Tuesday, July 19, 2016

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje ashiriki maadhimisho miaka 59 ya Aga Khan kuongoza Ismailia

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,  Dkt. Susan Kolimba (Mb.), akizungumza katika maadhimisho ya Miaka 59  ya Kiongozi Mkuu wa Madhehebu ya Shia Ismailia, Mtukufu Aga Khan tangu aliposhika nafasi hiyo.Katika hotuba yake Dkt. Kolimba alitumia nafasi hiyo kumpongeza Mtukufu Aga khan kwa mafanikio katika kipindi cha uongozi wake na kwa kuendelea kushirikiana na Tanzania katika miradi mbalimbali ya maendeleo iliyochini ya Taasisi yake. Kulia ni Mwakilishi Mkazi wa Ismailia hapa nchini, Bw. Amin Kurji.  
Mkurugenzi wa masuala ya kidiplomasia katika Taasisi ya Aga Khan,  Balozi Arif Lalani pamoja na wageni waalikwa waliohudhuria hafla hiyo wakimsikiliza Mhe. Kolimba (hayupo pichani) alipokuwa akiendelea kuzungumza kwenye maadhimisho hayo.
Katibu wa Naibu Waziri, Bw. Adam Isara(Kulia) akifuatilia hotuba ya Mhe. Kolimba pamoja na Afisa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bi. Hellen Mgeta. 
Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Ushirikiano wa Kimataifa Bi. Ramla Khamis (wa pili kutoka kushoto), akiwa pamoja na Maafisa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki wakati wa hafla hiyo.  
Sehemu ya wageni waalikwa waliohudhuria hafla hiyo nao wakimsikiliza Dkt. Kolimba, wa pili kutoka kulia ni Balozi wa Japan hapa nchini Mhe. Masaharu Yoshinda.
Wageni waalikwa . 
Mhe. Dkt. Kolimba na Bw. Kurji wakiwatakia afya njema Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli na Mtukufu Aga Khan wakati wa hafla hiyo. 
Dkt. Kolimba akitambulishwa kwa wageni waalikwa na Bw. Kurji
Dkt. Susan Kolimba akipokea maelezo kutoka kwa mtaalam aliyebuni mchoro waa Chuo Kikuu cha  Aga Khan kitakachojengwa Jijini Arusha.


Picha na Reginald Philip

Monday, July 18, 2016

Tanzania yapewa tuzo za ustawi wa jamii na ushirikishaji wa wanawake katika mkutano wa AU

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki akiwa na Balozi wa Tanzania nchini Ethiopia Mhe. Naimi Aziz (kulia) na Mkurugenzi wa Idara ya Afrika Balozi Samwel Shelukindo mara baada ya kukabidhiwa tuzo za Tanzania. 
Balozi Augustine Mahiga, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki akipokeza tuzo za Tanzania kutoka kwa afisa wa Umoja wa Afrika wakati wa Mkutano wa Umoja wa Afrika.


Na. Immaculate Makilika – MAELEZO
Serikali ya Tanzania imepewa tuzo 2 za masuala ya Ustawi wa Jamii pamoja na ushirikishwaji wa wanawake katika ngazi ya maamuzi ya Serikali na Taasisi mbalimbali katika Mkutano wa 27 wa Umoja wa Nchi za Afrika (AU) uliofanyika hivi karibuni Kigali nchini Rwanda.
Hayo yamesemwa leo jijini Dar es salaam na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi, Augustine Mahiga, wakati alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari kuhusu mambo yaliyojadiliwa katika mkutano wa 27 wa Umoja wa nchi za Afrika uliofanyika hivi karibuni Kigali nchini Rwanda.
“Tanzania imetambuliwa na AU kama nchi ambayo kwa miaka 15 sasa imekua na mikakati mbalimbali ya kitaifa ya kuzingatia haki za wanawake na kutimiza malengo ya Milenia,” alisema Balozi Mahiga
Aliongeza kuwa Tanzania ni kati ya nchi tano bora katika bara la Afrika ambazo zimepewa tuzo hizo.
Katika hatua nyingine, Balozi Mahiga amasema kuwa katika mkutano huo wa 27 viongozi wa Afrika walizungumzia mambo mbalimbali ikiwemo hati ya kusafiria Afrika (passport), ambayo itawezesha watu wa bara hilo kusafiri katika nchi zote za Afrika.
Balozi Mahiga aliongeza kuwa, lengo la kuanza kutumia hati hiyo ya kusafiria kwa nchi za Afrika ni kutoa vikwazo vilivyokuwepo wakati wa kutembelea na kusafiri ndani ya nchi hizo.
Aidha, Balozi Maiga amesema kwamba, kutolewa kwa hati ya kusafiria ya Afrika ni ishara ya Umoja na mshikamano, hati hizo zimeanza kutolewa kwa marais na viongozi wa Serikali wa nchi ambazo zilihudhuria mkutano huo. Hati hizo zitatumika kwa kuzingatia sheria za kila nchi.
Hali kadhalika, mkutano huo ulijadili migogoro ya nchi za Burundi na Sudani Kusini ambapo viongozi hao walikubaliana kupeleka Jeshi la Umoja wa Afrika nchini Sudani Kusini ili kutenganisha majeshi ya pande mbili zinazoendelea kupigana nchini humo.
Aidha, mgogoro wa Burundi bado unaendelea kupatiwa ufumbuzi kutokana na jitihada mbalimbali zinazoendelea kufanywa na Rais Mstaafu Benjamin Mkapa, ambaye aliteuliwa na mapema mwaka huu na viongozi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.
Mkutano wa 27 wa Umoja wa nchi za Afrika wenye wanachama 54 ulifanyika Kigali nchini Rwanda tarehe 18 mwezi huu, ukiwa ni mkutano wa pili kwa mwaka huu ulikua na kauli mbiu inayosema mwaka wa haki za binadamu.

