Friday, February 9, 2024

TANZANIA – POLAND KUENDELEA KUSHIRIKIANA KIUCHUMI

Rais wa Jamhuri ya Poland Mhe. Andrzej Duda akisalimia na mwenyeji wake Rais Samia Suluhu Hassan Ikulu jijini Dar es Salaam


Rais wa Jamhuri ya Poland Mhe. Andrzej Duda akisaini kitabu cha wageni alipowasili Ikulu jijini Dar es Salaam huku mwenyeji wake Rais Samia Suluhu Hassan akimuangalia

Rais wa Jamhuri ya Poland Mhe. Andrzej Duda akiwa Ikulu jijini Dar es Salaam

Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan akizungumza na waandishi wa Habari Ikulu jijini Dar es Salaam

Rais wa Jamhuri ya Poland Mhe. Andrzej Duda akizungumza na waandishi wa Habari Ikulu jijini Dar es Salaam

 Rais wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akiwa na Rais wa Jamhuri ya Poland Mhe. Andrzej Duda wakizungumza na waandishi wa Habari Ikulu jijini Dar es Salaamkuelezea waliyokubaliana kutekeleza baada ya mazungumzo yao



Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Jamhuri ya Poland zimekubaliana kuendeleza ushirikiano katika sekta za kimkakati ikiwemo elimu, kilimo, biashara na uwekezaji ili  kukuza uchumi kwa manufaa ya pande zote mbili.

Hayo yamebainishwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Poland, Mhe. Andrzej Duda walipozungumza na waandishi wa habari Ikulu, jijini Dar es Salaam.

Akizungumza katika mkutano huo,  Mhe. Rais Samia ameeleza kuwa Tanzania na Poland zimekuwa na ushirikiano mzuri kwa zaidi ya miaka 60 huku wakishirikiana kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo hususan katika sekta ya Afya.

“Poland inatusaidia katika sekta ya afya, kuna miradi mitano ambayo Poland inafadhili katika Hospitali za Agah Khan, Kituo cha afya cha Chanika, Hospitali ya Temeke, Mwananyamala na Hospitali ya wilaya ya Nyamagana,” alisema Mhe. Rais Samia

Amesema wamekubaliana na Poland kuendelea kushirikiana katika sekta za kimkakati za elimu, kilimo, nishati, madini, biashara, uwekezaji na utalii

 “Katika mazungumzo yetu tumeelekeza timu za pande zote mbili kukaa na kufanya majadiliano ya mara kwa mara ili kubaini maeneo mapya ya ushirikiano ambayo yatatusaidia kupiga hatua kwa haraka zaidi katika kukuza biashara na uwekezaji na utalii kwa manufaa ya watu wetu” Alisema Rais Samia.


Ameishukuru Poland kupitia Wakala wake wa Mikopo kwa kukubali kuipatia Tanzania mkopo utakawezesha ujenzi wa Reli ya Kisasa ya SGR ambapo itahusisha ujenzi wa Lot 3 na Lot 4.

Hii ni hatua kubwa sana katika kutekeleza miradi ya kimkakati ambao pia utasaidia kukuza ujuzi wa wataalam wetu, tunawashukuru sana  kwa kukubali kutupatia mkopo huo,” alisema Mhe. Rais Samia.

Amesema wamekubaliana kuendelea kushirikiana katika sekta za utalii, biashara na uwekezaji ili kuongeza idadi ya watalii wanaokuja Tanzania kutoka Poland pamoja na kuinua kiwango cha biashara na kuvutia wawaekezaji zaidi kutoka Poland.

Amesema wamekubaliana kuwa wataalam wao watazungumza na kukubaliana namna bora na kuanzisha usafiri wa moja kwa
moja kutoka Poland hadi Tanzania haşa ikizingatiwa kuwa kuna idadi kubwa ya watalii kutoka Poland wanaokuja nchini.

“Kumekuwa na ongezeko la watalii ambapo kwa mwaka 2023 tulipokea watalii 41,000 na kwa mwezi mmoja tu uliopita tulipokea watalii 6,000 walioenda visiwani Zanzibar kutalii,” alisema.

Amesema amewakaribisha wawekezaji kutoka Poland waje Tanzania kwani fursa za uwekezaji ni nyingi.

Naye Rais Duda akizungumza katika mkutano huo ameishukuru Tanzania kwa kuendelea kushirikiana na Poland kitendo ambacho kilianza tangu wakati wa vita ya pili ya ambapo Tanzania iliwapokea raia wa Poland waliokuja Tanzania kutafuta Hifadhi wakati huo

Amewashukuru wananchi wa Arusha kwa kuendelea kuishi na   wananchi wa Poland na kuyaenzi makaburi ya watu hao.

Kadhalika amesisitiza kuwa, atahakikisha utalii, uwekezaji na biashara kati ya Tanzania na Poland unaongezeka kwani anajua Tanzania ni kituo kinachovutia na anaamini kuwa kuongezeka huko kutasaidia kutengeneza ajira kwa vijana, kuongeza ufanisi kwa kuleta mifumo ya kisasa ya kuendesha benki.

Ameahidi kuwa atahakikisha kampuni ya Poland ambazo zipo vizuri katika teknolojia ya mawasiliano zinakuja kwa wingi kuwekeza nchini.

“ Kwa kuanzia tutaanza na kampuni inayotengeneza Taa za nishati mbadala tutaangalia jinsi kampuni hiyo inakuja Tanzania kuwekeza,” alisema Mhe. Rais Duda.

No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.