Thursday, February 10, 2022

WATANZANIA WAASWA KUILINDA NCHI

Imeelezwa kuwa jukumu la kulinda nchi ni la kila Mtanzania na vijana wanatakiwa kuwa mstari wa mbele kwa kuwa wao ni chachu ya ukuaji uchumi wa nchi na viongozi watarajiwa wa Taifa hili.

Kauli hiyo imetolewa leo na Mkurugenzi wa Ushirikiano wa Kikanda katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Agnes Kayola wakati alipokuwa anafungua semina ya siku moja kwa wanafunzi wa shule za sekondari za jijini Dodoma.

Balozi Kayola alisema Wizara imekuwa na utaratibu wa kutoa elimu kwa wanafunzi ili wao kama vijana wawe na elimu stahiki kuhusu masuala ya kikanda na kimataifa ambayo yatawawezesha kushiriki kikamilifu katika kutumia fursa za mtangamano ukiwemo wa Jumuiya ya Afrika Mashariki ( EAC).

Alieleza kuwa katika Jumuiya ya Afrika Mashariki, vijana wametambuliwa kama kundi muhimu kwa maendeleo ya jumuiya hiyo, hivyo utoaji wa elimu hiyo ni muhimu ili vijana wafahamu fursa zilizopo katika nyanja mbalimbali za uchumi, utamaduni, elimu na siasa na namna na ya kuzichangamkia. 

Aliwambia wanafunzi hao kuwa Sera ya Vijana ya EAC imeweka bayana haki za vijana kuwa na uhuru wa kutembea na kuweka makazi kwenye nchi yoyote ya Jumuiya kwa madhumuni mbalimbali kama kutafuta elimu, ajira au kufanya biashara, hivyo ni muhimu kwa vijana hao wanapoelekea kuhitimisha masomo yao ya sekondari ni vyema wakaweka mipango ya kuchangamkia furza za EAC.

Balozi Kayola alihitimisha hotuba yake kwa kuwasihi vijana hao kuwa mabalozi waźuri wa Tanzania katika safari yao ya maisha na kuwaelimisha wanafunzi wenzao na jamii kwa ujumla ambao kwa sababu mbalimbali hawakuweza kupata elimu hiyo.

Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki imejiwekea utaratibu wa kuelimisha makundi mbalimbali katika Jumuiya yakiwemo ya wanafunzi kuhusu Sera ya Mambo ya Nje. Na katika semina hiyo wanafunzi hao walielimishwa kuhusu majukumu ya Wizara, utekelezaji wa Sera ya Mambo ya Nje, hatua za mtangamano wa EAC na fursa zake pamoja mchakato wa kuelekea shirikisho la kisiasa la EAC.

Semina ya siku moja kwa wanafunzi wa shule za sekondari za jijini Dodoma masuala mbalimbali ya Mtangamo wa Jumuiya ya Afrika Mashariki ikiendelea 

Sehemu ya wadau wakifuatilia semina ya siku moja kwa wanafunzi wa shule za sekondari za jijini Dodoma iliyofanyika kwenye ukumbi wa informatics katika Chuo Kikuu cha Dodoma

Picha ya patoja
Mkurugenzi wa Idara ya Ushirikiano wa Kikanda Balozi Agness Kayola akitoa hotuba ya ufunguzi wa semina ya siku moja kwa wanafunzi wa shule za sekondari za jijini Dodoma. Kushoto ni Mkurugenzi wa Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali Bw. Emmanuel Buhohela. Wote kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki

Semina ikiendelea
Semina ikiendelea

No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.