Sunday, July 17, 2016

NEPAD yahimiza Viwanda Barani Afrika

Kikao cha NEPAD kikiendelea
Dkt. Ibrahim Mayaki, Mkurugenzi Mtendaji wa Mpango wa Maendeleo Afrika 


TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

NEPAD yahimiza uanzishwaji wa Viwanda ili kukwamua uchumi wa Bara la Afrika
KIGALI, Rwanda

Afrika inahitaji juhudi za pamoja ili kukuza sekta ya viwanda ambayo itasaidia kwa kiasi kubwa kunyanyua uchumi wa bara la Afrika na hatimaye kupunguza umaskini na kuleta maisha bora.

Hayo yamesemwa na Mtendaji Mkuu wa NEPAD, chombo cha utendaji cha Umoja wa Afrika, Dkt. Ibrahim Mayaki wakati wa Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Nchi za Umoja wa Afrika zilizopo kwenye mpango huo wa maendeleo barani Afrika.

Kwenye upande wa ajira na viwanda kwa mfano, Dkt. Miyaki alisema kuwa bara la Afrika kwa sasa ndilo lenye vijana wengi kuzidi mabara mengine duniani hivyo kuna nguvu kazi kubwa ambayo isipotafutiwa mpango mahsusi wa ajira kutazidisha umasikini barani humo. Viwanda vya Afrika vikiongezeka, ajira kwa vijana zitapatikana, uzalishaji utaongezeka na biashara ndani ya Afrika itashamiri.

“Changamoto kubwa barani Afrika ni biashara, ambapo nchi haziuziani bidhaa zake, miundombinu hafifu na umasikini uliokihiri” alisema na kuongeza kuwa wakati muafaka umefika kwa Afrika kuweka mikakati endelevu ya pamoja baina ya nchi za Kiafrika ili kuhakikisha changamoto hizi zinatafutiwa ufumbuzi.

Wakati wa ufunguzi wa mkutano huo wa Mpango wa Maendeleo Afrika (NEPAD) uliofanyika pembezoni mwa Mkutano wa Umoja wa Afrika Jijini Kigali Rwanda, wajumbe walielezwa kuwa biashara ina nafasi kubwa ya kuchochea ukuaji wa uchumi wa viwanda barani Afrika iwapo misingi imara ya kuendeleza biashara na viwanda itazingatiwa.

Akizungumzia hali halisi nchini Tanzania, Mhe. Augustine Mahiga, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki ambaye alimwakilisha Mhe. Rais Magufuli kwenye mkutano huo, alisema “NEPAD pia wametambua kwamba biashara ya ndani barani Afrika inaendelea kuwa na jukumu kubwa katika ukuaji wa uchumi na viwanda vya nchi zetu za Kiafrika”.

Hivi karibuni Waziri Mahia alitangaza Bungeni kuwa Wizara yake sasa inaweka mikakati madhubuti kwa ajili ya utekelezaji wa Sera ya Mambo ya Nje yenye muelekeo wa uchumi wa viwanda (Economic Diplomacy of Industrialization) ambao utazingatia dhamira ya Serikali ya Tanzania kunyanyua sekta ya viwanda.

