Saturday, February 10, 2024

WANANCHI TOENI MAONI KWA AJILI YA SERA YENYE TIJA, WAZIRI


Makongamano ya wadau yanayoendelea nchini kuhusu marekebisho ya Sera ya Mambo ya Nje ya Mwaka 2001 yanalenga kukusanya maoni yatakayosaidia kutengeneza Sera ya Mambo ya Nje Bora itakayoongoza ushirikiano wenye tija baina ya Tanzania na nchi nyingine, mashirika ya kikanda na kimataifa.

Hayo yamesemwa leo tarehe 10 Februari 2024 na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Ikulu - Zamzibar, Mhe. Ali Suleiman Ameir wakati akisoma hotuba ya ufunguzi ya Kongamano la nne la wadau lililofanyika kisiwani Pemba.

Makongamano hayo yanayoratibiwa kwa ushirikiano baina ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Ofisi ya Rais-Zanzibar na Taasisi ya Uongozi yametajwa kuwa ni kielelezo cha utawala bora ambao unahimiza ushirikishwaji wa wananchi katika utengenezaji wa Sera za Taifa.

Akizungumza katika kongamano hilo, Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk (Mb) amesisitiza umuhimu wa wananchi walioshiriki kongamano hilo kutoa maoni yao kwa uhuru bila woga. Alisema maoni yao yatasaidia kutengeneza Sera ya Mambo ya Nje madhubuti itakayoifanya Tanzania kutetea maslahi yake katika majukwaa ya Kimataifa na kukabiliana na changamoto zinazojitokeza katika dunia ya sasa.

Alisema mijadala yao ya kurekebisha Sera ya Mambo ya Nje itatoa mwelekeo wa kuboresha maeneo mapya yanayopendekezwa ambayo ni pamoja na masuala ya uchumi wa Buluu, diaspora, mabadiliko ya tabianchi, kubidhaisha Lugha ya Kiswahili na kulinda mila na desturi za Tanzania.

Balozi Mbarouk alimsifu Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa utekelezaji mzuri wa Sera ya Mambo ya Nje ambao umesaidia kuongezeka kwa ajira za Watanzania katika mashirika ya kikanda na Kimataifa, masoko ya bidhaa za Tanzania Nje ya nchi, misaada na mikopo ya Maendeleo, uenyeji wa taasisi za kimataifa nchini na ujenzi wa miradi ya Maendeleo katika sekta mbalimbali za miundombinu, nishati, kilimo, elimu na afya.

Kongamano hilo ambalo ni mwendelezo wa makongamano yaliyofanyika Arusha, Dar Es Salaam na Unguja limehudhuriwa na viongozi mbalimbali wakiwemo Mkuu wa Mkoa wa Kusini-Pemba, Mhe. Matar Zahor Masoud; Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais-Zanzibar, Bw. Salehe Juma Mussa, Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Said Shwaibu Mussa; baadhi ya Mabalozi wa Tanzania nje ya nchi; wawakilishi wa vyama vya siasa; asasi za kiraia; jumuiya za kidini na wananchi kwa ujumla.


Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Ikulu-Zanzibar, Mhe.  Ali Suleiman Ameir akitoa hotuba ya ufunguzi ya Kongamano la Wadau kuhusu kukusanya maoni ya marekebisho ya Sera Mpya ya Mambo ya Nje ya Mwaka 2001 lililofanyika Pemba tarehe 10 Februari 2024

 Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk (Mb) akizungumza na wadau walioshiriki katika kongamano la kutoa maoni kuhusu marekebisho ya Sera Mpya ya Mambo ya Nje ya Mwaka 2001 lililofanyika Pemba tarehe 10 Februari 2024

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Ikulu - Zanzibar, Mhe. Ali Suleiman Ameir akisalimiana na na baadhi ya viongozi wa Serikali na wajumbe walioshiriki Kongamano la kukusanya maoni kuhusu marekebisho ya Sera ya Mambo ya Nje ya Mwaka 2001 lililofanyika Pemba tarehe 10 Februari 2024

Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais-Ikulu Zanzibar, Bw. Salehe Juma Mussa akitoa neno wakati wa Kongamano la Wadau kuhusu kukusanya maoni ya marekebisho ya Sera Mpya ya Mambo ya Nje ya Mwaka 2001 lililofanyika Pemba tarehe 10 Februari 2024
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Ikulu - Zanzibar, Mhe. Ali Suleiman Ameir (kulia) na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk (Mb) ambao walikuwa wenyeviti wenza katika Kongamano la kukusanya maoni kuhusu marekebisho ya Sera ya Mambo ya Nje ya Mwaka 2001 lililofanyika Pemba tarehe 10 Februari 2024

Kongamano la kukusanya maoni kuhusu marekebisho ya Sera ya Mambo ya Nje ya Mwaka 2001 lililofanyika Pemba tarehe 10 Februari 2024 likiendelea.

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk (Mb) akisalimiana na baadhi ya viongozi wa Serikali na wajumbe walioshiriki Kongamano la kukusanya maoni kuhusu marekebisho ya Sera ya Mambo ya Nje ya Mwaka 2001 lililofanyika Pemba tarehe 10 Februari 2024

Friday, February 9, 2024

RAIS WA POLAND ATEMBELEA HOSPITALI YA AGHAKHAN

 

Rais wa Jamhuri ya Poland Mheshimiwa Andrzej Duda akizungumza bada ya kutembelea mradi wa matibabu ya dharura unaoendeshwa katika hospitali ya Aghakhan jijini Dar es Salaam ili kujionea utekelezaji wa mradi huo.

Rais wa Jamhuri ya Poland Mheshimiwa Andrzej Duda (mwenye tai nyekundu) na Mke wake Bibi Agata Kornhouser-Duda (kushoto) walipotembelea mradi wa matibabu ya dharura unaoendeshwa katika hospitali ya Aghakhan jijini Dar es Salaam ili kujionea utekelezaji wa mradi huo.


Mke wa Rais wa Poland  Bibi Agata Kornhouser-Duda akizungumza kitu walipotembelea mradi wa matibabu ya dharura unaoendeshwa katika hospitali ya Aghakhan jijini Dar es Salaam ili kujionea utekelezaji wa mradi huo




 

 

Rais wa Jamhuri ya Poland Mheshimiwa Andrzej Duda na Mke wake Agata Kornhouser-Duda wametembelea mradi wa matibabu ya dharura unaoendeshwa katika hospitali ya Aghakhan jijini Dar es Salaam ili kujionea utekelezaji wa mradi huo.

Kupitia Mradi huo Serikali ya Poland imetoa msaada wa Dola za Marekani 1,136,703 kwa ajili ya kusaidia utekelezaji wa mradi huo unaolenga kutoa msaada kwa sekta ya matibabu na kusaidia elimu ya wahudumu wa afya katika mkoa wa Dar es Salaam.

Poland pia inafadhili miradi kama hiyo katika Hospitali za Temeke, Mwananyamala, kituo cha Afya Chamazi na Hospitali ya Wilaya ya Nyamagana ya mkoani Mwanza.

 

TANZANIA – POLAND KUENDELEA KUSHIRIKIANA KIUCHUMI

Rais wa Jamhuri ya Poland Mhe. Andrzej Duda akisalimia na mwenyeji wake Rais Samia Suluhu Hassan Ikulu jijini Dar es Salaam


Rais wa Jamhuri ya Poland Mhe. Andrzej Duda akisaini kitabu cha wageni alipowasili Ikulu jijini Dar es Salaam huku mwenyeji wake Rais Samia Suluhu Hassan akimuangalia

Rais wa Jamhuri ya Poland Mhe. Andrzej Duda akiwa Ikulu jijini Dar es Salaam

Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan akizungumza na waandishi wa Habari Ikulu jijini Dar es Salaam

