo Tanzania (ACT), Sister Cities International na Thunderbird School of Global Management. Lengo la Kongamano hilo lilikua ni kuimarisha mauzo ya bidhaa za kilimo za Tanzania nchini Marekani.

Kongamano hilo lilishirikisha wajumbe kutoka Serikali za Tanzania na Marekani, Wafanyabishara na wadau wa kilimo wa nchi hizo mbili na Taasisi za Fedha, ambapo Waziri wa Kilimo Mhe. Prof. Adolf Mkenda (Mb), ameshiriki kwenye Kongamano hilo, kadhalika, Meya wa Jiji la   Helena-West, Arkansas, Mstahiki Kevin Smith naye pia ameshiriki.

Wakati wa Kongamano hilo, fursa mbalimbali za biashara ya mazao kati ya Tanzania na Marekani zilijadiliwa. Mazao hayo ni pamoja na maparachichi, ufuta, samaki, asali, kokoa, mchele, mvinyo, pareto, na mazao ya bahari.

Akizungumza kwenye Mkutano huo, pamoja na kueleza jitihada zinazochukuliwa na Serikali katika kuboresha sekta ya kilimo na kuongeza mauzo ya nje, Mhe. Waziri Prof. Mkenda ameeleza pia changamoto zilizopo kwenye sekta hiyo pamoja na fursa za uwekezaji pamoja na kuwasihi wawekezaji kutoka Marekani kuwekeza katika sekta ya kilimo.

Kwa upande wake, Meya Kevin Smith ameeleza kwamba Jiji lake la Helena-West linalima mchele kwa wingi na lipo tayari kushirikiana na Tanzania katika biashara ya zao hilo.

Akizungumza kwenye Kongamano hilo, Balozi wa Tanzania nchini Marekani Mhe. Dkt. Elsie Sia Kanza, ameeleza kuwa Kongamano hilo ni mwanzo wa makongamano mengine mengi ya namna hiyo, kwa sababu Ubalozi umejizatiti kuimarisha mauzo ya bidhaa mbalimbali za Tanzania nchini Marekani, hasa bidhaa za kilimo. Pamoja na mambo mengine, Balozi Kanza ameahidi Ubalozi utaendelea kushirikiana na mwekezaji au mfanyabiashara yeyote mwenye lengo la kuwekeza Tanzania.

Waziri wa Kilimo Mhe. Prof. Adolf Mkenda (Mb), akiwasilisha hotuba yake kwenye Kongamano hilo lililofanyika kwa njia ya mtandao 


Balozi wa Tanzani nchini Marekani Dkt. Elsie Kanza akiwa pamoja na wajumbe wa Ubalozi wakishiriki kwenye Kongamano hilo 


Sehemu ya Wajumbe walioshiriki katika Kongamano   


Balozi Kanza akizungumza wakati wa kongamano  


Meya Kevin Smith wa Jimbo la Helena-West Arkansas, nchini Marekani akizungumza wakati wa Kongamano



Tuesday, December 7, 2021

WAZIRI MULAMULA APOKEA HATI ZA UTAMBULISHO ZA MKURUGENZI MKAZI WA FAO

Na Mwandishi wetu, Dar

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula (Mb) amepokea Hati za Utambulisho za Mkurugenzi Mkazi wa Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO) Dkt. Nyabenyi Tipo katika Ofisi ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam.

Mara baada ya kupokea hati hizo Balozi Mulamula ametumia fursa hiyo kumweleza Mkurugenzi Mkazi huyo vipaumbele vya Serikali katika mpango mzima wa kuendeleza kilimo pamoja na mpango Mkakati wa Maendeleo wa Umoja wa Mataifa ‘Strategic Development Cooperation programme’.

Pia viongozi hao wameangalia maeneo ambayo yatapewa kipaumbele katika uwekezaji wa miundombinu, uzalishaji zaidi lakini pia kuangalia jinsi gani mazao yanayolimwa yanatunzwa vizuri.

