Wednesday, October 21, 2020

TROIKA YA SADC YARIDHISHWA NA MAZINGIRA YA UCHAGUZI MKUU

Asasi ya Ushirikiano wa Siasa,Ulinzi na Usalama (TROIKA) ya Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) imeridhishwa na mazingira ya hali ya siasa nchini Tanzania yanaruhusu kufanyika kwa uchaguzi mkuu wa Octoba 28,2020 na kwamba wataendelea kufuatilia mazingira ya uchaguzi huo.

Akizungumza katika Mkutano uliofanyika kwa njia ya mtandao Jijini Dar es Salaam Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Prof. Palamagamba John Kabudi amesema TROIKA imekuwa ikifuatilia kwa ukaribu tangu awali mchakato wa uchaguzi hapa nchini na kwamba imeridhishwa na mazingira ya amani yaliyopo hali inayoruhusu uchaguzi huo kufanyika.  

"Leo katika mkutano wangu na TROKA ulifanyika kwa njia ya mtandao mwenyekiti wa TROIKA ambaye pia ni Waziri wa Mambo ya Nje wa Botswana Dkt. Lemogang Kwape ameoneshwa mazingira ya hali ya siasa nchini Tanzania yanaruhusu kufanyika kwa uchaguzi mkuu wa Octoba 28, 2020 na kwamba wataendelea kufuatilia mazingira ya uchaguzi huo," Amesema Prof. Kabudi

Prof. Kabudi ameongeza kuwa ni kwa mara ya kwanza katika historia ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ipate uhuru kwamba uchaguzi huu unagharamiwa kwa fedha ya walipa kodi maamuzi ambayo yamefanyika kwa kutambua kuwa demokrasia ndio jambo kubwa katika uhai,utashi na kielelezo cha Taifa ambalo ni huru kama ilivyo Tanzania.

Kuhusu waangalizi wa kimataifa wa uchaguzi mkuu wa Octoba 28, Prof Kabudi amesema TROIKA imefanya tathimini ya awali ya hali ya usalama na kisiasa na kwamba Tanzania inategemea kuwapokea waangalizi kutoka Umoja wa Afrika na wale wa kutoka katika nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki.

 Katika tukio jingine Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Prof. Palamagamba John Kabudi amepokea nakala za hati za utambulisho za Mkurugenzi Mkazi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Chakula Duniani (WFP) Sarah Gordon-Gibson.

Katika mazungumzo yao Prof. Kabudi amesema WFP imekuwa ni miongoni mwa mashirika ya Kimataifa ambayo yanaushirikiano mzuri na Tanzania ambapo kwa mwaka 2018 WFP imenunua tani 160,000 za nafaka na 2019 wamenunua tani 36,000 zenye thamani ya shilingi bilioni 21 fedha ambazo zimesaidia wakulima wadogowadogo katika kuboresha kilimo.  

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkazi wa Shirika la Mpango wa Chakula Duniani (WFP) Sarah Gordon-Gibson amesema wamejadiliana namna ya kuendeleza ushirikiano baina ya pande hizo mbili hususani kusaidia wakulima wadogowadogo nchini kuboresha kilimo,kuboresha mazingira ya lishe na kwamba shirika hilo lina mpango wa kuongeza msaada wanaoutoa kwa Tanzania. 

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Prof. Palamagamba John Kabudi akieleza jambo wakati mkutano wa TROIKA ukiendelea. Mkutano huo ulifanyika kwa njia ya mtandao leo Jijini Dar es Salaam.  


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Prof. Palamagamba John Kabudi akipokea nakala ya hati za utambulisho za Mkurugenzi Mkazi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Chakula Duniani (WFP) Sarah Gordon-Gibson leo jijini Dar es Salaam


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Prof. Palamagamba John Kabudi akiongea na Mkurugenzi Mkazi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Chakula Duniani (WFP) Sarah Gordon-Gibson leo jijini Dar es Salaam


Mkurugenzi Mkazi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Chakula Duniani (WFP) Sarah Gordon-Gibson akimueleza jambo Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Prof. Palamagamba John Kabudi leo jijini Dar es Salaam



No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.