“Nimewaelekeza wasaidizi wangu wamualike maalamu wa Kamisheni ya Uchumi ya Umoja wa Mataifa ili aje kutuelezea umuhimu wa agenda hii ya biashara na uchumi wa viwanda nchini kwetu” alisema Waziri Mahiga.

Alimalizia kuwa “ili utekelezaji wa mkakati wa Diplomasia ya Uchumi wa Viwanda ufanikiwe, ni muhimu Serikali nzima na nchi kwa ujumla kuwa thabiti kwenye kutekeleza sera za viwanda na za uchumi na kuzingatia misingi ya kufanya biashara iliyoelezwa hapa na wataalamu”.

Akielezea umuhimu wa Afrika kukuza viwanda kwa ajili ya kujikwamua kiuchumi, Katibu Mtendaji wa Kamisheni ya Uchumi ya Umoja wa Mataifa Dkt. Carlos Lopez alisema kuwa japokuwa Afrika imechelewa kufanya mapiduzi ya viwanda ikilinganishwa na yale ya Ulaya miaka 200 iliyopita, bado Afrika ina nafasi kubwa ya kunyanyua uchumi wake kupitia viwanda na biashara ya ndani baina ya nchi zake.

Kilele cha Mkutano wa 27 wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika unatarajiwa kufunguliwa tarehe 17-18 Julai ambapo Wakuu hao wanatarajiwa  kupitisha ajenda kadhaa ikiwemo uchaguzi wa Kamishna na Kauli Mbiu ya mwaka huu ambayo ni Haki za Binadamu, Haki za Wanawake.   

Mwisho.

Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje, Ushirikiano wa Afrika Mashariki


 17 Julai 2016.

Friday, July 15, 2016

Kikao cha 39 cha Baraza la Mawaziri wa Umoja wa Afrika pichani

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Dkt. Augustine Mahiga (Mb.) mwenye miwani mbele, akijadiliana jambo na Mkurugenzi wa Idaya Afrika Balozi Samweli Shelukindo katika Mkutano wa 29 wa Umoja wa Afrika, Mkutano huo umewakutanisha Mawaziri wa Mambo ya Nje kutoka nchi 54 Mkutano huo umefanyika nchini Rwanda. 
Waziri Mahiga akifuatilia Mkutano uliokuwa ukiendelea, nyuma kulia ni Balozi Shelukindo na  Balozi Naimi Azizi nao wakiwa katika kikao hicho.

Sehemu ya Baraza la Mawaziri wa Umoja wa Afrika 

Kikao cha 39 cha Baraza la Mawaziri wa Umoja wa Afrika



Waziri Mahiga ahudhuria Kikao cha 29 cha Baraza la Mawaziri wa Umoja wa Afrika

KIGALI, Rwanda

Kikao cha 29 cha Baraza la Mawaziri wa Nchi 54 zinazounda Umoja wa Afrika kimekamilika Jijini Rwanda leo huku mawaziri hao wa mambo ya nje wakisisitiza amani na usalama na utekelezaji wa haraka wa maamuzi yenye lengo la kuleta maendeleo ya kiuchumi na kunyanyua maisha ya wananchi barani Afrika.

Akifugua kikao hicho, Mwenyekiti wa Kamisheni ya Umoja wa Afrika Mhe. Dkt. Nkosozana Dlamini Zuma amesema kuna umuhimu wa kuhakikisha Afrika iko salama na ina amani baina yake na wananchi wake,  ili kufikia malengo ya kijikwamua kiuchumi barani Afrika. Aliwaasa Mawaziri hao kusimamia kikamilifu na kuharakisha utekelezaji wa maazimio mbalimbali yanayowekwa na chombo hicho muhimu kwa Afrika ili kuharakisha maendeleo ya Afrika.

Alielezea umuhimu wa kuharakisha utatuzi wa migogoro sugu barani Afrika ambayo sio tu inahatarisha usalama wa raia wa maeneo hayo, lakini pia husababisha raia hao kupoteza makazi yao ya kudumu na kukimbilia nchi nyingine, tatizo ambalo linarudisha nyuma maendeleo ya bara la Afrika.