“Tumejadili mbalimbali ikiwa ni pamoja na mpango wa FAo wa kusaidia nchi kuwa na bidhaa zinazozitambulisha nchi husika katika masoko ya kimataifa,” amesama Balozi Mulamula.

Pamoja na mambo mengine, Balozi Mulamula amemhakikishia Mkurugenzi Mkazi wa FAO kuwa Tanzania itaendelea kushirikiana kwa karibu na FAO katika kutekeleza miradi mbalimbali hasa mradi wa maendeleo wa miaka mitano.

Kwa Upande wake, Mkurugenzi Mkazi wa Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO) Dkt. Nyabenyi Tipo amesema atahakikisha FAO inatekeleza vipaumbele vya Serikali ya Tanzania pamoja na kuongeza ushirikiano wake kwa maslahi ya pande zote mbili.

“Mara baada ya kuwasilisha Hati za Utambulisho kwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, tumejadili jinsi ya kusaidia kupunguza athari za mabadiliko ya tabia nchi, kupunguza utapiamlo na kuona ni jinsi gani FAO inaweza kusaidia Tanzania katika kuboresha lishe kwa watanzania na changamoto mbalimbali zinazoikabili sekta ya kilimo kwa ujumla,” amesema Dkt. Tipo

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula (Mb) akipokea Hati za Utambulisho za Mkurugenzi Mkazi wa Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO) Dkt. Nyabenyi Tipo katika Ofisi ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula akiongea na Mkurugenzi Mkazi wa Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO) Dkt. Nyabenyi Tipo katika Ofisi ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam


Mkurugenzi Mkazi wa Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO) Dkt. Nyabenyi Tipo akimueleza jambo Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula mara baada ya kumkabidhi Hati za Utambulisho katika Ofisi ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam


Mwakilishi Msaidizi wa FAO Bwana Charles Tulahi akieleza jambo wakati wa kikao baina ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula na Mkurugenzi Mkazi wa Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO) Dkt. Nyabenyi Tipo katika Ofisi ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula na Mkurugenzi Mkazi wa Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO) Dkt. Nyabenyi Tipo wakiwa katika picha ya pamoja na badhi ya maafisa kutoka Wizarani pamoja na Ofisi za FAO 




WAZIRI MULAMULA AIPONGEZA FINLAND KWA KURIDHIA MKAKATI MPYA WA USHIRIKIANO NA TANZANIA

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Liberata Mulamula ameipongeza Serikali ya Finland kwa kuridhia Mkakati Mpya wa ushirikiano kati yake na Tanzania kuanzia mwaka 2021 hadi 2025 ikiwa ni pamoja na mchango wa nchi hiyo kwenye miradi mbalimbali ya maendeleo hapa nchini.

Pongezi hizo zimetolewa na Mhe. Waziri Mulamula alipozungumza wakati wa maadhimisho ya miaka 104 ya uhuru wa Taifa la Finland yaliyofanyika jijini Dar es Salaam tarehe 06 Desemba 2021 na kuhudhuriwa na wageni waalikwa mbalimbali wakiwemo Mabalozi na Wakauu wa Mashirika ya Kimataifa waliopo nchini.

Balozi Mulamula amesema kuwa, kuridhiwa kwa mkakati huo mpya wa ushirikiano kati ya Tanzania na Finland kunadhihiridha jinsi ambavyo nchi hiyo imedhamiria kuendelea kushrikiana na Tanzania ili kuiwezesha kukamilisha agenda na miradi mbalimbali ya maendeleo inayotekelezwa hapa nchini kwa ushirikiano na nchi hiyo.

“Tanzania inatoa shukrani kwa Serikali ya Finland kwa kuridhia Mkakati Mpya wa Ushirikiano na Tanzania kuanzia mwaka 2021 hadi 2025. Kuridhiwa kwa Mkakati huu kunadhihirisha namna ambavyo Serikali ya Finland ipo tayari kuendelea kushirikiana na Tanzania ili kuwezesha utekelezaji wa agenda za maendeleo zilizopo” amesema Waziri Mulamula.