Rais wa Jamhuri ya Poland Mhe. Andrzej Duda akizungumza na waandishi wa Habari Ikulu jijini Dar es Salaam

 Rais wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akiwa na Rais wa Jamhuri ya Poland Mhe. Andrzej Duda wakizungumza na waandishi wa Habari Ikulu jijini Dar es Salaamkuelezea waliyokubaliana kutekeleza baada ya mazungumzo yao



Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Jamhuri ya Poland zimekubaliana kuendeleza ushirikiano katika sekta za kimkakati ikiwemo elimu, kilimo, biashara na uwekezaji ili  kukuza uchumi kwa manufaa ya pande zote mbili.

Hayo yamebainishwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Poland, Mhe. Andrzej Duda walipozungumza na waandishi wa habari Ikulu, jijini Dar es Salaam.

Akizungumza katika mkutano huo,  Mhe. Rais Samia ameeleza kuwa Tanzania na Poland zimekuwa na ushirikiano mzuri kwa zaidi ya miaka 60 huku wakishirikiana kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo hususan katika sekta ya Afya.

“Poland inatusaidia katika sekta ya afya, kuna miradi mitano ambayo Poland inafadhili katika Hospitali za Agah Khan, Kituo cha afya cha Chanika, Hospitali ya Temeke, Mwananyamala na Hospitali ya wilaya ya Nyamagana,” alisema Mhe. Rais Samia

Amesema wamekubaliana na Poland kuendelea kushirikiana katika sekta za kimkakati za elimu, kilimo, nishati, madini, biashara, uwekezaji na utalii

 “Katika mazungumzo yetu tumeelekeza timu za pande zote mbili kukaa na kufanya majadiliano ya mara kwa mara ili kubaini maeneo mapya ya ushirikiano ambayo yatatusaidia kupiga hatua kwa haraka zaidi katika kukuza biashara na uwekezaji na utalii kwa manufaa ya watu wetu” Alisema Rais Samia.


Ameishukuru Poland kupitia Wakala wake wa Mikopo kwa kukubali kuipatia Tanzania mkopo utakawezesha ujenzi wa Reli ya Kisasa ya SGR ambapo itahusisha ujenzi wa Lot 3 na Lot 4.

Hii ni hatua kubwa sana katika kutekeleza miradi ya kimkakati ambao pia utasaidia kukuza ujuzi wa wataalam wetu, tunawashukuru sana  kwa kukubali kutupatia mkopo huo,” alisema Mhe. Rais Samia.

Amesema wamekubaliana kuendelea kushirikiana katika sekta za utalii, biashara na uwekezaji ili kuongeza idadi ya watalii wanaokuja Tanzania kutoka Poland pamoja na kuinua kiwango cha biashara na kuvutia wawaekezaji zaidi kutoka Poland.

Amesema wamekubaliana kuwa wataalam wao watazungumza na kukubaliana namna bora na kuanzisha usafiri wa moja kwa
moja kutoka Poland hadi Tanzania haÅŸa ikizingatiwa kuwa kuna idadi kubwa ya watalii kutoka Poland wanaokuja nchini.

“Kumekuwa na ongezeko la watalii ambapo kwa mwaka 2023 tulipokea watalii 41,000 na kwa mwezi mmoja tu uliopita tulipokea watalii 6,000 walioenda visiwani Zanzibar kutalii,” alisema.

Amesema amewakaribisha wawekezaji kutoka Poland waje Tanzania kwani fursa za uwekezaji ni nyingi.

Naye Rais Duda akizungumza katika mkutano huo ameishukuru Tanzania kwa kuendelea kushirikiana na Poland kitendo ambacho kilianza tangu wakati wa vita ya pili ya ambapo Tanzania iliwapokea raia wa Poland waliokuja Tanzania kutafuta Hifadhi wakati huo

Amewashukuru wananchi wa Arusha kwa kuendelea kuishi na   wananchi wa Poland na kuyaenzi makaburi ya watu hao.

