Friday, July 15, 2016

Kikao cha 39 cha Baraza la Mawaziri wa Umoja wa Afrika



Waziri Mahiga ahudhuria Kikao cha 29 cha Baraza la Mawaziri wa Umoja wa Afrika

KIGALI, Rwanda

Kikao cha 29 cha Baraza la Mawaziri wa Nchi 54 zinazounda Umoja wa Afrika kimekamilika Jijini Rwanda leo huku mawaziri hao wa mambo ya nje wakisisitiza amani na usalama na utekelezaji wa haraka wa maamuzi yenye lengo la kuleta maendeleo ya kiuchumi na kunyanyua maisha ya wananchi barani Afrika.

Akifugua kikao hicho, Mwenyekiti wa Kamisheni ya Umoja wa Afrika Mhe. Dkt. Nkosozana Dlamini Zuma amesema kuna umuhimu wa kuhakikisha Afrika iko salama na ina amani baina yake na wananchi wake,  ili kufikia malengo ya kijikwamua kiuchumi barani Afrika. Aliwaasa Mawaziri hao kusimamia kikamilifu na kuharakisha utekelezaji wa maazimio mbalimbali yanayowekwa na chombo hicho muhimu kwa Afrika ili kuharakisha maendeleo ya Afrika.

Alielezea umuhimu wa kuharakisha utatuzi wa migogoro sugu barani Afrika ambayo sio tu inahatarisha usalama wa raia wa maeneo hayo, lakini pia husababisha raia hao kupoteza makazi yao ya kudumu na kukimbilia nchi nyingine, tatizo ambalo linarudisha nyuma maendeleo ya bara la Afrika.

Alikemea mgogoro unaoendelea Sudani Kusini na kukumbusha Mawaziri hao ahadi ya Umoja wa Afrika iliyowekwa na nchi wanachama wakati wakiadhimisha miaka 50 ya umoja huo ya kunyamazisha bunduki ifikapo mwaka 2020.

“Waheshimiwa Mawaziri, unawajibu wa kuweka dhamira ya dhati ili ku timiza ahadi hiyo kwa Waafrika na kwa vizazi vijavyo barani mwetu“ alisema. gt5“

Dkt. Zuma akiwa na mwenyeji wa Kikao hicho cha mawaziri, Mhe. Louise Mushekiwabo, Waziri wa Mambo ya Nje wa Rwanda kwa pamoja walihimiza suala la ulinzi na usalama barani Afrika lina umuhimu wa kipekee na ndio maana kauli mbiu ya Mkutano Mkuu wa 27 wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika nchini Rwanda imejijkia kwenye haki za binadamu hususan haki za wanawake.

“Tutumie kauli mbiu hii kama chachu ya kukataa kabisa migogoro barani kwetu, na pale inapoanza tuwahi kuitafutia ufumbuzi kabla haijaeuka kuwa vita“ alisema Kamishna Zuma kwa kumalizia.

Akitoa maoni yake kuhusu msisitizo wa amani na usalama kwenye kikao hicho cha siku mbili, Mhe. Augustine Mahiga, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki na Mwenyekiti Baraza la Mawaziri wa Afrika Mashariki  alielezea kuwa Serikali ya Tanzania inafuatilia kwa karibu amri ya kusitisha mapigano iliyotolewa na viongozi wakuu wawili wa Sudani ya Kusini, yaani Rais Salva Kiir na makamu wake. Alisema ni hatua muhimu ya kuhakikisha usalama wa raia na kuleta amani ya kudumu nchini humo.

Kikao cha Baraza la Mawaziri wa Umoja wa Afrika kilitanguliwa na Kikao cha Mabalozi wanaowakilisha nchi zao kwenye makao makuu ya UA nchini Ethiopia. Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali unatarajiwa kuanza tarehe 17-18 Julai, ambapo Mhe. Samia Suluhu Hassan, Makamu wa Rais atamwakilisha Mhe. Dkt. John Pombe Joseph Maufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje, Ushirikiano wa Afrika Mashariki

 15 Julai 2016.

No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.