Balozi Mulamula amesema kwamba, katika kipindi cha miaka 56 ya ushirikiano wa kidiplomasia kati ya Tanzania na Finland, nchi hiyo imechangia kwa kiasi kikubwa maendeleo ya nchi hii kwa kuchangia miradi ya maendeleo kwenye sekta mbalimbali zikiwemo elimu, utunzaji wa mazingira na misitu, nishati, TEHAMA na program za kuwawezesha wanawake kiuchumi. 

Ameongeza kusema kuwa, miongoni mwa masuala muhimu ya kupigiwa mfano kwenye ushirikiano huu ni pamoja na nchi hiyo kuwezesha kuanzishwa kwa Mpango wa Kuboresha ukusanyaji Kodi ambao kwa kiasi kikubwa umechangia kuongezeka kwa ukusanyaji mapato ya ndani hapa nchini. Pia, Finland kupitia Mchakato wa Helsinki kuhusu masuala ya utandawazi na demokrasia, uliwezesha kuanzishwa kwa Taasisi ya Uongozi (Uongozi Institute) ambayo hutoa mafunzo kwa viongozi waaandamizi serikalini na wadau mbalimbali katika kuwajengea uwezo wa utendaji kazi zao za kila siku.

Katika kuwawezesha wanawake kiuchumi, Balozi Mulamula amesema, Serikali ya Finland kupitia ubalozi wake hapa nchini umeanzisha program mbalimbali za kuwawezesha wanawake kujikwamua kiuchumi ikiwemo ile ya “Wanawake Wanaweza”.

Kwa upande wake, Balozi wa Finland hapa nchini, Mhe. Riitta Swan amesema nchi yake itaendelea kushirikiana na Serikali kwenye miradi mbalimbali ya maendeleo na kuipongeza Tanzania Bara inapoelekea kusherehekea miaka 60 ya uhuru.

Tanzania na Finland zilianzisha rasmi ushirikiano wa kidiplomasia mwaka 1965.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Liberata Mulamula akizungumza kama mgeni rasmi kwenye maadhimisho ya miaka 104 ya uhuru wa Taifa la Finland yaliyofanyika tarehe 06 Desemba 2021 jijini Dar es Salaam. Maadhimisho hayo ambayo yaliandaliwa  na Balozi wa Finland hapa nchini, Mhe. Riita Swan, yalihudhuriwa pia na Mabalozi na Wakuu wa Mashirika ya Kimataifa waliopo nchini.
Sehemu ya Mabalozi na wageni waalikwa wakimsikiliza Mhe. Balozi Mulamula (hayupo pichani) akizungumza wakati wa maadhimisho ya miaka 104 ya uhuru wa Taifa la Finland. Kulia ni Mkurugenzi wa Idara ya Ulaya na Amerika katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Swahiba Mndeme.

Balozi wa Finland nchini, Mhe. Riitta Swan akizungumza wakati wa maadhimisho ya miaka 104 ya uhuru wa Finland.

Sehemu ya Mabalozi na wageni waalikwa wakimsikiliza Mhe. Baloz Swan (hayupo) pichani.

Mhe. Balozi Mulamula na Mhe. Balozi Swan pamoja na wageni waalikwa wakiwa wametulia wakati nyimbo za Taifa la Finland na Tanzania zikiimbwa kuadhimisha miaka 104 ya uhuru wa Taifa la Finland.


Maafisa kutoka Ubalozi wa Finland wakiimba wimbo kwa Lugha ya Kifini kuwaburudisha wageni waalikwa wakati wa maadhimisho ya miaka 104 ya Taifa la Finland
Mhe. Waziri Mulamula akiwa ameongozana na mume wake, Dkt. George Mulamula wakipokelewa na Balozi wa Finland nchini, Mhe. Riitta Swan pamoja na mume wake walipowasili Ubalozi wa Finland kwa ajili ya kushiriki maadhimisho ya miaka 104 ya Finland.