Kadhalika amesisitiza kuwa, atahakikisha utalii, uwekezaji na biashara kati ya Tanzania na Poland unaongezeka kwani anajua Tanzania ni kituo kinachovutia na anaamini kuwa kuongezeka huko kutasaidia kutengeneza ajira kwa vijana, kuongeza ufanisi kwa kuleta mifumo ya kisasa ya kuendesha benki.

Ameahidi kuwa atahakikisha kampuni ya Poland ambazo zipo vizuri katika teknolojia ya mawasiliano zinakuja kwa wingi kuwekeza nchini.

“ Kwa kuanzia tutaanza na kampuni inayotengeneza Taa za nishati mbadala tutaangalia jinsi kampuni hiyo inakuja Tanzania kuwekeza,” alisema Mhe. Rais Duda.

RAIS WA POLAND APOKELEWA RASMI IKULU

 

 

 

 

 

Rais wa Jamhuri ya Poland Mhe. Andrzej Duda akisalimiana na mwenyeji wake Rais Dkt. Samia Suluhu Hassa alipowasili Ikulu jijini Dar es Salaam na kupokelewa rasmi 

 Mhe. Rais Duda alipowasili Ikulu jijini Dar es Salaam na kupokelewa na mwenyeji wake  Rais Samia Suluhu Hassan
 

Mheshimiwa Rais Andrzej Duda wa Poland akikagua gwaride la heshima katika hafla ya kumkaribisha Tanzania iliyofanywa na mwenyeji wake Rais wa Jamhuri ya  Muungano wa Tanzania,  Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Ikulu jijini Dar es Salaam leo tarehe 9 Februari, 2024.

Mheshimiwa Rais Andrzej Duda wa Poland akikagua gwaride la heshima katika hafla ya kumkaribisha Tanzania iliyofanywa na mwenyeji wake Rais wa Jamhuri ya  Muungano wa Tanzania,  Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Ikulu jijini Dar es Salaam leo tarehe 9 Februari, 2024.

Mheshimiwa Rais Andrzej Duda wa Poland akikagua gwaride la heshima katika hafla ya kumkaribisha Tanzania iliyofanywa na mwenyeji wake Rais wa Jamhuri ya  Muungano wa Tanzania,  Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Ikulu jijini Dar es Salaam leo tarehe 9 Februari, 2024.

Rais wa Jamhuri ya Poland Mhe. Andrzej Duda akipokea salamu za heshima na mwenyeji wake Rais Dkt. Samia Suluhu Hassa alipowasili Ikulu jijini Dar es Salaam na kupokelewa rasmi 

 
Baadhi ya viongozi mbalimbali wa serikali waliposhiriki mapokezi rasmi ya Rais wa Jamhuri ya Poland Mhe. Andrzej Duda aalipowasili Ikulu jijini Dar es Salaam na kupokelewa rasmi 

Rais wa Jamhuri ya Poland, Mheshimiwa Andrzej Duda amepokelewa rasmi Ikulu, jijini Dar es Salaam na mwenyeji wake Rais wa Jamhuri ya  Muungano wa Tanzania,  Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan

Alipowasili Ikulu Mhe. Rais Duda alipigiwa mizinga 21 na kukagua gwaride  lililoandaliwa maalum kwa heshima yake  kuungana na Mhe. Rais Samia katika mazungumzo ya  faragha
 

Mhe. Rais Duda yuko nchini kwa Ziara ya Kitaifa ya siku mbili na kuwa Rais wa kwanza wa Poland kufanya ziara ya Kitaifa Tanzania

 



DKT. SHELUKINDO AONGOZA UJUMBE WA TANZANIA KUSHIRIKI MKUTANO WA KAMATI YA SIASA NA DIPLOMASIA YA SADC

Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Dkt. Samwel Shelukindo ameongoza ujumbe wa Tanzania kushiriki Mkutano wa Kamati ya Siasa na Diplomasia (Inter-State Politics and Diplomacy Committee — ISPDC) ya SADC uliofanyika kwa njia ya mtandao tarehe 09 Februari, 2024.

