Friday, January 14, 2022

TANZANIA KUENDELEA KUSHIRIKIANA NA MISRI KATIKA KUBORESHA SEKTA YA AFYA

Serikali ya Tanzania imepokea tani 16 za Dawa, Vifaa Tiba na Vifaa Kinga ikiwa ni msaada wenye thamani ya shillingi milioni 864 kutoka Serikali ya Misri.

Akizungumza kwa niaba ya Serikali wakati wa hafla fupi ya kupokea shehena ya dawa hizo iliyofanyika hivi karibuni jijini Dar es Salaam, Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Prof.  Abel Makubi amesema Tanzania inaishukuru Serikali ya Misri kwa msaada huo muhimu kwa wananchi wa Tanzania na kwamba itandelea kuimarisha ushirikiano na Serikali ya Misri hususan katika kuboresha sekta ya afya na kuahidi kuusimamia kikamilifu msaada huo ili uwafikie walengwa kwa wakati.

Pia aliongeza kusema kuwa,  msaada huo umewasili wakati mwafaka ambao Tanzania inaendelea kuboresha sekta ya afya kwa kusogeza huduma za afya kwa wananchi pamoja na kuongeza upatikanaji wa Dawa na Vifaa Tiba katika maeneo ya mijini na vijijini.


Aidha, alipongeza ushirikiano wa kidiplomasia uliopo kati ya Tanzania na Misri ambao umekuwa wa manufaa makubwa tangu kuanzishwa kwake na kupongeza jitihada zinazofanywa na Mhe. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika kuboresha Sekta ya Afya nchini ambapo alisema msaada huo ni miongoni mwa matokeo ya ziara ya Mhe. Rais aliyoifanya nchini Misri mwezi Novemba, 2021.


"Kwa niaba ya Serikali ya Tanzania na pia kwa niaba ya Waziri wa Afya. Mhe. Ummy Mwalimu napokea msaada huu wa Dawa na Vifaa Tiba wenye thamani zaidi ya shilingi milioni 800 kutoka Serikali ya Misri. Kama Serikali, tunaendelea kuboresha na kusogeza huduma za afya kwa wananchi hivyo msaada huu utachangia jitihada hizo. Ninakuomba Mhe. Balozi ufikishe salamu zetu za shukrani kwa Mhe. Abdel Fattah Al-Sisi, Rais wa Misri kwa msaada huu ambao tumeupokea kwa dhati na utatimiza lengo lilokusudiwa la kuwasaidia wananchi wa Tanzania" alisema Dkt. Makubi.


Kwa upande wake, Balozi wa Misri hapa nchini. Mhe. Mohamed Gaber Mohamed Abulwafa amesema nchi yake itaendelea kushirikiana na Tanzania na inaunga mkono jitihada za Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi makini wa Mhe. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania za kuwaletea watanzania maendeleo kupitia sekta mbalimbali ikiwemo ya afya.


Kadhalika, Mhe. Balozi Abulwafa alieleza kuwa, mbali na ushirikiano wa Tanzania na Misri kwenye sekta ya afya, Nchi yake itaendelea kushirikiana na Tanzania katika kutoa fursa za mafunzo ya kuwajengea uwezo watu wa sekta ya afya na fani mbalimbali kwa watanzania.

Hafla hiyo ilihudhuriwa pia na Katibu Mkuu wa Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Dkt. Faraji Kasidi Mnyepe, Mganga Mkuu wa Serikali, Dkt. Aifelo Sichwale, Mfamasia Mkuu wa Serikali, Bw. Daudi Msasi, Kaimu Mkuu wa Itifaki katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bw. Celestine Kakele na Maafisa Waandamizi kutoka Serikalini.

 Balozi wa Misri hapa nchini, Mhe. Mohamed Gaber Mohamed Abulwafa (katikati) akimkabidhi Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Prof. Abel Makubi (wa pili kulia) msaada wa Dawa na Vifaa Tiba kutoka Serikali ya Misri. Wengine katika picha ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Dkt. Faraji Kasidi Mnyepe ( wa pili kushoto), Mganga Mkuu wa Serikali, Dkt. Aifelo Sichalwe (wa kwanza kushoto) na Mwambata Jeshi wa Ubalozi wa Misri, Brigedia Sherif Farag Mohamed (wa kwanza kulia). Hafla ya makabidhiano ya msaada huo imefanyika jijini dar es Salaam hivi karibuni.
Mhe. Balozi Abulwafa akimkabidhi Prof. Makubi huku viongozi wengine wakishuhudia. Kulia ni Kaimu Mkuu wa Itifaki na Mwakilishi wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bw. Celestine Kakele.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Prof. Abel Makubi kwa pamoja na Balozi wa Misri nchini, Mhe. Mohamed Gaber Mohamed Abulwafa wakisaini Hati ya Makabidhiano ya Dawa na Vifaa Tiba vilivyopokelewa nchini kutoka Misri
Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Prof. Abel Makubi kwa pamoja na Balozi wa Misri nchini, Mhe. Mohamed Gaber Mohamed Abulwafa wakibadilishana Hati ya Makabidhiano waliyosaini wakati wa mapokezi ya Dawa na Vifaa Tiba  kutoka Misri
Balozi wa Misri nchini, Mhe. Mohamed Gaber Mohamed Abulwafa akizungumza mara baada ya kukabidhi msaada wa Dawa na Vifaa Tiba  kkwa Serikali ya Tanzania
Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Prof. Abel Makubi akizungumza  kwa niaba ya Serikali mara baada ya kupokea msaada wa  Dawa na Vifaa Tiba  kutoka Misri
Viongozi wakiwa katika picha ya pamoja
Picha ya pamoja ya viongozi na wadau mbalimbali

Afisa Mambo ya Nje katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bibi Faith Masaka akibadilishana mawazo na Afisa kutoka Ubalozi wa Misri hapa nchini, Bw. Mahmoud Hamdy Khalifa wakati wa hafla ya makabidhiano ya Dawa na Vifaa Tiba kutoka Misri


























 

No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.