Saturday, December 4, 2021

STAMICO, SUNESS LTD ZASAINI MKATABA WA MASHRIKIANO

Na Mwandishi wetu, Roma

Shirika la Taifa la Madini (STAMICO) limesaini mkataba wa makubaliano ya awali na Kampuni ya Suness Limited ya Italia kwa ajili ya kuendeleza mradi mkubwa wa Shaba katika Mkoa Kilimanjaro. Suness Limited ni kampuni ya Kiitaliano inayojishughulisha na uchimbaji madini na Kampuni hiyo imeonesha utayari wa kushirikiana na STAMICO katika kuendeleza kwa pamoja mradi wa shaba.

Akiongea mara baada ya kusaini mkataba huo leo Jijini Roma Italia, Mkurugenzi Mtendaji wa STAMICO Dkt. Venance Mwasse amesema kuwa mkataba umesainiwa kupitia jukwaa la biashara na uwekezaji lililofanyika Jijini Roma Italia tarehe 02 – 03 Disemba 2021.

Pamoja na mambo mengine, STAMICO wameweza kuelezea juu ya mradi wa mkubwa wa shaba unaopatikana katika Mkoa wa Kilimanjaro ambapo pia mwekezaji  ameonesha nia ya kuingia ubia na STAMICO.

“Shirika lina mradi wake mkubwa wa Shaba mkoani Kilimanjaro wenye kiasi kikubwa cha mashapu ya Shaba na kupitia jukwa la wafanyabiashara na uwekezaji lililofanyika Roma Italia, tumewaeleza juu ya mradi huo na wenzetu wameonesha kuvutiwa na mradi huo na tukakubaliana kusaini makubaliano ya awali na baadae watakuja Tanzania ili kwa pamoja twende kwenye eneo la mradi husika na mwishowe tuingie katika makubaliano ya pamoja ya kuendeleza mradi huo,” Amesema Dkt. Mwasse

Naye Rais wa Kampuni ya Sunless Bw. Sandro Calo amesema kuwa amefurahishwa na utiaji saini wa awali wa mkataba wa makubaliano kwa ajili ya kushirikiana na Serikali ya Tanzania katika kuendeleza kwa pamoja mradi wa Shaba

“Nimefurahia kuanza kwa makubaliano haya mapya ambayo yataleja matokeo chanya kati ya nchi ya Tanzania na Italia na naahidi kuendeleza ushirikiano huu kwa maslahi mapana ya pande zote mbili katika sekta hii ya madini,” amesema Bw. Calo.

Utiaji saini wa makubaliano hayo umeshuhudiwa  na Naibu Waziri, Wizara ya Madini Mhe. Prof. Shukrani Manya, Balozi wa Tanzania Nchini Italia, Mhe. Mahmoud Thabiti Kombo, Mkurugenzi Idara ya Diplomasia ya Uchumi katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Edwin Rutageruka pamoja na Mkurugenzi wa Kampuni ya Utalii ya Zanzibar Classic Safaris, Bw. Yussuf Salim Njama.

Mkurugenzi Mtendaji wa STAMICO Dkt. Venance Mwasse pamoja na Rais wa Kampuni ya Sunless Bw. Sandro Calo wakisaini mkataba wa makubaliano ya awali kwa ajili ya kuendeleza mradi mkubwa wa Shaba katika Mkoa Kilimanjaro. Utiaji saini wa mkataba huo umeshuhudiwa  na Naibu Waziri, Wizara ya Madini Mhe. Prof. Shukrani Manya, Balozi wa Tanzania Nchini Italia, Mhe. Mahmoud Thabiti Kombo pamoja Mkurugenzi Idara ya Diplomasia ya Uchumi katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Edwin Rutageruka Jijini Roma, Italia. 


Mkurugenzi Mtendaji wa STAMICO Dkt. Venance Mwasse akibadilishana mkataba wa makubaliano ya awali kwa ajili ya kuendeleza mradi mkubwa wa Shaba katika Mkoa Kilimanjaro na Rais wa Kampuni ya Sunless Bw. Sandro Calo mara baada ya kusainiwa wakisaini kwa mkataba huo leo Jijini Roma, Italia 


Mkurugenzi Mtendaji wa STAMICO Dkt. Venance Mwasse pamoja na Rais wa Kampuni ya Sunless Bw. Sandro Calo wakionesha mkataba wa makubaliano ya awali kwa ajili ya kuendeleza mradi mkubwa wa Shaba katika Mkoa Kilimanjaro na mara baada ya kusainiwa leo Jijini Roma, Italia 



No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.