Mkutano huo umeongozwa na Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa wa Jamhuri ya Zambia, Bi. Etambuyu Gundersen ambaye ni Mwenyekiti wa Kamati ya Makatibu Wakuu ya Asasi ya Siasa, Ulinzi na Usalama ya SADC.

Mkutano huo uliitishwa kujadili masuala ya kisiasa na diplomasia katika kanda. Aidha, Mkutano umetoa salamu za pole kwa Serikali na wananchi wa Jamhuri ya Namibia kufuatia kifo cha Hayati Dkt. Hage Geingob, Rais wa Jamhuri ya Namibia na Mwenyekiti aliyemaliza muda wake wa Asasi ya Siasa, Ulinzi na Usalama kilichotokea hivi karibuni.






RAIS WA POLAND AWASILI TANZANIA KWA ZIARA YA KITAIFA

 











Rais wa Jamhuri ya Poland, Mheshimiwa Andrzej Duda amewasili nchini kwa Ziara ya Kitaifa ya siku mbili.

Katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere Jijini Dar es Salaam Mhe. Rais Duda na mkewe Agata Kornhauser-Duda wamepokelewa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. January Makamba, Waziri wa Fedha Mhe. Mwigulu Nchemba, Waziri wa Utalii na Mambo ya Kale Zanzibar Mhe. Mudrick Soraga na viongozi wengine waandamizi wa Serikali.

Ziara hii ni ya kwanza kwa Rais kutoka Poland kutembelea Tanzania tangu kuanza kwa ushirikiano wa uwili kati ya nchi hizi ikilenga kuimarisha ushirikiano katika miradi mbalimbali ya maendeleo kwenye sekta za kilimo, kodi, viwanda na biashara, utalii, elimu, usafiri, afya, tiba za mifugo, na maji.

Kwa kupitia ziara hii maeneo mapya ya ushirikiano yataibuliwa kati ya Tanzania na Poland kupitia sekta za ulinzi na usalama, nishati, madini, ulinzi wa mitandao, utamaduni na uchumi wa buluu.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan atampokea rasmi Rais Duda Ikulu, Dar es salaam Februari 9, 2024 kwa mazungumzo na baadaye watazungumza na waandishi wa habari.

Akiwa nchini, Rais Duda anatarajiwa kutembelea mradi wa matibabu ya dharura katika Hospitali ya Aghakhan, Dar es Salaam kujionea utekelezaji wa mradi huo ambao Serikali ya Poland imetoa msaada wa Dola za Kimarekani milioni 1.136  kufadhili mradi huo wenye lengo la kutoa msaada kwa sekta ya matibabu na kusaidia elimu ya wahudumu wa afya katika mkoa wa Dar es Salaam.




Thursday, February 8, 2024

DKT. KIBESSE ATETA NA GAVANA WA KAUNTI YA KISUMU

Balozi wa Tanzania nchini Kenya, Mhe. Dkt. Bernard Kibesse amefanya ziara katika Kaunti ya Kisumu ambapo pamoja na mambo mengine, amekutana kwa mazungumzo na Gavana wa Kaunti ya Kisumu – Kenya, Mhe. Prof. Peter Nyon’go, tarehe 8 Februari 2024. 

 Balozi Kibese na Gavana Nyong’o wamekubaliana kuandaa mkutano wa ujirani mwema kati ya mikoa ya Tanzania na Kenya inayopakana kwenye eneo la Ziwa Victoria ili kuweka mikakati ya kuimarisha ushirikiano wa kijamii, kibishara na kiusalama katika maeneo hayo ikiwemo mikoa ya Mwanza na Mara kwa upande wa Tanzania na Kisumu na Migori kwa upande wa Kenya

Vilevile wamekubaliana kufuatilia mpango wa kuwa na miundombinu ya barabara inayopita kwenye mwambao wa Ziwa Victoria upande wa Tanzania na Kenya.