 

Monday, December 6, 2021

MKUTANO WA 21 WA BARAZA LA MAWAZIRI LA KISEKTA LA AFYA WA EAC UMEFUNGULIWA MJINI ZANZIBAR

Mkutano wa 21 wa Baraza la Mawaziri la Kisekta (BLM) la Afya wa Jumuiya ya Afrika Mashariki umefunguliwa leo tarehe 06 Desemba 2021 katika Hotel Verde mjini Zanzibar.

Mkutano huo umeanza na ngazi ya Maafisa Waandamizi kwa lengo la kuandaa taarifa zitakazowasilishwa katika mkutano wa Makatibu Wakuu na Mawaziri. Pia unafanyika ukiwa umewakutanisha nchi wanachama wote isipokuwa wajumbe wawili (Rwanda na Sudan ya Kusini) ambao wanashiriki mkutano kwa njia ya mtandao. 

Akifungua mkutano Naibu Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki anayeshughulikia Sekta za Uzalishaji na Jamii, Mhe. Christophe Bazivamo ameeleza umuhimu wa mkutano wa sekta ya afya hasa wakati huu ambapo dunia imetangaza kuwepo kwa wimbi la nne la janga la UVIKO-19.

Mhe. Bazivamo amesisitiza nchi wanachama wa jumuiya ya Afrika Mashariki kuendelea kushirikiana na kamati ya uratibu ya UVIKO-19 ya jumuiya hiyo ili kuweza kuhakikisha tahadhari zinaendelea kutiliwa mkazo sambamba na utolewaji wa chanjo ili kuweza kudhibiti maambukizi mapya ya ugonjwa huo na kuruhusu kuendelea kwa shughuli za kiuchumi kwa ustawi wa wananchi.

“Hakuna nchi iliyo salama dhidi ya janga la UVIKO-19 kwakuwa kama nchi nyingine ndani ya jumuiya haipo salama ni hatari kwa jumuiya yetu na dunia kwa ujumla” alisema Mhe. Bazivamo

Pia alifafanua, kupitia mkutano huo nchi wanachama zitapata fursa ya kusikia taarifa zitakazowasilishwa na kila nchi ili kwa pamoja kuweza kuchangia na kushauri namna bora ya kukabiliana na janga hilo, kuwasilisha changamoto, na maoni yatakayosaidia kusimamia afya za wananchi kwa ujumla.

Vilevile masuala mtambuka yanayozigusa nchi wanachama yatapata nafasi ya kujadiliwa na kupatiwa suluhu ya pamoja. Masuala hayo ni pamoja na; taratibu za kufuatwa mipakani wakati janga la UVIKO-19 likiendelea kudhibitiwa, taratibu za upimaji wa UVIKO-19 ndani ya jumuiya, na kuwezesha usafiri huru wa wafanyakazi, huduma, ajira na bidhaa unasimamiwa kwa maslahi mapana ya jumuiya.

Mkutano huo unafanyika katika ngazi tofauti kwa utaratibu ufuatao:- Tarehe 06 -  08 Desemba 2021 ni Mkutano wa ngazi ya Watalaamu; Tarehe 09 Desemba 2021 ni Mkutano wa ngazi ya Makatibu Wakuu; na tarehe 10 Desemba 2021 ni Mkutano wa ngazi ya Mawaziri.

Ujumbe wa Tanzania katika mkutano wa ngazi ya watalaamu umeongozwa na Dkt. Abdul S. Ali, Mganga Mkuu na Mkurugenzi Mkuu wa Wizara ya Afya ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, akishirikiana na Bw. Eliabi Chodota Mkurugenzi wa Idara ya Miundombinu ya Uchumi na Huduma za Jamii katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki.

