Tuesday, November 10, 2020

COMORO YAIPONGEZA TANZANIA KWA UCHAGUZI HURU, AMANI NA HAKI

Rais wa Visiwa vya Comoro Mheshimiwa Azali Assouman ameipongeza Serikali ya Tanzania kwa kufanya uchaguzi huru, amani na haki.

Rais wa Visiwa vya Comoro ameipongeza Tanzania leo jijini Dar es Salaam wakati alipokuwa katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa tayari kuondoka nchini na kurejea Comoro baada ya kushuhudia hafla ya uapisho wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Joseph Magufuli uliofanyika Novemba 5 Jijini Dodoma.

Rais Assouman anasema Tanzania ni nchi ya Amani na utulivu wa kisiasa kwani wakati wote wa tukio la kuapishwa kwa Dkt Magufuli aliona mambo ambayo yanapaswa kuigwa na mataifa mengine hususan kwenye nyakati za uchaguzi.

"Kwa kweli tangu nimefika hapa Tanzania nimeona mambo mazuri na ambayo tunapaswa kuyaiga sisi viongozi wa mataifa mengine," Amesema Rais Assouman

Mbali na kujifunza masuala mbalimbali ikiwemo ya uchaguzi, pia Rais Assouman ameliahidi ushirikiano kwa Serikali ya Tanzania katika Nyanja za mbalimbali ikiwemo diplomasia ya uchumi, biashara, uwekezaji na utalii.

“Najisikia niko nyumbani kwa sababu uhusiano wetu umeimarishwa zaidi, mahusiano yetu yamekuwa katika masuala ya kijamii, utamaduni, biashara na mambo mengine mengi” Amebainisha Rais Assouman.

Kwa upande wake, Balozi wa Tanzania nchini Comoro, Mhe. Sylvester Mabumba amesema kuwa Serikali ya Tanzania itaendelea kushirikiana na Comoro katika kuhakikisha kuwa sera ya uchumi wa nchi zote mbili unakua zaidi.

"Sisi tuatendelea kushirikiana vyema na Comoro kibiashara ili kukuza sera ya 2025 tunaifikia ipasavyo kwa kuhakikisha kuwa uchumi wetu unafikia kiwango cha juu sana, naamini kuwa tunapokuwa na masoko ya uhakika Viswa vya Comoro uchumi wetu utakuwa zaidi," Amesema Balozi Mabumba.

Kwa Upande wake Balozi wa Visiwa Vya Comoro nchini Tanzania mhe. Dkt. Ahmada El Badaoui Mohamed amesema kuwa kuna fursa nyingi za kiuchumi ambazo Comoro na Tanzania zinaweza kushirikiana.

Rais Assouman aliwasili nchini Novemba 4 kwa ajili ya kuhudhuria hafla ya uapisho wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli uliofanyika Novemba 5 Jijini Dodoma ambapo baada ya shughuli hiyo alipata fursa ya kutembelea hifadhi ya Taifa ya Ngorongoro ambapo na kujiona vivutio mbalimbali vya utalii nchini.

Serikali ya Tanzania na Visiwa Comoro zimekuwa zikishirikiana katika sekta mbalimbali ikiwemo, elimu, afya, biashara na uwekezaji.


Rais wa Visiwa  vya Comoro, Mhe. Azali Assouman akiongea na waandishi wa habari katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa Julius Nyerere (JNIA),kabla ya kuondoka nchini na kurejea nchini Comoro. Kulia ni Balozi wa Tanzania nchini Comoro, Mhe.Sylivester Mabunda  akifuatiwa na Balozi wa Visiwa vya Comoro nchini Mhe. Dkt. Ahmada El Badaoui Mohamed.   


Rais wa Visiwa  vya Comoro, Mhe. Azali Assouman akiondoka katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa Julius Nyerere (JNIA), baada ya kushuhudia hafla ya Uapisho wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt.John Pombe Magufuli iliyofanyika Novemba  5, 2020 Jijini Dodoma na Baadaye alitembelea Hifadhi ya Taifa ya Ngorongoro


Rais wa Visiwa  vya Comoro, Mhe. Azali Assouman, akiangalia kikundi cha ngoma   kabla ya kuondoka katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa Julius Nyerere (JNIA), baada ya kushuhudia hafla ya Uapisho wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt.John Pombe Magufuli iliyofanyika Novemba 5, 2020, Jijini Dodoma na Baadaye alitembelea Hifadhi ya Taifa ya Ngorongoro

Kikundi cha Ngoma kikiburudisha katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa Julius Nyerere kabla ya kuondoka kwa Rais wa Visiwa  vya Comoro, Mhe. Azali Assouman



Rais wa Visiwa  vya Comoro, Mhe. Azali Assouman, akiagana na Balozi wa Tanzania nchini Comoro, Mhe.Sylivester Mabunda katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa Julius Nyerere (JNIA), Jijini Dar es Salaam


Rais wa Visiwa  vya Comoro, Mhe. Azali Assouman, akiaga tayari kwa  kuondoka katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa Julius Nyerere(JNIA), kwa kutumia Ndege ya Shirika la Ndege la Tanzania (Air Tanzania)





No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.