Wednesday, December 19, 2018

Tanzania na Morocco kuimarisha ushirikiano katika sekta ya afya

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Mhe. Ummy Mwalimu akiwa kwenye mazungumzo na Waziri wa Afya wa Morocco, Mhe. Prof. Anas Doukkali yaliyofanyika jijini New Delhi, India wakati wa Mkutano Maalum wa 4 wa Afya ya Mama na Mtoto uliofanyika jijini humo hivi karibuni. Pamoja na mambo mengine Mawaziri hao walikubaliana kuimarisha ushirikiano kwenye sekta ya afya hususan katika kutoa mafunzo kwa madaktari na wauguzi na kubadilishana ujuzi.
Mawaziri wakiendelea na mazungumzo huku wajumbe waliofuatana nao kutoka Tanzania na Morocco wakifuatilia mazungumzo hayo
Mhe. Waziri Ummy akiagana na Mhe. Prof Anas mara baada ya mazungumzo yao.
=======================================================
TANZANIA NA MOROCCO KUIMARISHA USHIRIKIANO KATIKA SEKTA YA AFYA

Mhe.Ummy Mwalimu  amekutana na kufanya mazungumzo na Mhe.Prof. Anas Doukkali, Waziri wa Afya wa Falme ya Morocco pembezoni mwa Mkutano Maalum wa 4 wa Afya ya Mama na Mtoto uliofanyika jijini New Delhi hivi karibuni.

Pamoja na mambo mengine, Mawaziri hao walijadili namna ya kukuza na kuimarisha ushirikiano kati ya Tanzania na Morocco hususan katika Sekta ya Afya ikiwemo uzalishaji wa dawa za binadamu, mafunzo kwa wataalam wa afya, wakiwemo Madaktari, Wauguzi hususan wa idara za wagonjwa mahututi katika Hospitali zote za Mikoa na Wilaya.

Aidha, walijadili namna ya kubadilishana ujuzi wa Wataalam wa Afya kwa ajili ya kuwaongezea ujuzi, kuimarisha huduma za afya katika kukinga magonjwa yasiyoambukiza (NCDs) na yanayoambukiza kama vile VVU/UKIMWI pamoja kuimarisha huduma za mama na motto.

Kwa upande wake, Mhe. Ummy aliiomba Serikali ya Morocco kusaidia kujenga Hospitali ya Wazazi (Maternity Hospital) jijini Dodoma ambapo Mhe. Prof. Anas amesema atapeleka ombi hilo kwa Mfalme wa Morocco, Mtukufu Mfalme Mohamed VI.

Katika kuhakikisha makubaliano hayo, yanatekelezwa mapema, wamekubaliana Wizara kuteua Mtumishi Mwandamizi mmoja awe mratibu wa masuala hayo. Pia, wamekubaliana kuwa uandaliwe Mkataba wa Ushirikiano (MoU) ili waweze kusaini makaubaliano hayo na kuanza kuyatekeleza mapema iwezekanavyo.             

Sambamba na hilo, Waziri wa Afya wa Morocco, Mhe. Prof. Anas ameahidi kuitembelea Tanzania mwishoni mwa mwezi Februari, 2019 ili kujionea utoaji wa huduma za afya nchini, ambapo ameahidi kuja na Wataalam wa Wizara yake pamoja na Wawekezaji kutoka Morocco hususan kwenye eneo la viwanda vya dawa.

-Mwisho-


No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.