Wajumbe wengine walioshiriki mkutano huo wanatoka Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na watoto – Tanzania Bara, Wizara ya Afya, Ustawi wa Jami, Wazee, Jinsia, na watoto – Tanzania Zanzibar; Wizara ya Elimu,Sayansi na Teknolojia, pamoja na taasisi zilizo chini ya Wizara za Afya.

=============================================================


Mwenyekiti wa Mkutano ngazi ya Wataalamu kutoka Jamhuri ya Kenya, Dkt. Kuria Francis akiwakaribisha wajumbe katika Mkutano wa 21 wa Baraza la Mawaziri la Kisekta la Afya wa Jumuiya ya Afrika Mashariki uliofunguliwa leo tarehe 6 Desemba 2021 katika Hotel Verde Mjini Zanzibar.

Kiongozi wa ujumbe wa Tanzania ambaye pia ni Mganga Mkuu na Mkurugenzi Mkuu wa Wizara ya Afya ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Dkt. Abdul S. Said (kushoto) pamoja na Mkurugenzi wa Idara ya Miundombinu ya Uchumi na Huduma za Jamii katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bw. Eliabi Chodota wakifatilia mkutano. 

Ujumbe wa Tanzania ukifuatilia mkutano.

Sehemu nyingine ya ujumbe wa Tanzania

Ujumbe kutoka Jamhuri ya Burundi

Ujumbe kutoka Jamhuri ya Kenya

Ujumbe kutoka Jamhuri ya Uganda.

Matukio katika Ufunguzi wa Maonesho ya 21 ya Wajasiliamali wa Afrika Mashariki

    Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Prof. Kitila Mkumbo (Mb) kushoto akiwa katika banda la Serikali ya Tanzania kupata maelezo kuhusu Maonesho ya 21 ya Wajasiliamali ya Afrika Mashariki. Wengine katika picha kutoka kulia ni Mkuu wa Mkoa wa Mwanza,  Mhe. Mhandisi. Robert Gabriel Luhumbi; Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu-Sera, Bunge, Vijana, Kazi, Ajira na Watu wwenye Ulemavu, Mhe. Jenista Mhagama na Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Peter Mathuki.
Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Prof. Kitila Mkumbo akikata utepe kuashiria ufunguzi rasmi wa Maonesho ya 21 ya Wajasiliamali ya Afrika Mashariki yanayofanyika jijini Mwanza kuanzia tarehe 2 hadi 12 Desemba 2021.
Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Prof. Kitila Mkumbo (Mb) na ujumbe wake wakielekea kwenye mabanda ya wajasiliamali wanaoshiriki kwenye Maonesho ya 21 ya Wajasiliamali ya Afrika Mashariki yanayofanyika jijini Mwanza kuanzia tarehe 2 hadi 12 Desemba 2021. 

Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Prof. Kitila Mkumbo (Mb) 
akiangalia moja ya bidhaa zinazotengenezwa na wajasiliamali kwenye Maonesho ya 21 ya Wajasiliamali ya Afrika Mashariki yanayofanyika jijini Mwanza kuanzia tarehe 2 hadi 12 Desemba 2021.
Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Prof. Kitila Mkumbo (Mb) akiwa kwenye Banda la Vijana wa CCM mkoa wa Mwanza linalouza bidhaa za CCM kwenye Maonesho ya 21 ya Wajasiliamali ya Afrika Mashariki yanayofanyika jijini Mwanza kuanzia tarehe 2 hadi 12 Desemba 2021. 


Bidhaa mbalimbali zenye ubora wa hali ya juu zilizobuniwa na wajasiliamali kutoka nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki

Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Prof. Kitila Mkumbo (Mb) akiwa katika vazi la utamaduni la Sudan Kusini alilovalishwa baada ya kuwasili kwenye banda la nchi hiyo.

Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Prof. Kitila Mkumbo (Mb) akikabidhiwa zawadi ya picha yake ya kuchora katika moja ya mabanda ya Watanzaia.



