Saturday, July 28, 2018

TAARIFA KUHUSU MATOKEO YA AWALI YA NAFASI ZA AJIRA ZA SADC


TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

KUHUSU MATOKEO YA AWALI YA NAFASI ZA AJIRA KATIKA SEKRETARIATI YA SADC ZILIZOTANGAZWA                                              KWA MWAKA 2018


Sekretarieti ya SADC ilitangaza nafasi 50 katika kada mbalimbali mwezi wa Mei, 2018. Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais, Menejimenti na Utumishi ilitangaza nafasi hizo kupitia vyombo mbalimbali vya habari.

Wizara inapenda kuutangazia umma kuwa baada ya mchujo wa duru ya kwanza uliofanywa na Kikosi Kazi Maalum, jumla ya waombaji 141 kati ya waombaji 1,472 wamepita katika uchambuzi wa awali. Katika muktadha huo, Wizara inaweka orodha ya awali ya mchujo wa Tanzania ya waombaji waliochaguliwa katika nafasi mbalimbali pamoja na jedwali lenye kuonyesha idadi ya waombaji hao.

Wizara inapenda kuutaarifu umma na waombaji wa nafasi za ajira zilizotangazwa na SADC kuwa taarifa zaidi itatolewa Sekretarieti ya SADC kwa wale tu watakao kuwa kwenye orodha ya mchujo wa duru ya pili (shortlisted) utakayofanywa na Sekretarieti ya SADC.

Aidha, tutakumbuka kuwa mwezi wa Mei, 2017 Sekretarieti ya SADC ilitangaza nafasi 48 ambapo zoezi la usaili wake lilikamilika mwaka huu. Kwenye nafasi 48, Tanzania imefanikiwa kupata nafasi tano za kimkakati. Nafasi hizo zinaainishwa kama ifuatazo:

i.      Afisa Mwandamizi anayeshughulikia masuala ya Sera na Mikakati ya Maendeleo, (Senior Officer - Policy and Strategy Development);

ii.    Afisa Mwandamizi Mipango anayeshughulikia masuala ya Viwanda na Ushindani, (Senior Programme Officer - Industrialization and Competitiveness);

iii.   Afisa Mipango anayeshughulikia masuala ya Ushuru na Utaratibu, (Programme Officer Customs and Procedures);

iv.   Afisa anayeshughulikia masuala ya Ufuatiliaji, Tathmini na utoaji wa Taarifa, (Monitoring, Evaluation and Reporting Officer); na

v.    Afisa anayeshughulikia masuala ya Fedha na Bajeti, (Finance Officer - Treasury and Budget )

Tunawapongeza kwa dhati wote waliochaguliwa na kufanikiwa kuingia kwenye orodha ya mchujo wa awali uliofanyika Tanzania kwa mwaka 2018. 

Aidha, kwa aina ya pekee, tunawapongeza maafisa waliochaguliwa kwenye nafasi tano (5) zilizotajwa na tunawatakia kila la heri katika mjukumu yao mapya sambamba na kuwasihi daima kukumbuka kuwa wanaliwakilisha Taifa letu kwenye nafasi hizo.

Mwisho, Wizara inapenda kutaarifu kuwa itaendelea kuzitangaza fursa kama hizi zitapojitokeza kupitia SADC na Jumuiya zingine za Kikanda na Kimataifa ambazo Tanzania ni nchi mwanachama, kwa manufaa ya watanzania wote. Hivyo, tunawaomba Watanzania wasikate tamaa na wasisite kuwasilisha maombi ya ajira kama hizi pale fursa zinapojitokeza.


Imetolewa na:

Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,

Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,

Dar es Salaam,

27 Julai, 2018


No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.