Friday, July 6, 2012

Mkutano wa Waziri Membe na Mabalozi wa EU na Marekani



TAARIFA KUHUSU MKUTANO WA MHE. BERNARD MEMBE (MB), WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA KIMATAIFA NA MABALOZI WA NCHI ZA UMOJA WA ULAYA NA MAREKANI PAMOJA NA WAANDISHI WA HABARI TAREHE 05 JULAI 2012

Leo tarehe 05 Julai 2012, Mhe. Bernard Kamilius Membe (Mb),Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa amekutana na Waandishi wa Habari pamoja na Mabalozi wa Nchi za Umoja wa Ulaya na Marekani hapa nchini kwa lengo la kutoa msimamo wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuhusu kuwepo kwa uvumi kwamba Meli za Iran zimesajiliwa na kupeperusha bendera ya Tanzania kama ilivyotangazwa katika vyombo vya habari ndani na nje ya nchi.

Katika mazungumzo yake na Waandishi wa Habari na baadaye Mabalozi, Mhe. Waziri alieleza kwamba Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ilipata taarifa kuhusu meli za Iran kusajiliwa na kupeperusha bendera ya Tanzania kupitia kwenye vyombo vya habari.

Alisema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ilichukua hatua ya kuitaka Mamlaka ya Usafiri wa Baharini ya Zanzibar – Zanzibar Marine Authority (ZMA) ambayo kwa Sheria Na. 3 ya mwaka 2009 ina mamlaka ya kusajili meli za Kimataifa kuchuguza tuhuma hizo na kutoa taarifa.

Aidha, aliwatanabaisha Waandishi na Mabalozi kwamba Mamlaka ya Usafiri wa Baharini Zanzibar ilichukua hatua za kumtaka Wakala wake wa kusajili meli, Kampuni ya PHILTEX yenye makao yake makuu Dubai, Falme za Kiarabu (UAE) kutoa taarifa kama kati ya meli 399 zilizosajiliwa kuna meli za Iran.

Nayo Kampuni ya PHILTEX ilitoa taarifa kuwa kati ya meli zilizosajiliwa hakuna meli hata moja ya Iran. Hata hivyo, waliongeza kuwa meli zilizosajiliwa hivi karibuni zilikuwa na usajili wa Cyprus na Malta.

Aidha, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa ilimwita Balozi wa Iran nchini ili kujua kama kuna ukweli kuwa baadhi ya meli zilizosajiliwa ni za Iran. Balozi alikataa kabisa kuwa hakuna meli za Iran zilizosajiliwa Zanzibar na zinazopeperusha bendera ya Tanzania.

Taarifa hizi kutoka kwenye vyombo vya habari, Kampuni ya PHILTEX na Ubalozi wa Iran nchini zimepelekea Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kufanya uchunguzi wa kina ili kuthibitisha kama kweli kuna meli za Iran zilizosajiliwa Zanzibar na zinazopeperusha bendera ya Tanzania.

Ili kupata ukweli wa tuhuma hizo, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeomba nchi za Umoja wa Ulaya na Marekani kusaidia katika uchunguzi. Mhe. Waziri, aliwakabidhi Barua za Kibalozi kuwasilisha rasmi ombi hilo.

Mhe. Waziri Membe aliwahidi waandishi wa Habari na Mabalozi hao kwamba kuwa baada ya uchunguzi kukamilika na ukweli kubainika, serikali ya Jamhuri ya Muungano itachukuwa hatua za haraka ikiwemo kufuta usajili wa meli zote zitakazogundulika kuwa ni za Iran.



No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.