Tuesday, December 11, 2018

Siku ya Tanzania ilivyosherehekewa sambamba na maonesho ya Jua Kali/Nguvu kazi

Gavana wa Kaunti ya Uasin Gishu, Jackson K. Mandgo alipokuwa akizungumza na wajasirimali katika sherehe ya siku ya Tanzania viwanja vya michezo Kaunti ya Uasin Gishu mjini Eldoret katika maonesho ya Jua Kali/Nguvu Kazi yanayoendelea mjini hapo. Kushoto ni Balozi wa Tanzania nchini Kenya, Mhe. Dkt. Pindi Chana.

Gavana wa Kaunti ya Uasin Gishu, Mhe. Jackson K. Mandgo akiweka saini kitabu cha wageni mara baada ya kufika  kwenye banda la  Tanzania lililopo kwenye viwanja vya michezo vya Kaunti ya Uasin Gishu mjini Eldoret katika maonesho ya Jua Kali/Nguvu Kazi. Mhe.Mandgo alikuwa mgeni rasmi katika sherehe ya siku ya Tanzania katika maonesho hayo zilizofanyika tarehe 9 Desemba 2018. Kulia ni Balozi wa Tanzania nchini Kenya, Mhe. Dkt. Pindi Chana na kushoto ni Seneta wa Kaunti ya Uasin Gishu, Mhe. Profesa Margrate Kamar.

Gavana wa Kaunti ya Uasin Gishu, Mhe. Mandgo akipanda mti ikiwa ni kumbukumbu ya maadhimisho ya miaka 57 ya Uhuru wa Tanzania Bara zilizoadhimishwa leo tarehe 09 Desemba 2018. Wanaoshuhudia tukio hilo ni pamoja na  Balozi wa Tanzania nchini Kenya, Mhe. Dkt. Pindi Chana
Gavana wa Kaunti ya Uasin Gishu, Mhe. Jackson K. Mandgo akinunua nguo alipotembelea Banda la Wajasiriamali wa Tanzania baada ya kufurahia bidhaa mbalimbali zikiwemo nguo. Balozi wa Tanzania nchini Kenya, Mhe. Dkt. Pindi Chana aliambatana na Gavana huyo kutembelea mabanda ya wajasiriamali kutoka Tanzania.



Gavana wa Kaunti ya Uasin Gishu, Mhe. Jackson K. Mandgo akivishwa vazi la kabila la Wamaasai kutoka Tanzania na kukabidhiwa mkuki na Balozi wa Tanzania nchini Kenya, Mhe.Dkt. Pindi Chana wakati wa sherehe ya siku ya Tanzania zilizofanyika sambamba na maonesho ya Jua Kali/Nguvu Kazi
===============================================

Gavana wa Kaunti ya Uasin Gishu nchini Kenya, Mhe. Jackson K. Mandgo amezishauri Serikali za Nchi Wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki kuweka bidhaa za wajasiriamali katika maduka makubwa (super market) ili wananchi kuzinunua na kuacha tabia ya kuthamini bidhaa za kutoka nje.

Gavana Mandgo aliyasema hayo wakati wa kusherehekea siku ya Tanzania iliyofanyika sambamba na maonesho ya 19 ya Afrika Mashariki ya Jua kali/Nguvu Kazi yanayoendelea katika Viwanja vya michezo vya Kaunti ya Uasin Gishu mjini Eldoret Kenya ambapo alikuwa mgeni rasmi kwenye siku ya Tanzania. Mhe. Mandgo alisema kwamba bidhaa za wajasirimali kutoka nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki zinakidhi vigezo vya kuuzwa katika maduka hayo kutokana na kuwa na  ubora wake.

Katika maonesho ya Jua Kali/Nguvu Kazi kila nchi husherehekea siku yake kwa kutangaza bidhaa na utamaduni wake. Tanzania ilitumia fursa hiyo kusherehekea miaka 57 ya Uhuru wa Tanzania Bara iliyoadhimishwa nchini kote tarehe 9 Desemba 2018.

Gavana Mandgo alisema kwamba wajasiriamali wanauwezo mkubwa wa kutengeneza  bidhaa bora ambazo kwa bahati mbaya hazipatikani katika maduka makubwa (super makert) hivyo alitoa wito kuwa wakati umefika sasa kwa bidhaa hizo kuuzwa katika maduka hayo.

Aidha alizishauri nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki kuvitumia Vituo vya Elimu za Ufundi kama VETA hapa nchini, kutoa taaluma zaidi kwa wajasiriamali kwa lengo la kuzalisha bidhaa zenye ubora na viwango vya kimataifa.

Alisema kwamba  Serikali ya Kenya hususan Kaunti ya Uasin Gishu ya  Eldoret itapeleka Mswada katika Baraza lake kwa kufanyia marekebisho ya sheria ya kutoa vyeti kwa wajasiriamali ambao watatahiniwa kwa  ubora wa bidhaa ambazo wanazalisha badala ya kufanya mitihani ya kuandika.

Pia alizitaka ofisi zote za Serikali ya Kaunti ya Uasin Gishu, kutumia samani zinazotengenezwa na wajasiriamali kutokana  na kuwa  ni madhubuti na zenye ubora kuliko zilivyotengenezwa kutoka  nje ya Afrika Mashariki.

Gavana Mandgo ameipongeza Tanzania  kwa kusherehekea miaka 57 ya Uhuru wa Tanzania Bara.


No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.