 

Sunday, December 5, 2021

Wajasiriamali Wahimizwa Kutengeneza Bidhaa zenye Ubora


Na Mwandishi Maalum, Mwanza

Wajasiriamali wametakiwa kuendelea kuboresha bidhaa zao ili kudhibiti soko la nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) na hatimaye Afrika nzima, hususan katika kipindi hiki Bara la Afrika limeanzisha Soko Huru la Biashara (CfTA).

Hayo yamesemwa leo tarehe 4 Desemba 2021 na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Vijana, Kazi, Ajira na Watu Wenye Ulemavu, Mhe. Jenista Mhagama (Mb) ambaye alikuwa Mgeni Rasmi katika Siku ya Tanzania kwenye Maonesho ya 21 ya wajasiliamali ya Jumuiya ya Afrika Mashariki yanayofanyika jijini Mwanza kuanzia tarehe 2 hadi 12 Desemaba 2021.

“Nimetembelea mabanda ya wajasiriamali na kushuhudia bidhaa zenye ubora wa hali ya juu. Hivyo, tuendelee kuboresha bidhaa zetu ili tuingie masoko mengine badala ya kutegemea soko la Jumuiya ya Afrika Mashariki pekee”, Waziri Mhagama alisema.

Waziri Mhagama alitoa ahadi kuwa Serikali ya Tanzania itaendelea kushirikiana na nchi nyingine za Jumuiya, kuimarisha maonesho hayo ili yaweze kupanua soko, kuongeza ajira, kukuza uchumi na hatimaye kuondoa umasikini kwa raia wa nchi wanachama wa EAC.

Maonesho hayo ambayo yatafunguliwa rasmi tarehe 5 Desemba 2021 na Waziri wa Viwanda na Biashara, Prof. Kitila Mkumbo (Mb) kwa niaba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan yanapambwa na shughuli mbalimbali zikiwemo mafunzo kwa wajasiriamali yenye mada tofauti tofauti kama vile; vikwazo visivyo vya kibiashara, wepesi wa kufanya biashara ndani ya Jumuiya, fursa za biashara katika nchi ya Sudan Kusini, UVIKO-19 na biashara na namna ya kusafirisha bidhaa baina ya nchi za Jumuiya.

Mada hizo zinazowasilishwa na wabobezi kutoka sekta mbalimbali, zikiwemo Wizara ya Viwanda na Biashara, Sekretarieti ya Jumuiya ya Afrika Mashariki na taasisi zinazosimamia urasimishaji wa bidhaa, kwa siku ya tarehe 4 Desemba 2021, wajasiliamali wamejifunza falsafa ya Kaizen ambayo inahimiza umuhimu wa mjasiriamali kuboresha utendaji wake kila siku katika maeneo yote kama ya ubunifu, utafutaji wa masoko, vifungashio, utoaji wa huduma kwa mteja n.k.

Mkurugenzi wa Biashara na Forodha wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, Bw. Keneth Bagamuhunda alieleza namna maonesho hayo yanavyondelea kuimarika mwaka hadi mwaka na kubainisha kuwa maonesho ya mwaka huu yameandaliwa vizuri na washiriki wamekuwa wengi zaidi ukilinganisha na miaka mingine.

Wajasiriamali zaidi ya 900 wanashiriki maonesho hayo wakiwemo 420 wa Kitanzania kutoka maeneo mbalimbali ikiwa ni pamoja na Zanzibar. Aidha, viongozi wa Serikali akiwemo Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Mhe. Mhandisi. Robert Gabriel Luhumbi; Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-Zanzibar, Kazi, Uchumi na Uwekezaji, Mhe. Mudriki Soragha; Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu, Vijana, Kazi na Ajira, Mhe. Patrobas Katambi; Waziri wa Jiji la Kampala, Hajatti. Minsa Kabanda; wabunge wanne kutoka Uganda waliungana na Mhe. Mhagama katika Siku ya Tanzania kwenye maoesho hayo.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu-Sera, Bunge, Vijana, Kazi, Ajira na Watu wenye Ulemavu, Mhe. Jenista Mhagama akihutubia wajasiliamali wanaoshiriki maonesho ya 21 ya wajasiriamali wa EAC jijini Mwanza.

