Wednesday, February 14, 2024

RAIS SAMIA AINISHA MAENEO MUHIMU YA UWEKEZAJI NCHINI KWA WAWEKEZAJI WA NORWAY

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt Samia Suluhu Hassan amewakaribisha wawekezaji kutoka Norway kuja kuwekeza nchini kwenye sekta zinazogusa maisha ya wananchi wengi na kukuza uchumi wa nchi ikiwemo nishati mbadala, kilimo, gesi na mafuta, mifuko ya uwekezaji na usafirishaji.


Mhe. Rais Samia ametoa wito huo alipohutubia Wajumbe walioshiriki Kongamano la Biashara na Uwekezaji kati ya Tanzania na Norway liliofanyika jijini Oslo, tarehe 13 Februari 2024


Mhe. Dkt. Samia ambaye aliongozana na Mwana Mfalme wa Norway Haakon kwenye Kongamano hilo amesema Tanzania inahitaji wawekezaji wenye nia thabiti kuja kuwekeza  mitaji yao nchini  kwenye sekta  ambazo kwa kiasi kikubwa zinagusa maisha ya wananchi moja kwa moja kama vile chakula, umeme, mafuta na usafirishaji.


Amesema Tanzania ni sehemu salama kwa wawekezaji kutoka Norway kuwekeza mitaji yao kwakuwa Serikali imeboresha sheria mbalimbali za uwekezaji na kwamba kijografia Tanzania inafikika kwa urahisi na inapakana na nchi nane ambazo ni soko kubwa kwa wawekezaji na pia Tanzania ni nchi ya amani inayoamini katika usawa na utawala wa sheria.

Akizungumzia kilimo, Mhe. Rais Samia amewaeleza wawekezaji hao kwamba  bado sehemu kubwa ya ardhi ya Tanzania haijatumika ipasavyo kwenye sekta ya kilimo ambapo zipo Hekta milioni 44 zinazofaa kwa kilimo na kati ya hizo Hekta milioni 29.4 zinafaa kwa kilimo cha umwagiliaji 

Ameongeza kuwa, Tanzania ni nchi ya 10 duniani kwa uzalishaji wa zao la Alizeti na ni nchi ya pili Afrika kwa uzalishaji wa zao hilo ambalo bidhaa zake ikiwemo mafuta zinahitajika kwa wingi nchini na nchi jirani.

Kuhusu nishati mbadala, Mhe. Rais Samia amewahamasisha wawekezaji hao kuchangamkia fursa za umeme wa jua na upepo kwani bado Tanzania inahitaji kuwa na uhakika wa upatikaji wa nishati mbalimbali ikiwemo umeme wa uhakika.


Awali akizungumza katika Kongamano hilo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji, Mhe. Prof. Kitila Mkumbo amempongeza Mhe. Rais Samia kwa kuhamasisha wawekezaji kutoka nje na ndani ya nchi na namna ambavyo ameendelea kutambua mchango wa sekta binafsi kwenye uchumi na maendeleo ya nchi.


Mhe. Rais Samia yuko katika ziara ya kitaifa ya  siku tatu nchini Norway,  amefuatana na Mawaziri mbalimbali akiwemo Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. January Makamba, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji, Mhe. Prof. Kitila Mkumbo, Waziri wa Nci, Ofisi ya Makamu wa Rais-Mazingira, Mhe. Selemani Jafo, Waziri wa Kilimo, Mhe. Hussein Bashe, Waziri wa Fedha, Zanzibar, Mhe. Saada Mkuya, Makatibu Wakuu na Watendaji Wakuu wa Taasisi mbalimbali.

Kongamano hilo limehudhuriwa na zaidi ya Wawekezaji na Wafanyabiashara 150 kutoka Norway na Tanzania. 



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akihutubia kwenye Kongamano la Biashara na Uwekezaji kati ya Tanzania na Norway lililofanyika jijini Oslo. Mhe. Rais Samia yupo nchini Norway kwa ziara ya kitaifa ya siku tatu kuanzia tarehe 13 hadi 15 Februari 2024 kwa mwaliko wa Mfalme wa Norway Herald V.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. January Makamba akishiriki Kongamano la Biashara na Uwekezaji kati ya Tanzania na Norway lililofanyika Oslo. Kulia ni Balozi wa Tanzania nchini Norway mwenye makazi yake nchini Sweden, Mhe. Grace Olotu
Waziri wa Nchi, ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji, Mhe. Prof. Kitila Mkumbo akizungumza wakati wa Kongamano hilo.
Waziri wa Viwanda na Biashara wa Norway, Mhe. Jan Christian Vestre naye akizungumza wakati wa Kongamano la Biashara na Uwekezaji kati ya Tanzania na Norway
Kongamano likiendelea
Mhe. Rais Samia akizungumza kwenye Majadiliano ya Ngazi ya Juu kuhusu  Usawa wa Kijinsia na Siasa katika Biashara wakati wa Kongamano la Biashara na Uwekezaji kati ya Tanzania na Norway
Mshauri wa Rais, Siasa na Uhusiano na Jamii, Mhe. William Lukuvi nae akishiriki Kongamano la Biashara na Uwekezaji jijini Oslo. Wengine ni Mkurugenzi wa Kitengo cha Sheria katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dkt. Gift Kweka (aliyesuka nywele)


Mratibu wa Kongamano la Biashara na Uwekezaji kati ya Tanzania na Norway ambaye pia ni Mkurugenzi wa Idara ya Biashara za Kimataifa na Diplomasia ya Uchumi katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi John Ulanga akifuatilia Kongamano hilo
Mhe. Balozi Grace Olotu akishiriki Kongamano hilo na wajumbe wengine kutoka Norway
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TanTrade) Bi. Latifa M.Khamis akishiriki Kongamano hilo
Sehemu ya Washiriki kutoka Tanzania
Afisa Mambo ya Nje Mkuu kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,Bw. Magabilo Murobi akishiriki Kongamano hilo
Sehemu ya ujumbe kutoka Norway wakishiriki Kongamano











 

No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.