Alikemea mgogoro unaoendelea Sudani Kusini na kukumbusha Mawaziri hao ahadi ya Umoja wa Afrika iliyowekwa na nchi wanachama wakati wakiadhimisha miaka 50 ya umoja huo ya kunyamazisha bunduki ifikapo mwaka 2020.

“Waheshimiwa Mawaziri, unawajibu wa kuweka dhamira ya dhati ili ku timiza ahadi hiyo kwa Waafrika na kwa vizazi vijavyo barani mwetu“ alisema. gt5“

Dkt. Zuma akiwa na mwenyeji wa Kikao hicho cha mawaziri, Mhe. Louise Mushekiwabo, Waziri wa Mambo ya Nje wa Rwanda kwa pamoja walihimiza suala la ulinzi na usalama barani Afrika lina umuhimu wa kipekee na ndio maana kauli mbiu ya Mkutano Mkuu wa 27 wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika nchini Rwanda imejijkia kwenye haki za binadamu hususan haki za wanawake.

“Tutumie kauli mbiu hii kama chachu ya kukataa kabisa migogoro barani kwetu, na pale inapoanza tuwahi kuitafutia ufumbuzi kabla haijaeuka kuwa vita“ alisema Kamishna Zuma kwa kumalizia.

Akitoa maoni yake kuhusu msisitizo wa amani na usalama kwenye kikao hicho cha siku mbili, Mhe. Augustine Mahiga, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki na Mwenyekiti Baraza la Mawaziri wa Afrika Mashariki  alielezea kuwa Serikali ya Tanzania inafuatilia kwa karibu amri ya kusitisha mapigano iliyotolewa na viongozi wakuu wawili wa Sudani ya Kusini, yaani Rais Salva Kiir na makamu wake. Alisema ni hatua muhimu ya kuhakikisha usalama wa raia na kuleta amani ya kudumu nchini humo.

Kikao cha Baraza la Mawaziri wa Umoja wa Afrika kilitanguliwa na Kikao cha Mabalozi wanaowakilisha nchi zao kwenye makao makuu ya UA nchini Ethiopia. Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali unatarajiwa kuanza tarehe 17-18 Julai, ambapo Mhe. Samia Suluhu Hassan, Makamu wa Rais atamwakilisha Mhe. Dkt. John Pombe Joseph Maufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje, Ushirikiano wa Afrika Mashariki

 15 Julai 2016.

Tuesday, July 12, 2016

Balozi wa Tanzania nchini Kuwait akutana na Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Maendeleo wa nchi hiyo

Balozi wa Tanzania nchini Kuwait, Mhe. Dkt. Mahdhi Juma Maalim akiwa katika picha ya pamoja na Bw. Abdulwahab Al-Bader, Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Maendeleo wa Kuwait-Kuwait Fund for Arab Economic Development (KFAED). Mhe. Dkt. Maalim alikutana na kufanya mazungumzo na Bw. Al-Bader ambapo walijadili masuala muhimu katika kuharakisha utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maedneleo ambayo inasubiri ufadhili wa mfuko huo. Aidha, Balozi Maalim alisifu mchango mkubwa wa KFAED katika kufanikisha miradi mbalimbali ya maendeleo nchini Tanzania na kumwahidi  Mkurugenzi huyo kuendelea kutoa ushirikiano wa kutosha katika juhudi za kuimarisha zaidi mahusiano kati ya Tanzania na Kuwait hususan KFAED.
Balozi Dkt. Maalim akiwa na Mkurugenzi Mkuu, Bw. Al-Bader pamoja na baadhi ya Maafisa wa KFAED.

Waziri Mahiga apokea msaada wa madawati 105 kutoka Jumuiya ya Mabohora nchini

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Dkt. Augustine Mahiga (Mb.), akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kumaliza zoezi la makabidhiano ya madawati kutoka Jumuiya ya Mabohora iliyopo hapa nchini, jumuiya hiyo imechangia jumla ya madawati 105 yenye thamani ya shilingi milioni kumi. Hii ni katika kuiunga  mkono Serikali kwenye zoezi la kuchangia madawati nchi nzima lililo tangazwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli, Madawati hayo yametengenezwa hapa nchini na Kampuni ya Jambo. Tukio hilo lilifanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Julius Nyerere uliopo jijini Dar es Salaam.
Makamu Mwenyekiti wa Jumuiya ya Mabohora, Mhe. Shehe Zainuddin Adamjee naye akizungumza na waandishi wa habari kwenye makabidhiano ya madawati.
Sehemu ya Waandishi wa Habari wakisikiliza kwa makini Waziri Mahiga (hayupo pichani)
Sehemu ya wawakilishi wa Jumuiya hiyo wakimsikiliza kwa makini Mhe. Waziri Mahiga
Waziri Mahiga akiwaonyesha waandishi wa habari moja ya dawati kati ya yaliyotolewa na Jumuiya ya Mabohora. Wizara itakabidhi madawati hayo kwa Mamlaka husika  kwa ajili ya kusambazwa.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Dkt. Augustine Mahiga (Mb.) akiwa na Viongozi Wakuu wa Jumuiya ya Mabohora nchini, Mhe. Shekh Tayabali Hamzabhai ( (kushoto) na Shekh Zainuddin Adamjee, Makamu Mwenyekiti (kulia) wakati wa hafla fupi ya kukabidhi madawati.