Baadhi ya wajasiriamali wakisikiliza kwa makini hotuba ya Mgeni Rasmi, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu-Sera, Bunge, Vijana, Kazi, Ajira na Watu wenye Ulemavu, Mhe. Jenista Mhagama


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu-Sera, Bunge, Vijana, Kazi, Ajira na Watu wenye Ulemavu, Mhe. Jenista Mhagama akifurahi kufuatia Mkurugenzi wa Ajira katika Wizara yake ambaye pia ni Mwenyekiti wa maandalizi ya Maonesho ya 21 ya wajasiriamali ya EAC, Bw. Ali Msaki (kulia) kukabidhiwa cheti kutokana na kuratibu vizuri maaandalizi hayo. Anayekabidhi cheti ni Mkurugenzi wa Biashara na Forodha wa Sekretarieti ya EAC, Bw. Keneth Bagamuhunda.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu-Sera, Bunge, Vijana, Kazi, Ajira na Watu wenye Ulemavu, Mhe. Jenista Mhagama akipata maelezo kutoka kwa Mkurugenzi wa Biashara na Forodha wa Sekretarieti ya EAC, Bw. Keneth Bagamuhunda katika Banda la Sekretarieti ya EAC.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu-Sera, Bunge, Vijana, Kazi, Ajira na Watu wenye Ulemavu, Mhe. Jenista Mhagama akisaini Kitabu cha Wageni katika Banda la Serikali ya Tanzania. Aliyesimama ni Afisa wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bi. Semeni Nandonde.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu-Sera, Bunge, Vijana, Kazi, Ajira na Watu wenye Ulemavu, Mhe. Jenista Mhagama pamoja na wajasiriamali wakionesha bidhaa mbalimbali zinazotengenezwa nchini.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu-Sera, Bunge, Vijana, Kazi, Ajira na Watu wenye Ulemavu, Mhe. Jenista Mhagama akiangalia bidhaa zinazotengenezwa na wajasiriamali wa EAC.

Bidhaa zina viwango vizuri, hongereni sana wajasiriamali kwa kazi nzuri.

Wajasiriamali wanatengeneza hadi vitanda kwa ajili ya matumizi ya wagonjwa katik hospitali zetu. 

Bidhaa zimefungashwa vizuri

Hongereni wajasiliamali kwa ubunifu wenu, hakika nchi za EAC zinasonga kwa kasi katika biashara na uwekezaji.

Mkurugenzi wa Biashara, Uwekezaji na Sekta za Uzalishaji katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bw. Bernard Haule (katikati) wakikamilisha jambo na maafisa wa Wizara hiyo, Bw. Hassan Mnondwa na Bi. Semeni Nandonde.

Burdani ni moja ya jambo linalofurahiwa na washiriki pamoja na wale wanaotembelea maonesho ya 21 ya wajasiriamali ya EAC jijini Mwanza.

Saturday, December 4, 2021

STAMICO, SUNESS LTD ZASAINI MKATABA WA MASHRIKIANO

Na Mwandishi wetu, Roma

Shirika la Taifa la Madini (STAMICO) limesaini mkataba wa makubaliano ya awali na Kampuni ya Suness Limited ya Italia kwa ajili ya kuendeleza mradi mkubwa wa Shaba katika Mkoa Kilimanjaro. Suness Limited ni kampuni ya Kiitaliano inayojishughulisha na uchimbaji madini na Kampuni hiyo imeonesha utayari wa kushirikiana na STAMICO katika kuendeleza kwa pamoja mradi wa shaba.