Gavana wa Kaunti ya Kisumu – Kenya, Mhe. Prof. Peter Nyon’go akizungumza na  Balozi wa Tanzania nchini Kenya, Mhe. Dkt. Bernard Kibesse (kushoto) alipomtembelea Ofisini kwake katika Kaunti ya Kisumu




WAZIRI MAKAMBA AKUTANA NA KATIBU WA NEC SIASA NA UHUSIANO WA KIMATAIFA WA CCM

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. January Makamba (Mb.) amekutana kwa mazungumzo na Katibu wa NEC Siasa na uhusiano wa kimataifa (SUKI), Ndugu Rabia Abdallah Hamid katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam.

Lengo la kikao cha viongozi hao ni kuangalia jinsi ambavyo Wizara inavyotekeleza Diplomasia ya Uchumi na uhusiano wa Kimataifa kupitia Ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM). 






Tuesday, February 6, 2024

WAZIRI MAKAMBA AKUTANA NA VIONGOZI WA TAASISI YA AMANI YA MARTI AHTISAARI.

 

 

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. January Makamba akizungumza na Balozi wa Finland nchini Mhe. Thereza Zitting walipokutana  katika Ofisi Ndogo za Wizara jijini Dar Es Salaam na kuzungumza na wawakilishi wa taasisi ya Amani ya Martti Ahtisaari.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. January Makamba akizungumza alipokutana na Balozi wa Finland nchini Mhe. Thereza Zitting na wawakilishi wa taasisi ya Amani ya Martti Ahtisaari (hawapo katika picha) walipokutana  katika Ofisi Ndogo za Wizara jijini Dar Es Salaam.


 Balozi wa Finland nchini Mhe. Thereza Zitting akizungumza katika kikao na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. January Makamba walipokutana  katika Ofisi Ndogo za Wizara jijini Dar Es Salaam na kuzungumza na wawakilishi wa taasisi ya Amani ya Martti Ahtisaari.

Mkuu wa Taasisi ya Marrti Ahtisaari Kanda ya Kusini mwa Jangwa la Sahara Bi. Tiina Kukkamaa-Bah akizungumza katika kilichofanyika katika Ofisi ndogo za wizara jijini Dar es Salaam kati ya taasisi hiyo na Waziri Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. January Makamba

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. January Makamba akizungumza katika na Balozi wa Finland nchini Mhe. Thereza Zitting  na wawakilishi wa taasisi ya Amani ya Martti Ahtisaari walipokutana  katika Ofisi Ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam



Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. January Makamba akizungumza katika picha ya pamoja na Balozi wa Finland nchini Mhe. Thereza Zitting  na wawakilishi wa taasisi ya Amani ya Martti Ahtisaari walipokutana  katika Ofisi Ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam


 


                
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. January Makamba amekutana na kuzungumza na viongozi wa taasisi ya Amani ya Martti Ahtisaari katika Ofisi Ndogo za Wizara jijini Dar Es Salaam.

Katika mazungumzo hayo viongozi hao wamekubaliana kuendelea kushirikiana na kufanya kazi pamoja ili kumuenzi na kuendeleza falsafa ya Mwanzilishi wa Taasisi hiyo na  Rais wa zamani wa Finland Haya Martti Ahtisaari katika kutafuta amani na kutatua migogoro duniani.

Akizungumza katika kikao hicho Mhe. Waziri Makamba amesema Tanzania iko tayari kushirikiana na taasisi hiyo ili kuendelea kuenzi azma ya hayati Martti Ahtasaari ya kutafuta amani na kutatua migogoro duniani.