Sunday, July 10, 2016

Rais Dkt. John Pombe Magufuli ampokea Waziri Mkuu wa India

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Dkt. John Pombe Magufuli akimpokea Waziri Mkuu wa India Mhe.  Narendra Modi mara baada ya kuwasili katika Viwanja vya Ikulu Jiji Dar es Salaam. Mhe. Modi yupo nchini kwa ziara ya kikazi ya siku mbili inayotarajiwa kumalizika leo.


Waziri Mkuu wa India Mhe. Modi akikabidhiwa maua na mtoto Elizabeth Jackson mara baada ya kupokelewa na Rais Dkt. John Pombe Magufuli.
Rais Dkt. John Pombe Magufuli akiwa amesimama na Mgeni wake, Waziri Mkuu wa India Mhe. Modi wakati nyimbo za Taifa zikipigwa mara baada ya kuwasili katika viwanja vya Ikulu.
Mhe. Modi akikagua gwaride la heshima mara baada ya kumalizika kupigwa nyimbo za Taifa.
Waziri Mkuu wa India Mhe. Narendra Modi akisalimiana na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Mama Samia Suluhu Hassan mara baada ya kuwasili katika viwanja vya Ikulu Jijini Dar es Salaam.
Rais Dkt. John Pombe Magufuli na Mgeni wake Mhe. Modi wakipunga mkono kuwasalimia wananchi waliojitokeza kumlaki mgeni katika viwanja vya Ikulu Jijini Dar es Salaam.
Rais Magufuli na mgeni wake Mhe. Modi wakipiga ngoma kuashiria furaha, mshikamano na ushirikiano wa kihistoria uliopo baina ya mataifa yao.
Rais Mhe. Dkt John Pombe Magufuli akiongoza kikao kilichofanyika Ikulu Jijini Dar es Salaam akiwa pamoja na mgeni wake Waziri Mkuu wa India na viongozi waandamizi wa Serikali za pande zote mbili. 
Waziri Mkuu wa India Mhe. Modi akiongea katika Kikao na Waandishi wa habari ambapo alieleza umuhimu wa kuimarisha ushirikiano uliopo baina ya Tanzania na India na pia aliahidi Serikali yake itaendelea kutoa ushirikiano katika sekta ya Afya, Elimu, Maji na Teknolojia ya Habari, pamoja na kuzidi kuibua maeneo mapya ya ushirikiano. 
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dktr. John Pombe Magufuli akiongea katika kikao na Waandishi wa Habari, ambapo alisema Serikali ya Tanzania itazidi kuimarisha ushirikiano na Serikali ya India hasa katika masuala ya kiuchumi ili kuweza kuboresha maisha ya wananchi wa mataifa yao.
Rais Dkt. John Pombe Magufuli akiwa na Mhe. Modi mara baada ya kumaliza vikao na mazungumzo yaliyofanyika Ikulu Jijini Dar es Salaam.


TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI


Ziara ya Waziri Mkuu wa India nchini Tanzania


Serikali ya India imeahidi kuipatia Tanzania msaada wa Dola za Marekani milioni 500 kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mbalimbali ya kipaumbele ili kuunga mkono juhudi za Serikali ya awamu ya tano ya kuifanya Tanzania kuwa nchi ya viwanda ifikapo mwaka 2020. 

Hayo yameelezwa leo Ikulu jijini Dar es Salaam na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Joseph Magufuli mara baaada ya kufanya mazungumzo na mgeni wake, Waziri Mkuu wa India, Mhe. Narendra Modi. Mhe. Modi aliwasili nchini jana kwa ziara ya Kitaifa ya Siku mbili.