Akiongea mara baada ya kusaini mkataba huo leo Jijini Roma Italia, Mkurugenzi Mtendaji wa STAMICO Dkt. Venance Mwasse amesema kuwa mkataba umesainiwa kupitia jukwaa la biashara na uwekezaji lililofanyika Jijini Roma Italia tarehe 02 – 03 Disemba 2021.

Pamoja na mambo mengine, STAMICO wameweza kuelezea juu ya mradi wa mkubwa wa shaba unaopatikana katika Mkoa wa Kilimanjaro ambapo pia mwekezaji  ameonesha nia ya kuingia ubia na STAMICO.

“Shirika lina mradi wake mkubwa wa Shaba mkoani Kilimanjaro wenye kiasi kikubwa cha mashapu ya Shaba na kupitia jukwa la wafanyabiashara na uwekezaji lililofanyika Roma Italia, tumewaeleza juu ya mradi huo na wenzetu wameonesha kuvutiwa na mradi huo na tukakubaliana kusaini makubaliano ya awali na baadae watakuja Tanzania ili kwa pamoja twende kwenye eneo la mradi husika na mwishowe tuingie katika makubaliano ya pamoja ya kuendeleza mradi huo,” Amesema Dkt. Mwasse

Naye Rais wa Kampuni ya Sunless Bw. Sandro Calo amesema kuwa amefurahishwa na utiaji saini wa awali wa mkataba wa makubaliano kwa ajili ya kushirikiana na Serikali ya Tanzania katika kuendeleza kwa pamoja mradi wa Shaba

“Nimefurahia kuanza kwa makubaliano haya mapya ambayo yataleja matokeo chanya kati ya nchi ya Tanzania na Italia na naahidi kuendeleza ushirikiano huu kwa maslahi mapana ya pande zote mbili katika sekta hii ya madini,” amesema Bw. Calo.

Utiaji saini wa makubaliano hayo umeshuhudiwa  na Naibu Waziri, Wizara ya Madini Mhe. Prof. Shukrani Manya, Balozi wa Tanzania Nchini Italia, Mhe. Mahmoud Thabiti Kombo, Mkurugenzi Idara ya Diplomasia ya Uchumi katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Edwin Rutageruka pamoja na Mkurugenzi wa Kampuni ya Utalii ya Zanzibar Classic Safaris, Bw. Yussuf Salim Njama.

Mkurugenzi Mtendaji wa STAMICO Dkt. Venance Mwasse pamoja na Rais wa Kampuni ya Sunless Bw. Sandro Calo wakisaini mkataba wa makubaliano ya awali kwa ajili ya kuendeleza mradi mkubwa wa Shaba katika Mkoa Kilimanjaro. Utiaji saini wa mkataba huo umeshuhudiwa  na Naibu Waziri, Wizara ya Madini Mhe. Prof. Shukrani Manya, Balozi wa Tanzania Nchini Italia, Mhe. Mahmoud Thabiti Kombo pamoja Mkurugenzi Idara ya Diplomasia ya Uchumi katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Edwin Rutageruka Jijini Roma, Italia. 


Mkurugenzi Mtendaji wa STAMICO Dkt. Venance Mwasse akibadilishana mkataba wa makubaliano ya awali kwa ajili ya kuendeleza mradi mkubwa wa Shaba katika Mkoa Kilimanjaro na Rais wa Kampuni ya Sunless Bw. Sandro Calo mara baada ya kusainiwa wakisaini kwa mkataba huo leo Jijini Roma, Italia 


Mkurugenzi Mtendaji wa STAMICO Dkt. Venance Mwasse pamoja na Rais wa Kampuni ya Sunless Bw. Sandro Calo wakionesha mkataba wa makubaliano ya awali kwa ajili ya kuendeleza mradi mkubwa wa Shaba katika Mkoa Kilimanjaro na mara baada ya kusainiwa leo Jijini Roma, Italia