“Tupo tayari kufanya kazi na taasisi yenu, tuko tayari kuandaa makubaliano rasmi kupitia Kituo cha Uhusiano cha Kimataifa. Pia, tuko tayari kuendelea kuwa marafiki wakubwa na kushiriki katika mashauriano kuhusu jinsi taasisi yenu itakavyoona inafaa, tunaweza kufuatilia jitihada za kutafuta amani katika eneo la ukanda wetu,” alisema Mhe. Waziri Makamba.

Balozi wa Finland nchini Mhe. Theresa Zitting  alisema Finland iko tayari kushirikiana na kufanya kazi na Tanzania kwa kuwa wanaona kuna nafasi Tanzania inaweza kushiriki katika kutafuta amani na usalama.

Naye Mkuu wa Taasisi ya Marrti Ahtisaari Kanda ya Kusini mwa Jangwa la Sahara Bi. Tiina Kukkamaa-Bah amesema Tanzania na viongozi wake walikuwa marafiki wazuri wa muasisi wa taasisi yao na kwa hali hiyo ndio maana wanapanga kushirikiana na Tanzania ili kuunga mkono jitihada za muanzilishi wao kutafuta amani na usalama katika eneo  la Kusini mwa jangwa la Sahara kupitia Ukanda wa Maziwa Makuu, SADC, Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Taasisi ya Martti Ahtisaari ni shirika lisilo la kiserikali la nchini Finland linalofanya kazi ya kuzuia na kutatua migogoro kupitia mazungumzo  na upatanishi, ilianzishwa mwaka 2000 na Rais wa zamani wa Finland na mshindi wa Tuzo ya Amani ya Nobel Hayati Martti Ahtisaari.

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI


 

Monday, February 5, 2024

USHAWISHI WA TANZANIA DUNIANI UTATEGEMEA NA UBORA WA SERA YA MAMBO YA NJE INAYOREKEBISHWA

    Imeelezwa kuwa ili Tanzania iweze kufikia malengo ya Maendeleo iliyojiwekea, lazima iwe na Sera Bora ya Mambo ya Nje inayozingatia maoni na matakwa ya makundi yote ya wadau nchini. 

Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-Ikulu Zanzibar, Mhe. Ali Suleiman Ameir ambaye alikuwa Mgeni Rasmi katika Kongamano la wadau la kukusanya maoni kuhusu marekebisho ya Sera Mpya ya Mambo ya Nje ya Mwaka 2001 lililofanyika kwenye Hoteli ya Golden Tulip mjini Zanzibar tarehe 05 Februari 2024. 

Kongamano hilo ambalo ni la tatu kufanyika ni utekelezaji wa maelekezo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kushirikisha wananchi kutoa maoni yatakayozingatiwa katika zoezi la kurekebisha Sera ya Mambo ya Nje ya Mwaka 2001. 

Mwenye dhamana ya kusimamia Sera hiyo, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. January Makamba (Mb) ametaja sababu za Wizara yake kuratibu makongamano hayo ambapo alisema linalofuata litafanyika Pemba tarehe 10 Februari 2024.

Alieleza kufanyika kwa makongamano hayo ni utekelezaji wa misingi ya utawala bora ambayo inasisitiza umuhimu wa kushirikisha wadau katika utungaji wa Sera za nchi, ikiwemo Sera ya Mambo ya Nje. 

Alieleza pia kuwa Sera ni Tamko linalotoa mwongozo namna nchi itakavyoshughulikia ushirikiano na uhusiano wake na dunia. Hivyo, utungaji wa Tamko muhimu kama hilo lazima lishirikishe wadau wote. 

Mhe. Makamba aliwambia washiriki wa Kongamano hilo kuwa Tanzania ina ushawishi mkubwa duniani tofauti na nguvu zake za kiuchumi na kijeshi kutokana na kuwa na Sera bora ya Mambo ya Nje. Hivyo, ili iendelee kuwa na ushawishi huo duniani lazima itungwe Sera imara itakayozingatia maoni ya wadau wote.

