Tuesday, September 15, 2020

NCHI 15 ZARUHUSIWA KULETA WAANGALIZI WA UCHAGUZI MKUU 2020

 Nchi 15 kupitia Balozi zao hapa nchini zimeruhusiwa kuleta waangalizi wa Kimataifa katika uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika mwezi Octoba, 2020 baada ya Balozi hizo kuwasilisha maombi na kufuata taratibu.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamagamba John Kabudi ameyasema hayo leo Jijini Dar es Salaam alipokutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa Umoja wa Ulaya Balozi Manfred Fanti na kuongeza kuwa uchaguzi wa mwaka huu kwa mara ya kwanza umekuwa tofauti na miaka iliyopita kwa kuwa unafanyika kwa kugharamiwa na fedha za ndani badala ya wahisani jambo ambalo baadhi ya watu walianza kuhofia kutokuwepo kwa waangalizi wa kimataifa katika uchaguzi.

"Huu ni uchaguzi mkuu ambao kwa mara ya kwanza kwa asilimia 100 tunaugharamia sisi wenyewe kama Serikali ya Tanzania, utaratibu wa uchaguzi chini ya sheria ya uchaguzi na chini ya utaratibu wa Kimataifa huwa tunakuwa na waangalizi wa uchaguzi na mwaka huu nchi hizo 15 kupitia balozi zao zimepata  kibali mara baada ya kufuata taratibu za kuomba kuleta waangalizi wa uchaguzi mkuu," Amesema Prof. Kabudi 

Mbali na Balozi wa Umoja wa Ulaya pia Prof. Kabudi amekutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa Italia hapa nchini Balozi Roberto Mengoni na baadae Balozi wa Poland Balozi Krzysztof Buzalski ambapo amewakabidhi vitabu vya sheria ya uchaguzi na kanuni za uchaguzi na miongozo mbalimbali inayohusu masuala ya uchaguzi ili kuwapa fursa ya kufahamu namna uchaguzi unavyoendeshwa hapa nchini hasusani baada ya uwepo wa malalamiko kutoka kwa baadhi ya vyama vya upinzani juu ya kuenguliwa kwa wagombea wao. 

Kwa upande wake Balozi wa Umoja wa Ulaya hapa nchini Balozi Manfred Fanti amesema Nchi za Umoja huo zimekuwa zikifuatilia kwa karibu mchakato wa kampeni za uchaguzi mkuu zinavyoendelea hapa nchini ambapo mpaka sasa wanaridhishwa na kampeni zinavyofanyika kwa uhuru na amani na sasa wanajiandaa na zoezi la uangalizi wa uchaguzi huo. 

Balozi wa Italia hapa nchini Mhe. Roberto Mengoni amesema amevutiwa na namna vyombo vya habari vimekuwa vikitoa nafasi kwa wagombea wote kwa uhuru na bila ya ubaguzi na kupongeza namna Watanzania wanavyojitokeza kwa wingi kusikiliza sera za wagombea mbali na tishio la corona na kwamba ana imani kuwa Kiongozi atakayechaguliwa atakuwa ametokana na utashi wa wananchi.

Mbali na masuala ya uchaguzi mkuu, Waziri Kabudi na Mabalozi hao wamejadili pia masuala ya kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia,maendeleo ya kiuchumi,biashara na uwekezaji katika sekta mbalimbali ikiwemo elimu,afya,maji na miundombinu.

Balozi wa Umoja wa Ulaya Balozi Manfred Fanti akimuelezea jambo Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Prof. Palamagamba John Kabudi walipokutana kwa mazungumzo leo jijini Dar es Salaam 


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Prof.   Kabudi akimkabidhi Balozi wa Italia nchini Balozi Roberto Mengoni vitabu vya sheria ya uchaguzi na kanuni za uchaguzi na miongozo mbalimbali inayohusu masuala ya uchaguzi      


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Prof. Palamagamba John Kabudi akimfafanulia jambo Balozi wa Poland hapa nchini, Balozi Krzysztof 




 

No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.