Rais Magufuli alieleza kuwa Tanzania na India zina uhusiano mzuri wa kihistoria ambao umekuwa na faida za kijamii na kiuchumi kwa pande zote mbili. Alitoa mfano namna India ilivyofadhili ukarabati na upanuzi wa miundombinu ya maji katika mikoa ya Dar es Salaam na Pwani kwa gharama ya Dola za Marekani milioni 178. 

Aidha, Rais Magufuli aliishukuru Serikali ya India kwa kuridhia kutoa kiasi kingine cha Dola za Marekani milioni 92 kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu ya maji kisiwani Zanzibar.  Rais Magufuli alielezea pia kuridhishwa na kiwango cha biashara kati ya Tanzania na India ambacho kimekuwa kikiongezeka mwaka hadi mwaka.

 Alisema kwa mwaka 2009, Tanzania iliiuzia India bidhaa zenye thamani ya Dola za Marekani milioni 187, kiwango hicho kimeongezeka na kufikia Dola za Marekani bilioni 1.29 mwaka 2015.


Viongozi hao wakiwa katika mazungumzo rasmi, walikubaliana kushirikiana katika sekta mbalimbali zikiwemo za kilimo, viwanda, afya, nishati na madini.


Kwa upande wa Kilimo, Rais Magufuli alitoa wito kwa wakulima wa Kitanzania kuongeza uzalishaji wa mazao ya jamii ya kunde hususan dengu kwa kuwa yana soko kubwa nchini India. Alisema India ni soko kubwa la  mazao hayo na imeahidi kusaidia pembejeo za kilimo ili kuongeza kiwango cha uzalishaji.


Kwa upande wa viwanda, mashirika ya viwanda vidogo ya India na Tanzania yamewekeana saini mkataba ambapo mashirika hayo yatafanya tathmini nchi nzima ya kubaini rasilimali zilizopo katika maeneo mbalimbali na aina ya viwanda vidogo vinavyoweza kuanzishwa kwenye maeneo hayo. Baada ya tathmini hiyo, Serikali ya India itatoa mkopo nafuu kwa ajili ya kujenga antamizi (incubators) za viwanda vidogo nchi nzima. Kupitia antamizi hizo, wananchi watapatiwa mafunzo maalum ya uzalishaji wa bidhaa, biashara na usimamizi wa fedha na baadaye kupewa mitaji kwa ajili ya kuanza shughuli za biashara.


Kwa upande wa sekta ya Afya, Rais Magufuli alimuomba Waziri Mkuu wa India kushawishi wawekezaji kuja kuwekeza nchini katika uzalishaji wa dawa za binadamu na vifaa tiba. “Nimemuomba Mhe. Modi na amekubali kuleta wawekezaji kuzalisha madawa na vifaa tiba hapa nchini. Hiyo itaipunguzia Serikali mzigo mkubwa wa matumizi ya fedha za kigeni kutokana na uagizaji wa bidhaa hizo kutoka nje ya nchi. 

Sambamba na hilo, Rais Magufuli ameshukuru Serikali ya India kwa kuipatia Hospitali ya Bugando mashine maalum kwa ajili ya kupima ugonjwa saratani. Mashine hiyo inatarajiwa kuwasili nchini wakati wowote kuanzia sasa.


Kuhusu sekta ya nishati na madini, viongozi hao walikubaliana kushirikiana katika kuendeleza sekta hiyo hapa nchini. Tanzania ina utajiri mkubwa wa gesi asilia  ikiwemo Helium na madini. Hivyo ni vizuri tukishirikiana na wenzetu kuendeleza sekta hiyo.  


Rais Magufuli alihitimisha taarifa yake kwa kueleza kuwa wameazimia kushirikiana na India katika ngazi za kitaifa, kikanda na kimataifa kuhakikisha kuwa pamoja na mambo mengine, mabadiliko ya mfumo katika Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa yanafanyika ili liwe na uwiano mzuri wa uwakilishi. Aidha, wameahidi kusaidiana katika kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi ambayo ni tishio kubwa kwa maendeleo endelevu ya dunia ya sasa.


Waziri Mkuu wa India alikuwa katika ziara yake ya pili barani Afrika tangu kuchaguliwa kwake mwaka 2014 ambapo alitembelea nchi za Msumbiji, Afrika Kusini, Tanzania na atahitimisha ziara yake nchini Kenya.  


Imetolewa na:

Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,

Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki

Dar es Salaam, 10 Julai 2016.