Aliendelea kueleza kuwa Sera ya Mambo ya Nje ina uhusiano wa moja kwa moja na malengo ya Maendeleo ya nchi. Hivyo, mchakato wa utungaji wa Sera ya Mambo ya Nje lazima ushirikishe wadau kwa kuwa maendeleo ni jambo linalomgusa kila mmoja. 

Alihitimisha hotuba yake kwa kutaja baadhi ya mambo yaliyosababisha Serikali kufanya marekebisho ya Sera hiyo. Mambo hayo ni pamoja na mabadiliko yanayotokea duniani kama mabadiliko ya tabianchi, uvumbuzi wa teknolojia mpya, kuibuka kwa wadau wapya wa maendeleo wenye nguvu na ushawishi na Watanzania wengi hawakuwepo wakati wa utungaji wa Sera Mpya ya Mambo ya Nje ya Mwaka 2001. 

Kongamano hilo limehudhuriwa na viongozi mbalimbali wakiwemo Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibi, Mhe. Idrisa Mustafa Kitwana: Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais-Ikulu Zanzibar, Bw. Salehe Juma Mussa, Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki (EAC), Balozi Stephen Mbundi, Naibu Katiibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Said Shaibu Mussa, Mabalozi wa Tanzania Nje ya Nchi, Mabolozi Wastaafu akiwemo Balozi Amina Salum Ali, viongozi wa Vyama vya Siasa, Asasi za Kiraia, Wakuu wa taasisi za Serikali na Sekta Binafsi, Wakuu wa Vyombo vya habari, wanazuoni na wananchi kwa ujumla. 

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Ikulu-Zanzibar, Mhe.  Ali Suleiman Ameir akitoa hotuba ya ufunguzi ya Kongamano la Wadau kuhusu kukusanya maoni ya marekebisho ya Sera Mpya ya Mambo ya Nje ya Mwaka 2001 lililofanyika Hoteli ya Golden Tulip mjini Zanzibar tarehe 05 Februari 2024
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. January Makamba (Mb) akitoa neno wakati wa ufunguzi wa Kongamano la Wadau kuhusu kukusanya maoni ya marekebisho ya Sera Mpya ya Mambo ya Nje ya Mwaka 2001 lililofanyika Hoteli ya Golden Tulip mjini Zanzibar tarehe 05 Februari 2024

Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais-Ikulu Zanzibar, Bw. Salehe Juma Mussa akitoa neno wakati wa 
Kongamano la Wadau kuhusu kukusanya maoni ya marekebisho ya Sera Mpya ya Mambo ya Nje ya Mwaka 2001 lililofanyika Hoteli ya Golden Tulip mjini Zanzibar tarehe 05 Februari 2024

Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Said Shaibu Mussa akimkaribisha Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. January Makamba kuhutubia Kongamano la Wadau kuhusu kukusanya maoni ya marekebisho ya Sera Mpya ya Mambo ya Nje ya Mwaka 2001 lililofanyika Hoteli ya Golden Tulip mjini Zanzibar tarehe 05 Februari 2024

Watu mbalimbali walioshiriki Kongamano la Wadau kuhusu kukusanya maoni ya marekebisho ya Sera Mpya ya Mambo ya Nje ya Mwaka 2001 lililofanyika Hoteli ya Golden Tulip mjini Zanzibar tarehe 05 Februari 2024
Mkurugenzi Msaidizi wa Idara ya Sera na Mipango katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bw. Justin Kisoka akiwasilisha mada kuhusu maeneo muhimu yanayopendekezwa katika marekebisho ya Sera ya Mambo ya Nje

Wadau mbalimbali wakifuatilia Kongamano la kukusanya maoni ya marekebisho ya Sera Mpya ya Mambo ya Nje ya Mwaka 2001 lililofanyika Hoteli ya Golden Tulip mjini Zanzibar tarehe 05 Februari 2024