Friday, November 13, 2020

WABUNGE WA AFRIKA MASHARIKI WAHIMIZWA KUTANGULIZA MASLAHI YA TANZANIA

 

Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Brigedia Jenerali Wilbert Ibuge amekutana na Wabunge wa Tanzania katika Bunge la Afrika Mashariki na kuwahimiza kutanguliza  maslahi ya Tanzania katika kutekeleza majukumu yao.

Mhe. Ibuge amesema hayo jijini Dodoma alipokutana na Wabunge hao na kusisitiza kuwa maslahi ya Tanzania ni lazima yawe kipaumbele chao katika kutekeleza majukumu yao  ili kufanikisha ushiriki wa Tanzania kikamilifu katika mtangamano wa  Jumuiya ya Afrika Mashariki.

 “Endeleeni kushikilia msimamo wa kutanguliza maslahi ya Tanzania siku zote, muendelee kufanya kazi hiyo nzuri  kwenye masuala mengine yote yanayogusa maslahi ya nchi yetu,” amesema Balozi Ibuge na kuongeza kuwa nafasi yao kama wabunge wa Afrika Mashariki inatokana na uwepo wa jimbo lao ambalo ni Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika Mtangamano huo.

Balozi Ibuge pia amewataka Wabunge hao kuwasiliana mara kwa mara na Serikali ili kupata maoni, ushauri na msimamo wa Serikali katika kujadili na kupitisha masuala mbalimbali ndani ya bunge hilo.

Balozi Ibuge amewataka wabunge hao kujiepusha na migogoro ndani ya Bunge na Jumuiya kwani kufanya hivyo kutaiwezesha Tanzania kujiweka sawa katika nyanja za siasa na diplomasia na kuwapongeza kwa utendaji kazi wao na hasa jinsi walivyoshughulikia suala la Muswada binafsi wa Marekebisho ya Sheria ya Usimamizi wa Forodha ya Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Akizungumza katika kikao hicho Mwenyekiti wa Wabunge hao Mhe. Adam Kimbisa aliishukuru Wizara kwa kukutana nao kuwapa muongozo wa namna ya kushughulikia mambo mbalimbali yanayoendelea ndani ya Bunge na Jumuiya kwa ujumla.

Mhe. Kimbisa alimuahakikishia Katibu Mkuu kuwa Wabunge hao  wataendelea kuhakikisha maslahi ya Tanzania yanazingatiwa katika hatua zote za mtangamano kupitia ushiriki wao katika Bunge la Afrika Mashariki.

 


Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Brigedia Jenerali Wilbert Ibuge akizungumza na Wabunge wa Tanzania katika Bunge la Afrika Mashariki (EALA) ofisini kwake Jijini Dodoma

Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Brigedia Jenerali Wilbert Ibuge katika Picha ya pamoja na Wabunge wa Tanzania katika Bunge la Afrika Mashariki (EALA) walipomtembelea ofisini kwake Jijini Dodoma




No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.